Kuliunga Mkono Neno la Mungu kwa Ushikamanifu
“Fanya yote yote uwezayo kujiweka mwenyewe mbele za Mungu katika hali ya kukubaliwa, mwanamume mfanya kazi asiye na lo lote la kuaibikia,ukitumia lile neno la ile kweli namna ipasavyo.”—2 Timotheo 2:15, NW
1, 2. Ni njia gani moja ambayo Mashahidi wa Yehova wanatumia ili kuliunga mkono Neno la Mungu kwa ushikamanifu?
“SOMA NENO LA MUNGU BIBLIA TAKATIFU KILA SIKU.” Maneno hayo yameandikwa kwa Kiingereza katika upande mmoja wa jengo kubwa lililoko Brooklyn, New York, karibu na Daraja la Brooklyn linalojulikana sana. Maneno hayo yameandikwa katika jengo la nani, na kwa sababu gani?
2 Yameandikwa kwenye kimoja cha viwanda vya uchapaji wa vitabu kinachoendeshwa na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, Biblia na Trakti, shirika la kidini linalohusiana na Mashahidi wa Yehova. Ishara yenye maneno hayo inafaa sana kutazamiwa iandikwe na Mashahidi wa Yehova kwenye upande wa majengo yao. Kwa sababu gani? Kwa sababu wao wanaamini kwamba mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu alikuwa akisema kweli zamani za kale alipoandika hivi: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.” (Zaburi 119:105) Ishara hiyo ni moja tu ya njia nyingi ambazo sisi Mashahidi tunatumia kuonyesha kwamba tunaliunga mkono Neno la Mungu kwa ushikamanifu.
3. Washikamanifu waliotutangulia waliliunga mkono Neno la Mungu kwa njia gani?
3 Kama vile Biblia yenyewe inavyoonyesha, kuna watu wengi waliotutangulia katika kuwa waunga-mkono washikamanifu wa lile Neno. Yapata miaka 3,500 iliyopita alikuwako Musa. Hakuna shaka kwamba yeye aliliunga mkono Neno la Mungu kwa ushikamanifu. Kwanza yeye aliwapitishia watu Neno la Mungu kwa maneno ya mdomo kisha akawapitishia kwa maneno yaliyoandikwa. Semi hizo za kimungu zinapatikana katika ile Pentateuko (vitabu vitano vya kwanza vya Biblia). Baada ya Yehova Mungu kumtumia nabii huyo mwenye juhudi alitumia watu wengine wengi wakawa wanenaji na makarani wake, na wote walikuwa kama Musa kwa kuliunga mkono Neno la Mungu kwa ushikamanifu. (2 Petro 1:21) Wengine wao walikuwa Samweli, Isaya, Yeremia, Ezekieli na Danieli, na wengine wengi.
Yesu Kristo na Mitume Wake
4. Ni nani aliyewapita waunga-mkono wote wa lile Neno, naye alionyeshaje kwamba aliliunga mkono?
4 Lakini bila shaka lo lote, mwenye kuwapita wote walioliunga mkono Neno la Mungu kwa ushikamanifu hakuwa mwingine ila Mwana mzaliwa wa kwanza wa Yehova Mungu, aliyekuja kuwa ‘mwanadamu Yesu Kristo.’ (Warumi 5:15) Mara nyingi yeye aliliunga mkono Neno la Baba yake kwa ushikamanifu akisema, “Imeandikwa,” kwa mfano alipokuwa akijibu vishawishi vya Shetani na wakati alipokuwa akiwajibu wapinzani wake wa kidini. (Mathayo 4:4, 7,10; 21:13; Yohana 6:45; 8:17) Zaidi ya hilo, kwa kutumikia kwa uaminifu akiwa nabii mkubwa kuliko Musa, alikuwa pia akiliunga mkono Neno la Mungu kwa ushikamanifu. (2 Wakorintho 1:20) Ndiyo, yeye aliihubiri na akaishi kulingana na ile kanuni inayosema “Neno lako [Mungu] ndiyo kweli.”—Yohana 17:17.
5, 6. (a) Petro na Paulo walionyeshaje kwamba waliliunga mkono lile Neno kwa ushikamanifu? (b) Katika habari hii, “mtumwa mwaminifu mwenye akili” alitokezwa kwa kusudi gani? (c) Kwa sababu gani “mtumwa” huyo alifunikwa akafichika kwa muda fulani?
