Amani na Usalama
Itakuja wakati gani?
Kutoka chanzo gani?
Itamaanisha nini kwa wanadamu?
“[Mungu] avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari ya [vita].”—Zab. 46:9.
LIKITAJA juu ya mambo yanayotazamiwa katika mwaka 1978 gazeti la kila juma liitwalo U.S. News & World Report lilisema katika toleo lake la Desemba 26, 1977, kwamba huu unapaswa kuwa “Mwaka wa Mageuzo.” Mwandikaji aliendelea kusema: ‘Maamuzi makubwa yanapaswa yafanywe juu ya mawazo yanayoongezeka ya matumaini mema kwa wakati ujao. Taabu? Ni nyingi. Lakini kuna wakati ujao wa amani na ufanisi.’ Kwa maneno hayo, gazeti hilo lilionyesha tumaini la watu milioni nyingi kwamba amani na usalama huenda zitapatikana karibuni.
Katika sehemu nyingi za dunia watu wanalia “Amani, Amani.” Lakini je! tunaweza kusema kwa kweli na kutumaini kabisa kwamba amani ya ulimwengu inaonekana leo? Au, pahali pake, je! hali si kama ilivyokuwa katika Israeli katika siku za nabii Yeremia? Hali ya ulimwengu ilikuwa yenye hatari wakati huo. Kwa sababu jeshi lenye nguvu sana la Babeli lilikuwa likisonga mbele katika shughuli (kazi) yake ya kuutiisha ulimwengu. Watu walikuwa wakitafuta kwa juhudi sana tumaini fulani la amani. Ingawaje nabii huyo alisema kwamba walikuwa “wakisema, Amani, Amani; wala hapana amani.”—Yer. 8:11.
MSINGI GANI WA AMANI?
Ikiwa ungepanga kujenga nyumba mpya, ungeijenga wapi? Je! ungechagua mtaa ulio na sifa mbaya kwa sababu ya uvunjaji wake wa sheria? Je! ungeijenga katika sehemu ambayo watu wanapigana kwa sababu ya tofauti za kabila, dini na jamii? Je! ungeenda kuishi katika sehemu ambayo watu wake hawaaminiki, wanachukiana na wanajaa jeuri ya kila namna? Zaidi ya hayo, unapojenga nyumba yako je! ungejaribu kuiwekea msingi wake kila namna ya makombora yenye kulipuka sana ili iwe “salama”? Bila shaka huwezi kuweka mipango ya nyumba kama hiyo!
Walakini, ulimwengu wa leo umejengwa kwa namna hiyo! Tangu vita ya kwanza iliyoenea pote ilipotokea mwaka 1914, hali ya ulimwengu imekuwa yenye jeuri inayozidi kuongezeka. Watu wengi wa dunia wamepatwa na chuki ya kitaifa, kikablia na ya kidini. Hata hivyo viongozi wa kisiasa wanadai kwamba wanaweza kuleta amani katika ujirani huu wa ulimwengu. Huenda wengine wakawa wanyofu katika madai yao. Lakini je! kweli wanaweza?
Wao wanajenga juu ya msingi wa namna gani? Je! ni msingi imara wa kutumainiana na kupendana? Au, pahali pake, ni msingi dhaifu wa woga na chuki? Kwa halisi, msingi ambao juu yake mamlaka za ulimwengu zinajenga ni wenye kulipuka. Wakati wa mwaka 1976 mataifa ya dunia yalitumia shilingi bilioni 2,364 (Z261 bilioni) kwa silaha, na katika mwaka 1977 hesabu hiyo ikafika shilingi bilioni 3,152 (Z348 bilioni). Mashindano ya kujiwekea silaha haizuiliki. Huu ni msingi wa namna gani wa kujengea amani na usalama wa ulimwengu? Tunaweza kusema tu kwamba hakuna tumaini na haiwezekani.
Nabii Danieli alisema juu ya izi hizi siku zetu alipokuwa akitabiri juu ya upeo wa mashindano ya karne nyingi kati ya “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini.” Leo wafalme hawa wawili wanafahamika kuwa pande mbili zinazoshindana za mataifa ya Kikomunisti na mataifa ya Kibepari yanayoshindania utawala wa ulimwengu. Yanaendelea na ujanja ule ule wa zamani: “Na katika habari za wafalme hao wawili; mioyo yao watanuia kutenda madhara, nao watasema uongo pamoja mezani; lakini hilo halitafanikiwa.” (Dan. 11:27) Wazidivyo kusema kwa sauti kubwa zaidi juu ya “amani na salama,” ndivyo mradi huu unaotamanika sana uzidivyo kuwa mbali nao. Nyumba ya amani ya kweli haiwezi kujengwa juu ya msingi wa kutotumainiana na wa mashindano ya kujiwekea silaha—msingi ulioimarishwa kwa silaha nyingi za atomiki na za namna nyingine. Haiwezi kujengwa hata kidogo katika hali ya chuki ya mataifa, uvunjaji wa sheria na jeuri.
“KAMA VILE MWIVI AJAVYO USIKU”
Hata hivyo, mataifa wanaendelea kusema juu ya “amani na salama.” Kwa kufanya hivyo mataifa wanatafuta jambo wasiloweza kulipata. Kwa maana Biblia inatabiri nini juu ya jitihada zao? Mtume Paulo anatuambia hivi: “Siku ya [Yehova] yaja kama vile mwivi ajavyo usiku. Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.” (1 The. 5:2, 3) Tayari mlio wa amani na usalama unaendelea kuongezeka. Na inaweza kutazamiwa kwamba, wakati mataifa watakapokuwa wakitoa sauti kubwa ya “amani na salama,” ndipo kwa ghafula “siku ya [Yehova]” itawafyatukia ikiwa na hasira yake yote. Itakuja kama vile mwivi afikavyo usiku bila kutazamiwa. Kama vile utungu mkali wa ghafula wa kuzaa mtoto, siku ya kufanya hesabu itawafikia mataifa ya dunia, nayo hukumu ya kimungu itatekelezwa juu yao.—Sef. 3:8.
Huu hautakuwa uharibifu usiozuilika, kama kwamba vita ya makombora ya atomiki itakayoharibu kabisa maendeleo yote katika dunia. Pahali pake, utakuwa ni uharibifu unaozuilika, unaochagua, ukiletwa na Mwenyezi Mungu juu ya “wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu.” (2 The. 1:8) Wapendao amani na usalama kweli kweli wanaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ataendelea kuwa kwao “kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.”—Zab. 46:1-7.
Matukio yenye kushtua yataonekana duniani wakati “dhiki kubwa” itakapokuwa ikiendelea. (Mt. 24:21) Italeta matokeo ambayo hayajapata kuletwa na mikutano ya mazungumzo ya kupunguza silaha—kumalizwa kabisa kwa silaha za mataifa. Tunakaribishwa tutazame kimbele mambo haya yatakayotetemesha ulimwengu: “Njoni [enyi watu] myatazame matendo ya [Yehova], jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. Avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari [ya vita].”—Zab. 46:8-9
Kuna kusudi la kitendo hiki cha kukata maneno cha Mwenyezi Mungu, Yehova. Kwa karne nyingi mataifa wameonyesha na wanaendelea kuonyesha kwamba hawawezi kuletea watu wa dunia amani thabiti (imara) na usalama. Wamepewa kila nafasi nao wamejaribu kila namna ya serikali. Walakini, wote wamejenga nyumba zao juu ya msingi usiofaa. Katika kushindana, sasa wanaendelea kuongeza silaha zao za atomiki pamoja na silaha nyingine zaidi na zaidi, wakishindana wao kwa wao huku wakijaribu kuweka usawa wa nguvu za silaha. Si ajabu kwamba Mwenyezi Mungu, Yehova, anakusudia kuuangamiza mpango kama huo usio na usalama na wenye kuleta maafa.
MSINGI WA AMANI YENYE KUENEA POTE
Walakini, Mwenyezi Mungu hataangamiza mataifa tu, pamoja na silaha zao, bali vilevile ataleta amani itakayoenea ulimwenguni pote. Nayo taratibu hii mpya itajengwa juu ya msingi gani? Kwa upande mmoja, kutakuwa na upendo na kutumainiana kati ya wanadamu wote. Wale watakaostahili kuishi katika hiyo taratibu mpya watakuwa watu wanaofuata amri mbili zilizo kuu kupita zote kama alivyonyesha Yesu Kristo: “Mpende [Yehova] Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote, na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako.” (Luka 10:27) Wao watakuwa wamekwisha sitawisha “tunda la roho,” ambalo ni “upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” Watakuwa wamekwisha “[vaa] utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.” (Gal. 5:22, 23, NW; Efe. 4:24) Watu waliojipatia sifa hizi na ambao wamejiweka wakf katika utumishi wa Mungu ndio watakaokuwa msingi wa taratibu mpya ya Mungu. Ufalme wake chini ya Kristo Yesu utafanikiwa sana wakati watu hao kutoka katika kila taifa, kabila na cheo watakapoungana katika jamii moja ulimwenguni pote yenye amani na usalama. Na kwa halisi watu mamilioni milioni wataingizwa katika jamii hiyo yenye furaha kupitia kwa ufufuo wa wafu.—Yohana 5:28, 29.
Bado kuna kusudi jingine, kusudi la maana sana la kuharibiwa kwa msingi wa uongo wa amani na usalama na kujengwa kwa msingi wa kweli na Mungu. Kusudi hilo ni kwamba enzi kuu ya Mungu wa kweli, Yehova, ipate kutukuzwa katika ulimwengu wote. Kwa sababu hiyo Yehova anatoa karibisho katika Zaburi 46:10 hivi: “Acheni, mjue ya kuwa Mimi ni Mungu, nitakuzwa katika mataifa, nitakuzwa katika nchi.” Wakati wanadamu wote wanapomtii Yehova Mungu kama Bwana Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote ndipo amani itakapoenea ulimwenguni pote. Wanapongojea wakati huo mzuri sana, wapendao amani ya kweli wanaweza kufurahia ulinzi wanaohakikishiwa na Yehova: “[Yehova] wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.” (Zab. 46:11) Kwa hiyo, mataifa wanapojenga misingi yenye kulipuka kwa amani na usalama usio thabiti, wote wanaotii onyo la Neno la Mungu, Biblia, wanaweza kusonga mbele kuelekea kwenye amani ya kweli na usalama unaohakikishwa na ufalme wa Mungu peke yake kupitia kwa Kristo Yesu.—Mt. 6:10.