Sura ya 27
Kuchapa na Kugawanya Neno Takatifu la Mungu Mwenyewe
UPANDE wa nje wa jengo kuu la kiwanda kwenye makao yao makuu, Mashahidi wa Yehova kwa miongo ya miaka wameonyesha ishara inayohimiza kila mtu hivi: “Soma Neno la Mungu Biblia Takatifu Kila Siku.”
Wao wenyewe ni wanafunzi wenye bidii wa Neno la Mungu. Kwa muda wa miaka wametumia aina mbalimbali za tafsiri ya Biblia katika jitihada ya kufahamu maana halisi ya Maandiko ya awali yaliyopuliziwa roho. Kila Shahidi hutiwa moyo kuwa na programu ya kibinafsi ya kusoma Biblia kila siku. Kwa kuongezea funzo lao la habari kuu ya Neno la Mungu, wao huendelea kusoma na kuzungumza juu ya Biblia yenyewe katika mikutano yao ya kutaniko. Kusudi lao si kutafuta maandiko ili wategemeze mawazo yao. Wao huitambua Biblia kuwa Neno lililopuliziwa la Mungu mwenyewe. Wanajua kwamba hiyo hutoa karipio na nidhamu, nao hujitahidi sana kupatanisha kufikiri kwao na mwenendo wao na yale inayosema.—2 Tim. 3:16, 17; linganisha 1 Wathesalonike 2:13.
Kwa sababu ya kusadikishwa kwao kwamba Biblia ni Neno takatifu la Mungu mwenyewe na kwa sababu wanajua habari njema za utukufu ambazo inazo, Mashahidi wa Yehova ni wahubiri na wagawanyaji wa Biblia wenye bidii.
Sosaiti Yenye Kuchapa Biblia
Ilikuwa katika 1896 kwamba rejezeo la moja kwa moja kwenye Biblia lilitiwa rasmi katika jina la shirika halali lililokuwa likitumiwa wakati huo na Wanafunzi wa Biblia katika kazi yao ya kuchapa. Wakati huo Zion’s Watch Tower Tract Society ilikuja kuitwa kihalali Watch Tower Bible and Tract Society.a Sosaiti haikuwa mchapaji na mjalidi wa Biblia mara hiyo, lakini ilikuwa mtangazaji wazo mwenye bidii, ikipanga mambo mengi hususa, ikiandaa mambo ya ziada yenye thamani, na kisha kupanga na mashirika ya kibiashara ili yazichape na kuzijalidi.
Hata kabla ya 1896, Sosaiti ilikuwa ikifanya mengi ikiwa mgawanyaji wa Biblia. Ilivuta fikira kwenye tafsiri mbalimbali za Biblia zilizopatikana, ikazinunua kwa wingi ili iweze kuzipata kwa bei nafuu, na kisha ikaziuza kwa bei ambayo nyakati nyingine ilikuwa asilimia 35 tu ya ile bei ya kawaida, si ili ipate faida ya kibiashara bali ili itoe utumishi kwa wasomaji wayo. Miongoni mwa Biblia hizo kulikuwa na chapa nyingi za King James Version zilizokuwa rahisi kubeba na kutumia, pia ‘Biblia za Walimu’ (King James Version ikiwa na misaada kama konkodansi, ramani, na marejezo ya pambizoni) zilizokuwa kubwa zaidi, The Emphatic Diaglott ikiwa na fasili ya mstari kati ya mstari wa Kigiriki na Kiingereza, tafsiri ya Leeser iliyotia maandiko ya Kiingereza kando ya yale ya Kiebrania, tafsiri ya Murdock kutoka Siria ya kale, The Newberry Bible yenye marejezo ya pambizoni yaliyoelekeza fikira kwenye sehemu ambazo jina la kimungu lilitokea katika lugha ya awali pamoja na mambo mengi yenye thamani yaliyoonyeshwa katika maandiko ya Kiebrania na Kigiriki, New Testament ya Tischendorf yenye marejezo ya vielezi-chini yaliyoonyesha maelezo tofauti-tofauti katika hati tatu kati ya zile za Biblia ya Kigiriki ya kale zilizo kamili zaidi (Sinaitic, Vatican, na Alexandrine), Biblia ya Variorum yenye vielezi-chini vilivyoonyesha si maandishi tofauti ya hati za kale tu bali pia tafsiri mbalimbali za sehemu za maandiko za wanachuo mashuhuri, na tafsiri halisi ya Young. Sosaiti pia ilitoa misaada kama vile Cruden’s Concordance na Analytical Concordance ya Young yenye maelezo juu ya maneno ya awali ya Kiebrania na Kigiriki. Katika miaka iliyofuata, mara nyingi Mashahidi wa Yehova duniani pote walipata maelfu mengi ya Biblia kutoka kwa sosaiti za Biblia katika lugha zozote zilizopatikana na wakazigawanya.
Mapema kama 1890, kulingana na ithibati inayopatikana, Sosaiti ilipanga kuwa na uchapaji wa pekee, wenye jina layo, wa Chapa ya Pili ya The New Testament Newly Translated and Critically Emphasised, kama ilivyotayarishwa na mtafsiri wa Biblia Mwingereza Joseph B. Rotherham. Kwa nini tafsiri hiyo? Kwa sababu ya uhalisi wayo na jitihada yayo ya kunufaika kikamili na utafiti uliokuwa umefanywa ili kuwa na maandiko ya Kigiriki yaliyo sahihi zaidi na kwa sababu msomaji alisaidiwa na alama zilizotumiwa na mtafsiri ili kutambulisha ni maneno au semi gani zilizokaziwa kipekee katika maandiko ya Kigiriki.
