Ushuhuda Mpya Wenye Kushangaza Watokea!
ALIKUWA wakihatarisha maisha zao walipokuwa wakitelemka genge waingie katika kile ambacho sasa kinajulikana kama Pango la Kuogofya. Hawakutarajia hata kidogo kwamba katikati ya mifupa ya watu wangepata jambo la maana sana linalohusu Biblia yako.
Ili ufahamu ilivyokuwa, wazia kwamba uko katika jangwa kavu sana, linaloonyeshwa katika ukurasa wa 10, milima iliyoko magharibi mwa Bahari ya Chumvi.
Katika upande wa kusini iko ngome ya Masada iliyo peke yake, ambapo, kituo cha mwisho kilichosalia cha Wayahudi wenye kuasi kilishindwa na Warumi katika mwaka 73 W.K. Katika upande wa kaskazini kunayo magofu ya Qumran. Hapa ndipo palipokuwa makao ya jamii ya Kiyahudi ambayo ilificha Kitabu cha Kukunja cha Bahari ya Chumvi cha Isaya kinachojulikana sana pamoja na maandishi mengine katika pango zilizokuwa karibu.
Mapema katika mwaka 1961, kikundi cha wataalamu kilisafiri kwenda kufanya uvumbuzi katika mapango yenye kuogofya katika mahali paitwapo Nahal Hever. Walikuwa na vyombo kama vile vya kugundua baruti, vya kujikinga na vumbi, kamba na miavuli kama inayotumiwa kuruka kutoka katika ndege. Ulikuwa mruko wenye hatari wa futi 260 (metres 80) mpaka kwenye mlango wa pango la namba 8, lililoitwa baadaye Pango la Kuogofya. Kukosea kidogo kungemaanisha kuanguka umbali wa futi (metres) nyingi kwenye miamba iliyokuwa chini.
Jina lenye kuogofya, Pango la Kuogofya, lilitokana na yale yaliyopatikana ndani na wavumbuzi—mifupa ya wanaume 40, wanawake na watoto. Walikuwa wafuasi wa Myahudi mpiga vita Bar Kokba, aliyeongoza vita kupigana na Rumi katika mwaka 132 W.K. Inasemekana kwamba huenda walinaswa humo wakafa njaa au kwa kukosa maji kwa kuwaogopa askari wa Kirumi waliokuwa wamepiga kambi juu ya genge hilo.
Lakini huenda ukashangaa na kuuliza, haya yote yanapatanaje na habari ya kama Yesu na mitume wake walitumia jina la Mungu la pekee, na, kwa kuongezea, kama limo ndani ya Biblia yako au midomoni mwako. Kinachounganisha haya kinapatikana katika vipande vidogo 9 vya hati ya ngozi za wanyama, vilivyokuwa na maandishi ya Kigiriki, vilivyochimbuliwa katika Pango la Kuogofya.
Wanachuo walipovichunguza kwa uangalifu sana, walifahamu kwamba vipande hivyo vilitokana na kitabu cha kukunja cha ngozi za wanyama cha wale Manabii Kumi na Wawili (Hosea mpaka Malaki). Yalikuwa maandishi ya awali ya Kigiriki yenye tarehe ya kati ya mwaka 50 K.W.K. na mwaka 50 W.K. Sasa, chanzo cha kitabu hicho cha kukunja kilikuwa kimejulikana, Pango la Kuogofya katika jangwa la Uyahudi. Hata ingawa huenda kwanza usione maana ya jambo hili, ni jambo la maana sana la kujulisha kama jina la Mungu linapaswa kuwa katika Biblia yako.
Ili jambo hili liwe na maana ya kweli kwako, tunahitaji kujua ni vitabu gani vya kukunja vilivyotumiwa na Yesu na mitume wake katika karne ya kwanza W.K.
NENO LA MUNGU KATIKA KIGIRIKI
Vitabu vya Biblia kuanzia na Mwanzo mpaka Malaki viliandikwa kwanza katika Kiebrania, kukiwa na sehemu ndogo zilizoandikwa katika Kiaramu. Walakini, Wayahudi walipotawanyika katika ulimwengu wa kale, walianza kutumia lugha iliyokuwa ikitumiwa na mataifa yote, yaani, Kigiriki. Kwa hiyo, wakati fulani karibu na mwaka 280 K.W.K., Maandiko ya Kiebrania yalianza kutafsiriwa katika Kigiriki, kukawa na kile kinachojulikana kama Greek Septuagint Version (LXX).
Wakati Yesu alipokuwa akianza huduma yake, tafsiri hii ilikuwa ikitumiwa katika sehemu nyingi na Wayahudi waliokuwa wakisema Kigiriki. Kutokana na maneno waliyoyatumia mitume kuandika tunafahamu kwamba walifahamiana na tafsiri ya Septuagint, na bila shaka naye Yesu vilevile.
Lakini je! tafsiri hiyo ya Kigiriki ilikuwa na jina la Mungu? Hati zilizo kamili zaidi za Septuagint ambazo zimesalia, ambazo tarehe zake ni kuanzia karne ya nne W.K., zinafunua hali yenye kushangaza. Mahali po pote palipokuwa na zile herufi nne (Tetragrammaton) katika Biblia ya Kiebrania, Septuagint ya Kigiriki iliweka maneno “Mungu” (Theos) na “Bwana” (Kyrios). Kwa hiyo, maoni ya wanachuo ni kwamba Yesu na mitume wake hawakutumia jina la pekee la Mungu. Imedaiwa kwamba, walipokuwa wakisoma au kutaja kutokana na Maandiko ya Kiebrania, walifuata desturi ya kutamka mahali pake maneno “Bwana” au “Mungu.” Na kwa habari ya nakala ya Septuagint waliyoitumia, hata haikuwa na Jina hilo.
Wanachuo wengi wa kidini wameshikilia maoni hayo kwa uthabiti. Lakini namna gani juu ya jambo lile lililopatikana katika Pango la Kuogofya?
JAMBO LA KUJULISHA KUTOKA UYAHUDI
Kumbuka kwamba Pango la Kuogofya, katika jangwa la Uyahudi lilikuwa na vipande vya ngozi za wanyama vya Manabii Kumi na Wawili, kutoka katika kitabu cha kukunja kilichokuwa kimeandikwa karibu na wakati wa kuzaliwa kwa Yesu. Vilikuwa vimeandikwa katika Kigiriki, vikiwa namna ya Septuagint. Lakini namna gani juu ya jina la Mungu. Ebu angalia picha ya vipande hivyo inayoonyeshwa hapa.
Vipande hivi kutoka katika jangwa la Uyahudi vilikuwa na jina la Mungu katika namna ya Kiebrania cha kale! Hata ingawa maandishi yenyewe yalikuwa katika lugha ya Kigiriki, jina la Mungu likiwa katika herufi za Kiebrania liliendelea kutumiwa. Jina la cheo la Kigiriki Kyrios halikutumiwa mahali pa zile herufi nne (Tetragrammaton), kama ilivyokuwa katika hati za Septuagint za karne zilizofuata.
Tena, hata nyakati za karibuni zaidi, jambo jingine lenye kujulisha la maana zaidi limekuwa likiangaliwa. Nalo vilevile, lina maana sana katika kujulisha kama jina la Mungu linapaswa kuwa katika Biblia yako, na kwa hiyo, kama unapaswa kuwa ukilitumia. Jambo hili lenye kujulisha lilitokea katika Cairo.
JAMBO LA KUJULISHA KUTOKA MISRI
Jambo hilo lenye kujulisha linapatikana katika vipande vya kitabu cha kale cha kukunja cha Kumbukumbu la Torati kilichoandikwa kwa mafunjo, vikiwa na orodha ya nyumba ya kuhifadhi vitu (museum) Fouad Papyri Namba 266. Ingawa vipande hivi vilikuwa vimepatikana katika miaka ya kuanzia na wa 1940, havikupatikana kwa wanachuo ili wavichunguze.
Katika mwaka 1950 tafsiri ya Kiingereza ya New World Translation of the Christian Greek Scriptures kwa mara ya kwanza ilichapa picha za vipande hivi visivyopatikana kwa urahisi. Hata hivyo, muda wote wa kuanzia na mwaka 1950 na hata wa kuanzia na wa 1960 wataalamu wengi hawakuweza kuvipata vipande hivi vyenyewe, wala hakuna kitabu kingine cha uchunguzi kilichokuwa kimechapa picha zake au kuvichunguza vyote. Mwishowe, sehemu ya mwaka wa 1971 ya kitabu Etudes de Papyrologie ilifanya hivyo. Lakini ni jambo gani lililokuwa la pekee sana juu ya vipande hivi? Na vinahusianaje na matumizi ya jina la Mungu?
Vile vya Fouad papyri 266 vilitayarishwa katika karne ya kwanza K.W.K. Haviko katika Kiebrania bali katika Kigiriki. Ebu tazama maandishi ya mfano wa Fouad 266 uliotolewa hapo chini. Je! wewe unaona kwamba, hata ingawa maandishi yenyewe yameandikwa katika Kigiriki, zile herufi nne (Tetragrammaton) katika herufi za mraba katika Kiebrania zimetumiwa? Kwa hiyo, mwandishi aliyeandika kitabu hiki cha kukunja cha mafunjo vilevile hakubadilisha maneno ya Kigiriki ya “Bwana” (Kyrios) au “Mungu.” Mahali pake, zaidi ya mara 30 aliweka—katikati ya maandishi ya Kigiriki—zile herufi nne (Tetragrammaton) katika herufi za Kiebrania!
Dakt. Paul E. Kahle wa Oxford alieleza kwamba vipande hivi “labda [vinayo] maandishi yaliyo kamili zaidi ya Septuagint ya Kumbukumbu la Torati ambayo yametufikia.” Na katika Studia Patristika, aliongeza hivi, “Tunayo hapa maandishi ya Kigiriki katika kitabu cha kukunja cha mafunjo ambayo yanaonyesha maandishi ya awali ya Septuagint katika njia inayotegemeka zaidi kuliko hati ya Codex Vaticanus na yaliyoandikwa zaidi ya miaka 400 mbele.” Na yaliendelea kutumia jina la Mungu la pekee, kama vilivyofanya vipande vya Kigiriki vya Manabii Kumi na Wawili kutoka jangwa la Uyahudi. Yote hayo yalipatana.
Katika Journal of Biblical Literature (Vol. 79, kur. 111-118), Dakt. Kahle alichunguza ushuhuda unaoendelea kuongezeka juu ya matumizi ya jina la Mungu kati ya Wayahudi akafanya uamuzi huu:
“Tafsiri zote za Biblia zilizotafsiriwa na Wayahudi kwa ajili ya Wayahudi, katika nyakati zilizotangulia Ukristo bila shaka zilitumia zile herufi nne za Kiebrania kama jina la Mungu, wala si [Kyrios], au kifupi chake, kama klnachopatikana katika [nakala za] Kikristo za Septuagint.”
Kuchaguliwa huku kwa jina la Mungu ili lihifadhiwe kwa uangalifu, kulionyeshwa hata katika maandishi ya lugha ya Kiebrania tangu karibu na karne ya kwanza. Katika nyingine za vitabu vya kukunja vya Kiebrania vilivyopatikana kutoka katika mapango yaliyo karibu na Bahari ya Chumvi, zile herufi nne (Tetragrammaton) ziliandikwa katika wino mwekundu au katika namna ya Kiebrania cha kale iliyoonekana kwa urahisi. J. P. Siegel alitoa maelezo juu ya hili hivi:
“Wakati hati za Qumran zilipovumbuliwa mara ya kwanza zaidi ya miaka 20 iliyopita jambo moja lililoshangaza juu yake, lilikuwa kupatikana kwa zile herufi nne, katika visehemu vichache vya maandiko, zikiwa zimeandikwa kwa herufi za Kiebrania cha kale . . . . Kwamba desturi hii inaonyesha heshima kubwa katika (ma) Jina la Mungu ni jambo la hakika.”—Hebrew Union College Annual, 1971.
Zaidi ya hayo, imeripotiwa kwamba katika Yerusalemu wa karne ya kwanza kulikuwako kitabu cha kukunja cha Kiebrania cha vile vitabu vitano vya Musa vikiwa na zile herufi nne (Tetragrammaton) zimeandikwa kwa dhahabu.—Israel Exploration Journal, Vol. 22, 1972, kur. 39-43.
Je! ushuhuda huu mpya haukuonyeshi kwa nguvu sana kwamba Yesu alifahamiana sana na alitumia jina la Mungu, awe alisoma Maandiko katika Kigiriki au Kiebrania?
[Picha katika ukurasa wa 7]
Vipande vya maandishi ya Bahari ya Chumvi katika Kigiriki, vikiwa na zile herufi nne (Tetragrammaton) katika Kiebrania (Hab. 2:15-20; 3:9-14)
[Picha katika ukurasa wa 8]
Herufi nne (Tetragrammaton katika vipande vya Septuagint kutoka Misri (Fouad Papyri 266)