5 Mitume wa Yesu walifuata mfano wake. Siku ya Pentekoste mtume Petro aliliunga mkono Neno la Mungu kwa ushikamanifu kwa kuonyesha kwa mkazo mwingi jinsi Yesu alivyoyatimiza maneno ya Daudi! (Matendo 2:22-36) Tena maandishi ya mtume Paulo yamejawa sana na mitajo ya Maandiko ya Kiebrania, kuonyesha jinsi yeye alivyoshughulikia sana kuliunga mkono Neno la Mungu kwa ushikamanifu. Yeye aliushikilia msimamo wa kusema: “Mungu aonekane kuwa [wa kweli] na kila mtu mwongo.” (Warumi 3:3, 4) Kwa kweli, Petro, Paulo na wafuasi wengine waaminifu wa Yesu Kristo walitumikia wakiwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” wakiwa “wakili mwaminifu,” kwa kuagizwa na Bwana wao, Yesu Kristo, walitolee kundi la Mungu chakula cha kiroho.—Mathayo 24:45-47; Luka 12:42-44.
6 Baada ya mitume kufa, jamii hiyo ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” iliacha kuonekana duniani, maana baadaye ilifunikwa ikafichika wakati shamba la Kikristo la ngano lilipokuja kuwa shamba lenye kujawa na magugu hasa.—Mathayo 13:37-43.
Kuja Kwenye Nyakati za Ki-Siku-Hizi
7, 8. (a) Ni wakati gani na kwa njia gani “mtumwa” alitokea tena? (b) Ameonyeshaje kwamba analiunga mkono lile Neno tangu miaka ya 1870?
7 Walakini, yapata miaka mia moja iliyopita, jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ilianza tena kujitokeza mbele ikiwa mwunga-mkono aliye mshikamanifu wa Neno la Mungu. Miaka ilipoendelea kupita jamii hiyo imezidi kuonekana wazi na ulimwengu. Mambo ya uhakika yanaonyesha kwamba leo “mtumwa” huyu anahusiana na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi.
8 Huyu “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ni Wakristo waaminifu, ambao wamejiweka wakf kabisa kwa Yehova kupitia Kristo na kuzaliwa kwa roho ya Mungu. Wao ni wanafunzi wa Biblia wenye juhudi ambao tangu miaka ya katikati ya 1870 wamejitokeza kwa uhodari waitetee Biblia wakionyesha ni Neno la Mungu kwa kutumia vitabu, vijitabu, magazeti na trakti, makala za magazeti ya kilimwengu na hotuba za watu wote. Mwaka 1886, walichapisha Sehemu ya Kwanza ya kitabu Studies in the Scriptures (Mafunzo Katika Maandiko). Katika sura ya 3, yenye kuitwa “Biblia Ikiwa Ufunuo wa Kimungu Wenye Kutazamwa kwa Fikira Zinazofaa,” kitabu hicho kiliitetea Biblia kwa ustadi mwingi sana. Uteteaji mwingine mkubwa wa Neno la Mungu ulikuwa katika sura ya 1 ya Sehemu ya Sita ya kitabu hicho (iliyopigwa chapa mwaka 1904). Sura hiyo ilikuwa ikisema “Hapo Mwanzo,” nayo ililikanusha vizuri sana lile fundisho la kukisia kwamba mwanadamu alitokea kwa mageuzi.
9-11. (a) Wakati wa miaka ya mwisho-mwisho wa 1800 na ya mwanzo-mwanzo wa 1900, ushikamanifu wa “mtumwa” kwa lile Neno umeonyeshwaje? (b) Tangu mwaka 1950, Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ilitokeza vifaa gani vikubwa-vikubwa ili kulieneza Neno la Mungu?
9 Mwisho-mwisho wa miaka ya 1800 na mwanzo-mwanzo wa miaka ya 1900, hawa Wanafunzi wa Biblia waaminifu, kama walivyojiita, walikuwa na juhudi katika kuiunga mkono Biblia kwa ushikamanifu kuwa ni Neno la Mungu. Walichapisha habari nyingi kuthibitisha ukweli wayo na kueleza sana pia utimizo wa unabii wayo mbalimbali na jinsi mtu anavyoweza kutumia kanuni za Biblia katika maisha yake. Mwaka 1914 walitokeza ule Mchezo wa Kuigizwa Wenye Picha za Uumbaji, wenye urefu wa saa 8, ambao kwa wazi sana ulitayarishwa “ili kuitetea Biblia kwa kuionyesha kuwa Neno la Mungu.”
