Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Daktari mmoja alisema kwamba mgonjwa anaweza kutolewa sehemu ya damu yake kabla ya kupasuliwa iwekwe akibani, ili itumiwe ikiwa damu itahitajiwa wakati wa kupasuliwa. Mkristo anapaswa kuyaonaje matumizi kama hayo ya damu yake mwenyewe?
Kulingana na maoni ya matabibu (waganga) huenda mpango huo ukaonekana unafaa sana. Kukubali kutiwa damu ya mtu mwingine mishipani kuna hatari kubwa. Kwa kuonekana tu kuna hatari kidogo tu mtu akitiwa damu yake mwenyewe mishipani. Kwa hiyo kati ya matabibu kuna maelekeo ya kutumia mpango wa kumtia mtu mishipani damu yake mwenyewe. Hii inahusu kutoa damu ya mgonjwa na “kuiweka akibani” kwa kusudi la kuitia mishipani inapohitajiwa. Ikiwa mwenye kuitoa haihitaji, damu hiyo inaweza kutumiwa na wagonjwa wengine.
Kama habari iliyo kurasa 16-19 za gazeti hili inavyoonyesha, kutia damu mishipani kunapingana na Biblia.a Maandiko yanafunua kwamba Mungu anaiona damu kuwa takatifu, nao watumishi wake wanapaswa kuiona vivyo hivyo. Kulingana na hili, Yehova Mungu aliwaambia Waisraeli kwamba wangeweza kufanya mambo mawili tu na damu. Kwanza, Mungu alisema hivi: “Nimewapa hiyo damu juu ya madhabahu [ya kutolewa dhabihu], ili kufanya upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu.” La pili, ikiwa damu ya mnyama haikutumiwa juu ya madhabahu, Mwisraeli alipaswa aimwage juu ya nchi katika njia hiyo alikubali kwamba uhai unatoka kwa Mungu na kwamba damu inayosimamia uhai haikuwa ikitumiwa kwa faida za kibinafsi. (Law. 17:11-14) Lakini je! kuiona damu katika njia hii ilikuwa jambo la watumishi wa Mungu waliokuwa chini ya torati peke yao? Kinyume cha hilo, kulingana na akili nzuri, waabudu wa kweli, walioishi kabla ya kupeanwa kwa Torati, tayari walikuwa wakiiona damu katika njia hii.
Mapema Mungu alikuwa amemwambia Nuhu na jamaa yake kwamba wanadamu hawakupaswa kula nyama ikiwa na damu ndani yake. (Mwa. 9:3, 4) Kwa hiyo wangefanya nini? Mnyama alipouawa kwa ajili ya chakula, damu yake ingemwagwa juu ya nchi. Damu ya uhai haikuwa ya na jamaa yake bali ilikuwa ya Mpaji-Uzima. Kulingana na hilo, ilifaa kuimwaga damu juu ya nchi, ambayo ndiyo ‘mahali pa kuweka miguu’ ya Mungu kwa njia ya mfano.—Isa. 66:1.
Amri hiyo iliyopewa Nuhu vilevile inatumika kwa Wakristo. Katika karne ya kwanza W.K., baraza iliyoongoza ya Wakristo ilitoa uamuzi, ulioungwa mkono na roho takatifu, kwamba Wakristo walipaswa “kushika mwiko wa vitu vinavyonyongwa na wa damu.” (Matendo 15:19, 28, 29, NW) Hiyo ingekuwa na maana gani katika kuifuata? Usemi hii “vitu vinavyonyongwa” unamaanisha nyama ya wanyama waliouawa katika njia iliyoacha damu katika nyama yao. Wakristo hawangekula nyama ya namna hiyo. Namna gani juu ya usemi ‘shika mwiko wa damu’? Hilo lingalikataza kutumia damu iliyokuwa imetolewa katika kiumbe huyo, kama walivyofanya wapagani wengine, waliotengeneza na kula utumbo wenye damu au chakula kingine kilichokuwa na damu au waliokunywa damu iliyotoka kwa wanyama au watu hodari waliouawa katika viwanja vya michezo. Wakristo hawawezi kufanya yo yote ya mambo hayo. Walipoiondoa damu kutoka kwa mnyama, wangefanya kama walivyofanya watumishi wa Mungu katika wakati uliopita, kujiepusha nayo. Katika njia hiyo wangeonyesha wanathamini utakatifu wa damu na uhai na vilevile waonyeshe kwamba wanategemea ubora wa damu ya Kristo.