Katika 1902 uchapaji wa pekee wa Chapa ya Mistari Sambamba ya Biblia ya Holman ulifanywa kwa mpango wa Watch Tower Society. Ilikuwa na pambizo zilizo pana ambazo ndani yazo kulichapwa marejezo ya mahali katika vichapo vya Watch Tower ambapo mistari mbalimbali ilielezwa, na pia ilikuwa na faharisi ikiorodhesha vichwa vingi vya habari pamoja na mitajo ya Maandiko na marejezo yenye msaada kwenye vichapo vya Sosaiti. Biblia hiyo ilikuwa na maneno ya tafsiri mbili—tafsiri ya King James ikiwa juu ya ile ya Revised Version mahali palipokuwa na tofauti yoyote. Pia ilitia ndani konkodansi yenye kutia mambo mengi iliyofahamisha mtumizi maana mbalimbali za maneno ya lugha ya awali.
Mwaka uo huo, Watch Tower Society ilimiliki mabamba ya kuchapia ya The Emphatic Diaglott, yanayotia ndani maandiko ya Kigiriki ya J. J. Griesbach ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (chapa ya 1796-1806) pamoja na tafsiri ya Kiingereza ya mistari kati ya mistari. Pamoja na hiyo kulikuwa na fasili ya maandiko ya Benjamin Wilson mzaliwa wa Uingereza, aliyekuwa akiishi Geneva, Illinois, Marekani. Mabamba hayo na haki ya kuwa wachapaji pekee yalikuwa yamenunuliwa na kisha Sosaiti ikapewa kuwa zawadi. Baada ya nakala ambazo tayari zilikuwa katika akiba kuweza kupelekewa watu, mipango ilifanywa na Sosaiti ili nakala zaidi zitokezwe, na hizo zilipatikana katika 1903.
Miaka minne baadaye, katika 1907, Chapa ya Wanafunzi wa Biblia ya King James Version ilichapwa. “Kitabu cha Walimu wa Biblia Waberoya” kilijalidiwa pamoja nayo ikiwa nyongeza. Hiyo ilitia ndani maelezo hususa ya mistari kutoka sehemu zote za Biblia, pamoja na marejezo kwenye vichapo vya Watch Tower kwa ajili ya maelezo kamili zaidi. Chapa yenye nyongeza iliyopanuliwa zaidi ilichapwa mwaka mmoja hivi baadaye.
Biblia hizo ziliagizwa kutoka kwa wachapaji na wajalidi katika vifungu vya kati ya 5,000 na 10,000 wakati mmoja, ili gharama isiwe kubwa. Sosaiti ilitamani kufanya tafsiri mbalimbali za Biblia na vifaa vya utafiti vinavyohusiana vipatikane kwa urahisi kwa watu wengi kadiri iwezekanavyo.
Kisha katika 1926 Watch Tower Society ilichukua hatua kubwa kwenda mbele katika kuhusika kwayo katika kuchapa Biblia.
Kuchapa Biblia Kwenye Matbaa Yetu Wenyewe
Ilikuwa miaka 36 baada ya Watch Tower Bible and Tract Society kuanza kutangaza Biblia kwa mara ya kwanza, kwamba iliweza kuchapa na kujalidi Biblia katika kiwanda chayo yenyewe. Biblia ya kwanza kutokezwa hivyo ilikuwa The Emphatic Diaglott, ambayo mabamba yayo yalikuwa mali ya Sosaiti kwa miaka 24. Katika Desemba 1926 Biblia hiyo ilichapwa kwenye matbaa-tambarare katika kiwanda cha Sosaiti cha Concord Street katika Brooklyn. Kufikia sasa, 427,924 yazo zimetokezwa.
Miaka 16 baadaye, katikati ya Vita ya Ulimwengu 2, Sosaiti ilianza kuchapa Biblia yote. Kwa kusudi hilo, mabamba ya King James Version yenye marejezo ya pambizoni yalinunuliwa katika 1942 kutoka kwa Kampuni ya A. J. Holman, ya Philadelphia, Pennsylvania. Tafsiri hiyo ya Biblia yote katika Kiingereza ilitokezwa, si kutoka kwa Vulgate ya Latini, bali kutoka kwa wanachuo walioweza kulinganisha tafsiri za mapema na Kiebrania Kiaramu, na Kigiriki cha awali. Konkodansi iliyotayarishwa na watumishi wa Yehova 150 wenye kushirikiana iliongezwa. Hiyo ilibuniwa kipekee ili kusaidia Mashahidi wa Yehova wapate upesi maandiko yanayofaa wanapokuwa katika huduma ya shambani na hivyo watumie Biblia kwa matokeo ikiwa “upanga wa roho,” ili kuondolea mbali na kufunua uwongo wa kidini. (Efe. 6:17, NW) Ili kufanya Biblia ipatikane kwa watu kila mahali kwa gharama ya chini, ilichapwa kwenye matbaa-mabamba-mviringo ya web—jambo ambalo halikuwa limepata kujaribiwa na wachapaji wengine wa Biblia. Kufikia 1992, jumla ya 1,858,368 ya Biblia hizo zilikuwa zimetokezwa.
Tamaa ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa zaidi tu ya kutia nakala za Biblia, kitabu chenyewe, mikononi mwa watu. Mashahidi walitaka kusaidia watu wajue jina la kibinafsi, pamoja na kusudi, la mtungaji wacho wa kimungu, Yehova Mungu. Kulikuwa na tafsiri katika Kiingereza—American Standard Version ya 1901—iliyotumia jina la kimungu katika sehemu zaidi ya 6,870 ambazo ilitokea katika vyanzo ambavyo kutoka kwavyo watafsiri walifanya kazi. Katika 1944, baada ya miezi kadhaa ya maafikiano, Watch Tower Society ilinunua haki ya kufanyiza seti za mabamba zenye mambo mengi ya Biblia hiyo kutoka kwa mabamba na maandishi yaliyotolewa na kampuni ya Thomas Nelson and Sons, ya New York. Wakati wa miaka 48 iliyofuata, nakala 1,039,482 zilitokezwa.
Steven Byington, wa Ballard Vale, Massachusetts, Marekani, alikuwa pia amefanyiza tafsiri ya Biblia ya Kiingereza cha kisasa ambayo ilitia jina la kimungu mahali palo pafaapo. Watch Tower Society ilimiliki hati ambayo haikuwa imechapwa bado katika 1951 na ikapata haki pekee ya kuchapa katika 1961. Tafsiri hiyo kamili ilichapwa katika 1972. Hadi kufikia 1992, kulikuwa na 262,573 zilizotokezwa.
Hata hivyo, wakati uo huo, jambo jingine lilikuwa likitokea.
Kutokeza Biblia New World Translation
Ilikuwa mapema katika Oktoba 1946 kwamba Nathan H. Knorr, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo, alipendekeza kwanza kwamba Sosaiti itokeze tafsiri mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kazi yenyewe ya tafsiri hiyo ilianza Desemba 2, 1947. Tafsiri yote ilipitiwa tena kwa uangalifu na halmashauri yote ya tafsiri, wote wakiwa Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho. Kisha, mnamo Septemba 3, 1949, Ndugu Knorr alifanya mkutano wa pamoja na baraza la wakurugenzi wa mashirika ya Sosaiti ya New York na Pennsylvania. Aliwatangazia kwamba New World Bible Translation Committee ilikuwa imekamilisha kazi ya tafsiri ya lugha ya kisasa ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na ilikuwa imeikabidhi Sosaiti ili ichapwe.b Hiyo ilikuwa tafsiri mpya kutoka kwa Kigiriki cha awali.
Je, kwa kweli kulikuwa na uhitaji wa tafsiri nyingine? Tayari wakati huo, Biblia yote ilikuwa imechapwa katika lugha 190 na angalau sehemu yayo ilikuwa imetafsiriwa katika lugha na lahaja 928 zaidi. Nyakati fulani-fulani, Mashahidi wa Yehova wametumia nyingi za tafsiri hizo. Lakini jambo hakika ni kwamba nyingi zazo zilifanyizwa na makasisi na wamishonari wa mafarakano ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo, na kwa kadiri inayotofautiana tafsiri zao ziliongozwa na falsafa za kipagani na mapokeo yasiyo ya kimaandiko ambayo mifumo yao ya kidini ilirithi kutoka zamani kutia na kupendelea uhakiki wa Biblia. Zaidi ya hayo, hati za Biblia za kale zaidi na zenye kutegemeka zaidi zilikuwa zikipatikana. Lugha ya Kigiriki ya karne ya kwanza ilikuwa ikieleweka kwa uwazi zaidi kama tokeo la uvumbuzi wa kiakiolojia. Pia, lugha ambazo katika hizo tafsiri hufanyizwa hupata mabadiliko katika muda wa miaka.
Mashahidi wa Yehova walitaka tafsiri ambayo ilitia ndani manufaa za usomi wa karibuni zaidi, tafsiri ambayo haikuwa imeongozwa na mafundisho na mapokeo ya Jumuiya ya Wakristo, tafsiri halisi ambayo ilitoa kwa uaminifu yale yaliyokuwa katika maandishi ya awali na hivyo ingeweza kuandaa msingi wa ukuzi wenye kuendelea katika ujuzi wa kweli ya kimungu, tafsiri ambayo ingekuwa wazi na yenye kueleweka kwa wasomaji wa kisasa. Biblia New World Translation of the Christian Greek Scriptures, iliyotolewa katika 1950, ilijazia uhitaji huo—angalau kwa sehemu hiyo ya Biblia. Mashahidi wa Yehova walipoanza kuitumia, wengi walisisimuliwa si kwa sababu tu lugha yayo ya kisasa ilikuwa rahisi kusoma bali kwa sababu walijua kwamba walikuwa wakipata uelewevu wa wazi zaidi katika maana ya Neno la Mungu lililopuliziwa.
Mojawapo mambo yenye kutokeza katika tafsiri hiyo ni kurudishwa kwa jina la kimungu, jina la kibinafsi la Mungu, Yehova, mara 237 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hiyo haikuwa tafsiri ya kwanza kurudisha jina hilo.c Lakini huenda ilikuwa ya kwanza kulirudisha kwa upatani katika maandiko yenyewe kutoka Mathayo hadi Ufunuo. Mazungumzo marefu juu ya jambo hilo katika dibaji yalionyesha msingi ufaao wa yale yaliyofanywa.
Baadaye, kuanzia mwaka 1953, Maandiko ya Kiebrania yalitafsiriwa katika Kiingereza na yakatolewa kwa kuendelea, katika mabuku matano tofauti. Kama vile ilivyokuwa imefanywa na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, uangalifu ulitumiwa ili kutafsiri yale yaliyokuwa katika maandiko ya lugha ya awali kwa uhalisi kwa kadiri iwezekanavyo. Uangalifu wa pekee ulitolewa ili kufanya matumizi ya maneno yapatane, yakionyesha kwa usahihi kitendo au hali iliyoonyeshwa katika vitenzi, na kutumia lugha rahisi ambayo ingeeleweka kwa urahisi na wasomaji wa kisasa. Mahali popote ambapo Tetragramatoni ilitokea katika maandiko ya Kiebrania, ilifasiliwa kwa kufaa kuwa jina la kibinafsi la Mungu, badala ya kutumia neno jingine tofauti, kama vile ilivyokuwa kawaida katika tafsiri nyingine nyingi. Makala za nyongeza na vielezi-chini katika mabuku hayo yaliwawezesha wanafunzi waangalifu wachunguze msingi wa fasili iliyotumiwa.
Katika Machi 13, 1960, New World Bible Translation Committee ilikamilisha usomaji wayo wa mwisho wa maandiko ya sehemu ya Biblia iliyokusudiwa iwe ya buku la tano. Hiyo ilikuwa miaka 12, miezi 3, na siku 11 baada ya kutafsiri kwenyewe kwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kuanza. Miezi michache baadaye, buku hilo la mwisho la Maandiko ya Kiebrania, likiwa limechapwa, lilitolewa ili ligawanywe.
Badala ya kuacha baada ya mradi huo kwisha, halmashauri ya tafsiri iliendelea kufanya kazi. Pitio lenye kutia mambo mengi la tafsiri yote lilifanywa. Kisha, Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures, chapa iliyosahihishwa katika buku moja, ilitangazwa na Watch Tower Society katika 1961. Ilifanywa ipatikane ili igawanywe kwa dola moja tu ili kwamba kila mtu, bila kujali hali yake ya kiuchumi, aweze kupata nakala ya Neno la Mungu.
Miaka miwili baadaye chapa ya pekee ya wanafunzi ilitangazwa. Hiyo iliweka pamoja mabuku yote ya awali katika jalada moja, yakiwa hayajasahihishwa, yakiwa na maelfu ya vielezi-chini vya thamani vya maandiko, kutia na mazungumzo ya dibaji na nyongeza. Pia ilidumisha marejezo-vitomeo yenye thamani yaliyoelekeza wasomaji kwenye maneno yaliyofanana, fikira au matukio yanayofanana, habari-maisha ya watu, mambo mengi ya kijiografia, kutimizwa kwa unabii mwingi, na manukuu ya moja kwa moja katika au kutoka kwa sehemu nyingine za Biblia.
Tangu chapa ya buku moja ya 1961 ilipotangazwa, nyingine nne zilizosahihishwa na kutiwa habari za kisasa zimetolewa. Chapa ya karibuni zaidi kati ya hizo ilikuwa katika 1984, wakati ambapo chapa yenye maandishi makubwa yenye nyongeza yenye mambo mengi, marejezo ya pambizoni kama 125,000, vielezi-chini vyenye kuelimisha vipatavyo 11,400, na konkodansi ilitangazwa. Sehemu mbalimbali za chapa hiyo husaidia wanafunzi waelewe kwa nini maandiko mbalimbali yahitaji kufasiliwa katika njia fulani ili kuwa sahihi, kutia na wakati ambapo maandiko yanaweza kufasiliwa kwa usahihi katika zaidi ya njia moja. Marejezo-vitomeo pia huwasaidia kuthamini upatano unaokamatana kati ya vitabu mbalimbali vya Biblia.
Ikiwa sehemu ya jitihada nyingi za New World Bible Translation Committee ili kusaidia wapendao Neno la Mungu kujua sana yaliyomo katika maandiko ya Koine ya awali (Kigiriki cha kawaida) ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, halmashauri hiyo ilitokeza The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures. Hiyo ilitangazwa kwanza na Watch Tower Society katika 1969 na kisha ikatiwa habari za kisasa katika 1985. Ina The New Testament in the Original Greek, kama ilivyotungwa na B. F. Westcott na F. J. A. Hort. Upande wa kulia wa ukurasa huo kuna maandiko ya New World Translation (chapa ya 1984 iliyosahihishwa na kutiwa habari za sasa). Lakini, kati ya mistari ya maandiko ya Kigiriki, kuna tafsiri nyingine, fasili iliyo halisi sana, ya neno kwa neno ya yale ambayo Kigiriki husema hasa kulingana na maana ya msingi na aina ya sarufi ya kila neno. Hilo huwawezesha hata wanafunzi ambao hawawezi kusoma Kigiriki wapate kujua yale hasa yaliyoko katika maandiko ya awali ya Kigiriki.
