Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 1/15 kur. 6-7
  • Mhalifu Apokea Msamaha wa Rais

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mhalifu Apokea Msamaha wa Rais
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAISHA KATIKA MUNTINLUPA
  • MAISHA KATIKA IWAHIG
  • KAFUNGULIWA
  • Je! Inawezekana Kutengeneza Wafungwa Wawe na Tabia Njema?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • “Mmebadili Maoni Yangu Juu ya Mashahidi wa Yehova”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Masimulizi ya Imani Kutoka Gereza Maarufu
    Amkeni!—2001
  • Je, Magereza Yanaendeleza Uhalifu?
    Amkeni!—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 1/15 kur. 6-7

Mhalifu Apokea Msamaha wa Rais

HUKO nyuma katika mwaka 1945, nilikuwa nikionwa kuwa Mkatoliki mwenye kushika dini sana. Nakumbuka siku moja ambayo nilienda kwa magoti kutoka mlango wa kanisa mpaka kwenye madhabahu ili nitimize nadhiri yangu. Wakati ule ule, nilikuwa mlevi wa kupindukia tena nilikuwa mshiriki wa kundi la wahalifu. Nilikuwa nikipata rafiki kwa urahisi kwa sababu nilikuwa nikitoa fedha kwa vyepesi. Kazi yangu ya kujipatia riziki ilikuwa kununua na kuuza mali ya wizi. Katika njia hii ningeweza kupata kiasi cha shilingi 11,000 (Z1,200) kila juma. Si ajabu kwamba nilikuwa mkarimu hivyo! Nilipoishi, Balicbalic, Manila, niliheshimiwa sana.

Niliheshimiwa kwa kuwa “jambazi lenye nguvu!” Lakini karibu nami kulikuwako “jambazi” jingine lililokuwa likiniona kuwa mpinzani wake. Siku moja, kundi langu la wahalifu na lake yalipambana. Nilimpiga risasi mpinzani wangu akafa; rafiki zake wakakimbia, nikawa mkuu zaidi. Huo ulikuwa mwaka 1947.

Walakini, sasa nililazimika kujificha nisikamatwe, kwa hiyo nilikimbilia kusini mwa Manila katika Cavite. Zawadi ya shilingi 1,100 (Z120) aliahidiwa kupewa ye yote ambaye angenikamata, na hiyo ilitosha kutia moyo hata rafiki mkubwa anisaliti. Katika Mei 1949 nilikamatwa, na, katika Mei 1,1951, nikahukumiwa kifungo cha maisha.

MAISHA KATIKA MUNTINLUPA

Siku iliyofuata nikiwa nimefungwa pingu mikononi nilipelekwa katika Gereza la Kitaifa katika Muntinlupa, Rizal. Nilipofika, mavazi yangu yalichukuliwa, nikapewa mavazi ya gereza. Namba yangu ilikuwa 11481-P. Mara tu nilipoingia ndani ya gereza, nilijiona katika hali isiyo ya kawaida. Nilijua kwamba nilikuwa nikiishi, lakini niliona kama kwamba nilikuwa katika shimo. Wale wafungwa wengine walikuwa kama wanyama. Sana sana nilichukia namna walivyokuwa wakiwalazimisha vijana wapya wafanye ngono za wanaume kwa wanaume pamoja nao. Moyoni mwangu niliwahurumia sana vijana hawa waliokuwa wakitendwa hivyo, nami niliazimia kwamba sitawatumia wanadamu wenzangu tena kujifaidi mwenyewe wala kuwadhulumu. Kwa hiyo nilijipa moyo nikamwomba Mungu anisaidie kuvumilia hali mbaya sana ambayo katika hiyo nilijikuta sasa.

Msimamizi wa gereza la Muntinlupa aliruhusu uhuru wa ibada, nako kulikuwa na vikundi vingi mbalimbali vilivyokuwa vikifanya ibada. Niliamini kwamba dini zote zilitoka kwa Mungu, kwa hiyo kwa muda kama wa miezi sita hivi nilihudhuria kila mkutano. Walakini, baada ya kutazama mwenendo na tabia zao, niliamua kwamba hamna ukweli ndani yao. Jambo moja nililopinga lilikuwa namna vikundi vingine vilivyokuwa vikileta wasichana warembo katika mikutano yao ili wavute wahudhuriaji wengi. Jambo hilo lilifanya wafungwa wengi wafanye mambo machafu baadaye.

Mwishowe, nilihudhuria mikutano iliyofanywa na Mashahidi wa Yehova. Nilivutiwa sana na njia yao ya kufundisha. Walifundisha kutokana na Biblia nayo ilikuwa yenye kuelimisha sana. Sana sana nilipendezwa na jina la Mungu. Mwishowe, nilijiweka wakf kwa Yehova nikabatizwa katika mwaka 1953. Nilianza kuhubiri wale wafungwa wengine pamoja na wafanya kazi katika Muntinlupa. Wengine wao walisikiliza, na baada ya kupita muda wengine wao walipata kuwa Mashahidi katika gereza hilo.

Tulipata magumu fulani juu ya kusaluti (kusalimu) bendera kwa sababu ya kupinga jambo hilo kwa kuongozwa na dhamiri zetu. Wakati mmoja tulilazimika kufungiwa peke yetu. Walakini, asubuhi moja, wafungwa elfu nyingi walikuwa wamekusanyika katika uwanja wa michezo wa gereza hilo. Bendera ilipandishwa na wote isipokuwa Mashahidi peke yao, ambao idadi yao ilikuwa kama 20 hivi wakati huo.

