Je! Inawezekana Kutengeneza Wafungwa Wawe na Tabia Njema?
“NAJIONA kuwa huru kabisa! Sina giza tena lililokuwa limeninasa hapo kwanza.”
“Ninafurahia kila siku ya maisha yangu!”
Haya ni maneno ya wafungwa wawili wa gereza la Iwahig la Koloni la Adhabu katika visiwa vya Filipino. Wote wawili walipatikana na hatia ya uuaji, nao wametumia miaka mingi katika gereza. Walakini wamepata jambo ambalo limewaletea furaha kubwa zaidi kuliko kitu kingine cho chote walichokuwa nacho katika miaka yao ya kwanza walipokuwa huru.
GEREZA LA IWAHIG
Gereza la Iwahig pamoja na Koloni la Adhabu—kulipa jina lake kamili—liko tofauti sana na magereza mengine. Liko katika kisiwa cha Palawan, kisiwa kirefu katika mfululizo wa visiwa vya Filipino vinavyoelekea kusini magharibi kuingia katika Bahari ya China. Gereza hilo lina eneo lenye ukubwa wa eka 95,410 (hectares 38,612), nalo linaweza kutosha wafungwa 5,000. Walakini, hawa huitwa kolonos (wale wanaoishi katika koloni) mahali pa kuitwa wafungwa.
Karibu eneo lote la gereza halina kuta ndefu au pao. Hakuna walinzi wenye bunduki, nao wafungwa huwa na uhuru wa kutembea-tembea. Wengine hawavai vazi la gereza. Idadi kubwa yao hulala katika vyumba vya kulala watu wengi nao hufanya kazi ya kukuza mimea inavyokuzwa zaidi katika koloni hiyo: Mchele, mahindi, mbata, miti ya kupasuliwa mbao, namna ya henzerani na namna mbalimbali za mianzi.
Kolonos hawa wanapokea fedha kidogo kila mwezi, ambazo wanaweza kuongezea kwa kufanyiza vitu kwa mikono na kuviuza. Wachache, ambao wameonyesha kwamba wanaweza kutumainiwa na wanaoweza kulisha jamaa zao, wanaruhusiwa wawalete katika koloni waishi humo. Jamaa hizi huishi pamoja katika nyumba za orofa zenye vyumba vingi; wanapewa mahitaji ya lazima bure, nao wanaweza kukuza chakula au kufuga mifugo ili kupunguza gharama.
Adabu nzuri inakaziwa, lakini kolonos wanapewa uhuru zaidi kadiri wanavyojionyesha kutumainika. Wengine hata wanatumiwa katika kuiongoza koloni hiyo. Zaidi ya hayo, wanapewa mazoezi katika ufundi wa namna mbalimbali, nao wale wasiojua kusoma na kuandika wanapewa mafundisho ya msingi katika kusoma na kuandika pamoja na kufanya hesabu. Wanaruhusiwa kuwa na tafrija, kutia na kuogelea, michezo ya kushindana ya namna mbalimbali, vipindi vya muziki pamoja na kwenda kula chakula nje, vilevile mikutano fulani ya kidini inaruhusiwa katika siku ya Jumapili.
Kwa muda wa miaka mingi Iwahig imekuwa mahali penye matokeo mazuri katika kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kufanya wanafunzi. Lakini utendaji huu wa Mashahidi wa Yehova ulianzaje?
KAZI YA KUHUBIRI KATIKA IWAHIG
Watu wengi wamehusika katika utendaji huu katika muda wa miaka mingi, naye Domingo Obispo alikuwa mmoja wa wale wa kwanza.a Alikuwa akitumikia kifungo cha muda mrefu katika gereza la Muntinlupa karibu na Manila, akaanza kuhudhuria mikutano iliyokuwa ikiongozwa katika gereza hilo na mzee mwenyeji wa Mashahidi wa Yehova. Mwishowe alikubali yale aliyokuwa akijifunza kutokana na Biblia, akawa Shahidi. Kisha, alipohamishwa na kupelekwa katika Iwahig, alishiriki na wengine yale aliyokuwa amejifunza.
Katika mfano mwingine, mmoja aliyekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova alitengwa na ushirika wa kundi kwa sababu ya mwenendo mbaya. Alifanya uvunjaji wa sheria wa namna mbaya sana mpaka akafungwa gerezani. Alipokuwa gerezani alianza kutubu, kama alivyofanya Mfalme Manase wa kale. (2 Nya. 33:10-13) Mwishowe, mwanamume huyu alihamishwa na kupelekwa katika gereza la Iwahig, alionana na wazee katika Kundi la Puerto Princesa lililoko karibu, nao waliweza kuona kwamba toba lake lilikuwa la kweli. Kwa hiyo alikubaliwa tena kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, naye akaanza kuhubiri katika koloni hilo.
Tena kulikuwako na mwanamume aliyetoroka kutoka gereza la Iwahig. Alikwenda katika mmojawapo wa miji katika kisiwa cha Palawan, akaanza kuishi humo kama raia wa kawaida. Mmoja wa Mashahidi wa Yehova alimhubiri naye mfungwa huyo aliyetoroka aliamini aliyoyasikia. Ndipo dhamiri yake ilipoanza kumsumbua, akaonana na mzee katika kundi lake. Afanyeje?
Mzee huyo Mkristo alimshauri kulingana na maneno ya mtume Paulo katika Warumi sura ya 13, mstari wa kwanza. Alionyeshwa kwamba Mkristo ana daraka la kumlipa Kaisari yaliyo ya Kaisari. Kwa hiyo, akiambatana na rafiki wengine Wakristo, alirudi katika koloni lile akajitoa. Sasa yeye ni mfungwa mwaminifu naye amepewa mgawo wa kuwafundisha wafungwa wenzake. Anatumia mgawo huo katika kueneza ujumbe wa Ukristo wa kweli.
Wengi wa wale wanaokuwa Mashahidi wa Yehova sasa katika Iwahig wamefikiwa kwa mahubiri yanayofanywa katika koloni hilo. Mmoja wao alipewa trakiti iliyokuwa na kichwa Je! Ni Aya Haya Tu katika Maisha? (katika Kiingereza). Alishangaa kuona kwamba Mashahidi wa Yehova wanafanya kazi katika gereza hilo, alikubali kujifunza Biblia akitumia kitabu cha kusaidia kujifunza Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Kwa kuitikia mambo aliyokuwa akijifunza, mwanamume huyo alibadilisha maisha yake polepole mpaka akastahili kubatizwa awe Mkristo.
Mahubiri ya nyumba kwa nyumba (au chumba kwa chumba) hasa hayaruhusiwi katika koloni hilo. Walakini, mara mbili kila juma wafungwa wanahesabiwa, na katika vipindi hivi wote wanakusanyika pamoja ili wakaguliwe waonekane kwamba hakuna anayekosekana. Huu ndio wakati unaotumiwa na Mashahidi kuwahubiri wafungwa wenzao. Mafunzo ya Biblia yanaongozwa chini ya miti au katika sehemu wanamokaa watazamaji wa michezo katika uwanja.
Vilevile, katika siku ya Jumapili wazee Wakristo kutoka Kundi la Puerto Princesa wanaruhusiwa kuongoza funzo la Biblia ndani ya gereza hilo, wakitumia gazeti la Mnara wa Mlinzi. Wenye kupendezwa wanaalikwa wahudhurie. Katika nyakati zilizopita mikutano hii ilikuwa ikifanyiwa katika maktaba ya gereza hilo, walakini, kwa kuthamini sana kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova, wasimamizi wa gereza hilo wamepanga sasa Jumba la Ufalme kubwa lijengwe na gharama zote zilipiwe na koloni hilo.
Hivi karibuni wenye mamlaka wamekuwa wakiruhusu kolonos wengine wahudhurie makusanyiko ya mzunguko ya Mashahidi wa Yehova yanayofanywa nje ya gereza hilo. Wazee kutoka makundi yaliyo karibu wanakubali kuwa na daraka juu ya wafungwa hawa, nao wanakuwa na mlinzi mmoja tu asiyekuwa na silaha. Wanavalia mavazi ya kiraia wala hawatiwi pingu mikononi. Katika kila mojawapo la makusanyiko matatu ya mzunguko yaliyokwisha, wengine wa wanaume hawa walibatizwa. Katika mwezi wa Mei, 1977 wawili kati ya 12 waliohudhuria walizamishwa. Wale Mashahidi wengine katika makusanyiko haya sikuzote wanafurahia kushirikiana na ndugu zao Wakristo kutoka Iwahig.
