Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 6/1 uku. 3
  • Je! Waweza Kukubali Makosa Yako?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Waweza Kukubali Makosa Yako?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ushupavu
  • Kiburi
  • Haya na Woga
  • Upole na Kusikiliza Shauri
  • Sababu Gani Ukubali Unapokosa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Je, Ni Vibaya Kuwa na Kiburi?
    Amkeni!—1999
  • Yafaa Kuzuia Kiburi Chako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Matokeo ya Kiburi—Ni Makubwa Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 6/1 uku. 3

Je! Waweza Kukubali Makosa Yako?

“NI WAJINGA na wafu tu ambao hawageuzi maoni yao.” Akasema mwandikaji S. R. Lowell. Vyo vyote iwavyo, kushikilia maoni fulani kipumbavu au kukataa kukubali makosa yetu ni udhaifu wa kawaida kati ya wanadamu.

Mfano wa kutokeza wa maoni kama hayo ulitukia katika mwaka 33 W.K. Kwa muda fulani kabla ya mwaka huo, Yesu wa Nazareti alikuwa amekuwa akihubiri na kufanya wanafunzi kuizunguka nchi ya Palestina. Sikuzote wakuu wa Kiyahudi walikuwa wakimpinga, wakikataa ushuhuda wa Kimaandiko pamoja na miujiza aliyotumia katika huduma yake kuonyesha kwamba yeye ndiye Masihi. Kisha, katika mwaka huo, Yesu akafanya tendo lenye nguvu sana karibu na Yerusalemu ambalo lingemsadikisha hata mpinzani aliye mkali kabisa. Mbele ya watu wengi, Yesu alimfufua mtu aliyekuwa amekufa kwa muda wa siku nne! —Yohana 11:30-45.

Kweli kweli, kama jambo lo lote lingehakikisha kwamba Yehova alikuwa akimwunga mkono Yesu, mwujiza huo ungefanya hivyo. Kwani, ni katika njia gani nyingine ufufuo kutoka kwa wafu ungeweza kuelezwa? Wayahudi wengi walimkubali kwa sababu ya huo. Lakini namna gani viongozi wa Kiyahudi? Habari inasema kwamba “walifanya shauri la kumwua” Yesu. Na si hayo tu, bali pia “wakuu wa makuhani wakafanya shauri la kumwua Lazaro naye,” yule mtu ambaye Yesu alimfufua.​—Yohana 11:53; 12:10, 11.

Ushupavu

Ndiyo, badala ya kukubali kosa lao, Wayahudi hao walitaka kuondoa kila namna ya ushuhuda. Bila shaka tunalazimika kulaumu ushupavu wao. Mtu angefikiri kwamba badala ya kujionyesha kuwa wenye shingo ngumu hivyo, dhamiri zao zingewaongoza wageuze maoni yao. Lakini wao waliendelea, na baadaye, wakamwua Yesu—kosa ambalo lilikuwa baya zaidi na tendo la uhalifu lenye kulaumika zaidi lililopata kutendwa wakati wo wote.—1 Kor. 2:6-8.

Tena, ijapokuwa ushuhuda wote wa kufufuliwa kwa Yesu, walitaka kuwaangamiza mitume, ambao walikuwa mashahidi wa tendo hilo kuu la Mungu. Walakini mmoja wa viongozi wao walioheshimiwa sana, ijapokuwa yeye hakumkiri Yesu kuwa Masihi, aliwapa shauri ambalo lingewafanya wageuze maoni yao mara moja. Mtu huyo alikuwa Gamalieli mwalimu aliyejulikana sana. Baada ya kuwapa mifano ya wengine waliojidai kuwa Masihi lakini wafuasi wao wakaanguka, Gamalieli aliwaonya hivi: “Nawaambia, Jiepusheni na watu hawa, waacheni; kwa kuwa shauri hili au kazi hii ikiwa imetoka kwa binadamu, itavunjika, lakini ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi kuivunja; msije mkaonekana kuwa mnapigana na Mungu.”​—Matendo 5:34-39.