Wakati huo kulikuwa na mvua kubwa sana, nao wafungwa walikimbia ili wajikinge na mvua. Ni sisi Mashahidi peke yetu tulioachwa tukisimama huku tukinyeshewa na mvua, kwa kuwa hatukuwa tumepewa ruhusa ya kuondoka. Baadaye, msimamizi alituita akatuuliza sababu hatukukimbia kama wale wengine, lakini tulibaki tu tumesimama tukanyeshewa. Tulimweleza kwamba msimamo wetu juu ya kusaluti bendera haukumaanisha kwamba tulikuwa hatuiheshimu. Sababu ilikuwa kwamba tuliliona tenda hilo la kusaluti kuwa sherehe ya kidini. Tangu wakati huo, msimamo wetu juu ya jambo hili ulifahamika vizuri zaidi.

Katika mwaka 1957 karibu kila siku gereza la Muntinlupa lilikuwa na msukosuko uliotokezwa na vikundi vya wahalifu waliokuwa wakipingana waliokuwa na majina kama vile “OXO” na “Sigue-sigue.” Ili kusaidia kuendeleza amani na utengamano waliwachagua wale waliokuwa na mwenendo bora wakawapa migawo. Nilipewa mgawo wa kuwa bastonero, maana yake ni mfungwa ambaye ameaminiwa kuangalia wafungwa wengine. Kama zawadi kwa sababu ya kutimiza madaraka yangu kwa uaminifu, nilichaguliwa nikahamishwa kwenda katika Koloni la Adhabu la Iwahig katika Palawan.

MAISHA KATIKA IWAHIG

Katika Iwahig nilipewa kazi nyingine yenye madaraka​—⁠nilifanywa msimamizi wa chakula kwa wafungwa 800. Nilikuwa nikipokea chakula nikawa nikisimamia kipikwe pamoja na kukigawa kwa wanaume hao. Wenye mamlaka waliona kwamba mwenendo wangu ulikuwa mwema kwa sababu wafungwa walitosheka na uangalizi wangu, hali wengine waliokuwa wamepewa kazi yangu hiyo walikuwa wameuawa.

Siku moja, msimamizi wa Iwahig aliuliza sababu wafungwa walionekana kutosheka nami. Nilimwambia kwamba mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova na ya kwamba nilikuwa nikitumia kanuni za Biblia katika kazi yangu. Tangu wakati huo alinitumaini zaidi, nami nikapata uhuru zaidi wa kuwahubiri wafungwa wenzangu. Kama matokeo, nilikuwa nikiongoza funzo na kikundi cha watu 13. Upesi, nilionana na Shahidi wa Kundi la Puerto Princesa la mahali hapo, naye mmoja wa Mashahidi wa Yehova akatusaidia kuwa na mikutano ya kawaida ndani ya Iwahig.

Nilipokuwa katika Iwahig, nilisikia habari za kusanyiko la mataifa yote ambalo lingefanyiwa katika Manila’s Rizal Memorial Stadium katika mwezi wa Agosti ya mwaka 1963. Hiyo ilikuwa Julai 1, 1963. Miaka 10 ilikuwa imekwisha tangu nibatizwe, walakini, nilikuwa sijahudhuria kusanyiko lo lote la Mashahidi. Nilisikitika sana nikajawa na wasiwasi. Usiku huo sikuweza kulala kwa sababu ya kufikiri juu ya kusanyiko hilo, kwa hiyo, nilianza kusali, nikaomba nionyeshwe njia ambayo katika hiyo ningeweza kuhudhuria.

KAFUNGULIWA

Jioni moja nilimwandikia aliyekuwa rais wa Filipino katika wakati huo, Diosdado Macapagal. Nilimsihi anipe msamaha wa rais ili niweze kuhudhuria kusanyiko hilo. Julai 30 jibu lake likaja likiwa na maneno haya ya ajabu: “Ombi lako limekubaliwa.” Nililia kwa furaha. Agosti 10 nikafunguliwa. Agosti 15 nikaungana na jamaa yangu. Agosti 17 sote tulijiunga na maelfu ya ndugu Wakristo katika kusanyiko hilo la mataifa. Maneno ya kueleza furaha yangu katika wakati huo hayawezi kupatikana. Mungu alikuwa amenifadhili sana.

Baada ya kusanyiko hilo niliweza kuendelea na utumishi wangu kwa Yehova Mungu nikiwa mtu huru. Ijapokuwa nilikuwa nimekuwa gerezani, niliweza kupata kazi ya kuajiriwa ili niweze kuangalia jamaa yangu kama impasavyo mwanamume Mkristo. Tajiri wangu anayeniajiri sasa anajua kwamba nimekuwa gerezani, lakini anajua vilevile kwamba sasa mimi ni Mkristo; kwa hiyo anitumaini kazini kwangu.

Kundini, nimepata kuendelea nikawa mzee. Lengo langu maishani ni kuendelea kumtumikia Yehova kwa moyo wangu wote, pamoja na mke wangu na watoto. Nalo tumaini letu ni kukubaliwa Naye, na kupokea baraka yake ya uzima katika paradiso ya kidunia inayokaribia sana sasa.​—⁠Imetolewa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki