Kristo Aliyetundikwa Juu ya Mti, “Hekima ya Mungu”
“Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mleta hoja wa [taratibu hii ya mambo]? Je! Mungu hakuifanya hekima ya [ulimwengu huu] kuwa upumbavu?”—1 Kor. 1:20.
1. (a) Ni hali gani ya kidini ya Wayahudi iliyopinduliwa na Yesu? (b) Ni mabadiliko gani yaliyofuata kuhubiri kwa wafuasi wake?
TAIFA la Kiyahudi lilikuwa limekuwa chini ya agano la Torati ya Musa kwa muda wa zaidi ya karne 15. Waandishi wao walikuwa wameendeleza na kuzidisha mapokeo mengi ajabu wakifasiri torati hii na kueleza juu ya matumizi yake katika maisha yao ya kila siku. Sababu moja ya hili ilikuwa kuwatenganisha Wayahudi na Mataifa, na katika njia hiyo wahifadhi dini yao bila kuchafuliwa na mafundisho ya kidini ya wapagani. Walakini kufikia hapo yule mwanadamu Yesu alikuwa amekwisha kuja na kudai kwamba yeye ndiye aliyekuwa Masihi, na alikuwa amekwisha laumu mapokeo ya wenye hekima na waandishi wao, na kusema kwamba angeimaliza torati ya Musa kwa kuitimiza, na mwishowe alikuwa amekwisha tundikwa juu ya mti akishtakiwa kuwa mkufuru. Kufuata hapo, wafuasi wake waitwao Wakristo, walihubiri kufufuka kwake wakaeneza mafundisho yake katika Palestina yote na hata ulimwengu wote uliotawaliwa na Rumi. Sio Wayahudi peke yao bali vilevile elfu nyingi za watu wa Mataifa walijiunga nao, nayo makundi ya Kikristo yakaundwa kila mahali. Agano la torati lilikuwa limemalizwa. Lilikuwa limetimiza kusudi lake likiwa kama kiongozi chakuwaelekeza watu kwa Kristo na likawa limetundikwa juu ya mti wa mateso wa Kristo. Sasa waabudu wa Yehova walikuwa chini ya agano jipya. Sheria haikuwa tena imeandikwa katika vibao vya mawe bali katika mioyo ya wanadamu.— Gal. 3:10-25; Ebr. 10:15-18.
2. Ni jambo gani lililokuwa gumu kwa Wayahudi waliogeuka kuwa Wakristo, naye Paulo alipambana na hatari hiyo kwa kutoa sababu gani?
2 Matukio haya yenye maana sana yaliutetemesha sana ulimwengu, kwa habari ya dini. Lilikuwa jambo gumu sana kwa Mafarisayo na Wayahudi wengine waliogeuka wakawa Wakristo kukubali uhakika wa kwamba Yesu alikuwa ameitimiza torati ya Musa hivyo akamaliza lazima ya kuifuata. Walijaribu kuingiza mengine ya matakwa yake katika makundi ya Kikristo. (Matendo 15:1-19) Paulo, aliyekuwa mtume kwa Mataifa, alitoa sababu zenye nguvu sana kupinga jitihada hizi: “Katika [uhuru] huo Kristo alituandika huru; kwa hiyo simameni, wala msinaswe tena chini ya kongwa la utumwa. Tazama, mimi Paulo nawaambia ninyi ya kwamba, mkitahiriwa, Kristo hatawafaidia neno. Tena namshuhudia kila mtu atahiriwaye, kwamba ni wajibu wake kuitimiza torati yote. Mmetengwa na Kristo, ninyi mtakao kuhesabiwa haki kwa sheria; mmeanguka na kutoka katika hali ya neema.” (Gal. 5:1-4; 3:10-14) Wayahudi waliokuwa bado kugeuka walikuwa ‘wakiubatilisha mti wa mateso wa Kristo’ kwa kuzitumainia kazi za Torati, badala ya kufahamu uhitaji wa “Kristo [aliyetundikwa juu ya mti]” kama dhabihu ya ukombozi. Wayahudi wengine waliogeuka walishikilia sehemu fulani za Torati, kwa hiyo wakiwa na wajibu wa kuitimiza yote, na katika njia hiyo ‘wakabatilisha Kristo aliyetundikwa juu ya mti.’—1 Kor. 1:17.
PAULO NA WANAFILOSOFIA (WATU WENYE ELIMU) WAGIRIKI
3. (a) Paulo alifanya nini kwa sababu ya wanafilosofia Wagiriki? (b) Nao hao wanafilosofia walifanya nini kwa sababu ya Paulo huko Athene?
3 Paulo vilevile alionya juu ya kuiga njia za wanafilosofia Wagiriki. Rumi ilikuwa imekuwa mamlaka ya ulimwengu mahali pa Ugiriki, walakini utamaduni na filosofia za Wagiriki ndizo zilizokuwa zikifuatwa na mamlaka hiyo. Wote Wayahudi kwa Wagiriki wa taratibu hiyo ya mambo walikuwa na wenye hekima wao, waandishi wao, na wenye kuleta maneno ya kushindana. Paulo aliuliza hivi: “Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mleta hoja wa [taratibu hii ya mambo]? Je! Mungu hakuifanya hekima ya [ulimwengu huu] kuwa ni upumbavu?” Wanafilosofia Wagiriki pamoja na marabi Wayahudi walikuwa na sifa ya kuwa wenye kuleta maneno ya kushindana naye Paulo anaweka vikundi vyote viwili pamoja: “Wayahudi wanataka ishara, na [Wagiriki] wanatafuta hekima; bali sisi tunamhubiri Kristo, [aliyetundikwa juu ya mti]; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa [Wagiriki] ni upuzi.” (1 Kor. 1:20, 22, 23) Paulo yeye mwenyewe alipata kujua habari za wanafilosofia Wagiriki na namna walivyopenda kuleta maneno ya kushindana kwa sababu ya yale yaliyompata Athene. Matendo 17:16-21 kinaonyesha hili:
“Paulo alipokuwa akiwangojea huko Athene na kuona jinsi mji ule ulivyojaa sanamu, roho yake ilichukizwa sana ndani yake. Basi katika sinagogi akahojiana na Wayahudi na waliomcha Mungu, na wale waliokutana naye sokoni kila siku. Na baadhi ya Waepikureo na Wastoiko, wenye ujuzi, wakakutana naye. Wengine wakasema, Mpuzi [“mpayukaji,” NW] huyu anataka kusema nini’? Wengine walisema, Anaonekana kuwa mtangaza habari za miungu migeni, kwa maana alikuwa akihubiri habari za Yesu na ufufuo. Wakamshika, wakamchukua Areopago, wakasema. Je! twaweza kujua maana ya elimu hii mpya unayoinena? Kwa maana unaleta mambo mageni masikioni mwetu, tutapenda kujua, basi, namna ya mambo haya. Kwa maana Waathene na wageni waliokaa huko walikuwa hawana nafasi kwa neno lo lote ila kutoa habari za jambo jipya.”
4. Wengine wa wanafilosofia hao walimwonaje Paulo, naye Paulo aliwahubiri nini?
4 Wanafilosofia hao kwa dhihaka walimwita Paulo mpayukaji, tafsiri ya neno la Kigiriki spermologos, maana yake “mwokotaji wa mbegu.” Lilikuwa likitumiwa kumaanisha kunguru au ndege mwingine mwokotaji wa mbegu, lilitumiwa kwa habari ya mtu aliyetembea-tembea barabara za mji na sokoni akiokota vipande vya vyakula vilivyoanguka kutoka katika mizigo ya watu; kwa hiyo, mtu aliyetegemea kulishwa na wengine. Katika njia ya mfano na katika matumizi ya Kiathene, neno hilo lilitumiwa kumaanisha mtu aliyeokota vipande vya habari kutoka kwa watu wengine na kuvitumia avute wengine, huku akiwa mtumiaji tu wa maneno ya wengine asiyejua kitu. Walakini, Paulo hakuwa mpayukaji asiyefaa kitu. Aliwahubiri juu ya “Mungu aliyefanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo,” kwamba yeye “ndiye anayewapa wote uzima na pumzi” na ya kwamba “alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika [mtu] mmoja.” Kwa habari za Yesu, Paulo alisema kwamba Mungu ‘amemfufua katika wafu.’ Hilo lilifanya wengine wadhihaki, lakini wengine waliamini wakajiunga na Paulo.—Matendo 17:24-26, 31-34.
WANAFILOSOFIA WALIFUNDISHA NAFSI HAIFI
5. (a) Ni mafundisho gani ya wanafilosofia yaliyofanya ufufuo uonekane kuwa upuzi? (b) Ni mafundisho gani ya elimu ya dini ya Orpheus yalikuwako kabla ya mafundisho ya kisasa ya kidini ya hell (kuteswa motoni) na masamaha ya dhambi?
5 Kwa sababu gani kutajwa kwa ufufuo kulifanya wengine wadhihaki? Je! kulipingana na nyingine za hekima za filosofia zao, na kwa sababu hiyo kukawafanya kuuona ufufuo kama upuzi. Kulingana na Maandiko, ufufuo ni jambo la akili. Ikiwa, kama vile Biblia isemavyo, mtu anakufa kama mnyama na kupotea, na hana ufahamu, anarudia mavumbini, ni nafsi iliyokufa, basi ufufuo ndio tumaini lake peke yake la kuishi tena. (Zab. 146:4; Mhu. 3:18-20; 9:5, 10; Eze. 18:4, NW) Walakini ufufuo haukuwa jambo la akili kwa wanafilosofia hao Wagiriki! Ulikuwa upuzi mtupu! Wengi wa wanafilosofia hao Wagiriki walifundisha kwamba mwanadamu alikuwa na nafsi isiyoweza kufa, na kwa hiyo hakuhitaji ufufuo. Wastoiko waliokuwa kati ya wasikilizaji wa Paulo waliamini kwamba nafsi iliendelea kuishi baada ya mwili kufa. Mapema sana kabla ya hapo, mwanafilosofia Mgiriki Thales (wa karne ya saba K.W.K.) alifundisha kwamba kulikuwako na nafsi isiyoweza kufa katika vyuma, mimea, wanyama na wanadamu. Nguvu hiyo ya uhai, alisema, inabadili umbo lakini haifi hata kidogo.a Katika karne ya sita K.W.K. mwanahesabu mashuhuri (mwenye kujulikana sana) Pythagoras alisema kwamba baada ya kifo nafsi ilikwenda Hadeze itakaswe, kisha ikarudi kuingia mwili mpya, na kwamba iliendelea katika mfululizo huu wa kutoka mwili mmoja kwenda mwingine mpaka mwishowe inamalizia kwa kuingia katika uzima ulio safi kabisa.b “Kwa wazi nafsi inaonekana kuwa isiyokufa,” akasema Plato akitaja maneno ya Socrates (wa karne ya tano K.W.K.)c Orpheus, ambaye ndiye chanzo cha namna ya ibada ya siri ya karne ya saba K.W.K., alianzisha mafundisho ya kidini yanayojulikana kwa jina lake, ambayo yalifundisha kwamba baada ya kifo, nafsi ilienda Hadeze ikahukumiwe. Habari ya Will Durant, katika Sehemu ya Pili ya kitabu The Story of Civilization, kur. 190, 191 inaendelea kusema hivi:
“Ikiwa hukumu iliiona na makosa kungekuwa na adhabu kali sana. Namna moja ya fundisho hilo iliwazia adhabu hii kuwa ya milele, na baadaye ikayapa mafundisho ya kidini wazo la hell. Namna nyingine ilichukua wazo la kuhama-hama kutoka mwili mmoja kwenda mwingine: nafsi ilizaliwa mara nyingi sana katika maisha yenye furaha zaidi na zaidi au yenye taabu zaidi na zaidi kuliko yaliyotangulia kulingana na usafi au uchafu wa maisha yaliyotangulia; nao mfululizo huu wa kuzaliwa tena ungeendelea mpaka usafi kamili ufikiwe, ndipo nafsi ilipokubaliwa kuingia katika Visiwa vya Waliobarikiwa. Namna nyingine ilitoa tumaini la kwamba adhabu katika Hadeze ingeweza kumalizwa kupitia kwa matendo ya toba aliyoyafanya mtu kabla ya kufa, au, na rafiki zake, baada ya kifo chake. Katika njia hii fundisho la kidini la purgatori na la msamaha wa dhambi kwa kupokea sakramenti (ushirika) yalitokea.”
WANAFILOSOFIA WAGIRIKI WALIFUNDISHA MAGEUZI
6. Ni kwa sababu gani kuhubiri kwa Paulo kwamba Yehova Mungu ndiye Muumba wa uhai wote vilevile kuliwafanya waione hotuba ya Paulo kuwa upuzi?
6 Alipokuwa akisema na wanafilosofia katika Athene, Paulo alisema kwamba Yehova Mungu ndiye Muumba wa ulimwengu na vyote vilivyomo, kutia na mimea, wanyama na wanadamu. Kwa kufanya hivyo, alikuwa akipingana tena na wanafilosofia Wagiriki. Wanafilosofia Waepikureo waliokuwa kati ya wasikilizaji wake waliamini kwamba uhai ulijianzisha wenyewe kwa ghafula ukaendelea kukua katika hali bora kwa bahati kupitia kwa maendeleo ya vitu vyenye uhai, ambayo wanasema kwamba vilivyo dhaifu vinakufa, na vyenye afya vinaishi na kuzaana. Kitabu The Encyclopedia Americana, Kitabu cha 10, ukurasa 606, kinasema hivi:
“Wagiriki, kwa ujumla, kidogo walikuwa na wazo la kwamba vitu vilivyo hai vina maendeleo ya polepole, wazo la kuondolewa kwa makosa katika kuzaana, na kwa hivyo, wazo la kuokoka kwa vilivyo bora zaidi, wazo la kugeuka kwa viungo au kugeuka kwa maumbile fulani ili yapate kufaa makusudi fulani, uumbaji wenye akili unaofanya kazi sikuzote katika [viumbe] vya asili, vilevile wazo la kwamba viumbe vya asili vinaongozwa na mambo ya asili yanayotokea kwa sababu ya sheria ya bahati iliyowekwa mwanzoni.”
7. Kwamba mageuzi si kisio la kisasa inaonyeshwa na mafundisho gani ya (a) Anaximander? (b) Anaxagoras? (c) Empedocles? (d) Aristotle
7 Akieleza kwa wazi hata zaidi, mwanafilosofia Mgiriki Anaximander, wa karne ya sita K.W.K., alifundisha kama ifuatavyo:
“Viumbe vilivyo hai vilitokea polepole kutokana na umajimaji wa kwanza; wanyama wa nchi kavu walikuwa samaki mwanzoni, na ilikuwa baada tu ya nchi kuwa kavu ndipo wakapata umbo walilonalo sasa. Mwanadamu vilevile alikuwa samaki; katika wakati wake wa kutokea wa mapema sana hangeweza kuzaliwa kama anavyofanya sasa, kwa sababu angekuwa hawezi hata kidogo kujipatia chakula, angaliangamizwa.”d
Kwa habari ya fundisho la Anaxagoras (wa karne ya tano K.W.K.), tunasoma hivi:
“Viumbe vyote vilivyo hai vilitoka ardhini hapo mwanzo, umajimaji, na joto, kisha vikaanza kuzaana vyenyewe kwa vyenyewe. Mwanadamu ameendelea kuliko wanyama wengine kwa sababu hali yake ya kusimama wima iliipa mikono yake nafasi ya kukamata vitu.”e
Kwa habari ya Empedocles, tunasoma hivi:
“Kwa mfano, Empedocles (wa 493-435 K.W.K.), ambaye ameitwa ‘mwanzishi wa wazo la mageuzi,’ aliamini kwamba chanzo cha uhai chaweza kuelezwa kwamba ulijitokeza wenyewe, tena aliamini kwamba namna mbalimbali za uhai hazikutokea wakati ule ule. Uhai wa mimea ulitangulia, halafu ule wa wanyama ulitokea baada ya mfululizo mrefu wa majaribio, walakini chanzo cha viumbe vyenye uhai ni jambo lililofanyika polepole sana. [Hapa viumbe vingi vikubwa ajabu vilivyotokea vinatajwa.] Walakini viumbe visivyo vya asili vilimalizika upesi kwa sababu havikuweza kuzaana. Baada ya kumalizika kwa viumbe hivyo vikubwa ajabu namna nyingine zilitokea ambazo ziliweza kujitunza na kuzaana. Kwa hiyo, ikiwa mmoja anataka, anaweza kuona katika mawazo ya Empedocles mwanzo wa makisio ya maendeleo ya vitu vyenye uhai, yaani, kwamba viumbe dhaifu vinakwisha, na vyenye afya vinaendelea kuzaana.”f
Mwanafilosofia mashuhuri (anayejulikana sana) Aristotle (wa 384-322 K.W.K.) aliandika hivi:
“Viumbe vya asili vinatokana polepole na vitu visivyo na uhai kuwa wanyama wenye uhai hata inakuwa vigumu kujua kabisa mpaka wavyo. . . . Hivyo, baada ya vitu visivyo na uhai katika maendeleo yavyo kunatokea namna ya mimea . . . Katika mimea kuna hali yenye kuendelea kugeuka kuwa wanyama. . . . Na kwa hiyo katika kuendelea kwa wanyama kuna tofauti zinazokuja polepole. . . . Ukucha wa mwanadamu ni kama vile ukucha wa mnyama au ndege, mkono ni mfano wa gando la kaa, manyoya ni mfano wa gamba la samaki.”g
WALIPOFUSHWA NA HEKIMA YAO WENYEWE
8. Ni hekima gani ya Wayahudi na Wagiriki iliyowapofusha wasiione hekima ya Mungu?
8 Hekima ya waandishi wa Kiyahudi na ya wanafilosofia Wagiriki iliwapofusha wasiione hekima ya Mungu, Kristo aliyetundikwa juu ya mti. Paulo aliandika: “Kwa maana katika hekima ya Mungu, [ulimwengu usiopata] kumjua Mungu kwa hekima yake, Mungu alipenda kuwaokoa [waaminio] kwa upuzi wa lile neno linalohubiriwa.” Kuhubiri huku kulikuwa upuzi kwa Wayahudi. Hekima yao iliwafundisha kwamba wangeokolewa kwa matendo ya Torati, kwa kusaidia maskini, na kwa sababu ya sifa njema ya babu zao, sana sana Ibrahimu. Zaidi ya hayo, wao hawakutaka Masihi dhaifu anayejiachilia atundikwe juu ya mti wa mateso! Kuhubiri huku vilevile kulikuwa upuzi kwa Wagiriki. Wao hawakutaka Myahudi aliyeuawa kama mhalifu wa kuwaokoa—wao walikuwa na nafsi ambazo hasingekufa hata kidogo!—1 Kor. 1:21.
9. (a) Ni jambo gani ambalo asingelifanya Paulo ili kuhubiri kwake kukubalike zaidi? (b) Ni jambo gani Paulo na Petro walilotangulia kuliona, nao walifanya nini kwa sababu hiyo?
9 Kwa hiyo Paulo aliliandikia kundi katika Korintho onyo lake. Hekima, iwe ile ya waandishi wa Kiyahudi yenye mapokeo yake yenye mambo mengi mno ya kisheria, au ile ya wanafilosofia Wagiriki yenye sababu za werevu, ingewafanya wauone mti wa mateso wa Kristo kuwa ubatili ikiwa wangeshawishwa na hekima ya namna hiyo. Paulo hangechanganya neno la Mungu na filosofia hizo ili likubalike zaidi na Wakristo Wayahudi au Wagiriki waliotaka kuingiza ndani imani zao za kale. Yeye hangeliharibu kwa kutia uchafu wa namna hiyo ili likubaliwe zaidi na ulimwengu ambao hekima yake ilikuwa upuzi kwa Mungu. (2 Kor. 2:17; 4:2; 11:13) Wote wawili mtume Paulo na mtume Petro walitangulia kuuona wakati uliokuwa unakuja ambao katika huo mafundisho ya uongo kutoka kwa Wayahudi na kwa watu wa Mataifa yangechafua ukweli wa Kristo aliyetundikwa juu ya mti, wakatoa maonyo haya:
Matendo 20:29, 30: “Najua mimi ya kuwa baada ya kuondoka kwangu mbwamwitu wakali wataingia kwenu, wasilihurumie kundi; tena katika ninyi wenyewe watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.”
2 Tim. 4:3, 4: “Maana utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia waalimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti; nao watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo.”
2 Pet. 2:1: “Lakini kuliondokea manabii wa uongo katika wale watu, kama vile kwenu kutakavyokuwako waalimu wa uongo, watakaoingiza kwa werevu uzushi wa kupoteza, wakimkana hata Bwana aliyewanunua, wakijiletea uharibifu usiokawia.”
10. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba maonyo yao hayakuwa ya bure?
10 Baadaye historia inashuhudia kwamba maonyo ya mitume hao yalikuwa ya kweli. Kitabu The Encyclopaedia Britannica (chapa ya 1976) kinasema: “Tangu katikati ya karne ya pili AD, Wakristo waliofundishwa filosofia ya Wagiriki walianza kuona lazima ya kuonyesha imani yao katika maneno yake, ili watosheleze akili zao na vilevile ili wageuze wapagani wenye elimu.” Vilevile, The New Schaff Herzog Encyclopedia of Religious Knowledge kinasema kwamba: “Nao, wengi wa Wakristo wa kwanza, waliona mambo fulani yenye kuvutia katika mafundisho ya kidini ya Plato, wakayatumia kuwa silaha za kulinda na kuenezea Ukristo, au wakazichanganya kweli za Ukristo na mawazo ya Plato.”
11. Ni mambo gani ya hakika yanayoonyesha kwamba idadi kubwa ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo leo wamedharau maonyo ya Paulo na Petro?
11 Mambo hayajabadilika sana muda wote huo mpaka siku yetu ya leo. Idadi (hesabu) iliyo kubwa sana ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ingali inafundisha mafundisho kama vile nafsi isiyoweza kufa, Utatu na mengineyo, ambayo yaliingia polepole katika Ukristo uliokuwa umeasi imani ya kweli tangu karne ya pili W.K. kutokana na filosofia za Wagiriki. Nao Wagiriki, waliyatoa kutoka katika mafundisho ya kale, kwa kuwa yanarudi nyuma mpaka dini za Wamisri na Wababeli. Vilevile dini nyingi leo zinafundisha kwamba Mungu alitumia mageuzi katika kuumba vitu, zikitaka kuyafanya mafundisho yao ya kidini yawe ya kisasa, lakini kwa kweli wakiyakubali makosa ya filosofia za Wagiriki. Wanakataa ukweli wa Biblia wa kwamba Yehova Mungu aliumba viumbe vyenye uhai duniani, kwamba viumbe hivyo vinazaa “kwa jinsi yake,” kwamba Yehova ni wa tangu milele na ni mwenye nguvu zote na kwamba Kristo Yesu ni Mwanawe aliye na mwanzo na aliye chini yake. Nao wengine, kama vile Wayahudi wa karne ya kwanza, hawamwoni Yesu kama ukombozi tena ambao katika huo wanadamu watiifu wanaweza kupata uzima wa milele.
12. Leo Wakristo waaminifu milioni nyingi wanaitikiaje ujumbe wa Paulo alioandikia kundi la Korintho?
12 Inafurahisha kujua kwamba hekima hii ya kidini na kifilosofia inayomwona Kristo aliyetundikwa juu ya mti kuwa upuzi na udhaifu, inaonwa na mamilioni wengi waliopo duniani leo kuwa upumbavu mtupu. Wao wanaitikia tangazo la Paulo aliloandikia kundi la Kikristo la Korintho, yaani: “Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu. Kwa sababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una nguvu zaidi ya wanadamu.” Wanatangaza jambo hili duniani pote kwa ajili ya wote wanaotafuta hekima: ‘KRISTO ALIYETUNDIKWA JUU YA MTI, NGUVU YA MUNGU! KRISTO ALIYETUNDIKWA JUU YA MTI, HEKIMA YA MUNGU!’—1 Kor. 1:24, 25.
—Kutoka The Watchtower May 15, 1978.
[Maelezo ya Chini]
a a The Story of Civilization, Sehemu ya Pili, uku.137.
b b Ibid., uku. 165.
c c Imesemwa hivyo mara nyingi katika Phaedo ya Plato.
d a The Story of Civilization, Sehemu ya Pili, uku. 139.
e b Ibid., uku. 340.
f The Encyclopedia Americana, Kitabu cha 10, uku. 606.
g History of Animals, cha Aristotle viii, I; i, I.
[Picha katika ukurasa wa 11]
Paulo aliposema juu ya ufufuo kwa wanafilosofia Waathene, wengine walidhihaki lakini wengine walimwamini