Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 2/1 kur. 19-22
  • Sababu Gani Ukubali Unapokosa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sababu Gani Ukubali Unapokosa?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sababu Ambayo Huenda Ikatufanya Tusikubali
  • Matokeo Yasiyofaa
  • Mifano ya Kutoka Zamani
  • Matokeo Mazuri
  • Misaada ya Kusaidia Kushinda Maelekeo hayo
  • Kwa Nini Ukubali Kosa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Ninaweza Kurekebishaje Makosa Yangu?
    Majibu Ya Maswali 10 Ambayo Vijana Huuliza
  • Je! Waweza Kukubali Makosa Yako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Nifanye Nini Ninapokosea?
    Vijana Huuliza
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 2/1 kur. 19-22

Sababu Gani Ukubali Unapokosa?

WATU pekee wasiofanya makosa ni wafu.” Hilo limesemwa juu ya wanadamu wasiokamilika. Na unapofikiria mambo, ni nani asiyefanya makosa nyakati nyingine? Ni nani asiyekosea?

Neno la Mungu, Biblia Takatifu, linaonyesha wazi kwamba sote tunafanya makosa, kwa maana linasema: “Hakuna mwanadamu mwenye haki hapa duniani, ambaye afanya mema, asifanye dhambi.” Katika Biblia, maneno ya Kiebrania na ya Kigiriki yanayotafsiriwa “dhambi” kwa halisi maana yake ni “kuikosa shabaha”​—kufanya kosa kwa kadiri matakwa ya Mungu yanavyohusika.​—Mhubiri 7:20.

Hata hivyo, ijapokuwa ni kawaida kukosea, kufanya makosa​—ndiyo, kufanya dhambi​—ni vigumu kama nini kukubali! Ikiwa wewe ni mume na baba, je! unajikuta ukitaka kuepa ikiwa ni wakati wa kukubali kwa mke wako au watoto wako au watoto wako kwamba umekosa? Ikiwa wewe una cheo cha uangalizi, je! hujikuti ukisita kukubali kwa wale walio chini yako kwamba umefanya kosa? Iko namna iyo hiyo na wake, watoto, wafanyi kazi na wale walio katika hali nyingine.

Sababu Ambayo Huenda Ikatufanya Tusikubali

Inaonekana kuwa asili ya wanadamu kujaribu kujitetea. Tulipokuwa watoto wachanga, ilikuwa vigumu kama nini wazazi wetu kutufanya tukubali kwamba tulikosa na kwamba tulipaswa kuomba radhi! Huenda tukaonyesha maoni yayo hayo tukiwa watu wazima. Hivyo huenda mtu akajaribu kutoa udhuru kwamba alilofanya halikuwa kosa kweli, kwamba ni mtu mwingine aliyekuwa mwenye hatia, au kwamba hali zisizo za kawaida ndizo zilizosababisha.

Sana sana inaonekana kuwa vigumu kwa wale walio na vyeo vya madaraka kukubali kuwa wamekosa. Sababu ni nini? Bila shaka mara nyingi hii ni kwa sababu ya kiburi. Wanahangaikia yale ambayo huenda wengine wakafikiri; wanataka kuhifadhi heshima yao. Lakini, hapo ndipo kushindwa kukubali kuwa umekosa huenda kukawa sababu ya kujisikia kukosa usalama. Huenda mtu akadhani kwamba cheo chake kinahatirishwa akikubali kosa.

Bila shaka watu fulani wanasita kukubali kwamba wao wanakosa au wamekosa kwa sababu ya hasara ambayo huenda wakalipia kosa lao. Hivyo, huenda mfanyi kazi wa reli akawa amesababisha msiba mkubwa kwa sababu ya kutojali. Lakini akikubali kwamba alikosa, huenda akapoteza kazi yake au hata kufungwa. Au, kwa habari ya mganga, huenda akalipa gharama kubwa kwa sababu ya utibabu wake wa uzembe, na huenda kukubali kosa kukamgharimu yeye au kampuni yake ya bima fedha nyingi sana.

Hapo tena, huenda mtu akapata shida ya kuona hakika mambo jinsi yalivyo. Ni kama Biblia inavyosema, “Ni nani awezaye kuyatambua makosa yake?” Isitoshe, huenda moyo ukaendeleza maoni yanayotuzuia kukubali kosa letu. Ndiyo, “moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote . . . Nani awezaye kuujua?”​—Zaburi 19:12; Yeremia 17:9.

Matokeo Yasiyofaa

Huenda ubinafsi wa kipumbavu ukatufanya tujitetee badala ya kukubali kwamba tumekosa. Lakini bila kujali sababu yetu, kukataa kukubali tunapokosa kuna matokeo yasiyofaa. Kwa mfano, kunaweza kuharibu uhusiano mzuri pamoja na washiriki wa jamaa zetu au pamoja na wale tunaofanya kazi nao au kuabudu pamoja. Kwa kukataa kukubali tunapokosa, ama tunajaribu saburi ya wengine ama tunawapotezea heshima yao. Na inaelekea sana kwamba tunafanyiza kizuizi kinachozuia upashanaji habari mzuri.

Lililo zito kuliko na hilo ni uhakika wa kwamba kukataa kukubali tunapokosa kunatulemeza na dhamiri yenye hatia, hasa iwapo mtu mwingine analaumiwa kwa lile kosa ambalo sisi tumefanya. Na iwapo tunakataa kukubali kosa moja, huenda hilo likawa ni zoea. Tukiisha kukataa kukubali makosa madogo, huenda upesi tukakataa kukubali yale yaliyo makubwa, yote kwa hasara yetu. Matokeo yake ni kwamba hata katika habari ya dhambi nzito dhamiri yetu huenda ikafa ganzi kana kwamba imechomwa kwa chuma cha moto. (1 Timotheo 4:1, 2) Zaidi ya yote, mwendo huo hauna budi kuharibu uhusiano wetu pamoja na Muumba wetu, Yehova Mungu.

Mifano ya Kutoka Zamani

Kushindwa kukubali kwamba tumekosa kwa kujaribu kuwawekelea wengine lawama kunatuweka upande wa watu wasiofaa. Kwa kutokutii kwake, yule mtu wa kwanza, Adamu, alimlaumu ‘yule mwanamke ambaye Mungu alimpa.’ Naye Hawa akamlaumu nyoka. Walakini, Mungu hakuzikubali sababu hizo za kujitetea bali aliwataka watu hao wa kwanza wawili watoe sababu. Halafu kulikuwa na Mfalme Sauli, aliyeshindwa kutekeleza kabisa hukumu ya Mungu juu ya Waamaleki waovu. Sauli alipoulizwa sababu gani, alilaumu watu wake. Lakini Mungu hakukubali sababu hiyo ya kujitetea.​—Mwanzo 3:12-19; 1 Samweli 15:15-23.

Kwa upande mwingine, Biblia inatupa mifano ya kuonyesha kwamba imetupasa tukubali tunapokosa. Kati ya hiyo ni ule wa Yuda. Yeye alikosa katika shughuli zake pamoja na Tamari binti-mkwewe mjane. Alipokabilishwa daraka lake la kumtia mimba, Yuda alikubali, akisema: “Yeye ni mwenye haki kuliko mimi.” (Mwanzo 38:26) Lakini angalau alikubali kwamba alikuwa amekosa.

Kisha alikuwako Mfalme Daudi. Yeye alifanya mambo mbalimbali ili afiche dhambi yake aliyofanya pamoja na Bathsheba. Alipokabiliwa na nabii Nathani, Daudi aliungama, akisema: “Nimemfanyia [Yehova] dhambi.” (2 Samweli 12:13) Ndiyo, Daudi alikubali hivyo kwamba yeye alikuwa na hatia ya kosa.

Matokeo Mazuri

Itafaa tuikumbuke mifano hiyo ya zamani na kukubali tunapokosa. Kati ya mambo mengine, kufanya hivyo kunatokeza uhusiano ulio bora pamoja na jamaa zetu. Vilevile tutapatana vizuri zaidi na wakubwa wetu kwa kutokujaribu mno saburi yao. Kwa wazi, tunaambiwa katika Maandiko hivi: “Iwapo roho ya mtawala inapanda juu yako, usiache mahali pako mwenyewe. Kwa maana utulivu wenyewe unapunguza dhambi zilizo kubwa”​—ndiyo, hata makosa yaliyo mazito sana.​—Mhubiri 10:4, NW.

Namna gani tukiwa katika cheo chenye madaraka? Kuwa na nia ya kukubali kwamba tumekosa kutatupatia heshima kutoka kwa wale walio chini yetu. Zaidi ya hayo, tukiwa na maoni hayo tutakuwa katika hali ya kufanya maendeleo ya kushinda udhaifu wetu.

Sana sana ni jambo la lazima kwamba tudumishe dhamiri safi na uhusiano mzuri pamoja na Mungu wetu. Kwa sababu hiyo, iwapo tunafanya kosa zito, jambo la kwanza, na tukubali kwamba tumefanya dhambi. Katika sala yenye bidii, na tumwombe Baba yetu wa kimbingu atupe msamaha wenye rehema kupitia Yesu Kristo. (Zaburi 103:10-14; 1 Yohana 2:1, 2) Vilevile na tufaidike sana na msaada wa kiroho unaopatikana kwetu. (Yakobo 5:13-16) Huo ndio mwendo wa hekima, kwa maana Neno la Mungu linatuambia: “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema.”​—Mithali 28:13.

Misaada ya Kusaidia Kushinda Maelekeo hayo

Kwa wazi, tunahitaji msaada ikiwa tutashinda maelekeo hayo ya kutokukubali tunapofanya kosa. Mara nyingi ucheshi utasaidia, hasa ikiwa kosa si zito mno au kubwa sana. Hivyo mke mmoja mzuri wa nyumbani alikuwa akibeba sahani kadha za chakula wakati alipojikwaa akaangusha lundo zima, akizivunja zote. Alipoona hivyo, alianza kicheko, kwa maana kwake ilionekana kuwa jambo hilo halingeweza kumpata yeye. Lakini likampata! Ndiyo, mara nyingi ucheshi utatuzuia tusijione wenyewe kwa uzito mno, ambayo mara nyingi ndiyo sababu inayotufanya tusikubali kwamba tumekosa.

Unyofu na kufikiria wengine vilevile unatakwa. Ikiwa watu fulani wana haki ya kujua kwamba tumekosa, imetupasa tuwe na nia ya kulikubali kosa. Sana sana kufikiria wengine kumepasa kutuongoze tukubali iwapo mtu mwingine angelaumiwa na kupata hasara kwa sababu ya kosa letu. Maneno haya ya Yesu yanahusu hilo: “Na kama mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.”​—Luka 6:31.

Unyenyekevu vilevile utatusaidia tukubali kosa. Tunapofikiria sana jambo hilo, kushindwa kukubali kosa kunakaribia kuwa unafiki, sivyo? Wala mtu mwenye kiburi wala mnafiki hana kibali ya Mungu.​—Mithali 21:4; Yakobo 3:17.

Kudumisha uhusiano wa karibu sana na Yehova kutakuwa msaada mkubwa kuliko yote katika kuwa na nia ya kukubali tunapofanya kosa. Sababu gani? Kwa sababu tutaelekea kumpelekea mahangaikio na makosa yetu yote katika sala ya unyenyekevu. Kisha, tukiwa na hakika ya kupata msaada na rehema yake, tutakuwa na “amani ya Mungu” isiyo na kifani.​—Wafilipi 4:6, 7.

Basi, kwa kuwa sote tunakosa, na tukiri makosa yetu. Tunapokosa na tukubali kwa unyenyekevu. Ndipo acheni tujitahidi kutengeneza makosa yetu, kwa faida yetu wenyewe na kwa faida ya wengine.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Daudi aliungama: “Nimemfanyia [Yehova] dhambi”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki