Jambo Jipya Juu ya Jina la Mungu?
KATIKA kurasa zilizotangulia tumechunguza ushuhuda mpya wenye kushangaza juu ya matumizi ya jina la Mungu katika wakati Yesu na mitume wake walipokuwa duniani.
Je! wewe unaona uamuzi unaoonyeshwa na ushuhuda huu? Unahusianaje na yale unayopaswa kuona katika Biblia yako na namna unavyopaswa kuliona jina la Mungu? Ebu angalia uamuzi uliofikiwa na mtaalamu mmoja anayejulikana sana aliyechunguza ushuhuda wa hati:
Karibu mwaka mmoja hivi uliopita, Mtaalamu wa dini katika Chuo Kikuu cha Georgia (U.S.A.), alipambana na maulizo makubwa yanayopatikana katika Journal of Biblical Literature. (Vol. 96, Na. 1, 1977 kur. 63-83) Makala yake inaanza hivi:
“Uvumbuzi wa hivi karibuni katika Misri na katika Jangwa la Uyahudi unatusaidia tuone namna jina la Mungu lilivyotumiwa kweli kweli katika nyakati zilizotangulia Ukristo.”
Ndipo alipozungumza juu ya maandishi ya awali ya Kigiriki ya nyakati zilizotangulia Ukristo ambayo umeona picha zake katika kurasa zilizotangulia. Juu ya maoni yaliyokubaliwa hapo mbele kwamba katika Septuagint jina la cheo la Kigiriki Kyrios lilitumiwa sikuzote mahali pa jina la Mungu, tunasoma hivi:
“Kutokana na uvumbuzi huu sasa tunaweza kusema tukiwa na uhakika karibu wote kwamba jina la Mungu, יהוה, halikuandikwa [Kyrios] katika Biblia ya Kigiriki katika nyakati zilizotangulia Ukristo, mara nyingi sana kama ilivyodhaniwa.”
Namna gani juu ya vitabu vyote vya kukunja vya Bahari ya Chumvi? Mtaalamu Howard anaandika hivi:
“Labda jambo la maana sana tunaloweza kuona kutokana na mfano huu wa matumizi yanayotofautiana ya jina la Mungu ni kwamba [zile herufi nne] Tetragram zilionwa kuwa takatifu sana. . . . Katika kunakili maandishi ya Biblia yenyewe ya awali [zile herufi nne] Tetragram zililindwa sana. Kulindwa huku kwa [zile herufi nne] Tetragram kuliendelezwa hata katika tafsiri ya Kigiriki ya maandishi ya awali ya Biblia.”
LAKINI NAMNA GANI JUU YA YESU NA WANAFUNZI WAKE?
Ingawa huenda haya yote yaliyotangulia kusemwa yakawa na maana ya pekee kwa wanachuo, yanahusianaje na Biblia yako? Wewe unapaswa kuwa na maoni gani juu ya matumizi ya jina la pekee la Mungu?
Mtaalamu Howard anafanya uamuzi wa maana sana. Kwanza, anasema hivi:
“Tunajua kwa hakika kwamba Wayahudi waliokuwa wakisema Kigiriki waliendelea kuandika יהוה katika Maandiko yao ya Kigiriki. Kuongezea hayo, haielekei sana kwamba Wakristo wa kwanza wenye kusema Kigiriki waliopenda kuhifadhi desturi hiyo waliacha kuitumia. . . . Lingekuwa jambo lisilo la kawaida kabisa kuacha kutumia [zile herufi nne] Tetragram katika maandishi ya Biblia yenyewe.”
Waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo walifanya nini walipokuwa wakitumia maneno kutoka katika vitabu vya Biblia ya Kiebrania, ama kutoka Kiebrania cha asili au kutoka katika tafsiri ya Kigiriki? Je! walitumia zile herufi nne (Tetragrammaton) zilipopatikana katika habari waliyokuwa wakitumia maneno yake? Kwa kutumia msingi wa ushuhuda unaopatikana sasa, Mtaalamu Howard anaeleza hivi:
“Kwa kuwa [zile herufi nne] Tetragram bado zilikuwa zimeandikwa katika nakala za Biblia ya Kigiriki ambazo ndizo zilizokuwa Maandiko ya kanisa la kwanza, ni jambo la akili kuamini kwamba waandikaji wa [Agano Jipya], walihifadhi [zile herufi nne] Tetragram katika maandishi ya Biblia. Kulingana na desturi ya Wayahudi wa nyakati zilizotangulia Ukristo tunaweza kufikiri kwamba maandishi ya [Agano Jipya] yalitia [zile herufi nne] Tetragram katika maandiko yaliyotumiwa kutoka [Agano la Kale].”
Kwa sababu gani, basi, zile herufi nne (Tetragrammaton) hazimo katika nakala zote zilizopo sasa za “Agano Jipya”? Je! inawezekana kwamba jina la Mungu liliondolewa baada ya mitume kufa? Hivyo ndivyo ushuhuda unavyoonyesha. Mtaalamu Howard anaendelea kusema hivi:
“[Zile herufi nne] Tetragram katika maneno yaliyotumiwa [kutoka Agano la Kale], bila shaka, zingeendelea kuwako maadamu zilipoendelea kutumiwa katika nakala za Kikristo za LXX [tafsiri ya Kigiriki]. Walakini zilipoondolewa katika [Agano la Kale] la Kigiriki, vilevile ziliondolewa katika maneno ya [Agano la Kale] yaliyokuwa yametumiwa katika [Agano Jipya].”