10 Wakiwa wanaliunga mkono Neno la Mungu kwa ushikamanifu na kuonyesha kwamba wao walikuwa na bidii ya kulieneza likiwa limechapwa katika vitabu, jina la shirika lao lilibadilishwa mwaka 1896 likawa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, Biblia na Trakti. Mwaka 1902 Sosaiti iliweza kuwa na Biblia inayoitwa The Emphatic Diaglott iliyotafsiriwa na Wilson, kisha ikasimamia ugawaji wa Biblia hiyo. Mwaka 1907 Sosaiti ilichapisha chapa ya King James Version na wakaiita Biblia ya Waberea. Jina hilo lilichaguliwa kutokana na Wakristo Waberea ambao ‘waliyachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo aliyowaambia Paulo ndivyo yalivyokuwa.’ (Matendo 17:11) Ilikuwa na maelezo ya nyongeza yenye kurasa zaidi ya 700 zenye kutoa maana ya kila andiko moja moja na orodha za maandiko yenye kuunga mkono habari karibu 40 za Biblia. Ilikuwa pia na orodha ya kialfabeti (utaratibu wa herufi A, B, C, n.k.) yenye kurasa 100 za maneno yale makubwa-makubwa yaliyotumiwa ndani. Mwaka 1926 Sosaiti ilianza kuipiga chapa Biblia The Emphatic Diaglott katika mashine zayo yenyewe, huko Brooklyn. Mwaka 1942 Sosaiti ikachapisha chapa ya King James Version pamoja na vitabu vingi vya mafunzo ya maana sana, na katika mwaka 1944 ikachapisha Biblia American Standard Version, pamoja na vitabu vingine vya mafunzo kama vile vya hapo kwanza. Tafsiri hiyo ya Biblia ililitafsiri jina Yehova kwa uaminifu kulingana na maandishi ya kwanza ya Kiebrania.
11 Kufikia mwaka 1950 Sosaiti iliichapisha New World Translation of the Christian Greek Scriptures kwa sababu ilitaka kuliunga mkono Neno la Mungu kwa ushikamanifu. Halafu Maandiko ya Kiebrania yalitafsiriwa yakiwa katika sehemu moja moja za vitabu 5, kisha Biblia nzima ikatokea mwaka 1961 ikiwa kitabu kimoja. Kati ya mwaka 1926 na 1980 Mashahidi wa Yehova walitokeza Biblia 43,860,000.
Sababu Iliyofanya Tafsiri Mpya Ihitajiwe
12, 13. Sababu ya kwanza iliyofanya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” apendezwe na kutokeza tafsiri mpya ya Biblia ilikuwa nini?
12 Kwa sababu gani huyu “mtumwa mwaminifu mwenye akili” alipendezwa kuwe na tafsiri mpya, yaani, New World Translation of the Holy Scriptures?
13 Kwanza kabisa, hati za Biblia zenye maandishi ya zamani zaidi na zenye kuaminika zaidi zimevumbuliwa kwa sababu ya uchimbuzi-ardhi wa wabukuzi na wanachuo wa Biblia, na hati hizo zina maandishi ya lugha zile za kwanza-kwanza. Hivyo leo kuna hati nzuri sana za maandishi ya Biblia za karne ya tano na nne za Wakati wa Kawaida wetu, tena kuna sehemu-sehemu zilizoandikwa kwenye karatasi zilizotengenezwa kwa mafunjo (majani marefu ya majini) za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo za huko nyuma katikati ya karne ya pili. Vilevile, Vitabu vya Kukunja vya Bahari ya Chumvi vya Maandiko ya Kiebrania, ambavyo ni vya kabla ya Wakati wa Kawaida wetu, vimeeleza vifungu vya Biblia kwa njia nzuri zaidi. Hati ya maandishi ya Biblia ikiwa ya zamani zaidi, ndivyo inavyoelekea zaidi kulingana na hati za maandishi ya kwanza kabisa ya waandikaji walioongozwa na Mungu, hati ambazo hakuna hata moja kati yazo iliyopo leo.
14. Sababu ya pili ni nini? Toa mfano.
14 Sababu ya pili iliyofanya kuwe na uhitaji wa tafsiri mpya-mpya zaidi na kufanya tafsiri hizo ziwe na maendeleo ya kurekebisha mambo fulani kuhusiana na zile za kwanza ni kwamba lugha ya Kigiriki iliyotumiwa karne ya kwanza inaeleweka vizuri zaidi siku hizi. Wakati ulipozidi kupita wabukuzi walivumbua kwa wingi sehemu-sehemu za maandishi yaliyoandikwa katika mafunjo ambazo ziliandikwa huko nyuma wakati ule ule Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalipokuwa yakiandikwa. Sehemu-sehemu hizo za maandishi yaliyoandikwa kwenye mafunjo, zinazohusu mambo ya maisha ya kila siku, zilionyesha ni aina gani ya Kigiriki iliyotumiwa na waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Mfano halisi wa jambo hilo ni neno “Racca” lililo kwenye Mathayo 5:22 katika nyingine za tafsiri za zamani zaidi. Kwa kuwa watafsiri hawakujua maana ya neno hilo, wao waliliandika kwa kubadili kidogo tu herufi hizo ili neno lenyewe litamkike kwa namna ya Kiingereza, lakini maana ya neno hilo ilibaki bila kufahamiwa. Lakini sasa maana yalo inajulikana na kwa hiyo Biblia ya New World Translation inalitafsiri neno hilo kuwa na maana ya “neno la madharau lisiloneneka.” Kama unavyoweza kuona, maarifa yaliyoongezeka juu ya lugha zilizotumiwa kuiandika Biblia kule mwanzoni kabisa yanafanya tafsiri zieleweke vizuri zaidi.
15. Toa mfano wa sababu ya tatu.
15 Sababu ya tatu inayofanya tafsiri mpya zihitajiwe ni kwamba lugha zile zile zinazotumiwa kutafsiri Biblia kutokana na maneno ya lugha ya kwanza zinapata mabadiliko ya usemi baada ya miaka mingi kupita. Kiingereza kilichotumiwa na Wycliffe mtafsiri wa Biblia wa karne ya 14 kinatofautiana sana na lugha iliyotumiwa na watafsiri wa King James Version mwanzoni-mwanzoni mwa karne ya 17. Tena Kiingereza kimefanyiwa mabadiliko mengi sana hata baada ya hapo. Maneno mengine yamekuwa na maana iliyo kinyume cha vile yalivyokuwa yakimaanisha hapo kwanza. Kwa mfano neno “let” la Kiingereza lilikuwa na maana ya “kuzuia” siku za Mfalme James, lakini leo linamaanisha “kuruhusu” (kuachilia).
16. Kama inavyoonyeshwa na Matendo 20:30 na 2 Timotheo 4:3, 4, sababu nyingine iliyofanya “mtumwa” aanze shughuli ya kutafsiri Biblia inaweza kuwa ilikuwa nini?
16 Mwisho, moja ya sababu zile kubwa zilizofanya Biblia ya New World Translation itokezwe ni kwamba Biblia inahitaji kueleweka kwa usahihi. Hatuwezi kuukataa uhakika wa kwamba mtu hutafsiri kulingana na imani zake za kidini. Kwa kweli, inakuwa hivyo wakati neno au andiko fulani linapokuwa katika hali ya kuweza kutafsiriwa kwa zaidi ya njia moja. Kwa sababu nyakati nyingine watafsiri huharibu maana ya ile lugha ya kwanza katika vifungu vinavyoelekea kupingana na imani zao, wakiiharibu kwa kujua au kwa kutokujua, ilikuwa lazima kabisa tafsiri fulani itokezwe na wanaume ambao walilishikilia Neno la Mungu kwa ushikamanifu.
Ukosefu wa Kushikilia Neno la Mungu kwa Ushikamanifu
17. Ni mifano gani kati ya mingine kadha inayoonyesha mistari ya uongo iliyopenyezwa ndani ya maandishi ya Biblia?
17 Kwa sababu waandishi fulani hawakushikilia Neno la Mungu kwa ushikamanifu, sehemu nzima-nzima za mistari ya uongo zimepenya ndani ya yale yanayoitwa “Maandishi Yaliyopokewa,” ambayo yalitegemewa na Biblia ya King James Version wakati wa kuitafsiri. Mistari hiyo iliongezwa kwenye maandishi ya kwanza yaliyoongozwa na Mungu. Mifano michache ni Yohana 8:1-11 na Marko 16:9-20. Mfano mwingine wa kifungu cha uongo unapatikana kwenye 1 Yohana 5:7, 8. Hapo maneno “mbinguni, Baba, na Neno, na Roho Mtakatifu, na watatu hawa ni umoja” (au “mmoja” katika King James) yanaelekea kuliunga mkono fundisho la Utatu. Lakini uchunguzi umefanywa ikaonekana wazi kwamba maneno hayo yaliongezwa na mwandishi mdanganyifu miaka zaidi ya 1,000 baada ya kumalizika kwa uandikaji wa Maandiko yaliyoongozwa na Mungu.
18, 19. (a) Watafsiri wengine wamelichezea-chezea Neno la Mungu na wakalitafsiri vibaya kwa njia gani? (b) Jambo hilo limetukiaje kwa habari ya maandiko yanayohusu hali ya wafu?
18 Sana-sana wenye kutokeza Biblia za kisasa zenye kufupiza-fupiza mistari kwa muhtasari ndio wamejijasirisha sana kutoa maana zisizofaa, nyakati nyingine katika maandiko yenyewe na nyakati nyingine katika maelezo yaliyo chini ya ukurasa. Kwa mfano, kwenye Mhubiri 9:5, 10, The Living Bible ya Taylor inasema hivi: “Kwa maana wale wanaoishi angalau wajua kwamba wao watakufa! Lakini wale wafu hawajui jambo lo lote.” Na “Jambo lo lote wewe wafanya, fanya vizuri, kwa maana katika kifo, ambako wewe unakwenda, hakuna kufanya kazi wala kufanya mipango, wala kujua, wala kufahamu.” Kwa sababu mtafsiri hakukubaliana na maneno hayo yaliyoongozwa na Mungu, yeye aliongeza maelezo haya chini ya ukurasa: “Hayo ni maoni ya Sulemani ya kuvunjika moyo, wala hayaonyeshi alijua kweli ya Mungu juu ya mambo haya!”
19 Tafsiri hiyo inalieleza vibaya Neno la Mungu kwenye Zaburi 115:17 pia. Hapo King James Version inasema hivi: “Wale wafu hawamsifu BWANA, wala wo wote ambao waenda chini ndani ya kimya.” Lakini mtafsiri wa The Living Bible anaonekana kwamba anaamini wafu wanapokufa wanaendelea kuishi mahali kwingineko, naye anaonyesha hivyo kwa kuutafsiri mstari huo hivi: “Wale wafu hawawezi kuimba sifa kwa Yehova hapa juu ya dunia.”
20. Kwa habari ya Yohana 1:1, imani ya Utatu wa miungu imeingiaje katika tafsiri fulani, lakini ni njia gani nyingine ya kutafsiri iliyo sahihi na yenye kukubalika?
20 Lakini na iangaliwe kwamba pasipo shaka mtafsiri wa Biblia atakosea nyakati nyingine kwa sababu ya kukosa ufahamu sahihi wa Neno la Mungu, hata ikiwa yeye ana nia nzuri sana. Kwa mfano, karibu watafsiri wote wanauamini Utatu wa miungu na kwa hiyo wanaitafsiri Yohana 1:1 hivi: “Naye Neno alikuwa Mungu.” Lakini mstari huo unaweza kutafsiriwa kwa usahihi kwa njia nyingine, tukikumbuka kwamba neno la Kigiriki Theos halikuandikwa likiwa limetanguliwa na neno kama “ndiye” ili kuonyesha kwamba Neno alikuwa “ndiye” Mungu. Kwa sababu hiyo, tafsiri inayoitwa An American Translation inakitafsiri hivi kifungu hicho cha maneno, “Na huyo Neno alikuwa wa kimungu.” Biblia ya New World Translation inakitafsiri kifungu hicho kwa kusema, “Na huyo Neno alikuwa mungu” (neno “mungu” likiwa na “m” ndogo). Wala si tafsiri hiyo pekee inayofanya hivyo. Vivyo hivyo ndivyo kifungu hicho kilivyotafsiriwa huko nyuma mwaka wa 1807 wakati tafsiri ya Askofu Mkuu Newcome ilipofanyiwa masahihisho (marekebisho).
Kuliunga Mkono Jina la Mungu kwa Ushikamanifu
21. Tafsiri nyingine za kisasa za Biblia zinampingaje Mungu mwenyewe?
21 Walakini, njia moja iliyo mbaya sana ambayo tafsiri nyingi zaidi za kisasa zinakosa kulishikilia Neno la Mungu kwa ushikamanifu ni wakati zinapokosa kuliandika jina la Mungu Yehova jinsi lipasavyo kuandikwa, jina ambalo linamtofautisha yeye na wengine. Jina hilo katika Kiebrania linasimamiwa na neno la herufi nne zinazojulikana kuwa Tetragramatoni. Uthibitisho wa kwamba Yehova Mungu mwenyewe analichukua jina lake mwenyewe kuwa la maana sana unaweza kuonekana kwa uhakika wa kwamba yeye aliwapa waandikaji wa Kiebrania roho yake ili walitumie jina hilo jumla ya mara 6,961 katika Maandiko ya Kiebrania. (Hiyo ni pamoja na zile mara 134 ambazo waandishi wa Kiebrania waliliondoa jina hilo kwa makusudi.)
22, 23. (a) Ni jambo gani linaloonyesha ni kosa kutafsiri jina la Mungu kwa kutumia jina linalotumika kwa mtu ye yote tu? (b) The Jerusalem Bible inatoaje maoni ya unyofu juu ya jambo hili? (c) Kulingana na waandikaji fulani, kwa sababu gani inafaa zaidi kulitumia jina “Yehova” badala ya “Yahweh”?
22 Jambo la hakika ni kwamba Muumba anatajwa katika Maandiko ya Kiebrania mara nyingi kwa jina lake Yehova linalomtofautisha na wengine, kuliko jumla ya mara anazotajwa kwa kutumia maneno yale yote yaliyo ya cheo tu. Zaidi ya hilo, haileti maana hata kidogo kutafsiri jina la pekee la mtu, kama vile Yehova, kwa kuweka mahali pake jina la mtu ye yote tu kama vile Bwana; kama vile isivyoleta maana kutafsiri “Rolls Royce” (jina la motokaa iliyo ya bei kubwa zaidi ulimwenguni) kwa kuiita “motokaa” au “gari” tu, na hali motokaa na gari ni nyingi sana. Ingawa Biblia inayoitwa Jerusalem Bible inapendelea kutumia “Yahweh” badala ya Yehova,” Biblia hiyo inataja sababu thabiti ya kulitumia jina hilo badala ya kusema “Bwana.” Dibaji ya tafsiri hiyo ya Biblia inasema: “Kusema, ‘Bwana ni Mungu,’ kwa uhakika ni kurudia-rudia jambo moja tu bila kutoa maana, lakini kusema Yahweh ni Mungu’ si kurudia-rudia jambo lile lile.”
23 Basi je! jina “Yahweh” linapasa kutumiwa badala ya “Yehova”? Si lazima iwe hivyo. Kulingana na Canon D. D. Williams wa Cambridge “ushuhuda unaonyesha sivyo, na unakuwa karibu kuthibitisha kwamba, Yahweh siyo yaliyokuwa matamko ya kweli ya Tetragramatoni.” Biblia Hebraica, iliyochapishwa katika Stuttgart mwaka 1951, inaweka vokali “e” na “a” ili neno hilo lisomwe kuwa “Yeh·wah.” Chapa hiyo ya Biblia ilitumiwa na Halmashauri ya Tafsiri ya Biblia ya New World. Gustav Oehler, profesa wa Tubingen, anasema hivi: “Kuanzia hapa na kuendelea mimi ninalitumia neno Yehova, kwa sababu, ni wazi kwamba jina hili limezoeleka likawa asili yetu katika maneno tunayoyatumia kwa ukawaida, na haliwezi kuondolewa libadilishwe na jingine.” Katika tafsiri yake ya Emphasized Bible, mtafsiri Rotherham alikuwa mmoja kati ya watafsiri wa kwanza kuitumia ile namna ya “Yahweh.” Walakini, katika kitabu chake Studies in the Psalms (Mafunzo Katika Zile Zaburi), ambacho kilichapishwa mara ya kwanza baada ya yeye kufa, alirudia matumizi ya “Yehova,” akasema alifanya hivyo kwa sababu ya “kutaka watu wote wajisomee na kujisikilia wenyewe.”
“Yehova” Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo
24. (a) Ni mara ngapi Biblia ya New World Translation inatumia jina la Yehova katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo? (b) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba tafsiri zilizotangulia hiyo zilifanya ivyo hivyo?
24 Lakini namna gani matumizi ya jina “Yehova” katika lile linaloitwa Agano Jipya, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo? Katika New World Translation jina hilo linaonekana mara 237. Ingawa huenda jambo hilo likaonekana la ajabu sana, hiyo siyo kamwe tafsiri ya kwanza kulitumia jina hilo katika sehemu hiyo ya Biblia. Jina hilo lilitumiwa hapo hata huko nyuma mwaka 1796, wakati Brentano mtafsiri Mjeremani alipolitumia neno “Yehova” kwenye Marko 12:29. Vilevile iko ile tafsiri inayoitwa Emphatic Diaglott, ambayo ni tafsiri yenye kuonyesha maneno yaliyotafsiriwa katika Kiingereza chini ya kila mstari wa maneno ya Maandiko ya Kikristo yaliyoandikwa katika Kigiriki, nayo ilichapishwa mara ya kwanza mwaka 1864. Tafsiri hiyo inalitumia jina “Yehova” mara nyingi inapotaja-taja maneno ya Maandiko ya Kiebrania ambamo jina hilo linaonekana, nayo inafanya hivyo jumla ya mara 18. Kwa mfano, angalia Mathayo 22:37, 44; Marko 12:29, 30; Luka 20:42.
25. (a) Ni ushuhuda gani wa hivi majuzi unaoonyesha kwamba jina la Mungu lilikuwa katika maandishi ya kwanza ya Maandiko ya Kigiriki? (b) Ni badiliko gani linaloonekana kwamba lilitokea katika sehemu mbili katika karne ya pili W.K.?
25 Sababu inayofanya ionekane kuwa ajabu sana jina “Yehova” kuonekana katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ni kwamba kwa karne nyingi ilidhaniwa kwamba jina hilo halikuandikwa katika tafsiri Septuagint ya Maandiko ya Kiebrania yaliyotumiwa na Yesu na mitume wake. Lakini mambo ambayo yamevumbuliwa hivi majuzi yanathibitisha kabisa kwamba Tetragramatoni (zile herufi nne zenye kusimamia jina la Mungu) ilikuwa katika tafsiri Septuagint ya nyakati hizo. Kwa hiyo Profesa Howard wa Chuo Kikuu cha Georgia anasema hivi: “Sisi tunajua kwa uhakika kwamba Wayahudi wenye kusema Kigiriki waliendelea kuandika [ile Tetragramatoni] ndani ya Maandiko ya Kigiriki waliyokuwa nayo. Tena, haielekei sana kuwa Wakristo wa kwanza waliokuwa Wayahudi wenye kusema Kigiriki, wasiotaka kubadili mambo ya kikale, hawakuyafuata matumizi hayo. . . . Lingalikuwa jambo la kuwashangaza mno kuiondoa Tetragramu katika maandishi yaliyo ya kwanza ya Biblia.” Kwa hiyo profesa huyo anamaliza kwa kusema: “Kwa kuwa Tetragramu bado iliandikwa katika nakala za Biblia ya Kigiriki zilizotumiwa zikiwa ndiyo Maandiko ya kanisa la kwanza, ni jambo la akili nzuri kukata maneno kwamba waandikaji wa A[gano] J[ipya] waliiacha Tetragramu ibaki ndani ya maandishi ya kwanza ya Biblia walipokuwa wakitaja maneno kutoka kwenye Maandiko. Juu ya utaratibu uliofuatwa na Wayahudi wa nyakati zilizoutangulia Ukristo tunaweza kuwaza kwamba maandishi ya kwanza ya A[gano] J[ipya] yalikuwa na Tetragramu katika maneno yaliyotajwa” kutokana na Agano la Kale. Vilevile Profesa Howard anaandika kwamba wakati Tetragramatoni ilipoondolewa katika tafsiri Septuagint, iliondolewa pia katika Maandiko ya Kiebrania yaliyokuwa yameandikwa katika Maandiko Kigiriki ya Kikristo. Ni wazi kwamba badiliko hilo lilitukia mwanzoni mwa karne ya pili W.K. Hakuna shaka kwamba jina Yehova linastahili kuwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kama tunavyoliona katika New World Translation.
26. Biblia ya New World Translation ina kanuni gani za kuifanya iliingize lile Jina katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo?
26 Biblia ya New World Translation inaongeza pia jina “Yehova” katika sehemu ambako jina hilo linaonekana katika maneno yaliyotumiwa kutokana na Maandiko ya Kiebrania. Kwa sababu gani inafanya hivyo? Ili kumsaidia msomaji ajue kama ni Yehova Mungu au ni Yesu Kristo anayetajwa wakati neno “Bwana” [Kyrios] linapoonekana katika maandishi ya Kigiriki. Je! kuna kanuni yo yote nzuri inayotegemewa ili kufanya hivyo? Ndivyo kwa maana katika tafsiri za Kiebrania zipatazo 20 za Maandiko ya Kigiriki tunaona jambo ilo hilo. Vilevile kuna tafsiri nyingi za wamisionari za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zinazofanya ivyo hivyo. Kwa mfano, tafsiri ya Kijapani, ambayo ni moja ya tafsiri zilizo za zamani zaidi za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, inalitumia sana jina “Ehoba” (Yehova).
27. Kwa sababu gani inawapasa watumishi wa Mungu walio washikamanifu waitumie kwa ukamili Biblia ya New World Translation, nao wataitumia hata hali ijapokuwa namna gani?
27 Lakini hata kama wanachuo wanaochunguza Kiebrania na Kigiriki wa Jumuiya ya Wakristo wataisifu au wailaumu Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures, bado ukweli ni kwamba Biblia hiyo ilitokezwa na wanaume waliolishikilia Neno la Mungu kwa ushikamanifu. Kwa uhakika Biblia hiyo ni msaada mkubwa katika ‘kutuhekimisha hata tupate wokovu na katika kutusaidia tuwe kamili, tuwe tumekamilishwa tupate kutenda kila tendo jema.’ (2 Timotheo 3:15-17) Acheni sisi sote tulio na tafsiri nzuri hii tupate baraka za kuitumia kwa ukamili.
—Kutoka The Watchtower, March 15,1982.
VITU HIVI NA WATU HAWA VIMELIUNGAJE MKONO NENO LA MUNGU KWA USHIKAMANIFU, NA KWA SABABU GANI?
◻ Makao makuu ya Mashahidi wa Yehova (au majengo yao)
◻ Yesu Kristo na mitume wake
◻ “Mtumwa mwaminifu mwenye akili” wa nyakati za kisasa
◻ Waandishi walionakili na wakarudia kunakili maandishi ya Biblia
◻ Watafsiri wa kwanza-kwanza waliolitafsiri katika lugha za kisasa
◻ Watafsiri wa tafsiri za Biblia za hivi majuzi
◻ Halmashauri ya Tafsiri ya Biblia ya “New World”
[Sanduku katika ukurasa wa 19]
Wakati mmoja mtafsiri Mwamerika aligombanishwa vikali na msomaji wa Biblia kwa sababu ‘alikivunja-vunja Kiingereza kile kizuri’ cha tafsiri ya Biblia inayoitwa King James Version, na bila shaka huyo mwenye kulalamika alikuwa akikipendelea kile Kiingereza cha kikale cha tafsiri hiyo. Mtafsiri alipojaribu kueleza kwamba uzuri wenye kupendeza wa ujumbe wenyewe ndio wa maana kuliko uzuri wa usemi unaotumiwa, mwenye kumlaumu alijibu hivi: “Mimi siujali hata kidogo ujumbe wenyewe. Mimi siamini kuna Mungu.”
[Sanduku katika ukurasa wa 19]
Mradi wa kutafsiri Biblia, au tuseme wa tafsiri ya namna yo yote tu, unapasa kuwa ni kumsaidia msomaji wa maneno yaliyotafsiriwa aupokee ujumbe uliotafsiriwa ukiwa na uzito ule ule, aupokee kiakili na kimoyoni, ndiyo, hata kiroho, ili awe ni kama kwamba anayasoma Maandiko katika lugha ile ya kwanza.
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
Edgar Goodspeed ambaye ni mtafsiri wa Biblia alimwandikia hivi mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwa habari ya tafsiri ya Biblia ya New World Translation of the Christian Greek Scriptures: “Mimi napendezwa na kazi yenu ya umisheni, na hata napendezwa na jambo la kwamba mnaifanya ulimwenguni pote, na tena nafurahishwa sana na tafsiri ile yenye kueleza mambo waziwazi bila vizuizi, na yenye uthabiti mwingi. Tafsiri hiyo inaonyesha imetungwa kwa ujuzi mwingi sana ulio timamu, kama mimi niwezavyo kushuhudia.”
A. Thompson wa Uingereza, ambaye ni mwanachuo wa Kiebrania na Kigiriki, aliandika yanayofuata katika kitabu The Differentiator, akisema habari ya kisehemu kimoja cha New World Translation of the Hebrew Scriptures: Mimi ningeipendekeza kuwa jitihada yenye unyofu iliyofanywa ili kuonyesha mambo wazi, kwa kuyatafsiri Maandiko Matakatifu katika Kiingereza cha kisasa. Haionekani jaribio lo lote lilifanywa kukazia mafundisho au mawazo ya kipekee ili yafuatwe na watu.”
Kitabu Eerdman’s Handbook to the Bible kinaipanga Biblia ya New Worid Translation kati ya tafsiri 14 ‘za Kiingereza zilizo kubwa-kubwa katika karne ya 20.’
[Picha katika ukurasa wa 18]
(Maandishi haya yanasema,
SOMA NENO LA MUNGU BIBLIA TAKATIFU KILA SIKU.)
[Picha katika ukurasa wa 21]
Tetragramatoni katika sehemu sehemu za “Septuagint” zilizotoka Misri (Mafunjo ya Fouad ya 266)
Mafunjo haya yalichapishwa hapo zamani na Mashahidi wa Yehova ili yaonekane wazi na watu. Kuonekana kwa jina la Mungu hapa kulitokeza msingi wa kutumia jina “Yehova” katika Biblia ya New World Translation