Daktari Anayethamini
TULIPOMTEMBELEA Dakt. M, tulimweleza kwamba sisi tu Mashahidi wa Yehova na kwamba tulikuwa na kitu tulichotaka kumpa. Alikuwa mwenye furaha akatukaribisha ndani mara moja, wakati wote huo alikuwa akituchekesha, akisema: “Lazima mlipe dola 15.00 mwingiapo ndani!” Tulimtolea kijitabu Blood tukamweleza kwamba tulikuwa tunatoa nakala moja kwa kila daktari, daktari wa kike na wakili ili wafahamiane zaidi na maoni ya Mashahidi na sababu hatukubali damu.
Daktari huyo alisema kwamba, ingawa alitumikia katika kikosi cha M.A.S.H. katika Korea na alikuwa ametia watu wengi damu mishipani, yeye aliamini kwamba kila mtu anapaswa kufanya uamuzi wake mwenyewe juu ya litakalofanywa na mwili wake. Vilevile alikubaliana na jambo la kumtibu “mwanadamu mzima,” kwa kuwa kutia mtu damu mishipani kwa nguvu kunaweza kutokeza matatizo (magumu) ya akili.
Baada ya kuzungumza naye Yohana 17:3, nilimtolea uandikishaji wa Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, nilieleza kwamba zitamsaidia ajue Biblia zaidi na namna Mungu atakavyoondolea wanadamu matatizo haya. Alikubali kuandikisha magazeti yote mawili, akisema: “naona kwamba haya yataniletea faida kubwa.”
Alieleza sababu ya kuwapenda Mashahidi wa Yehova. Wakati mmoja alivunjikiwa na gari lake akiwa katika barabara moja kuu ya Pennsylvania nayo motokaa nyingine ikaja kumsaidia. Watu hao, si kwamba tu walimsaidia kupeleka gari lake kwenye kituo cha mafuta, bali vilevile walikaa pale pale pamoja naye mpaka gari lake likatengezwa wakawa na hakika kwamba angeweza kuendelea na safari yake. Kabla ya kuondoka, walimwachia nakala za magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Hivyo akajua kwamba walikuwa Mashahidi wa Yehova. Alitaja mara kadha namna walivyomwonyesha fadhili nyingi wakijitaabisha ili wamsaidie.—Imetolewa.