Kwa Nini Ukubali Kosa?
HILO lilikuwa mojawapo makabiliano ya kivita yasiyo ya kawaida zaidi katika historia. Mjumbe mmoja mwanamke asiye na silaha aliwarejesha nyumbani askari-jeshi 400 wenye nia ngumu waliokuwa wameazimia kujilipiza kisasi kwa ajili ya matusi fulani. Baada ya kusikia sihi za mwanamke mmoja tu aliye hodari, kiongozi wa watu hao aliacha mradi wake.
Kiongozi huyo alikuwa Daudi, ambaye baadaye alikuja kuwa mfalme wa Israeli. Alimsikiliza yule mwanamke Abigaili kwa sababu alitaka kumpendeza Mungu. Abigaili alipomwonyesha kwa busara kwamba kumlipa kisasi mume wake, Nabali, kungesababisha hatia ya damu, Daudi alipaza sauti hivi: “Na ahimidiwe BWANA [Yehova, NW], Mungu wa Israeli, ambaye amekuleta hivi leo kunilaki; na ibarikiwe busara yako, na ubarikiwe wewe, uliyenizuia hivi leo nisimwage damu, wala kujilipiza kisasi kwa mkono wangu mwenyewe.” Daudi alishukuru kwamba Mungu alimtumia Abigaili kumzuia asifanye kosa zito.—1 Samweli 25:9-35.
Katika zaburi moja, Daudi aliuliza hivi: “Ni nani awezaye kuyatambua makosa yake?” (Zaburi 19:12) Kama vile yeye, huenda tusitambue makosa yetu isipokuwa yakionyeshwa kwetu na mtu fulani. Kwenye pindi nyingine matokeo yasiyofaa hutulazimisha tung’amue kwamba tumekosea, hatujawa wenye hekima, au tumetenda bila fadhili.
Hakuna Sababu ya Kukata Tamaa
Ingawa sisi sote hufanya makosa, hayo hayapasi yawe sababu ya kukata tamaa. Balozi Edward John Phelps alionelea hivi: “Mwanamume ambaye hafanyi makosa kwa kawaida huwa hafanyi lolote.” Na mwanafunzi Mkristo Yakobo alisema hivi: “Twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi.” (Yakobo 3:2) Je! mtoto angejifunza kutembea bila kujikwaa wakati wowote? La, kwani mtoto hujifunza kutokana na makosa na kuendelea kujaribu mpaka usawaziko unatimizwa.
Ili kuwa na maisha yenye usawaziko, sisi twahitaji pia kujifunza kutokana na makosa yetu na yale ya wengine. Kwa kuwa Biblia husimulia maono ya wengi ambao hali zao huenda zikafanana na zetu wenyewe, twaweza kusaidiwa kuepuka kufanya makosa yaleyale waliyoyafanya. Basi, twaweza kujifunza nini kutokana na makosa yao?
Unyenyekevu Sifa Iliyo Muhimu
Somo moja ni kwamba Mungu hawahukumu wote wanaofanya makosa lakini huwahukumu wale tu wanaokataa kuyarekebisha ikiwa hilo lawezekana. Mfalme Sauli wa Israeli hakuyatii maagizo ya Yehova juu ya uangamizo wa Waamaleki. Alipokabiliwa na nabii Samweli, kwanza Sauli alipunguza uzito wa mambo kisha akajaribu kulaumu wengine. Alihangaikia zaidi asitwezwe mbele ya wanaume wake kuliko kukosolewa. Kwa hiyo, ‘Yehova alimkataa asiwe mfalme.’—1 Samweli 15:20-23, 30.
Ingawa Daudi, mwandamizi wa Sauli, alifanya makosa mazito, alisamehewa kwa sababu alikubali shauri na nidhamu kwa unyenyekevu. Unyenyekevu wa Daudi ulimsukuma atii maneno ya Abigaili. Majeshi yake yalikuwa tayari kabisa kupigana. Lakini, akiwa mbele ya watu wake, Daudi alikubali kwamba alikuwa amefanya uamuzi usio na msingi. Muda wote wa maisha yake, unyenyekevu wa jinsi hiyo ulimsaidia Daudi ajaribu kupata msamaha na kurekebisha hatua zake.
Unyenyekevu pia huwasukuma watumishi wa Yehova warekebishe maneno yasiyofikiriwa kimbele. Katika kikao kimoja cha hukumu mbele ya Sanhedrini, kuhani mkuu aliamuru kwamba Paulo apigwe kofi. Mtume huyo alijibu vikali: “Mungu atakupiga wewe, ukuta uliopakwa chokaa.” (Matendo 23:3) Labda kwa sababu ya kutoona vizuri, Paulo hakung’amua yeye alikuwa akimwambia nani hivyo mpaka wale waliokuwa wamesimama karibu walipouliza: “Je! unamtukana Kuhani Mkuu wa Mungu?” Ndipo, Paulo akakiri kosa lake mara moja, akisema: “Sikujua, ndugu zangu, ya kuwa yeye ni Kuhani Mkuu; maana imeandikwa, Usimnenee mabaya mkuu wa watu wako.” (Matendo 23:4, 5; Kutoka 22:28) Ndiyo, Paulo alikubali kosa lake kwa unyenyekevu.
Walikubali Makosa
Biblia huonyesha pia kwamba watu fulani walibadili njia yao ya kufikiri yenye makosa. Mathalani, fikiria yule mtunga-zaburi Asafu. Kwa sababu watu waovu walionekana kuwa na hali njema, alisema hivi: “Hakika nimejisafisha moyo wangu bure.” Lakini Asafu alirudiwa na fahamu zake baada ya kwenda kwenye nyumba ya Yehova na kutafakari juu ya manufaa za ibada safi. Zaidi ya hayo, alikubali kosa lake katika Zaburi 73.
Yona pia aliruhusu kufikiri kusikofaa kuharibu maoni yake. Baada ya kuhubiri katika Ninawi, alihangaikia kutetewa kwake kibinafsi badala ya kuokoka kwa wakaaji wa jiji hilo. Yona hakupendezwa wakati Yehova alipokosa kuwaadhibu Waninawi ijapokuwa toba yao, lakini Mungu alimsahihisha. Yona alikuja kung’amua kwamba maoni yake yalikuwa yenye kosa, kwani kitabu cha Biblia chenye jina lake hukiri makosa yake kwa haki.—Yona 3:10–4:11.
Akidhani kimakosa kwamba Yehova Mungu, wala si Shetani Ibilisi, ndiye alikuwa akisababisha msononeko wake, yule mtu Ayubu alijaribu kuthibitisha kwamba yeye hakustahili mateso yake. Hakutambua suala lililokuwa kuu zaidi: Je! watumishi wa Mungu wangebaki wakiwa waaminifu-washikamanifu kwake wakiwa chini ya mtihani? (Ayubu 1:9-12) Baada ya Elihu na vilevile Yehova kumsaidia Ayubu aone kosa lake, alikubali hivi: “Nimesema maneno nisiyoyafahamu . . . Kwa sababu hiyo najichukia nafsi yangu, na kutubu katika mavumbi na majivu.”—Ayubu 42:3, 6.
Kukubali makosa hutusaidia kudumisha uhusiano mzuri na Mungu. Kama vile vielelezo vilivyokwisha kutajwa vionyeshavyo, yeye hatatuhukumu kwa ajili ya makosa yetu tukiyakubali na kufanya kadiri tuwezavyo kurekebisha kufikiri kusikofaa, maneno yasiyofikiriwa kimbele, au matendo ya kipumbavu. Twaweza kutumiaje ujuzi huo?
Kufanya Jambo Fulani Kuhusu Makosa Yetu
Kukiri kosa kwa unyenyekevu na kufanya jambo fulani kulihusu kwaweza kuimarisha vifungo vya familia. Mathalani, labda kwa sababu ya uchovu au udhiko, huenda ikawa mzazi alikuwa mwonevu katika kumtia mtoto wake nidhamu. Kukataa kusahihisha kosa hilo kwaweza kuwa na matokeo mabaya. Kwa sababu hiyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Nanyi, akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana [Yehova, NW].”—Waefeso 6:4.
Mkristo mchanga aitwaye Paul akumbuka hivi kwa uchangamfu: “Sikuzote Baba aliomba radhi ikiwa alihisi kwamba alikuwa ameitikia kwa tendo lenye kupita kiasi. Hilo lilinisaidia kumstahi.” Ni jambo la kuamuliwa binafsi kama kuomba radhi kunahitajika katika hali hususa. Hata hivyo, kuomba radhi kwahitaji kufuatwa na jitihada nyingi za kuepuka makosa ayo hayo katika wakati ujao.
Namna gani ikiwa mume au mke afanya kosa lisababishalo msononeko? Kukubali waziwazi, kuomba radhi kutoka moyoni, na roho ya kusamehe kutasaidia kudumisha uhusiano wao wenye upendo. (Waefeso 5:33; Wakolosai 3:13) Jesús, mwanamume Mhispania mwenye hali-moyo imara aliye katika miaka yake ya 50, si mwenye kiburi sana asiweze kumwomba radhi mke wake, Albina. “Tuna desturi ya kuombana radhi tunapoudhiana,” mke wake asema. “Hilo hutusaidia tuvumiliane kwa upendo.”
Mzee Afanyapo Kosa
Kukubali makosa na kuomba radhi kwa moyo mweupe kutasaidia pia wazee Wakristo wafanye kazi pamoja kwa upatano na ‘kuheshimiana.’ (Warumi 12:10) Huenda mzee akasita kukubali kosa kwa sababu ahofu kwamba hilo litadhoofisha mamlaka yake katika kutaniko. Hata hivyo, kujaribu kutetea, kupuuza, au kupunguza uzito wa kosa kwaelekea zaidi kuwasababisha wengine wakose kuwa na uhakika katika uangalizi wake. Ndugu mkomavu aombaye radhi kwa unyenyekevu, labda kwa sababu ya maneno yasiyofikiriwa kimbele, hujipa staha ya wengine.
Fernando, mzee mmoja katika Uhispania, akumbuka pindi fulani ambayo mwangalizi wa mzunguko aliyekuwa akisimamia kusanyiko kubwa la wazee alitoa taarifa isiyo sahihi kuhusu jinsi mkutano upasavyo kuongozwa. Ndugu mmoja aliposahihisha kwa staha yale aliyokuwa amesema, mwangalizi huyo wa mzunguko alikiri mara moja kwamba alikuwa amekosea. Fernando akumbuka hivi: “Nilipomwona akikubali kosa lake mbele ya wazee wote hao, hilo lilinivutia sana. Nilimstahi zaidi sana baada ya kuomba radhi huko. Kielelezo chake kilinifunza jinsi ilivyo muhimu kutambua kupungukiwa kwangu mwenyewe.”
Uwe Mwepesi Kukubali Kosa
Kwa kawaida kuomba radhi huthaminiwa, hasa kunapofanywa upesi. Kwa kweli, yafaa zaidi tukikubali kosa upesi. Kutoa kielezi: Mnamo Oktoba 31, 1992, Papa John Paul 2 alikubali kwamba lile Baraza la Kuhukumu Wazushi wa Kidini lilikuwa limetenda “kimakosa” miaka 360 iliyopita kwa kumwadhibu Galileo kwa sababu ya kudai kwamba dunia si kitovu cha ulimwengu wote mzima. Lakini, kuahirisha kuomba radhi kwa muda mrefu sana kwaelekea kupunguza thamani yako.
Ndivyo ilivyo katika mahusiano ya kibinafsi. Kuomba radhi upesi kwaweza kuponya udhiko lililosababishwa na neno au tendo lisilo la fadhili. Yesu alitusihi tusikawie kufanya amani, akisema: “Ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako.” (Mathayo 5:23, 24) Mara nyingi, kurejesha mahusiano yenye amani hutaka tu tukubali kwamba tulishughulikia mambo isivyofaa na kuomba msamaha. Kadiri tungojavyo, ndivyo inakuwa vigumu zaidi kufanya hivyo.
Wenye Furaha Kukubali Makosa
Kama vile vielelezo vya Sauli na Daudi vionyeshavyo, njia tunayoshughulikia makosa yetu yaweza kuathiri maisha zetu. Sauli alikinza shauri kwa ukaidi, na makosa yake yaliongezeka, hatimaye yakifikia upeo katika kifo chake akiwa bila upendeleo wa Mungu. Hata hivyo, yajapokuwa makosa na dhambi za Daudi, alikubali kukosolewa kwa hali ya toba akabaki akiwa mwaminifu kwa Yehova. (Linganisha Zaburi 32:3-5.) Je! hiyo si tamaa yetu?
Thawabu iliyo kuu zaidi ya kukubali na kurekebisha kosa au kutubu dhambi ni kujua kwamba imesamehewa na Mungu. “Mwenye furaha ni yule, . . . ambaye dhambi yake imefunikwa,” akasema Daudi. “Mwenye furaha ni yule, ambaye Yehova hahesabu kosa lake.” (Zaburi 32:1, 2, NW) Basi, ni jambo la hekima kama nini kukubali kosa!
[Picha katika ukurasa wa 29]
Je! mtoto angejifunza kutembea bila kujikwaa wakati wowote?