KUTENGENEZWA KWA TABIA KUNALETA MATOKEO
Utendaji wa Mashahidi wa Yehova umekuwa na matokeo ya kuwageuza kabisa wahalifu fulani waliokuwa wabaya sana wawe na tabia njema. Ijapokuwa kweli kwamba mara nyingi watu hurudia maisha yao ya uhalifu wanapotoka gerezani, wengi wa hawa wamegeuka kabisa. Kwa kutumia maneno ya mtume Paulo, ‘wameoshwa’ wakawa safi.—1 Kor. 6:11.
Kudumu kwa mageuzo haya kunaonekana katika yaliyoonwa na mwanamume mmoja ambaye baada ya kutumikia kifungo cha miaka 15 kwa kuwa mwuaji, alifunguliwa akawa painia, kama Mashahidi wa Yehova wanavyowaita wahubiri wa wakati wote. Wengine waliofunguliwa wamefanya maendeleo hata wakawa wazee wanaoheshimiwa katika kundi la Kikristo wanaloshirikiana nalo.
Mradi hasa wa Koloni la Adhabu la Iwahig ni ‘kuwageuza’ wafungwa, sio ‘kuwaadhibu.’ Kwa hiyo, jamii ya wasimamizi inafurahishwa sana na mabadiliko wanayoona katika wafungwa ambao wamekuwa Mashahidi wa Yehova. Msimamizi mmoja alipaza sauti hivi: “Laiti wafungwa wote hapa wangekuwa Mashahidi wa Yehova!”
Makamu wa Afisa wa Ulinzi katika koloni hili alisema hivi: “Nataka dini hii ipate wafuasi wengi hapa, kwa sababu nimeona kwamba mara tu wanapokuwa Mashahidi wa Yehova naona mambo mengi mema katika mazoea na tabia zao.
“Huyo mshiriki wenu, Sanchez, alikuwa mtoa-matata namba moja hapa—mlevi, mvuta tumbako sana, alijaa kila namna ya ubaya. Alinisumbua sikuzote. Vile alivyoweza kugeuka sijui. Ninalojua ni kwamba alipata kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova ikawa hivyo!”
SABABU GANI WANAGEUKA
Ni kitu gani kinachowageuza wauaji, wenye kulala na wanawake kwa nguvu, wenye kuteketeza mali za wengine makusudi na wauaji wa siri wa kuajiliwa, wakawa Wakristo wenye kuishi maisha mema? Kulingana na maneno ya wanaume hawa wenyewe, ni nguvu yenye kugeuza ya Neno la Mungu pamoja na mashirika mema ya watu wanaomwogopa Mungu. Mmoja alisema kwamba alivutwa na ahadi ya Biblia ya uzima wa milele, na kwamba Mungu angefuta kila chozi katika macho ya wanadamu wanaotaabika, na kuondoa magonjwa na mauti. (Yohana 5:24; Ufu. 21:4) Kwa kuwa alikuwa ameona mambo mengi mabaya katika maisha, ahadi hizi zilivuta moyo wake.
Mwingine alisema kwamba upendo wa kidugu wa Ukristo wa kweli umo kati ya wafungwa ambao wamekuwa mashahidi wa Yehova, nao ndio uliomvuta. Sasa anasema kwamba anataka ajitahidi awe “mtumishi mwema wa Yehova Mungu.”
Wengine walisema kwamba waliposhirikiana na Mashahidi wa Yehova, ndipo kwa mara ya kwanza katika maisha zao zote walipotendewa kama watu wema. Uhakika wa upendo huu unaonekana kwa habari ya mfungwa mmoja katika wakati alipokuwa akifunguliwa. Alisema kwamba “macho yake yalijaa machozi” kwa sababu alilazimika kuachana na ndugu zake wapendwa Wakristo.
Kwa hiyo, hata katika gereza, nguvu za Biblia za kuponya mioyo na kugeuza watu zinaonyeshwa. Wanapopata nuru ya Neno la Mungu, wanaume hawa, waliokuwa wamefungwa kwa sababu ya makosa waliyofanya hapo zamani, wanapata uhuru wa kweli aliouahidi Yesu aliposema: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:32) Wanashukuru sana fadhili zisizostahilika za Mungu wao, Yehova, aliyewaruhusu kupata uhuru wa kweli na kutengenezwa upya milele hata wanapokuwa gerezani. Utafurahia kusoma haya yaliyoonwa yanayotolewa na mmoja wa wanaume hawa.
[Maelezo ya Chini]
a Unaweza kusoma aliyoyaona Domingo Obispo kama anavyoyaeleza kuanzia ukurasa 6 katika gazeti hili.