Hata hivyo, wakuu Wayahudi hawakusikiliza shauri la Gamalieli. Kwa kuwa, wakati fulani baadaye, wakati Mkristo Stefano aliposimama mbele yao na kuwaambia kwamba wao ni watu wenye shingo ngumu, “wakachomwa mioyo [lakini si kwa kutubu au kwa unyofu], wakamsagia meno.” Kisha, “wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao,” na mwishowe wakamwua Stefano kwa kumpiga kwa mawe.​—Matendo 7:51-60.

Hata kukiwa na mifano kama hiyo, mara nyingi ushupavu unasifiwa sana ulimwenguni. Hata hivyo, Biblia inaushirikisha na uasi na moyo mbaya—mambo ambayo inampasa Mkristo ajiepushe nayo. (Zab. 78:8) Vilevile Biblia inatupatia mifano, kama ule wa Farao wa Misri na Wayahudi katika siku za Waamuzi, na namna walivyoteseka kwa sababu ya ushupavu wao.​—Kut. 14:8, 26-28; Amu. 2:19-23.

Kwa hiyo, mtu akijichunguza mwenyewe na kuona kwamba kwa asili yeye ana maelekeo ya kuwa mshupavu, au haelekei sana kusikiliza maoni ya wengine, ni vizuri kuliona hili kuwa tatizo. Kwa vyo vyote, si wenye ushupavu, bali ‘wanyenyekevu ndio hupewa neema na Mungu.’ Na zaidi, si wenye shingo ngumu au wenye kushikilia kauli yao, bali wapole ndio ‘watakaoirithi nchi.’​—Mit. 3:34; Zb. 37:11.

Kiburi

Nyakati nyingine tatizo haliwi ushupavu tu. Huenda likahusiana na sifa nyingine—-kiburi. Inawezaje kuwa hivyo? Basi, ebu fikiria. Unamjua msimamizi kazini ambaye akifanya kosa naye aonyeshwe kosa hilo, anakataa kulikubali au anajaribu kumlaumu mtu mwingine kwa sababu ya kosa hilo? Au, labda, umepata kumsikia mzee kundini akisema jambo fulani lisilo sahihi bila kukusudia, na kisha anakataa kulikubali. Huenda sababu ya hili ikawa kiburi, kujiona kwamba mtu mwenye cheo kama chake hapaswi kuonekana na kosa. Nyakati nyingine wazazi na waalimu wanakuwa na maoni kama hayo, wakiogopa kwamba watapoteza heshima na uongozi wao wakikubali kosa, na kudhoofisha mamlaka yao.

Wazo jingine linalohusiana na kiburi ni lile la kutojiaibisha. Katika nchi za Mashariki (za Asia) wengine wanaona afadhali wafe kuliko kuaibika. Na wengi wetu, tuwe twaishi katika nchi za Mashariki au za Magharibi (za Uzunguni), tunapenda sana kutojiaibisha, twapenda kulinda sifa yetu, namna watu wanavyotuona. Sana sana jambo hilo linasababishwa na kiburi.

Je! kiburi ni sifa ambayo Wakristo wanapaswa kusitawisha? Basi, tunapofikiria watu wenye kiburi, ni watu wa namna gani wanaokuja akilini mwetu? Watu kama vile Senakeribu, Farao na mfalme wa Babeli (na hata Ibilisi mwenyewe). (1 Tim. 3:6) Ni kweli, wafalme hawa walisifiwa na kuogopwa na watu wa siku zao, walakini Yehova aliwaonaje? Biblia yasema hivi: “Kiburi na majivuno . . . [mimi Yehova] nakichukia.” (Mit. 8:13) Nao utukufu wa watu hao uko wapi leo?

Haya na Woga

Watu wengine wanaweza kukataa kukubali makosa yao kwa sababu nyingine. Labda wanaogopa au kuona haya. Wakifanya jambo linalowaaibisha, wakiulizwa waeleze sababu yake, aibu yaweza kuwafanya wasikubali mambo ya hakika au wajaribu kujitetea, wakijaribu kuifanya dhamiri yao iache kuwachoma. Watu kama hao wanahitaji kusitawisha sifa kama vile imani, unyenyekevu na upendo kwa Mungu. Yehova ana nia ya kusamehe hata dhambi zilizo nzito sana. Ikiwa mwenye dhambi atamtumaini Mungu na kuitumaini dhabihu ya Mwanawe na kuungama waziwazi dhambi yake kwa Mungu, dhamiri yake itasafishwa. (Ebr. 9:14) Kwa kuwa Maandiko yanazungumza juu ya namna Yesu Kristo alivyo Kuhani Mkuu wetu mwenye huruma, na kutushauri hivi: “Kwa hiyo, na tukikaribie kiti cha enzi cha fadhili zisizostahilika tukiwa na uhuru wa kusema, tupate kupokea rehema na kuona fadhili zisizostahilika za kutusaidia wakati unaofaa.”​—Ebr. 4:15, 16, NW; 1 Yohana 2:1, 2.

Kusema kweli, tunapata faida gani kwa kukataa kukubali lawama kwa sababu ya matendo yetu? Ni kweli kwamba huenda tusiadibiwe wakati huo, lakini, “cho chote apandacho mtu ndicho atakachovuna.” (Gal. 6:7) Ingawaje huenda watu wasijue juu ya dhambi zetu, “[Yehova] huipima mioyo.” (Mit. 21:2) Mtume Paulo anatuonya akisema hivi: “Sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu. Kwa kuwa imeandikwa, Kama niishivyo, anena [Yehova] kila goti litapigwa mbele zangu, na kila ulimi utamkiri Mungu. Basi ni hivyo, kila mtu miongoni mwetu atatoa habari zake mwenyewe mbele za Mungu.”​—Rum. 14:10-12.

Upole na Kusikiliza Shauri

Bila shaka kwa ushupavu hatumaanishi kuwa na kusudi imara ambalo kila Mkristo lazima awe nalo. Ni jambo lenye kusifika ikiwa mtumishi wa Mungu ‘ameimarika, na kuwa asiyetikisika’ katika ibada yake. (1 Kor. 15:58) Hili linatokana na makusudi mema, nalo lamaanisha kuwa imara katika mawazo na kanuni za Yehova, wala si zetu sisi wenyewe. Zaidi ya hayo, linapatana na sifa mbili za maana sana—upole na kusikiliza shauri.

Huenda wengine wakaona kwamba upole na kusikiliza shauri si sifa zinazowafaa watu wenye mamlaka. Walakini Musa, aliyekuwa mwangalizi wa watu wapata milioni tatu alikuwa “mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hes. 12:3) Tena imetajwa waziwazi kwamba inawapasa wazee Wakristo katika kundi la Mungu wawe wenye ‘kusikiliza shauri.’ (1 Tim. 3:1-3,NW) Ndiyo, mtu mwenye kusikiliza shauri na mpole hataliona kuwa jambo gumu kukubali kosa lake. Hataona haya sana, au kuwa na kiburi sana, au kujiona kukosa usalama sana asiweze kueleza mambo kama yalivyo, wala kuogopa kujiaibisha hakupaswi kuwe jambo la maana zaidi kuliko kusema kweli. Badala yake, yeye ataonyesha hekima itokayo juu, ambayo ni “yenye amani, yenye kusikiliza shauri, tayari kutii, imejaa rehema na matunda mema.”​—Yak. 3:17, NW.

Bila shaka wengi wetu hawataruhusu ushupavu utufanye tuue, kama vile walivyofanya viongozi wa Kiyahudi. Lakini tukiwa washupavu hata katika mambo madogo, Yehova hafurahi. (Luka 16:10) Tukitenda dhambi, inatupasa kukubali mara moja kuwa na hatia na kuiacha dhambi hiyo, tusiendelee ‘kugusa’ kitu hicho, na kisha tumwendee Mungu mara moja tukiwa na uhuru wa kusema ili tupate moyo uliosafishwa. Ikiwa jambo lo lote linatuzuia kumkaribia Mungu—kiburi, aibu, woga au jinginelo—inatupasa kupata msaada wa Mkristo mwingine aungane nasi katika sala kwa ajili yetu. (Yak. 5:16) Jambo tunalopaswa kuogopa si kuaibika au kukubali kosa, bali kumkasirisha Mungu kwa kutoungama kosa hilo kwake. Vilevile inatupasa kutambua rehema zake nyingi kwa wale wanaomjia kwa moyo wenye majuto, kwa kuwa yeye asema hivi: “Mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu.”​—Isa. 66:2.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki