Mahubiri ya Mlimani—Kuzuia Uzinzi na Talaka
BAADA ya kuzungumza juu ya hasara iletwayo na hasira yenye kuendelezwa, Yesu alielekeza fikira zake kwenye amri ya saba ya zile Amri Kumi, akisema: “Mmesikia kwamba imenenwa, usizini.”—Mt. 5:27; Kut. 20:14; Kum. 5:18.
Chini ya sheria ya Mungu adhabu ya uzinzi ilikuwa kali—kifo kwa wote wenye hatia. Hii ilihusu hata mwanamke aliyeposwa ambaye alifanya ngono na mwanamume mwingine isipokuwa yule aliyemchumbia.—Kum. 22:22-24.
Walakini, maelezo ya Yesu, yalienda hatua zaidi ya kule kukataza tendo la uzinzi. “Mimi nawaambia,” akasema, “Kila mtu [yaani, kila mwanamume aliyeoa] atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake.” (Mt. 5:28) Katika pindi nyingine, pia, Yesu alishirikisha uzinzi na tamaa za uasherati moyoni mwa mtu: “Kwa maana ndani ya mioyo ya watu,” akasema, “hutoka mawazo mabaya, . . . uzinzi.” (Marko 7:21, 22) Hili laweza kuonyeshwa na yale yaliyompata Daudi ambaye alimtazama akawashwa nyege na mke wa mwanamume mwingine, akafanya uzinzi.—2 Sam 11:2-4.
Hapa Yesu hazungumzi juu ya wazo la uasherati la mara kwa mara ambalo mtu huliondoa upesi. Mahali pake, anazungumza juu ya hali ambayo katika hiyo mtu huyu ‘huendelea kumtazama’ mwanamke, na kusitawisha tamaa. Mungu, ambaye “huutazama moyo,” anajua kwamba mwanamume aliyeoa ambaye hutamani sana kufanya uzinzi atafanya hivyo nafasi ikipatikana. (1 Sam. 16:7) Mungu huona kama kwamba tendo lenyewe limefanywa “moyoni mwake,” ambao ndio makao ya mapendo, tamaa na maongozi.
Mtu anawezaje kuepuka kufanya uzinzi? Akitumia usemi wa mfano, Yesu alitoa usemi huu: “Jicho lako la kuume likikukosesha, ling’oe ulitupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanum. Na mkono wako wa kuume ukikukosesha, ukate uutupe mbali nawe, kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee, wala mwili wako wote usitupwe katika jehanum.”—Mt. 5:29, 30.
Maandiko yanaueleza mwendo wa haki kama ‘kuenenda pamoja na Mungu.’ (Mwa. 5:22; 6:9) Namna gani ikiwa ‘jicho la kuume’ (hapa likifananisha uwezo wa mtu wa kuona sana) au “mkono wa kuume” (ukimaanisha anayofanya mtu, kama kwa mikono yake) ‘ukimkosesha’ mtu yaani, aanguke atoke katika njia ya kumtii Mungu? Inapokuwa hivyo, inampasa mtu achukue hatua inayofanana na kung’oa jicho au kukata mkono. Namna gani hivyo?
Kwa kuwa macho ni njia ya maana ya kupashana habari na akili, nayo yanaongoza sana maoni ya mtu ya ndani na matendo yake, inampasa mtu azuie macho yake yasitazame sana mambo yasiyofaa. (Mit. 4:25; Luka 11:34) Ayubu alionyesha maoni yanayofaa alipotoa usemi huu: “Nilifanya agano na macho yangu; basi nawezaje kumwangalia msichana?”—Ayubu 31:1.
Vivyo hivyo, kuna haja ya kujihadhari kwamba yale anayofanya mtu kwa mikono yake au viungo vingine vya mwili hayavunji kanuni za Biblia za adili. Juu ya hili, mtume Paulo anaandika hivi: “Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani.”—Kol. 3:5.
Ni jambo la kawaida watu kuwa tayari kupoteza mguu au mkono kwa halisi ili wahifadhi maisha yao. Lililo la maana hata zaidi, kulingana na Yesu, ni ‘kutupa’ macho na mikono, kwa usemi wa mfano, ili kuepuka mawazo na matendo ya uasherati, kwa maana ni kwa njia hii tu watu wanaweza kuepuka uharibifu wa milele unaofananishwa na Jehanum yenye moto, “jaa la takataka” karibu na Yerusalemu lililowaka moto usiku na mchana ili lichome uchafu wake.—Mt. 5:29, 30, J. B. Phillips.
“Imenenwa pia,” akaendelea Yesu, “mtu akimwacha mkewe, na ampe hati ya talaka.” (Mt. 5:31) Sheria ya Mungu kupitia kwa Musa iliruhusu mwanamume amtaliki mkewe “asipopata kibali machoni mwake, kwa kuwa ameona neno ovu kwake.” (Kum. 24:1-4) Kwa wazi, “neno ovu” lilimaanisha jambo jingine tofauti na uzinzi, kwa maana, kama vile ilivyoandikwa hapo juu, kosa hilo lilileta adhabu ya kifo chini ya sheria ya Musa. Hata hivyo, kwa kuwa Mungu ‘anachukia kutalikana,’ ni jambo la akili kwamba sababu nzuri za kufanya hivyo kwa lazima zilikuwa nzito, kama vile mke kuonyesha hana heshima hata kidogo kwa mume wake au kuletea jamaa aibu.—Mal. 2:16.
Ingawaje, hata katika visa vizito vya namna hiyo, Maandiko hayakuamuru wala kutia moyo talaka. Kama kizuizi cha kuvunjika kwa ndoa haraka, Mungu aliamuru kwamba ilimpasa mume anayemtaliki mkewe ampe “hati ya talaka.” Hii ilihitaji kuwe na wakati wa kutayarisha na kuifikiliza kisheria. Na pengine ilitia ndani kushauriana na watu wanaofaa wenye mamlaka ambao huenda walijaribu kwanza kuleta mapatano.
Walakini, kadiri wakati ulivyopita, wanaume Wayahudi walianza ‘kutenda mambo ya uhaini’ kwa wake zao kwa kuwataliki kwa sababu ndogondogo za kila namna. (Mal. 2:13-16) Katika siku za Yesu maoni yaliyokuwako ya waalimu wa kidini Wayahudi yalisema kwamba mtu angeweza kumtaliki mkewe “hata kwa kumpikia chakula vibaya.” Kulingana na kitabu cha kueleza Biblia cha lugha ya Kijeremani cha Strack na Billerbeck, semi nyingi katika maandishi ya kale ya Kiyahudi zinaonyesha “kwamba kati ya Wayahudi katika kipindi cha Mishna [kilichotia ndani siku za Yesu] hakuna ndoa ambayo mwanamume asingevunja katika njia iliyo halali kabisa, pasipo kukawia, kwa kutoa hati ya talaka.” Basi, haipaswi kushangaza kwamba, Mafarisayo walimwuliza Yesu kama talaka ilikuwa halali “kwa kila sababu.”—Mt. 19:3.
Maoni ya Yesu juu ya talaka yalikuwa nini? “Mimi nawaambia, kila mtu amwachaye mkewe, isipokuwa kwa habari ya uasherati, amfanya kuwa mzinzi; na mtu akimwoa yule aliyeachwa, azini.” (Mt. 5:32) Akiwa na mamlaka kamili kama Masihi na Mwana wa Mungu, Yesu alionyesha kwamba Baba yake hakupendezwa na waume wanaotaliki wake zao hata kwa msingi wa usemi wa Maandiko “neno ovu.” (Linganisha Mathayo 19:8) Tofauti na hiyo, mwanamume ambaye angemtaliki mkewe kwa sababu nyingine isipokuwa uasherati angemtia hatarini ya kuwa mzinzi ikiwa yeye angekuwa na uhusiano wa ngono na mwanamume mwingine, kwa sababu machoni pa Mungu ndoa haijavunjika. Yesu aliongeza kwamba ‘ye yote akioa mwanamke aliyeachwa,’ yaani, aliyetalikiwa kwa sababu zisizo za uasherati, “azini.”
Maneno haya ya Yesu yanafaa kweli kweli. Kukazia kwake kwamba uasherati ndio tu msingi wa talaka kunazuia wanaume na wanawake waliooana wanaotaka kumpendeza Mungu wasiachane kwa sababu nyinginezo. Nako kulaumu kwake mawazo ya uasherati ambayo huongoza kwenye uzinzi kunapunguza hata zaidi visa vya kuvunjika kwa ndoa. Kwa wale wanaotii shauri lake, Mahubiri ya Mlimani ni msaada wenye nguvu nyingi katika kuzuia uzinzi na talaka.