Je, kazi hiyo ya New World Translation ingenufaisha tu wale ambao wangeweza kusoma Kiingereza? Katika mahali pengi wamishonari wa Watch Tower walikuwa wakiona vigumu kupata Biblia za lugha za wenyeji za kutosha ili kuzigawanya kwa watu waliotamani kupata nakala za kibinafsi za Neno la Mungu. Katika sehemu fulani za ulimwengu, ilikuwa kawaida kwa wamishonari hao kuwa wagawanyaji wakuu wa Biblia zilizochapwa na sosaiti nyinginezo za Biblia. Lakini hilo halikuwapendeza wafanyakazi wa kidini waliowakilisha sosaiti hizo za Biblia. Isitoshe, baadhi ya Biblia hizo hazikuwa tafsiri zilizo bora zaidi.
Kutafsiri Katika Lugha Nyinginezo
Ule mwaka ambao New World Translation iliyo kamili ilipotokea kwa mara ya kwanza ikiwa katika buku moja, yaani, mwaka 1961, kikundi cha watafsiri wenye ujuzi kilikutana ili kutafsiri maandiko ya Kiingereza katika lugha nyinginezo sita zilizotumiwa sana—Kiholanzi, Kifaransa, Kijerumani, Kiitalia, Kireno, na Kihispania. Kutafsiri tena kutoka Kiingereza, pamoja na kulinganisha na Kiebrania na Kigiriki, kuliwezekana kwa sababu ya uhalisi wa tafsiri ya Kiingereza yenyewe. Watafsiri hao walifanya kazi wakiwa halmashauri ya kimataifa katika kushirikiana na New World Bible Translation Committee, kwenye makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn, New York. Katika 1963 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalichapwa na kutolewa katika lugha zote sita.
Kufikia 1992 New World Translation of the Holy Scriptures iliyo kamili ilipatikana katika lugha 12—Kicheki, Kidenmark, Kiholanzi, Kiingereza, Kifaransa, Kijerumani, Kiitalia, Kijapani, Kireno, Kislovaki, Kihispania, na Kisweden. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalipatikana katika lugha nyingine mbili. Hilo lilimaanisha kwamba tafsiri hiyo ilipatikana katika lugha za kienyeji za watu 1,400,000,000 hivi, au zaidi ya robo ya idadi ya watu wote duniani, na wengi zaidi walikuwa wakinufaika nayo kupitia kutafsiriwa kwa madondoo yayo katika lugha nyinginezo 97 katika Mnara wa Mlinzi. Hata hivyo wale waliosoma lugha hizo 97, walikuwa na hamu ya kupata New World Translation iliyo kamili katika lugha yao wenyewe. Kufikia 1992, tayari mipango ilikuwa ikiendelea ili kutokeza tafsiri hiyo katika lugha 16 kati ya hizo na kukamilisha Maandiko ya Kiebrania katika lugha 2 zilizokuwa na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pekee.
Kwa kuwa uchapaji wa Biblia hizo ulifanywa katika viwanda vya Sosaiti na wafanyakazi wa kujitolea, iliwezekana kuzitoa kwa gharama ya chini. Katika 1972 wakati Shahidi kutoka Austria alipomwonyesha mjalidi vitabu mmoja New World Translation katika Kijerumani na kumwuliza anafikiri hiyo ingegharimuje, mtu huyo alishangaa kujua kwamba mchango uliodokezwa ulikuwa sehemu moja kwa kumi ya bei aliyotaja.
Mifano fulani inaonyesha matokeo ya tafsiri hii. Katika Ufaransa, kwa karne nyingi Kanisa Katoliki lilikuwa limewakataza watu wa kawaida wasiwe na Biblia. Tafsiri za Wakatoliki zilizopatikana zilikuwa zenye gharama kubwa, na ni nyumba chache zilizokuwa nazo. Biblia New World Translation of the Christian Greek Scriptures ilitolewa katika Kifaransa mwaka 1963, ikifuatwa na Biblia yote katika 1974. Kufikia 1992 jumla ya pamoja ya nakala 2,437,711 za New World Translation zilikuwa zimesafirishwa ili zigawanywe katika Ufaransa; na idadi ya Mashahidi wa Yehova katika Ufaransa ikaongezeka kwa asilimia 488 wakati wa kipindi hichohicho, kufikia jumla ya 119,674.
Hali ilikuwa iyo hiyo katika Italia. Kwa muda mrefu watu walikuwa wamekatazwa kuwa na nakala ya Biblia. Baada ya kutolewa kwa chapa ya Kiitalia ya New World Translation hadi kufikia 1992, kulikuwa na nakala 3,597,220 zilizogawanywa; nyingi zazo zikiwa Biblia kamili. Watu walitaka kujichunguzia wenyewe yale yaliyomo katika Neno la Mungu. Kwa kupendeza, wakati wa kipindi hichohicho, idadi ya Mashahidi wa Yehova katika Italia ilipanda sana—kutoka 7,801 hadi 194,013.
Wakati New World Translation of the Christian Greek Scriptures ilipotolewa katika Kireno, kulikuwa na Mashahidi 30,118 tu katika Brazili na 1,798 katika Ureno. Wakati wa miaka iliyofuata, hadi kufikia 1992, jumla ya nakala 213,438 za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na nakala 4,153,738 za Biblia kamili katika Kireno zilipelekwa kwa watu mmoja-mmoja na makutaniko katika nchi hizo. Matokeo yalikuwa nini? Katika Brazili, wasifaji wa Yehova waliongezeka wakawa mara 11 zaidi; na katika Ureno, wakawa mara 22 zaidi. Makumi ya maelfu ya watu ambao hawakuwa wamepata kuwa na Biblia walishukuru kupata moja, na wengine walithamini kuwa na Biblia iliyotumia maneno ambayo wangeweza kuelewa. Wakati New World Translation of the Holy Scriptures—With References ilipotolewa katika Brazili, vyombo vya habari vilisema kwamba hiyo ilikuwa tafsiri iliyo kamili zaidi (yaani, yenye marejezo-vitomeo na vielezi-chini vingi) iliyopatikana nchini. Pia ilisema kwamba uchapaji wa kwanza ulikuwa mkubwa mara kumi zaidi ya chapa nyingi za kitaifa.
Chapa ya Kihispania ya New World Translation of the Christian Greek Scriptures ilitolewa pia katika 1963, ikifuatwa na Biblia kamili katika 1967. Kulikuwa na nakala 527,451 za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zilizochapwa, na baadaye, hadi kufikia 1992, jumla ya nakala 17,445,782 za Biblia kamili katika Kihispania. Hiyo ilitokeza ongezeko lenye kutazamisha la idadi ya wasifaji wa Yehova katika nchi zinazosema Kihispania. Hivyo, kuanzia 1963 hadi 1992, katika nchi ambazo watu wengi husema Kihispania ambapo Mashahidi wa Yehova huendelea na huduma yao, idadi zao zilikua kutoka 82,106 hadi 942,551. Na katika Marekani, mwaka 1992, kulikuwa na Mashahidi wa Yehova wengineo kama 130,224 wenye kusema Kihispania.
Haikuwa katika milki za Jumuiya ya Wakristo tu ambako New World Translation ilipokewa kwa idili. Katika mwaka wa kwanza wa kuchapwa kwa chapa ya Kijapani, ofisi ya tawi ya Japani ilipokea maagizo ya nakala nusu milioni.
Kufikia 1992 kuchapwa kwa New World Translation of the Holy Scriptures iliyo kamili, katika lugha 12 zilizopatikana wakati huo, kulifikia nakala 70,105,258. Zaidi ya hiyo, nakala 8,819,080 za sehemu za tafsiri hiyo zilikuwa zimechapwa.
Kutoa Biblia Katika Namna Nyingi
Kutumiwa kwa kompyuta katika shughuli za Watch Tower Society, kuanzia 1977, kumesaidia katika kutokezwa kwa Biblia, kama vile ambavyo kumesaidia katika njia nyinginezo za shughuli za uchapaji. Imesaidia watafsiri waweze kuwa na upatani zaidi katika kazi yao; pia imefanya iwe rahisi zaidi kuchapa Biblia katika namna mbalimbali.
Baada ya maandiko yote ya Biblia kutiwa ndani ya kompyuta, haikuwa vigumu kutumia mashine ya kupanga chapa kwa kupiga picha kielektroni ili kuchapa maandiko yakiwa katika unamnanamna wa ukubwa na sura. Kwanza, katika 1981, kulitokezwa chapa ya ukubwa wa kawaida katika Kiingereza yenye konkodansi na mambo mengine ya nyongeza yenye kusaidia. Hiyo ndiyo iliyokuwa chapa ya kwanza kuchapwa na Watch Tower Society kwenye matbaa ya ofseti ya web. Baada ya masahihisho kuingizwa katika maandishi yaliyohifadhiwa ndani ya kompyuta, chapa yenye maandishi makubwa ya Kiingereza ilitolewa katika 1984; hiyo ilitia ndani sehemu nyingi muhimu kwa ajili ya utafiti. Chapa ya ukubwa wa kawaida ya Biblia ya Kiingereza iyo hiyo iliyosahihishwa ilitolewa pia mwaka huo; marejezo-vitomeo na konkodansi ilitiwa ndani, lakini si vielezi-chini; na nyongeza yayo ilibuniwa ifae huduma ya shambani badala ya funzo la kina kirefu zaidi. Kisha, kwa manufaa ya wale waliotaka chapa ndogo sana ya mfukoni, hiyo ilitangazwa katika Kiingereza katika 1987. Chapa hizo zote zilitangazwa upesi katika lugha nyinginezo pia.
Kwa kuongezea, uangalifu ulitolewa ili kusaidia wale wenye mahitaji ya pekee. Ili kusaidia wale ambao wangeweza kuona lakini ambao walihitaji maandishi makubwa sana, New World Translation iliyo kamili ya lugha ya Kiingereza katika mabuku manne makubwa ilitangazwa katika 1985. Upesi chapa iyo hiyo ilichapwa katika Kijerumani, Kifaransa, Kihispania, na Kijapani. Kabla ya hapo, katika 1983, New World Translation of the Christian Greek Scriptures, katika mabuku manne, ilikuwa imetolewa katika Braille (chapa ya vipofu) ya Kiingereza cha gredi ya pili. Katika muda wa miaka mingine mitano, New World Translation iliyo kamili ilikuwa imetokezwa katika Braille ya Kiingereza katika mabuku 18.
Je, watu fulani wangesaidiwa ikiwa wangeweza kusikiliza rekodi ya Biblia? Bila shaka. Kwa hiyo Watch Tower Society ilianza kutokeza hiyo pia. Kaseti ya kwanza iliyorekodiwa ilikuwa The Good News According to John, katika Kiingereza, iliyotolewa katika 1978. Baadaye New World Translation yote katika Kiingereza ilifanywa ipatikane katika kaseti 75. Ile iliyoanza ikiwa kazi ndogo upesi ilikua ikawa mradi mkubwa. Upesi, ilipatikana katika lugha nyinginezo. Kufikia 1992 New World Translation, ikiwa yote au kwa sehemu, ilipatikana katika kaseti katika lugha 14. Mwanzoni, kazi ya baadhi ya matawi ilifanywa na kampuni za kibiashara. Hadi kufikia 1992, Watch Tower Society ilikuwa imetokeza kaseti kama hizo zaidi ya 31,000,000 kwa kutumia vifaa vyayo yenyewe.
Manufaa za kaseti za Biblia na njia ambazo kwazo zilitumiwa yalizidi sana matarajio ya awali. Katika sehemu zote za dunia, watu walikuwa wakitumia vinanda vya kaseti. Wengi ambao hawangeweza kusoma walisaidiwa katika njia hiyo kunufaika kibinafsi kutokana na Neno takatifu la Mungu. Wanawake waliweza kusikiliza kaseti walipokuwa wakifanya kazi za nyumbani. Wanaume walizisikiliza kwenye vinanda vya magari yao walipokuwa wakisafiri kwenda kazini. Uwezo wa kufundisha wa Shahidi mmoja-mmoja ulifanywa kuwa bora waliposikiliza Neno la Mungu kwa ukawaida na kutoa uangalifu kwa matamshi ya majina ya Biblia na njia ambayo vifungu vya Maandiko vilisomwa.
Kufikia 1992, chapa mbalimbali za New World Translation zilikuwa zikichapwa kwenye matbaa za Sosaiti katika Amerika Kaskazini na Kusini, Ulaya, na nchi za Mashariki. Jumla ya mabuku 78,924,338 yalikuwa yametokezwa na kufanywa yapatikane ili yagawanywe. Katika Brooklyn pekee, kulikuwa na matbaa kubwa tatu za ofseti ya web zenye mwendo wa kasi zilizotumiwa hasa kwa utokezaji wa Biblia. Kwa ujumla, matbaa hizo zaweza kutokeza Biblia 7,900 kwa saa, na nyakati nyingine zimehitajiwa zifanye kazi kwa wakati wa ziada.
Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova hutolea watu zaidi ya Biblia tu inayoweza kuwekwa tu juu ya rafu. Wao pia hutolea yeyote anayependezwa na Biblia—iwe anapata nakala kutoka kwa Mashahidi wa Yehova au la—funzo la Biblia nyumbani bila malipo. Mafunzo hayo hayaendelei daima. Baadhi ya wanafunzi huthamini kwa moyo yale wanayojifunza, wanakuwa Mashahidi waliobatizwa, na kisha kushiriki katika kufundisha wengine. Baada ya miezi kadhaa, ikiwa mtu hafanyi maendeleo yanayofaa katika kutumia yale ambayo anajifunza, mara nyingi mafunzo hukomeshwa ili kuendelea na watu wengine wanaopendezwa kikweli. Kufikia 1992, Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiandalia watu mmoja-mmoja na wenye nyumba kama 4,278,127 utumishi wa funzo la Biblia nyumbani bila malipo, mara nyingi kila juma.
Hivyo, Mashahidi wa Yehova ni watangazaji na wagawanyaji wa Biblia na ni walimu wa Neno takatifu la Mungu kwa njia isiyopata kufanywa na tengenezo jingine lolote.
[Maelezo ya Chini]
a Kama ilivyoonyeshwa na Watch Tower la Julai 15, 1892 (uku. 210), jina Watch Tower Bible and Tract Society lilikuwa limetumiwa kwa miaka mingi kabla ya jina hilo kusajiliwa kihalali. Trakti iliyochapwa katika 1890 katika ule mfululizo wa trakti za Old Theology ilitambulisha watangazaji kuwa Tower Bible and Tract Society.
b Tafsiri hiyo ilitolewa kwa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania ili ichapwe, pamoja na ombi kwamba majina ya watafsiri yasitangazwe kamwe. Walitaka heshima yote imwendee Yehova Mungu, Mtungaji wa Kimungu wa Neno lake lililopuliziwa.
c Baadhi ya tafsiri za mapema zaidi katika Kiebrania, Kijerumani, na Kiingereza zilirudisha jina la kimungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, pamoja na tafsiri nyingi za wamishonari.
[Sanduku katika ukurasa wa 609]
Tafsiri Mpya
Wakati buku la kwanza la “New World Translation of the Hebrew Scriptures” lilipotangazwa, Alexander Thomson, mhakiki wa Biblia Mwingereza, aliandika: “Tafsiri za awali za Maandiko ya Kiebrania hadi lugha ya Kiingereza ni chache sana. Kwa hiyo inatupatia furaha kubwa kukaribisha kutangazwa kwa sehemu ya kwanza ya New World Translation [ya Maandiko ya Kiebrania], Mwanzo hadi Ruthu. . . . Tafsiri hiyo kwa wazi imefanya jitihada ya pekee ili isomeke kwa urahisi. Hakuna yeyote ambaye angeweza kusema imepungukiwa katika upya na uasili. Matumizi ya maneno hayategemei tafsiri za awali hata kidogo.”—“The Differentiator,” Juni 1954, uku. 131.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 610]
“Maandiko Yenye Msamiati wa Hapohapo”
Katika “The Classical Journal,” Thomas N. Winter wa Chuo Kikuu cha Nebraska aliandika pitio la “The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures” ambayo alisema: “Hiyo ni tafsiri ya mistari kati ya mistari isiyo ya kawaida: uaminifu-maadili wa maandiko unadumishwa, na Kiingereza kinachotokea chini yayo ni maana ya neno la Kigiriki kimsingi. Hivyo sehemu ya mistari kati ya mistari ya kitabu hicho si tafsiri hata kidogo. Maandiko yenye msamiati wa hapohapo waieleza tafsiri hiyo kwa usahihi zaidi. Tafsiri katika Kiingereza safi hutokea katika safu nyembamba kwenye pambizo la upande wa kulia wa kurasa. . . .
“Maandiko hayo yanategemea yale ya Brooke F. Westcott na Fenton J. A. Hort (1881, iliyotokezwa tena), lakini tafsiri iliyofanywa na halmashauri isiyojitambulisha ni ya kisasa kabisa na sahihi kwa upatani.”—Toleo la Aprili-Mei la 1974, kur. 375-376.
[Picha]
Chapa za 1969 na 1985
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 611]
Maoni ya Mwanachuo Mwebrania
Kuhusu “New World Translation,” Profesa Dakt. Benjamin Kedar, mwanachuo Mwebrania katika Israeli, alisema hivi katika 1989: “Katika utafiti wangu wa lugha kuhusu Biblia ya Kiebrania na tafsiri mbalimbali, mara nyingi mimi hurejezea chapa ya Kiingereza ya ile inayoitwa ‘New World Translation.’ Katika kufanya hivyo, mimi huona hisia yangu ikithibitishwa tena na tena kwamba kitabu hicho chaonyesha jitihada ya unyoofu ili kupata uelewevu wa maandiko kwa usahihi kwa kadiri iwezekanavyo. Ikitoa uthibitisho wa utaalamu mkubwa wa lugha ya awali, inatafsiri maneno ya awali katika lugha ya pili kwa njia yenye kueleweka bila kukengeuka isivyo lazima kwenye muundo ule wa Kiebrania. . . . Kila taarifa ya lugha huruhusu nafasi fulani ya kufasiri au kutafsiri. Kwa hiyo utatuzi wa kilugha katika chochote kile waweza kubishaniwa. Lakini sijapata kamwe kugundua katika ‘New World Translation’ nia yoyote yenye upendeleo ya kutia jambo lisilo la kimaandiko.”
[Grafu katika ukurasa wa 613]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Ukuzi wa Mashahidi Tangu Kutangazwa kwa “New World Translation”
Ufaransa
150,000
100,000
50,000
1963 1970 1980 1992
Italia
150,000
100,000
50,000
1963 1970 1980 1992
Ureno na Brazili
300,000
200,000
100,000
1963 1970 1980 1992
Nchi Zenye Kusema Kihispania
900,000
600,000
300,000
1963 1970 1980 1992
[Picha katika ukurasa wa 604]
Tafsiri Chache Kati ya Zile Zilizotumiwa na Wanafunzi wa Biblia wa Ramaniema
Tafsiri halisi ya Young
Tafsiri ya Leeser (Kiebrania kando ya Kiingereza)
“New Testament” ya Tischendorf (yenye fasili tofauti-tofauti kutoka hati za Kigiriki MSS)
Tafsiri ya Murdock (kutoka Kisiria)
“The Emphatic Diaglott” (Kigiriki hadi Kiingereza)
Variorum Bible (yenye fasili mbalimbali za Kiingereza)
“The Newberry Bible” (yenye maandishi ya thamani pambizoni)
[Picha katika ukurasa wa 605]
Utangulizi wa chapa ya Rotherham “New Testament” iliyochapwa kwa ajili ya Watch Tower Society karibu 1890
[Picha katika ukurasa wa 606]
Chapa ya Mistari Sambamba ya Biblia ya Holman, kama ilivyochapwa kwa mpango wa Watch Tower Society katika 1902
[Picha katika ukurasa wa 606]
Chapa ya Watchtower ya “King James Version,” yenye konkodansi iliyobuniwa kipekee (1942)
[Picha katika ukurasa wa 607]
“American Standard Version,” tafsiri inayotumia jina la kimungu, Yehova, mara zaidi ya 6,870; chapa ya Watchtower (1944)
[Picha katika ukurasa wa 607]
Tafsiri ya Byington (1972)
[Picha katika ukurasa wa 608]
“New World Translation,” iliyotolewa kwanza katika Kiingereza katika mabuku sita, kuanzia 1950 hadi 1960; baadaye iliunganishwa katika chapa ya pekee ya wanafunzi
Ilitangazwa ikiwa buku moja lenye kutia mambo yote katika 1961
Chapa ya maandishi makubwa, yenye marejezo kwa ajili ya funzo, ilitangazwa katika 1984
[Picha katika ukurasa wa 612]
“New World Translation” imetolewa katika lugha zaidi kwa kuendelea
[Picha katika ukurasa wa 614]
“New World Translation” katika chapa kubwa sana
. . . katika Braille
. . . katika kaseti
. . . katika disketi za kompyuta