Kwa hiyo, ikiwa matabibu wanapendekeza kwamba Mkristo akubali sehemu ya damu yake itolewe iwekwe katika benki ya akiba ya damu kwa kusudi la kuwekwa mishipani wakati ujao, Mkristo anakuwa na uongozi kutoka kwa Biblia juu ya mwenendo unaofaa kufuatwa. Anaweza kutaja kwamba Waisraeli wa kale waliambiwa kwamba damu iliyoondolewa mwilini ilipaswa ‘kumwagwa juu ya nchi kama maji,’ kuonyesha kwamba ilitoka kwa Mungu na haikupaswa kuliwa ili kuendeleza uhai wa kiumbe cho chote cha kidunia. (Kum. 12:24) Tena anaweza kutaja amri iliyo wazi kwamba Wakristo ‘wanajiepusha na damu.’ Kulingana na maoni haya, angewezaje kukubali damu yake iwekwe katika benki ya kuweka damu ili baadaye iwekwe katika mishipa yake mwenyewe au ya mtu mwingine?
● Namna gani juu ya vitu kama bomba ya moyo na maini au mashine inayofanya kazi mahali pa figo? Je! Mkristo anaweza kutumia vitu hivyo?
Kunao mashahidi Wakristo wa Yehova ambao, kwa dhamiri njema, wamekubali vitu hivyo vitumiwe, ikiwa mashine hizo zingetumia umajimaji usio na damu, kama Ringer’s lactate solution (namna ya umajimaji wenye chumvi).
Kidude cha namna hii kinapokuwa kikitenda kazi, damu ya mgonjwa inatembea kutoka mshipa wa damu kupitia kwa mrija na katika mashine hiyo (ambapo inapigwa kama kwamba kwa bomba, na kutiwa hewa na/au kusafishwa) kisha inarudi kutembea katika mzunguko wake. Mashine hiyo inafanya kazi kwa muda fulani ambayo kwa kawaida inafanywa na viungo vya mgonjwa huyo.
Wakristo fulani wamewaza wakiongozwa na dhamiri zao kwamba damu yao inaendelea kutembea na ya kwamba mzunguko huo ulioko nje ya mwili unaweza kuonwa tu kama kitu kilichoongezwa tu katika mzunguko wa damu. Wameona kwamba kinalingana na kisehemu cha mrija unaoweza kuwekwa katika mwili upitishe damu katika sehemu ya mshipa iliyoziba.
Bila shaka, kila Mkristo anapaswa kufikiri juu ya yale yanayohusika katika kutumia vitu hivi na vinginevyo vinavyofanana navyo. Anaweza kujichunguza aone kama anaiona damu hiyo kama iliyouacha mwili wake kabisa na kwa hiyo inapaswa kutupwa au kama damu ambayo, kwa msingi, bado ni sehemu ya mzunguko wa damu yake. (Kum. 12:16) Ndipo anapoweza kufanya uamuzi ambao utamwacha akiwa na dhamiri njema mbele za Mungu.—1 Pet. 3:16.
● Je! ni vibaya kukubali kuchunguzwa damu?
Juu ya msingi wa maarifa yao ya Biblia, mashahidi wa Yehova wengi, ikiwa si wote, hawapingi uchunguzi kama huo. Kiasi kidogo cha damu kinachoondolewa mwilini hakiliwi au kutiwa katika mwili wa mtu mwingine. Kinachunguzwa tu kabla ya kutupiliwa mbali.—Kum. 15:23.
● Mkristo anapaswa kujali kadiri gani juu ya damu katika vyakula?
Mungu alimwambia Nuhu, na kwa hiyo jamii nzima ya kibinadamu hivi: “Kila kiendacho kilicho hai kitakuwa chakula chenu, . . . Bali nyama pamoja na uhai, yaani, damu yake, msile.” (Mwa. 9:3, 4) Kwa hiyo, waabudu wa kweli wanapaswa wajiepushe kula nyama ikiwa na damu iliyoachwa ndani yake au vyakula vingine ambavyo damu imeongezwa.
Hii inatuhitaji kujali kwa kadiri fulani. Kwa mfano, katika nchi fulani, wanyama wananyongwa, au wakauawa katika njia nyingine ambayo inaiacha damu ndani yao. Ikiwa hayo ndiyo mazoea ya mahali pao, Wakristo mara nyingi wananunua nyama kutoka kwa wanabiashara, wauza nyama au wakulima wanaojulikana kwamba wanauza nyama kutoka kwa wanyama ambao damu imeondolewa kabisa.
Walakini, sheria za serikali juu ya kuchinja wanyama katika nchi nyingi, kama kwa mfano, katika United States, zataka kwamba wanyama wawe wameondolewa damu kabisa. Kwa hiyo, Wakristo katika sehemu hizo hawahitaji kujali sana. Wanaweza kuwa huru kula nyama inayouzwa sokoni au inayouzwa katika mikahawa. (Linganisha 1 Wakorintho 10:25, 26, ambapo nyama iliyotolewa sadaka kwa sanamu inatajwa: “Kila kitu kiuzwacho sokoni kuleni, bila kuuliza-uliza, kwa ajili ya dhamiri; maana, Dunia ni mali ya [Yehova] na vyote viijazavyo.”) Walakini, huenda kukawa na uhitaji wa kuuliza juu ya nyama ya wanyama waliouawa mahali penu, kama vile nyama kutoka kwa wanyama “wa mwitu,” iwe imepatikana kutoka kwa mwindaji, mwuza nyama au katika mkahawa.
Lakini namna gani juu ya vyakula vilivyotengenezwa na kutiwa damu au vitu vilivyotengenezwa kwa damu kama umajimaji wenye protein?
Serikali fulani zinawataka watengenezaji wa vyakula waonyeshe katika labeli orodha ya vitu vilivyotumiwa kutengeneza chakula. Wakristo ambao wamechunguza labeli kwa muda fulani huenda wakawa wameona kwamba katika mahali pao damu haitumiwi hata kidogo katika vyakula. Kwa hiyo, huenda kwa kufaa wakawa walikuwa wakisoma labeli wakati tu walikuwa na sababu ya kufikiri kwamba huenda damu ikawa imeongezwa katika namna ‘fulani ya vyakula.
Walakini, majuzi, Jamhuri ya Mwungano ya Ujeremani ilipitisha sheria ikiziruhusu kampuni za nyama kutumia umajimaji wa damu uliokaushwa kiasi cha 2 kwa mia (au, katika hali nyingine, 10 kwa mia) katika ‘namna fulani za vyakula vinavyofanyizwa kwa nyama kama utumbo na vinginevyo . . . ‘ bila kuonyesha katika labeli. Mkristo anayetaka kuongozwa na dhamiri anaweza kufanya nini katika hali kama hiyo?
Anaweza kumwuliza mwuzaji wa nyama au mtengenezaji. Inasemekana kwamba, katika kujibu maulizo hayo, watengenezaji wa nchi fulani ya Scandinavia walitoa uhakikisho kwamba damu haitumiwi katika nyama wanazotengeneza; lakini hawataki kupoteza biashara yao. Walakini, katika sehemu fulani, Mashahidi waliouliza wauzaji wa nyama au watengenezaji wa nyama walipewa majibu yasiyotosheleza au yasiyo ya kweli. Inafaa kuonwa kwamba, hata ingawa sheria inaruhusu kampuni kuongeza damu bila kuionyesha, hii haina maana kwamba kampuni zote au hata nyingi zazo zinafanya hivyo.
Kwa hiyo, Wakristo, mmoja mmoja, lazima wajifanyie uamuzi juu ya watakalofanya. Dhamiri za wengine huenda zikawasukuma wajiepushe na cho chote ambacho wao wenyewe wana mashaka nacho au kuuliza maulizo wanayohitaji kuuliza ili kutuliza dhamiri zao. (Rum. 14:23) Katika hali fulani inapoelekea kwamba haiwezekani kupata habari kamili kwa kuuliza maulizo yanayofaa, Wakristo wengine huenda wakaamua: ‘Ikiwa hakuna sababu ya kutosha ya kunifanya nifikiri kwamba damu imetiwa au ikiwa hakuna njia yo yote ambayo kwayo naweza kujua, naweza ‘kula’ nikiwa na dhamiri njema.’ Hata hivyo, wanapaswa kufikiria maoni ya wengine, kama alivyoshauri Paulo—1 Kor. 10:28-30; Rum. 14:13-21.
Wakristo wa kweli wanapaswa kujali juu ya damu. Wanapaswa kufanya lo lote wawezalo waepuke kuvunja sheria ya Mungu iliyo wazi. Kuheshimu sana sheria hiyo ni jambo la maana sana. Kwa kufanya yote wawezayo “kujilinda nafsi zao . . . na damu,” watu wa Mungu wanaonyesha kwamba wanathamini utakatifu wa uhai na wa damu inayousimamia.—Matendo 21:25.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi tazama kijitabu Blood (1977).