“Hivyo wakati fulani karibu na mwanzo wa karne ya pili matumizi ya majina mengine mahali pa jina la Mungu ni lazima yawe yaliondoa [zile herufi nne] Tetragram katika Maagano yote mawili. Baada ya muda mfupi jina la Mungu lilisahauliwa kabisa katika kanisa la watu wa Mataifa isipokuwa kama lilivyokuwa likionyeshwa katika majina hayo mengine yaliyowekwa mahali pa jina la Mungu au mara kwa mara likakumbukwa na wanachuo.” (Ni sisi tumelaza maneno hayo)
HILO NI JIPYA! AU JE! NI JIPYA?
Wanachuo wengi ambao wamesoma Journal of Biblical Literature huenda walishangazwa na uamuzi uliofikiwa, yaani, kwamba jina la Mungu, Yehova (Yahweh) lilikuwako katika “Agano Jipya” lilipoandikwa hapo kwanza. Huenda ilionekana kuwa habari mpya, kwa kuwa inageuza maoni ambayo yamekuwa yakishikiliwa kwa muda mrefu kwamba waandikaji Wakristo waliepuke kutumia jina la Mungu. Lakini je! habari hii ni mpya?
Huko nyuma katika mwaka 1796 Dominikus von Brentano alitumia jina la Mungu katika mahali mbalimbali katika tafsiri yake ya Kijeremani ya “Agano Jipya.” Kwa mfano, ebu fikiria Marko 12:29, ambalo unaona limenakiliwa hapo juu. Yesu alikuwa ameulizwa, “Ni amri gani iliyo ya kwanza?” Tafsiri ya Brentano inasomwa hivi: “Amri iliyo ya kwanza, akajibu Yesu, ni hii: Sikiliza Israeli! Yehova, Mungu wetu, ndiye Mungu peke yake.”
29. Das allervornehmste Gebot, antwortete Jesus, ist dieß: Höre Israel! Jehovah, unser Gott, ist der einige Gott◊).
Je! Brentano alikuwa na sababu nzuri ya kuonyesha kwamba Yesu alitamka jina la Mungu? Ndiyo, kwa sababu Yesu alikuwa akitumia maneno katika Kumbukumbu la Torati 6:4, ambalo lina zile herufi nne (Tetragrammaton). Bila shaka Yesu hakuwa akifuata desturi kama walivyokuwa wakifanya viongozi wa kidini Wayahudi, kwa kuwa Yesu ‘alikuwa akifundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi.’ (Mt. 7:29) Yesu alisema hadharani kwamba alitamani kutukuza jina la Babaye, jina lake halisi pamoja na makusudi yaliyoshirikishwa na jina hilo. (Yohana 12:28) Na karibu na mwisho wa maisha yake ya kidunia yeye alisema kwamba alikuwa amelijulisha jina la Babaye. Kwa hiyo mfasiri Brentano alikuwa na msingi unaopatana na akili nzuri wa kuonyesha Yesu akitumia jina la Mungu alipotumia maneno yaliyokuwa nalo.—Yohana 17:6, 26.
Vivyo hivyo, habari ya Injili ya Mathayo peke yake ina mitajo 100 ya maneno yaliyotumiwa kutoka katika Maandiko ya Kiebrania. Katika mwaka 1950 tafsiri ya Kiingereza ya New World Translation of the Christian Greek Scriptures ilisema hivi juu ya Mathayo: “Mitajo hii ya maneno ilipotia ndani jina la Mungu, yeye angekuwa na wajibu wa kutia ndani kwa uaminifu [zile herufi nne] Tetragrammaton.”
Tafsiri hii katika mwaka wa 1950 ilifikia uamuzi ule ule ulioandikwa baadaye katika Journal of Biblical Literature katika mwaka 1977. Kulingana na ushuhuda wa kwamba waandikaji wa “Agano Jipya” walikutana na zile herufi nne (Tetragrammaton), wawe walitumia maneno kutoka maandishi ya awali ya Kiebrania au kutoka Septuagint ya Kigiriki, dibaji (utangulizi) ya New World Translation ilisema hivi:
“Mfasiri wa kisasa ana haki ya kutumia jina la Mungu mahali pa [maneno ya Kigiriki ya “Bwana” na “Mungu”] katika mahali ambapo Mathayo, n.k., anapotaja mistari, mafungu ya maneno pamoja na maneno kutoka katika Maandiko ya Kiebrania au LXX [tafsiri ya Kigiriki] ambapo jina la Mungu linapatikana.”
Kwa hiyo, maoni yaliyochukuliwa na Mtaalamu Howard katika mwaka 1977 si mapya kabisa. Walakini yanatokeza ushuhuda mzuri mpya ambao haukupatikana wakati New World Translation of the Christian Greek Scriptures ilipotumia jina “Yehova” mara 237 katika “Agano Jipya.”
Bila shaka, basi, jina la Mungu linapaswa kuwako katika tafsiri za Biblia. Ndipo linapopaswa kuwa, litumiwe na lithaminiwe na waabudu wote wa kweli wanaotamani kufanya kama Yesu—kutukuza jina la Babaye—na wanaosali, “Baba yetu uliye mbinguni jina lako litukuzwe.”—Mt. 6:9.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Nahal Hever, kuelekea upande wa mashariki juu ya Bahari ya Chumvi