Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 10/15 kur. 5-10
  • Kristo Aliyetundikwa Juu ya Mti, “Nguvu ya Mungu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kristo Aliyetundikwa Juu ya Mti, “Nguvu ya Mungu”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “TWATAKA KUONA ISHARA”
  • ISHARA WALIYOITAKA
  • “UDHAIFU WA MUNGU”
  • MTI WA MATESO HAUKUBATILISHWA
  • Masihi! Njia ya Mungu ya Wokovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Kwa Nini Walimkataa Masihi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • “Tumempata Mesiya”!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Je, Wewe Ungalimtambua Mesiya?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 10/15 kur. 5-10

Kristo Aliyetundikwa Juu ya Mti, “Nguvu ya Mungu”

“Wayahudi wanataka ishara, na Wayunani [Wagiriki] wanatafuta hekima; bali sisi tunamhubiri Kristo [aliyetundikwa juu ya mti] kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa [Wagiriki] ni upuzi.”​—Kor. 1:22, 23.

1. (a) Ni hali gani zilizokuwako katika kundi la Korintho zilizomfanya Paulo atie mkazo juu ya Kristo aliyetundikwa juu ya mti? (b) Ni mambo gani yaliyoonyeshwa na Paulo katika 1 Wakorintho 1:17-25 yanayotupasa sasa?

KUNDI la Korintho ndilo lililoandikiwa maneno hayo na mtume Paulo juu ya “[Kristo aliyetundikwa juu ya mti].” Korintho wa siku za Paulo ulikuwa mji wenye watu wa mataifa mengi, ukiwa na Warumi, Wagiriki, watu wa Mashariki na Wayahudi. Katika kundi la Kikristo lililokuwapo, kulikuwa na mtengano kwa kuwa vikundi mbalimbali vilijiunga na watu mmoja mmoja mashuhuri (hodari). Kwa sababu ya hili, Paulo alisema hivi: “Je! Kristo amegawanyika?” (1 Kor. 1:13) Huenda vilevile ikawa kulikuwa na maelekeo ya wengine wa Wayahudi Wakristo ya kutaka kushikilia mambo fulani ya Torati, au wengine wa mataifa mengine kuvutiwa na njia za usemaji wenye ufasaha mwingi za wanafilosofia Wagiriki. Walakini Injili haikupaswa kuhubiriwa kwa maneno makuu, wala haikupaswa kuchanganywa na hekima ya mapokeo ya kidini wala na makisio ya kifilosofia. Vyo vyote ilivyokuwa huko Korintho, mtume Paulo aliona uhitaji wa kukazia sana kuhubiri tu “[Kristo aliyetundikwa juu ya mti].” Maneno yake katika 1 Wakorintho 1:17-25 yalifanya hivyo, nayo ndiyo msingi wa makala hii na ile itakayofuata. Aliandika hivi:

“Maana Kristo [alinituma]. . . niihubiri Habari Njema; wala si kwa hekima ya maneno, [mti wa mateso] wa Kristo usije ukabatilika. Kwa sababu neno la [mti wa mateso] kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu. Kwa kuwa imeandikwa, Nitaihubiri hekima yao wenye hekima, na akili zao wenye akili nitazikataa. Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mleta hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu? Kwa maana katika hekima ya Mungu, dunia isipopata kumjua Mungu kwa hekima yake, Mungu alipenda kuwaokoa [waaminio] kwa upuzi wa lile neno linalohubiriwa. Kwa sababu Wayahudi wanataka ishara, na [Wagiriki] wanatafuta hekima; bali sisi tunamhubiri Krlsto, [aliyetundikwa juu ya mti]; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa [Wagiriki] ni upuzi; bali kwao waitwao, Wayahudi kwa [Wagiriki], ni Kristo nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu. Kwa sababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una nguvu zaidi ya wanadamu.”

2. Ni jambo gani lililoonyesha kutiwa mafuta kwa Yesu, naye alishiriki katika kazi gani?

2 Kama inavyoonyeshwa na maneno hayo yanayotajwa hapo, ‘Wayahudi walitaka ishara.’ Je! ishara za kutosha hazikutolewa na Yesu? Yeye alikuja katika mto Yordani katika mwaka 29 W.K. akajitolea abatizwe. Alipokuwa akitoka majini, roho ya Mungu mfano wa hua ilishuka juu yake, nayo sauti ya Yehova kutoka mbinguni ikasema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.” Baada ya kukaa siku 40 jangwani, na kushinda majaribu ya Ibilisi, Yesu alianza kuuhubiri ufalme na kufanya miujiza. Mathayo anaandika juu ya matokeo ya utendaji huu: “Naye alikuwa akizunguka katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri Habari Njema ya ufalme, na kuponya ugonjwa na udhaifu wa kila namna katika watu. Na habari zake zikaenea katika Shamu yote; wakamletea wote waliokuwa hawawezi walioshikwa na maradhi mbalimbali na mateso, wenye pepo, na wenye kifafa, na wenye kupooza; akawaponya. Na makutano mengi wakamfuata, kutoka Galilaya, na Dekapoli, na Yerusalemu, na Uyahudi, na ng’ambo ya Yordani.”​—Mt. 3:13-17; 4:23-25.

“TWATAKA KUONA ISHARA”

3. Ni ishara gani alizozifanya Yesu, hata hivyo waandishi walimwuliza nini?

3 Watu walishangazwa sana na miujiza yake hivi kwamba walijua kwamba yeye ndiye Masihi aliyeahidiwa. “Atakapokuja Kristo,” wakauliza, “je! atafanya ishara nyingi zaidi kuliko hizi alizozifanya [mtu] huyu?” Yesu aligeuza maji yakawa divai, akatembea juu ya maji, akatuliza upepo pamoja na bahari zilizokuwa zikivuma, akalisha maelfu kwa mwujiza kwa mikate michache na samaki wachache, akaponya wagonjwa, akafanya vilema watembee, akafumbua macho ya vipofu, akaponya wenye ukoma na hata akafufua wafu. Ni nani angeuliza zaidi ya hayo? Viongozi wa dini wa taifa la Kiyahudi wangefanya hivyo na walifanya hivyo. Walikuwa wamejionea wenyewe kwa macho yao ishara hizi za Yesu, na walikuwa wamepokea ripoti ya nyingine nyingi. Hata hivyo, waandishi na Mafarisayo walimjia Yesu na ulizo linaloelekea kuchukiza: “Mwalimu, twataka kuona ishara kwako.”​—Yohana 7:31; Mt. 12:38.

4, 5. Kwa sababu ya kazi yao, waandishi hawa pamoja na Mafarisayo walipaswa kujua mambo gani ambayo yalipaswa kuwasadikisha kwamba alikuwa Masihi?

4 Viongozi hawa wa kidini walipaswa kuwa watu wa mwisho kutaka ushuhuda zaidi kwa kuonyesha kwamba Yesu ndiye Masihi! Waandishi walitumia maisha yao yote wakijifunza Maandiko ya Kiebrania. Waliyachunguza kwa makini sana, na waliyabishania sana kati yao wenyewe wakitafuta uamuzi unaofaa juu ya matumizi yake. Walikuwa wamekusanya na kupanga mapokeo mengi yaliyosemekana kuwa yalieleza na kufanya Maandiko ya Kiebrania kufahamika vyepesi hata katika mambo yaliyo madogo zaidi. Na katika kuchunguza kwao bila shaka walijua juu ya unabii uliotabiri kuja kwa Masihi aliyeahidiwa.

5 Walijua, au sivyo, kwamba Masihi angekuwa wa kabila la Yuda, wa ukoo wa Daudi, azaliwe Bethlehemu, kwamba kuja kwake kungetangazwa na mmoja aliyefananishwa na Eliya, kwamba angechukua magonjwa na maumivu ya Wayahudi? Zaidi ya unabii 300 katika Maandiko ya Kiebrania juu ya kuja kwa mara ya kwanza kwa Masihi ulitimizwa katika Yesu​—mwingi wa huo unabii ukiwa umekwisha kutimizwa walipokuwa wakija kutaka ishara kwa Yesu. Yesu aliwakumbusha kwamba kwa sababu walikuwa wakijifunza Maandiko walipaswa kujua habari zake: “Mwayachunguza maandiko, kwa sababu mnadhani kwamba ninyi mna uzima wa milele ndani yake; na hayo ndiyo yanayonishuhudia.”​—Yohana 5:29.

6. Yesu alijibuje ulizo lao, na kwa sababu gani si kwa kudhihaki?

6 Hivyo, je! Mwana wa Mungu aliwatolea jibu la kuwanyamazisha waliposema: “Twataka kuona ishara kwako?” Na tuone: “Akajibu, akawaambia, Kizazi kibaya na cha zinaa chatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya nabii Yona. Kwani kama vile Yona alivyokuwa siku tatu mchana na usiku katika tumbo la nyangumi, hivyo ndivyo Mwana wa Adamu atakavyokuwa siku tatu mchana na usiku katika moyo wa nchi.” (Mt. 12:38-40) Hapana, Yesu hakuwakemea kwa sababu walidharau ishara nyingi za mwujiza zilizokuwa zimetolewa, au kwa sababu ya kushindwa kuhakikishwa na unabii wa Kimasihi uliokuwa umetimizwa katika yeye. Yeye aliwaelewa, tamaa yao, makosa yao, na jibu lake lililingana na hali hiyo.

ISHARA WALIYOITAKA

7, 8. Wayahudi walitaka kuona ishara gani, lakini ni ishara gani peke yake ambayo wangeona, na kwa sababu gani?

7 Yesu alijua ishara waliyotaka kuona. Habari zake zimeandikwa katika Danieli 7:13, 14: “Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye. Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo haitapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa.”

8 Hii ilikuwa ikionyesha kuja kwa mara ya pili kwa Masihi, wakati ambapo ufalme wa Kimasihi utakapochukua mahali pa serikali zote za wanadamu zenye uonezi na kuletea waabudu wa Yehova amani yenye kuendelea pamoja na utulivu duniani mwote. Watawala wa Kiyahudi walitaka Yesu aje na mamlaka ya ufalme, avunje-vunje nira zenye uonezi za Rumi, na kuwatukuza na uwezo wa kisiasa. Walikuwa wakijitanguliza mbele ya Yehova. Huku kulikuwa kuja kwa kwanza kwa Masihi, wakati ambapo angeteswa na kufa kama ukombozi akae kaburini sehemu ya siku tatu. Ishara hiyo ya kuja kwa mara ya kwanza ndiyo peke yake wangepata.

9. Wayahudi wa siku za Yesu walishindwa kufahamu jambo gani, na ni tamaa gani kubwa iliyowapofusha wasimkubali Yesu kuwa Masihi?

9 Si ishara peke yake ambayo Wayahudi hao walikosa kuona kutoka kwa Masihi; bali vilevile walipata kitu ambacho kiliwakwaza kabisa, yaani, Masihi aliyetundikwa juu ya mti! Paulo aliandika hivi: “Wayahudi wanataka ishara, na [Wagiriki] wanatafuta hekima; bali sisi tunamhubiri Kristo, [aliyetundikwa juu ya mti]; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa [Wagiriki] ni upuzi.” (1 Kor. 1:22, 23) Jambo lililowaangusha Wayahudi ni kushindwa kufahamu kwamba Masihi angekuja mara mbili. Kulikuwa na namna mbili za unabii katika Maandiko ya Kiebrania juu ya Masihi: namna moja juu ya kuja kwake kwa mara ya kwanza, na namna ya pili juu ya kuja kwake kwa mara ya pili. (Tazama orodha katika ukurasa wa 1148 katika kitabu Aid to Bible Understanding juu ya unabii wa kuja kwa mara ya kwanza na utimizo wake; mchache wa ule unaohusu kuja kwa mara ya pili ni Danieli 7:13, 14; 2:35, 44; Zaburi 2:1-9; 110:1-6.) Walakini, Wayahudi walishindwa kufahamu mara hizi mbili za kuja kwake. Wao waliamini kuja kwake mara moja tu. Wakitazamia kwa shauku nyingi sana Masihi wao aje akiwa na uwezo avunje nira za Warumi, walikosa kufahamu kwamba Masihi angekuja apate kutaabishwa, kuteswa, kukataliwa na kutundikwa juu ya mti. Kwa kweli, maoni yao juu ya Masihi yalikuwa yenye makosa. Unabii mwingi wa Kimasihi hawakuuona kuwa hivyo. Wayahudi wengine hata hawakuamini kwamba Masihi angekuja kama mtu. Wengine kwa sababu ya choyo hawakutaka aje ili Rumi isiwe na uadui kwa sababu yake. (Yohana 11:47, 48) Walakini, wengi walitaka aje akiwa mpiga vita awaokoe na Rumi.

“UDHAIFU WA MUNGU”

10. (a) Wayahudi walimwona Yesu kuwa “udhaifu wa Mungu” kwa sababu gani, naye alikuwa tofauti namna gani na masihi wa uongo wa karne ya kwanza W.K.? (b) Kama inavyoonyeshwa na The Interpreter’s Bible, ni hali gani iliyokuwako Palestina katika wakati huo iliyomfanya Yesu asikubaliwe na Wayahudi?

10 Yesu huyu alikuwa dhaifu sana machoni pao​—dhaifu sana asiyeweza kuwatimizia matumaini yao ya masihi ambaye angeponda Milki ya Kirumi. Je! yeye hakusema kwamba ufalme wake si wa ulimwengu huu na kwamba watumishi wake hawangepigana? Yeye alikataa kabisa ufalme ulipotolewa kwake. Alishauri ugeuze upande mwingine wa shavu! Walikuwa wakitazamia Masihi wakati huu​—lakini si huyu! (Yohana 18:36; 6:15; Mt. 5:39; Luka 3:15) Kitabu kiitwacho Book of Jewish Knowledge, chini ya “Masihi,” kinasema kwamba walikuwako watu kadha katika karne ya kwanza W.K. waliodai kuwa ndio Masihi, kisha kinaongeza hivi: “Sasa jambo lisilo la kawaida juu ya hawa waliodai kuwa Masihi lilikuwa kwamba kila mmoja wao alikuwa kichocheo cha uasi wa Wayahudi juu ya utawala wa Kirumi. Tofauti na alivyokuwa Yesu, . . . ‘masihi’ wengine wa wakati huo, wote, walikuwa wachochezi wapiga vita na watukuzaji wa taifa.” Kushindwa huku kulikotangulia kutajwa kwa Yesu kujionyesha kuwa Masihi mwenye nguvu lilikuwa jambo baya sana machoni pao, lakini alipokufa mwishowe kifo chenye aibu sana juu ya mti wa mateso hilo lilimfanya akataliwe kabisa! Kwa hiyo, katika 1 Wakorintho 1:25 mtume Paulo alionyesha kwamba Wayahudi walimwona [“Kristo aliyetundikwa juu ya mti”] kama “udhaifu [“kitu dhaifu cha,” NW] wa Mungu,” na walikwazwa kabisa. Juu ya hili kitabu The Interpreter’s Bible, Vol. 10, uku. 29 kinaeleza hivi:

“Matumaini ya kidini ya Wayahudi katika siku za Paulo yalikuwa juu ya msingi wa matazamio ya ufunuo wa ghafula, na wenye msiba wa kukombolewa na uonezi wa Kirumi: wao walitazamia mkombozi ambaye angefanya taifa hilo kuwa kuu kati ya mataifa ya ulimwengu. Mojawapo la [mambo] yaliyowafanya kuchukizwa sana na Yesu katika siku zake katika mwili ni kukataa kwake kulipa taifa hilo uongozi wa kivita, kama walivyofanya Wamakabayo. Katika siku za Paulo Palestina ilikuwa kama moto uliofungiwa ndani. Mawakili wa Rumi waliweza kuzima miali [ya moto] wa uasi uliokuwa ukilipuka mahali pale; lakini moto uliokuwa umefungiwa ndani lilikuwa jambo tofauti. Kama Yesu angetoa amri alipokuwa anapendwa sana na watu wengi, panga elfu nyingi zingechomozwa kutoka katika ala [mifuko] zao, na Rumi ingepatwa na shida ya kuzuia mlipuko wa mawazo ya kidini na utukuzo wa kitaifa wa Kiyahudi uliokuwa umefungiwa ndani yao. Kwa watu ambao fikira na roho zao zilikuwa zikiwashwa na mawazo kama hayo pamoja na matumaini ya ufunuo kama huo ishara ya ‘Kristo aliyesulubiwa’ ilikuwa kosa lenye kuchukiza sana. Kwao neno la msalaba lilikuwa jambo la kuchukiza sana. Hawangelishiriki hata kidogo.”

11. Ni jambo gani ambalo hata wanafunzi walioshirikiana sana na Yesu walishindwa kufahamu, na kwa sababu gani unajibu hivyo?

11 Hata wale walioshirikiana sana na Kristo Yesu hawakufahamu juu ya kuja kwa Masihi mara mbili mpaka baada ya muda fulani, na kwamba kuja huku kwa mara ya kwanza kungemalizika kwa ‘kutundikwa mtini kwa Kristo.’ Akiwa gerezani, Yohana Mbatizaji alisikia juu ya ishara za miujiza ya Yesu lakini inaelekea alitazamia zaidi, kwa kuwa alituma ulizo hili kwa Yesu: “Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine?” Petro alikubali kwamba Yesu ndiye Masihi, hata hivyo yeye hakufahamu ishara zilizotimiza kuja kwake kwa mara ya kwanza. (Mt. 16:16, 21-23) Hata baada ya kufa na kufufuka kwake Yesu, wanafunzi wake bado walikuwa wanatazamia kusimamishwa kwa ufalme wa kidunia katika kuja huku kwa mara ya kwanza. Waliuliza: “Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?”​—Mt. 11:2, 3.

MTI WA MATESO HAUKUBATILISHWA

12. Mwishowe, wengine wa viongozi wa kidini wa kiyahudi walijaribuje kuondoa tatizo la namna hizo mbili za unabii juu ya kuja huku kwa mara mbili?

12 Baada ya kumiminwa kwa roho takatifu katika Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wa Yesu walifahamu juu ya kuja huku kwa mara mbili na walihubiri kila mahali “yale ambayo manabii na Musa waliyasema, kwamba yatakuwa; ya kwamba Kristo hana budi kuteswa.” (Matendo 26:22, 23) Sababu zilizotolewa na Wakristo kutoka katika Maandiko ya Kiebrania pamoja na matumaini yaliyoharibika ya Wayahudi yaliwasukuma wanachuo wa Kiyahudi wa wakati wa baadaye kurudia kuufasiri unabii wa Kimasihi. Kwa mfano, Danieli 7:13 lilisema kwamba Masihi angekuja katika mawingu ya mbingu, lakini Zekaria 9:9 lilisema kwamba angekuja kwa unyenyekevu akipanda mwanapunda. Wazo moja linalopatikana katika kitabu cha mafundisho cha Wayahudi (Talmud) lilijaribu kuondoa tatizo hili kwa kufundisha kuja kwa mara moja tu​—kwamba ikiwa Israeli wangekuwa wenye kustahili, Masihi angekuja katika mawingu, lakini ikiwa Israeli wangekuwa wasiostahili angekuja akipanda mwanapunda. (Babylonian Talmud, Sanhedrin, 98a) Wazo jingine lilikubali namna zote mbili za unabii, ule wa kuja kwa mara ya kwanza na kwa mara ya pili, likasema kwamba kungekuwa na masihi wawili, mmoja mwana wa Yusufu na mwingine mwana wa Daudi, na katika wote wawili namna zote mbili za unabii zingetimizwa. (Edersheim’s Life and Times of Jesus the Messiah, Vol. II, kur. 434, 435) Walakini, wote wawili walipaswa kuja wakati mmoja.

13. (a) Ni imani gani za Wayahudi zilizowafanya wamkatae Yesu kama Masihi? (b) Imani hizi za Wayahudi zilibatilishaje mti wa mateso?

13 Hata hivyo, walishikilia kwamba Yesu hangekuwa mmojawapo wa masihi hao. Kwa kuwa Yesu hakufuata mapokeo ya waandishi, kitabu chao cha mafundisho kinasema kwamba kuyapinga kunastahili adhabu kubwa kuliko hata kuyapinga Maandiko ya Kiebrania. Vilevile, Yesu alisema kwamba angetimiza Torati ya Musa​—⁠hivyo aimalize. Walakini Wayahudi waliiona kuwa ni ya kuendelea milele, bila kufutwa milele. Zaidi ya hayo, Wayahudi waliamini kwamba wao hawakuhitaji Masihi ili waokolewe. Wao wangeingia katika ufalme katika njia tatu: Kwa kufanya matendo ya Torati, kwa kuwasaidia maskini, kwa kuwa na Ibrahimu kama baba yao. (Mt. 3:7-10; Rum. 3:20; 4:2, 3; 9:31, 32) Hekima kama hiyo ya waandishi ingebatilisha mti wa mateso, usihitajiwe kwa kuleta wokovu. Paulo alikuwa akifikiria hekima hii ya uongo alipokuwa akitofautisha ubatili wake na nguvu za Mungu, Kristo aliyetundikwa juu ya mti. Yeye hakutangaza “hekima ya maneno [yao]” kuwa “Habari Njema” “[mti wa mateso] wa Kristo usije ukabatilika, kwa sababu neno la [mti wa mateso] kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu.”​—1 Kor. 1:17, 18.

14. (a) Ni nani waliomdhihaki Yesu, na kwa maneno gani? (b) Matukio hayo ya wakati huo yalitoa uhakikisho gani?

14 Namna gani kama Yesu hakuenda kama kondoo machinjoni, mwenye taabu, mwenye kudharauliwa, asiyependwa, aliyekataliwa? (Isa. 53:1-7) Namna gani kama alionekana kuwa dhaifu asiyeweza kitu alipokuwa akining’inia juu ya mti wa mateso, wengine walipokuwa wakimdhihaki: “Ahaa! wewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga katika siku tatu jiponye nafsi yako, ushuke [juu ya mti wa mateso].” (Marko 15:29, 30) “Kadhalika na wale wakuu wa makuhani wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe.” (Mt. 27:41, 42) Matukio haya yalihakikisha kwamba Yesu alikuwa Masihi, badala ya kumwondolea haki ya kuwa Masihi.​—Zab. 118:22; Isa. 8:14; 28:16; 1 Pet. 2:4-8.

15. “Kristo [aliyetundikwa juu ya mti]” alionwaje na wale wanaopotea na wale wanaookolewa, na ni jambo gani linaloendelea kuwa la kweli ingawa kuwe na dhihaka za wenye kudhihaki?

15 Paulo ameazimia akazie mpango wa ukombozi wa Yehova kama njia peke yake ya kupatia wokovu. Wayahudi wanaweza kutaka ishara nao Wagiriki wanaweza kutamani sana hekima, lakini Paulo atahubiri “[Kristo aliyetundikwa juu ya mti],” hata ingawa Wayahudi watakwazwa nao Wagiriki wauone kuwa upumbavu​—“bali kwao waitwao, Wayahudi kwa [Wagiriki], ni Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu. Kwa sababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una nguvu zaidi ya wanadamu.” (1 Kor. 1:22-25) Waache Wayahudi na Wagiriki wamwone “[Kristo aliyetundikwa juu ya mti]” kuwa udhaifu na upumbavu; hata hivyo bado ni jambo lenye nguvu zaidi na lenye hekima zaidi ya mapokeo ya Kiyahudi na filosofia za Wagiriki. Sababu zaidi zinapatikana katika makala inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Ingawa Yesu alitembea juu ya maji na kufanya miujiza mingine mingi, viongozi wa kidini wa Kiyahudi walitaka “ishara”​—ushuhuda zaidi wa kuonyesha kwamba yeye ndiye aliyekuwa Masihi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki