Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 11/15 kur. 28-31
  • Je, Wewe Ungalimtambua Mesiya?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Wewe Ungalimtambua Mesiya?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Twataka Kuona Ishara Kwako”
  • “Wapenda Fedha”
  • “Kuhofu Wayahudi”
  • Je, kwa Kweli Wewe Unamtambua Mesiya?
  • Masihi! Njia ya Mungu ya Wokovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Kwa Nini Walimkataa Masihi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • “Tumempata Mesiya”!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Yesu Kristo—Ufunguo Uongozao Kwenye Ujuzi Juu ya Mungu
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 11/15 kur. 28-31

Je, Wewe Ungalimtambua Mesiya?

YESU KRISTO alitumia miaka mitatu u nusu akihubiri Neno la Mungu miongoni mwa Waisraeli. Lakini kufikia mwisho wa huduma yake ya kidunia, walio wengi wa watu walioishi siku yake walikuwa wamemkataa kuwa si Mesiya, au “Mtiwa-Mafuta” aliyeahidiwa wa Mungu. Kwa nini?

Biblia hutusaidia kutambua sababu kadha wa kadha zilizowafanya Wayahudi wa karne ya kwanza wasimtambue Yesu kuwa Mesiya. Sababu tatu kati yazo huwazuia watu wengi wasitambue wadhifa wa Yesu wa kisasa akiwa Mfalme wa Kimesiya anayetawala.

“Twataka Kuona Ishara Kwako”

Sababu moja iliyowafanya Wayahudi wa karne ya kwanza wasimtambue Mesiya ni kule kukataa kwao kukubali ishara za Kimaandiko zilizoelekeza kwenye Umesiya wake. Pindi kwa pindi, watu waliomsikiliza Yesu walidai kwamba afanye ishara ili kuthibitisha kwamba alitoka kwa Mungu. Mathalani, Mathayo 12:38 laripoti kwamba baadhi ya waandishi na Mafarisayo walisema hivi: “Mwalimu, twataka kuona ishara kwako.” Je, Yesu hakuwa amewaonyesha ishara mbalimbali tayari? Bila shaka alikuwa amewaonyesha.

Kufikia wakati huo Yesu alikuwa tayari amefanya miujiza kadha wa kadha. Alikuwa amegeuza maji yawe divai, alikuwa amemponya mvulana mahututi, alikuwa amemponya mama-mkwe wa Petro, alikuwa amemfanya mtu mwenye ukoma kuwa safi, alikuwa amemwezesha mtu aliyepooza kutembea, alikuwa amerudisha afya ya mwanamume aliyekuwa amekuwa mgonjwa kwa miaka 38, alikuwa ameurudisha mkono ulionyauka wa mtu kwenye kawaida yao, alikuwa amewatuliza watu wengi kutoka katika magonjwa yao yenye kutia kihoro, alikuwa amemponya mtumwa wa ofisa wa kijeshi, alikuwa amemrudisha mwana wa mjane kutoka kwa wafu, na alikuwa ameponya mtu aliye kipofu na bubu. Miujiza hiyo ilikuwa imetukia Kana, Kapernaumu, Yerusalemu, na Naini. Zaidi, habari juu ya miujiza hiyo ilikuwa imeenea kotekote katika Yudea na nchi yenye kuizunguka.—Yohana 2:1-12; 4:46-54; Mathayo 8:14-17; 8:1-4; 9:1-8; Yohana 5:1-9; Mathayo 12:9-14; Marko 3:7-12; Luka 7:1-10; 7:11-17; Mathayo 12:22.

Kwa wazi, kulikuwa na ishara za kutosha za kuthibitisha kwamba Yesu alikuwa Mesiya. Ingawa alifanya ishara nyingi sana mbele ya watu, hawakumwamini. Wale walioona ithibati ya kwamba Yesu alitumwa na Mungu lakini hawakumtambua kuwa Mesiya walikuwa vipofu kiroho. Mioyo yao ilikuwa migumu na haikuruhusu kweli ipenye.—Yohana 12:37-41.

Namna gani siku yetu? Watu fulani hupiga mbiu hivi, “Mimi huamini tu kile nikionacho kwa macho yangu mwenyewe.” Lakini je, kwa kweli huo ni mwendo wenye hekima wa kufuata? Unabii wa Biblia huonyesha kwamba tayari Yesu ametawazwa kuwa Mfalme wa kimbingu katika Ufalme wa Kimesiya. Kwa kuwa haonekani, twahitaji ishara ya kutusaidia kutambua utawala wake, uliotia alama mwanzo wa siku za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo. Je, wewe waitambua hiyo ishara?—Mathayo 24:3.

Kulingana na Biblia, mwanzo wa utawala wa Kristo akiwa Mfalme wa Kimesiya ungetiwa alama na vita, matetemeko ya dunia, upungufu wa chakula, na magonjwa ya kuambukiza, kwa kiwango kisicho na kifani. Katika “siku za mwisho,” mahusiano ya kibinadamu yangekuwa na sifa ya ubinafsi, pupa, na ukosefu wa kujizuia. (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:6, 7; Luka 21:10, 11) Zaidi ya ithibati ya kikronolojia, zaidi ya mambo 20 tofauti-tofauti huelekeza kwenye mwaka wa 1914 kuwa mwanzo wa utawala wa Mesiya.—Ona Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1993, ukurasa 5.

“Wapenda Fedha”

Ufuatiaji wa vitu vya kimwili ulikuwa sababu nyingine iliyowafanya Wayahudi wamkatae Yesu kuwa Mesiya. Kuupa utajiri umaana sana kuliwazuia wasimfuate Yesu. Mathalani, Mafarisayo walijulikana kuwa “wapenda fedha.” (Luka 16:14) Fikiria kisa cha mtawala mchanga fulani mwenye utajiri aliyemfikia Yesu na kumuuliza jinsi ya kupata uhai udumuo milele. “Zishike amri,” ndilo lililokuwa jibu la Yesu. “Haya yote nimeyashika; nimepungukiwa na nini tena?” akauliza yule kijana, yaonekana akihisi kwamba mengi zaidi ya kushika sheria fulani yalihitajiwa. “Ukauze ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate,” Yesu akamwambia. Ni fursa iliyoje—kuwa mwanafunzi wa Mesiya! Hata hivyo huyo mtawala akageukia mbali akiwa ametiwa kihoro. Kwa nini? Kwa sababu hazina duniani zilikuwa za maana kwake kuliko hazina mbinguni.—Mathayo 19:16-22.

Hali haikubadilika. Kuwa mfuasi wa kweli wa Mfalme wa Kimesiya humaanisha kutanguliza masilahi ya kiroho mbele ya kila kitu kingine chochote kile, kutia na mali za kidunia. Kwa wowote wale walio na mtazamo wa kufuatia vitu vya kimwili, huo ni mwito wa ushindani. Kwa kielelezo, wenzi wa ndoa wamishonari katika nchi moja ya Mashariki walizungumza na mwanamke juu ya Biblia. Wakiwa wanaamini kwamba angependa kujifunza zaidi juu ya Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo, wenzi hao wa ndoa walimtolea Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Aliitikiaje? “Je, magazeti haya yatanisaidia kuchuma fedha zaidi?” akauliza. Huyo mwanamke alipendezwa zaidi na vitu vya kimwili kuliko mambo ya kiroho.

Wenzi wa ndoa ao hao walijifunza Biblia pamoja na kijana aliyeanza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. “Unapoteza wakati wako,” wazazi wake wakamwambia. “Wapaswa kupata kazi nyingine wakati wa jioni na kuchuma fedha zaidi.” Inasikitisha kama nini wazazi wawatiapo moyo watoto wao watangulize vitu vya kimwili mbele ya kujifunza juu ya Mfalme wa Kimesiya! “Hata kwa utajiri wake wote mtawala hawezi kununua miaka elfu kumi ya uhai,” yasema mithali ya Kichina.

Wengi sasa wanatambua kwamba kujifunza juu ya Mfalme wa Kimesiya na kumfuata hakuruhusu upendo wa fedha. Shahidi wa Yehova aliyekuwa na biashara yake mwenyewe yenye machumo ya juu, alisema hivi: “Kuwa na fedha nyingi kwafurahisha lakini si kwa lazima. Fedha sizo zimfanyazo mtu kuwa na furaha.” Yeye sasa ni mshiriki wa familia ya Betheli katika ofisi ya tawi ya Watch Tower Society huko Ulaya.

“Kuhofu Wayahudi”

Kuhofu mwanadamu ni sababu nyingine iliyowafanya Wayahudi wasimkubali Yesu kuwa Mesiya. Kukubali waziwazi Umesiya wake kulimaanisha kuhatarisha sifa yao. Kwa wengine hilo lilikuwa gharama kubwa. Fikiria Nikodemo, mshiriki wa mahakama kuu ya Kiyahudi iitwayo Sanhedrini. Akiwa amevutiwa na ishara na mafundisho ya Yesu, alikiri hivi: “Rabi, twajua ya kuwa u mwalimu, umetoka kwa Mungu; kwa maana hakuna mtu awezaye kuzifanya ishara hizi uzifanyazo wewe, isipokuwa Mungu yu pamoja naye.” Hata hivyo Nikodemo alimtembelea Yesu wakati wa usiku, labda akiepuka kutambuliwa na Wayahudi wengine.—Yohana 3:1, 2.

Kwa walio wengi waliomsikia Yesu akisema, kibali cha wanadamu kilikuwa cha maana kuliko kile cha Mungu. (Yohana 5:44) Yesu alipokuwa Yerusalemu kwa ajili ya Msherehekeo wa Vibanda katika 32 W.K., “kulikuwako maongezi mengi ya kunong’oneza juu yake miongoni mwa umati.” Hakuna aliyesema juu ya Yesu hadharani “kwa sababu ya kuwahofu Wayahudi.” (Yohana 7:10-13, NW) Hata wazazi wa mtu aliyeponywa upofu na Yesu hawakuwa tayari kuukubali muujiza huo kuwa watoka kwa mwakilishi wa Mungu. Wao pia walikuwa “wakihofu Wayahudi.”—Yohana 9:13-23, NW.

Leo, watu fulani hutambua kwamba Yesu sasa anatawala akiwa Mfalme wa Kimesiya mbinguni, lakini wanaogopa kukubali hilo hadharani. Kwao kupoteza msimamo wao pamoja na wengine ni gharama kubwa. Mathalani, katika Ujerumani, Shahidi wa Yehova alikuwa na mazungumzo ya Biblia pamoja na mtu aliyekiri hivi: “Kile ambacho nyinyi Mashahidi huhubiri juu ya Biblia ni kweli. Lakini nikiwa Shahidi leo, kufikia kesho kila mtu atajua juu ya hilo. Watanifikiriaje kazini, katika ujirani, na katika kile kilabu ambacho familia yangu na mimi ni washiriki wacho? Singeweza kuvumilia hilo.”

Ni nini husababisha hali ya kuhofu wanadamu? Kiburi, kupenda umaarufu miongoni mwa familia na marafiki, kuogopa dhihaka na aibu, kuhangaishwa juu ya kuwa tofauti na watu walio wengi. Hisia hizo huthibitika kuwa jaribu hasa kwa wale wanaoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kwa kielelezo, mwanamke kijana mmoja alisisimuka kujifunza juu ya Paradiso ambayo Ufalme wa Kimesiya utatokeza duniani chini ya utawala wa Yesu Kristo. Lakini alikuwa mpenda disko sana, na hali ya kuhofu wanadamu ilimzuia asizungumze na wengine juu ya tumaini hilo. Mwishowe, alipata ujasiri wa kuzungumza kwa uhuru juu ya Biblia. Marafiki wake wa disko wakamkataa, lakini mume wake na wazazi wake wakaonyesha kupendezwa. Hatimaye, mwanamke huyo na mama yake wakabatizwa, na mume wake na baba yake wakaanza kujifunza Biblia. Ni thawabu iliyoje kwa sababu ya kushinda hali ya kuhofu mwanadamu!

Je, kwa Kweli Wewe Unamtambua Mesiya?

Yesu alipokuwa akifa kwenye mti wa mateso, baadhi ya wanafunzi wake walikuwapo. Walikuwa wamemtambua kuwa Mesiya aliyetabiriwa. Watawala Wayahudi walikuwapo pia, ambao kitamathali, walikuwa bado wakidai ishara. “Na ajiokoe mwenyewe, kama ndiye Kristo [au Mesiya] wa Mungu, mteule wake.” (Luka 23:35) Je, wasingeacha kamwe kuomba ishara? Yesu alikuwa amefanya miujiza chungu nzima. Kwa kuongezea, kuzaliwa kwake, huduma yake, kesi yake, kuuawa kwake na ufufuo wake, ulitimiza unabii mwingi wa Maandiko ya Kiebrania.—Ona “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa,” kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., kurasa 343-344.

Wapita njia walimtukana Yesu, wakiwa wamekataa uthibitisho wa Umesiya wake. (Mathayo 27:39, 40) Kwa kufuatia vitu vya kimwili, askari-jeshi waligawana mavazi ya Yesu miongoni mwao wenyewe, wakipigia kura vazi lake la ndani. (Yohana 19:23, 24) Hali ya kuhofu mwanadamu ilikuwa na fungu layo katika visa fulani. Mathalani, fikiria Yosefu wa Arimathea, mshiriki wa Sanhedrini. Alikuwa “mwanafunzi wa Yesu, (lakini kwa siri, kwa hofu ya Wayahudi).” Baada ya kifo cha Mesiya, Yosefu na Nikodemo waliushughulikia mwili wa Yesu. Hivyo Yosefu akashinda hali ya kuhofu kwake wanadamu.—Yohana 19:38-40.

Ikiwa ungalikuwa ukiishi katika karne ya kwanza, je, wewe ungalimtambua Yesu kuwa Mesiya? Kufanya hivyo kungalitaka kwamba ukubali uthibitisho wa Kimaandiko, ukatae fikira za kufuatia vitu vya kimwili, na usishindwe na hali ya kuhofu wanadamu. Katika siku hizi za mwisho, kila mmoja wetu apaswa kujiuliza mwenyewe, ‘Je, mimi namtambua Yesu sasa kuwa Mfalme wa Kimesiya wa kimbingu?’ Karibuni atatwaa shughuli za dunia. Hilo litukiapo, je, wewe utakuwa miongoni mwa wale ambao kwa kweli humtambua Yesu Kristo kuwa Mesiya aliyeahidiwa?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Usiupuuze kamwe kimakusudi uthibitisho wa kwamba Yesu ndiye Mfalme wa Kimesiya

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kujifunza juu ya Mesiya mara nyingi humaanisha kushinda hofu ya yale ambayo wengine huenda wakasema

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki