Mahubiri ya Mlimani—“Jiwekeeni Hazina Mbinguni”
AKIENDELEZA shauri lake juu ya uhitaji wa kuepuka unafiki katika kuabudu, Yesu alizungumza juu ya mtego wa kupenda mali. Alianza kwa kusema hivi: “Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba.”—Mt. 6:19.
Yesu alifahamu vizuri sana maelekeo ya wanadamu ya kuweka tumaini katika lundiko la mali. Aliwaonya wasikilizaji wake ‘waache’ (NW) kufanya hivyo, hakuna thamani yenye kudumu katika hazina za kidunia. Yawe ni mavazi ya bei ghali, fedha au mali nyinginezo vitu hivyo vilivyowekwa hazina havina budi kuchakaa. Kwa mfano, “nondo” anaweza kuharibu vitambaa vya thamani; madini ya thamani yaweza kuharibiwa na “kutu.” (Linganisha Yakobo 5:1-3.) Hata kabla ya kuchakaa kuna hatari ya kuibwa. Katika Palestina ya kale wevi walikuwa ‘wakivunja na kuiba’ kwa kutoboa kuta za udongo za nyumba.
Hivyo, Yesu alitangaza hivi: “Bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi.” (Mt. 6:20) Mtu anaweza kuweka hazina zisizoharibika kwa kuweka kumbukumbu “mbinguni” (yaani, pamoja na Mungu) la kazi njema. Kwa habari ya jambo hilo mtume Paulo aliwaonya Wakristo wenye utajiri “watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.”—1 Tim. 6:17-19; Tito 3:8.
Yesu alitoa sababu ya kuepuka kupenda mali: “Kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako.” (Mt. 6:21) “Hazina” ya mtu ni jambo lile analoliona kuwa la thamani kweli kweli. Juu ya jambo hilo anaweka “moyo” wake, chanzo cha makusudi, tamaa na mapendo. Iwapo hazina inayovutia moyo wa mtu ni yale tu ambayo ulimwengu huu unaweza kutoa, jambo hilo litaharibu uhusiano wake pamoja na Mungu, ambaye hutaka utumishi “kwa moyo mkamilifu.” —1 Nya. 28:9; Mt. 22:37.
Ili kuwasaidia wasikilizaji wake waepuke mtego wa kupenda mali. Yesu alitoa mifano miwili. Aliuanza wa kwanza kwa kusema hivi: “Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru.”—Mt. 6:22.
Ni jambo linalofaa kuliita jicho “taa ya mwili,” kwa kuwa nuru hufikia sehemu ya maono ya akili kupitia kwa macho. Mahali pa kwenda huku na huku ili kuona kila kitu, ‘jicho safi’ hutazama kitu kimoja peke yake. Katika njia ya mfano, kile ambacho mtu ‘hutazama kwa jicho’ lake kama kitu cha kukaziwa fikira na kutafakariwa kinakuwa na matokeo juu ya utu wake. Iwapo kufanya mapenzi ya Mungu ndio mradi mkuu maishani, ‘mwili wake wote utakuwa na nuru.’ Katika sehemu zote za maisha ataonyesha uangavu unaomtukuza Mungu na kufaidi wanadamu wenzake.—Linganisha Mithali 4:18, 25-27; Mathayo 5:14-16.
“Lakini jicho lako likiwa bovu,” akaendelea Yesu, “mwili wako wote utakuwa na giza.” (Mt. 6:23a) ‘Jicho bovu’ hutazama mambo mabaya kwa kuyatamani. (Angalia Mathayo 5:28; 2 Petro 2:14.) Kwa mtu anayefanya utajiri wa ulimwengu huu kuwa jambo kuu la kufuatia, ‘mwili wote utakuwa na giza.’—1 Tim. 6:9,10.
Akionyesha uzito wa jambo hilo, Yesu aliendelea kusema “Basi ile nuru iliyomo ndani yako ikiwa giza; si [ni] giza [kubwa] hilo!” (Mt. 6:23b) Sisi wanadamu tunakosa ukamilifu tangu kuzaliwa. (Rum. 5:12) Hata hivyo, hali ya mtu inakuwa mbaya zaidi akielekeza vibaya uwezo wake wa kupata maarifa (jicho la mfano). Kutamani utajiri huyaweka maisha yote ya mtu kwenye jambo moja. (Mit. 28:20) Ni kubwa kama nini,’ akatamka Yesu, giza hilo’ (NW) la wale ambao kupenda kwao hazina za kimwili huwaongoza wasukumie kando mambo ya kiroho.—Mt. 13:22.
Kisha Yesu akaongeza mfano wa pili: “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu.”—Mt. 6:24a.
Wenye kusikiliza Mahubiri ya Mlimani walikuwa wanafahamiana vizuri na utumwa, ambao ulifuata matakwa ya torati ya Musa. (Kut. 21:2, Law. 25:39-46) Mwenyeji wa mtumwa angeweza kumtazamia mtumwa ajitoe mwenyewe kabisa. (Linganisha Luka 17:7-10.) Inavutia kwamba, kitabu The Mishnah kinazungumza juu ya haki za “mtumwa mwenye wenyeji wawili,” kuonyesha kwamba katika pindi fulani mtumwa angeweza kuwa na mabwana wawili. Kuhusiana na maneno ya Yesu kwa habari hiyo, twasoma hivi katika kitabu Theological Dictionary of the New Testament:
“Mt. 6:24 na Lk. 16:13 yaelekea kuonyesha uwezekano wa mtumwa kuwa na wenyeji wawili wenye haki zinazolingana juu yake na hivyo wenye kudai utumishi unaolingana kwake. Hiyo ni hali ambayo ingeweza kuwa na iliyokuwapo. Hakika, kulikuwako watumwa ambao waliwekwa huru na bwana mmoja walakini si yule mwingine, hivyo wakawa nusu huru na nusu watumwa. Katika uhusiano huo [wa kuwa mtumwa mara mbili] kwa wazi, lilikuwa jambo lisilowezekana kabisa mtumwa kujitoa jinsi ile ile kwa wote wawili, sana sana kwa kuwa mapendezi na tamaa zao zingetofautiana sana. Yesu anaonyesha jambo hilo katika lugha ya watu walioishi katika wakati wake na watu Wake kwa kusema kwamba mtumwa huyo ange[penda] bwana huyu mmoja na [kuchukia] yule mwingine, yaani, kutoshikamana sana naye.”
Yesu alikazia somo kuu la mfano huo kwa kusema hivi: “Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.” (Mt. 6:24b) Usemi huo haumaanishi kwamba ni makosa kuwa na mali, bali, mahali pake, unakazia kwamba mtu hawezi “kutumikia” utajiri na wakati ule ule kumpa Mungu ibada kamili anayoihitaji. Mtu ambaye anampenda Mungu kweli kweli na kutaka kumtumikia kwa kukubalika anapaswa ‘kuchukia’ kabisa utumwa unaotokana na kufanya hazina za duniani kuwa mradi mkuu maishani.