Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 3/1 kur. 10-14
  • Upendo katika Matendo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Upendo katika Matendo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “NJIA ILIYO BORA”
  • NAMNA UPENDO UNAVYOPASWA KUONYESHWA KATIKA MATENDO
  • “UPENDO HAUPUNGUI NENO WAKATI WO WOTE”
  • “Endeleeni Kutembea Katika Upendo”
    Mkaribie Yehova
  • Upendo—“Njia Bora Zaidi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Fuateni Njia ya Upendo Ipitayo Zote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Upendo (Agape)—Usivyo na Ulivyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 3/1 kur. 10-14

Upendo katika Matendo

“Upendo haupungui neno wakati wo wote.”​—⁠1 Kor. 13:8.

1. Kwa sababu gani kukosekana kwa upendo wa kweli katika ulimwengu hakupaswi kutushangaze?

KATIKA ulimwengu huu, mara nyingi tunaona na kusikia neno “upendo.” Linaonekana katika nyimbo, vitabu na sinema na katika vikaratasi vya matangazo na katika vifungo vya mavazi. Hata hivyo tunaishi katika ulimwengu ambao upendo wa kujinyima unaonekana mara chache sana. Hilo halipaswi kuwa jambo la kushangaza, kwa kuwa watu wengi hutaja kwa makosa nyege (tamaa) na maono ya moyoni kuwa upendo. Wao hawafahamiani na upendo unaowatambulisha (unaoonyesha) wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo. Upendo huu unapita ule wa mtu kumpenda jirani yake kama anavyojipenda mwenyewe. Unatia ndani, kuwa na nia ya mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya ndugu zake Wakristo, ikiwa lazima. Hivyo mtu angekuwa akimwiga Yesu Kristo, aliyetoa uhai wake kwa kupenda kwa ajili ya wanadamu.​—⁠1 Yohana 3:​16-18.

2. Ni habari gani inayozungumzwa katika Wakorintho wa Kwanza sura ya 13?

2 Kwa wazi, upendo wa Kikristo ni wenye matendo, ukijionyesha katika mambo mema unayowafanyia wengine. Kwa kuwa ni maono tu ya moyoni, upendo huu hauwezi kufafanuliwa kwa urahisi. Walakini, njia ambayo katika hiyo unajionyesha inaweza kufafanuliwa. Na, katika 1 Wakorintho sura ya 13, tunaona ufafanuzi bora sana wa upendo ambao Wakristo wanapaswa kuwa nao. Katika sura hii mkazo hautiliwi juu ya upendo wa Mungu kwa wanadamu wala juu ya upendo wetu kwa Yehova Mungu. Bali mkazo unatiliwa juu ya namna upendo unavyopaswa kuonyeshwa wanadamu wenzetu.

3. Mengine ya magumu yaliyokuwako katika kundi la Korintho yalikuwa magumu gani?

3 Ndilo jambo walilohitaji Wakristo katika Korintho, kwa kuwa hawakuwa wakifurahia uhusiano (urafiki) bora kati yao wenyewe. Kama uchunguzi wa barua yote ya Wakorintho ya Kwanza unavyoonyesha wazi, kundi lililokuwako huko lilikuwa na magumu kama husuda (wivu), fitina, migawanyiko, kujisifu, uasherati, udanganyifu na kutumia wengine kujifaidi wenyewe. Wengine katika kundi la Korintho walitamani kujifanyia jina. Walitaka kushinda wengine katika uwezo wa kufanya mambo na katika karama (zawadi).​—⁠1 Kor. 1:​10, 11; 3:​2, 3; 4:6, 7; 5:​1, 2; 8:​7, 8; 8:​1, 2, 7-13; 11:​18, 19; 12:​14-18.

“NJIA ILIYO BORA”

4. Je! Wakristo wote katika karne ya kwanza walikuwa na karama zile zile?

4 Bila shaka, halikuwa kosa kuona karama zilizo kuu za roho kuwa jambo linalotamanika na mtu kutaka kutumikia kundi akiwa mtume, nabii au mwalimu. Walakini mtume Paulo aliwaambia: “Je! wote ni mitume? wote ni manabii? wote ni waalimu? wote wanatenda miujiza? wote wana karama za kuponya wagonjwa? wote wanena kwa lugha? wote wafasiri?” (1 Kor. 12:​29, 30) Hata hivyo, kulikuwako jambo ambalo wote katika kundi wangefanya. Kwa kweli, lilikuwa jambo bora zaidi kuliko kutafuta “karama zilizo kuu.” Hili linaonyeshwa wazi na namna mtume alivyowatia moyo: “Takeni sana karama zilizo kuu. Hata hivyo nawaonyesha njia iliyo bora.”​—⁠1 Kor. 12:31.

5, 6. (a) Mtume Paulo alimaanisha nini na usemi “njia iliyo bora”? (b) Alionyeshaje kwamba kuwa na uwezo wa kufanya mambo pamoja na karama silo lililokuwa jambo la maana zaidi kwa Wakristo wa kweli?

5 Njia hii iliyo bora ni njia gani? Ni njia ya upendo. Ndiyo, Wakristo katika Korintho walihitaji kubadili maoni yao juu ya “karama” na kuonyesha upendo wao kwa matendo. Akionyesha namna upendo ulivyo na thamani kubwa kuliko uwezo wa kufanya mambo pamoja na karama au vipawa, Paulo aliandika hivi: “Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa nabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo hainifaidii kitu.”​—⁠1 Kor. 13:​1-3.

6 Ikiwa Mkristo anaweza kusema lugha nyingine zaidi ya lugha yake ya kienyeji bila shaka hiyo inaweza kuwa karama yenye thamani. Kusema lugha ya malaika viumbe vya juu zaidi kuliko wanadamu yaweza kuwa karama kubwa hata zaidi. Walakini ikiwa mtu huyo angetumia karama hiyo kusitawisha sifa yake au ikiwa anaweza kuwa na makusudi mabaya katika njia nyingine yo yote, hangekuwa akiwajenga wanadamu wenzake, kutia na ndugu zake Wakristo. Yeye angekuwa kama mlio mkubwa ufanywao na chombo cha shaba au upatu. Zaidi ya hayo, pasipo upendo, karama za unabii, maarifa ya mwujiza na imani ya mwujiza hayawezi kuwajenga wengine. Karama au zawadi hizi hazingekuwa zikitumiwa kwa kufaa. Vivyo hivyo, mtu ambaye hutoa vitu vyake kwa ukarimu kusudi tu ajisifu, hangefaidika. Hangepata thawabu yo yote. Namna gani kama akichagua kupatwa na mateso au hata kufa, labda akiwa na kusudi la kuonekana hodari machoni pa wanadamu? Vivyo hivyo, ikiwa hampendi Mungu na wanadamu wenzake, nia yake ya kujinyima kuliko kukubwa zaidi hakuwezi kumfaidi katika njia yo yote yenye kudumu. Zaidi ya kusifiwa na wanadamu wafao, hangepata zawadi nyingine yo yote. (Linganisha Mathayo 6:​1-4.) Kwa kuwa upendo ni wa maana sana, kila mmoja wetu anapaswa kuangalia aone anaonyesha sifa hii bora sana kwa kadiri gani. Je! kweli sisi tunaitafuta “njia iliyo bora”?

NAMNA UPENDO UNAVYOPASWA KUONYESHWA KATIKA MATENDO

7. Tunaonyeshaje upendo tunapopatwa na hali zenye kujaribu?

7 Wakorintho wa Kwanza 13:4 linasema: “Upendo huvumilia, hufadhili.” Hii inahitaji nini kwetu? Tunapokasirishwa, tunapoonewa, tunaposumbuliwa au kusingiziwa, tunapaswa kufanya nini? Mtu mvumilivu anaepuka kutenda kwa haraka au kupiga makelele kwa hasira. Atavumilia kwa ustahimilivu chini ya hali zisizofaa, afanye hivyo akitumaini kwamba wale wanaomletea hali hizo zisizopendeza watasaidiwa kubadili njia zao. Kwa sababu iyo hiyo, tunapaswa kuwa wenye fadhili, si wakali, wakatili au wenye chuki, bali wenye huruma, wapole, wenye urafiki na wenye kusaidia wengine. (Linganisha Warumi 12:​20, 21; 1 Pet. 2:​18-23.) Kwa sababu ya kuwahangaikia waamini wenzetu, tunapaswa kuvumilia tabia pamoja na dhamiri dhaifu za wengine. Hatupaswi kusisitiza haki zetu lakini tuache kutumia uhuru wetu wa Kikristo kwa ukamili. Hivyo hatutawakwaza wengine, na kuwapa sababu ya kuacha ibada ya kweli.​—⁠Rum. 14:​1-4, 19-21.

8. Sababu gani hatuonyeshi upendo tunapotakabari na kujisifu pamoja na kuwa na wivu?

8 Tunaendelea kuambiwa: “Upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni.” (1 Kor. 13:4) Ikiwa kweli tunawapenda ndugu zetu Wakristo, tungewezaje kuwaonea wivu au kijicho kwa sababu ya mambo wanayotimiza, baraka zao au uwezo wao? Mahali pake, tungefurahi pamoja nao kwa sababu ya sehemu wanayoshiriki katika kulijenga kundi. (Rum. 12:​15, 16) Vivyo hivyo, tungewezaje kujipeleka mbele na kuzungumza juu ya yale tunayotimiza pamoja na maono yetu nyakati zote? Hili linaweza kuwavunja moyo wanaotusikiliza. Huenda wakaanza kufikiri kwamba wametimiza mambo madogo sana wakijilinganisha nasi. Kujivuna kwetu na kujisifu kungeweza kuwavunja wengine moyo na kumwondolea Yehova Mungu sifa anayostahili. Lo! namna hiyo ingekuwa kukosa upendo! Lingekuwa jambo bora zaidi kusema kidogo zaidi juu ya yale tumetimiza. Sisi ni watumishi tu wa Mungu, naye ndiye anayepaswa kusifiwa kwa sababu ya ukuzi wote wa kundi la Kikristo. (1 Kor. 3:5-9) Unyenyekevu utatulinda tusijifikirie makuu mno na utatuzuia tusijaribu kuwavuta wengine na ukuu tunaodhania kuwa nao.

9. Kwa kuwa upendo “haukosi kuwa na adabu,” hilo linatuhitaji tufanye nini?

9 Kuongezea hayo, upendo “haukosi kuwa na adabu.” (1 Kor. 13:5) Tunapokuwa na upendo halisi, tunachukia kila namna ya ubaya. Lakini mengi zaidi yanahusika. Usemi ‘kutokosa kuwa na adabu’ unaweza vilevile kumaanisha ‘kutokuwa mjeuri.’ (Tazama The New English Bible.) Katika mashirika yote, upendo unatokeza mwenendo unaofaa. Mtu mwenye upendo hadharau maskini na wenye uhitaji, akijiepusha na ushirika wao. Yeye hashirikiani na wachache tu anaochagua. (Linganisha Yakobo 2:​1-9.) Mwenendo unaofaa vile-vile unamaanisha kuheshimu mamlaka. Ikiwa tuna upendo halisi, tutaheshimu watu pamoja na mali zao. Bila shaka hilo linatia ndani mahali petu pa mikutano. Ni jambo lisilofaa kama nini watoto kuandika juu ya viti au kukimbia huku na huku, labda hata wakiangusha watu wengine! Mwenendo kama huo usio wa adabu haupaswi kuonekana katika kundi la Kikristo. Huonyesha sifa mbaya juu ya namna wazazi wanavyosimamia watoto wao.

10. Tunaweza kuonyeshaje kwamba hatutafuti faida zetu wenyewe?

10 Akiendelea kufafanua upendo, mtume Paulo anaandika hivi: “[Upendo] hautafuti mambo yake.” (1 Kor. 13:5) Ndiyo, unapendezwa na washiriki wote wa kundi​—⁠vijana kwa wazee, wagonjwa na walio dhaifu, wale wanaofanya kazi kwa bidii katika kufundisha, kuhubiri na kufanya wanafunzi. Upendo unakuwa macho kuona mahitaji ya waamini wenzetu, na unaitikia kwa haraka na kufadhili. Hausisitizi njia yake wenyewe. (1 Kor. 10:​23, 24) Sifa hii njema sana haihusiani hata kidogo na ile filosofia ya “mimi kwanza.” Haina uchoyo hata kidogo.

11. Kwa kuwa upendo “hauoni uchungu,”‏ tunapaswa kuepuka nini?

11 Kwa kuwa upendo “hauoni uchungu,” bila shaka ingekuwa makosa ikiwa tungetafuta sababu za kupiga makelele kwa hasira. (1 Kor. 13:5) Hatupaswi kuwa ‘wepesi wa kukasirika,’ na kuepuka kukasirika mara kwa mara. (Yak. 1:19) Katika jamaa, hii inawahitaji wote wavumilie makosa ya wengine. Na katika kundi, sana sana wazee wanapaswa kuweka mfano wa subira wakati ndugu na dada wanapoelekea kusahau na kutojali au wanaposhindwa kuona madaraka ya Kikristo kwa uzito.

12. Ni jambo gani linaloweza kuthibitisha kwamba hatuhesabu mabaya” tunayotendwa?

12 Zaidi ya hayo, kulingana na ufafanuzi wa Biblia wa upendo, hatupaswi ‘kuhesabu mabaya’ tunayofanyiwa. (1 Kor. 13:5) Kungekuwa kukosa upendo tukiweka kinyongo na kuwa tukihesabu-hesabu namna wengine walivyotukosea, kama kwamba tunaweka hesabu ya makosa yao. Wakati uliopita unapaswa kusahauliwa, nao wale waliotukosea hawapaswi kukosa kuonyeshwa fadhili.​—⁠Mit. 20:22; 24:29; 25:​21, 22.

13. Mengine ya mambo ya udhalimu ambayo upendo haufurahii ni mambo gani?

13 Ni jambo gani jingine ambalo upendo hautafanya? Upendo “haufurahii udhalimu.” (1 Kor. 13:6) Kwa hiyo, upendo haufurahi wakati wengine wanapotumbukia katika kosa, wanapojiaibisha na kuingia katika uharibifu. Wakristo wa kweli hawafurahi, wakisema kwamba mtu huyo alistahili kupatwa na yaliyompata. (Mit. 17:5; 24:​17, 18) Pamoja na hayo, hatupaswi kufurahi ikiwa mtu anajiponyoa kwa ujanja asipate adhabu anayostahili kupata. (Zab. 50:18) Hata hatupaswi kufurahia kuona mambo ya udhalimu yakionyeshwa katika sinema au vipindi vya television. Vilevile, lingekuwa jambo lisilofaa kuunga mkono washiriki wa kundi waasi, na kulaumu karipio walilopewa. Hilo haliwezi kumsaidia mkosaji achukue hatua ya kurudia afya ya kiroho na kuondoa udhaifu uliomwongoza katika kosa lake.

14. Upendo unafurahi pamoja na nini?

14 Tunapaswa kufurahia nini? Upendo “hufurahi pamoja na kweli.” Kwa sababu kweli inatofautishwa na udhalimu katika mstari huu, kwa wazi hii inamaanisha kwamba tunapaswa kufurahi tuonapo namna kweli inavyoongoza maisha za watu kwa nguvu sana na kutenda haki. Tunapaswa kufurahia mambo yote yanayoongoza kwenye baraka, yanayofaa na yenye kujenga wengine na yanayosaidia kuendeleza kweli na haki.

“UPENDO HAUPUNGUI NENO WAKATI WO WOTE”

15. Biblia inatupa uhakikisho gani kwamba upendo wa kweli hautapungukiwa na neno lo lote wakati wo wote?

15 Licha ya kuwa njia iliyo bora, njia ya upendo haitakwisha au ipungue. Tunaonyeshwa hili vizuri katika maneno haya: “Huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote. Upendo haupungui neno wakati wo wote.”​—⁠1 Kor. 13:​7, 8.

16. Upendo ‘unavumiliaje mambo yote’?

16 Kwa habari ya ‘kuvumilia mambo yote,’ upendo wa kweli hausukumiwi mbali kwa haraka, kuzuiliwa au kuachiliwa. Hauchukizwi kwa wepesi wala hauamui kwa haraka kwamba hakuna tumaini la wengine kufanya maendeleo. Tukiwa na upendo, tutaendelea kufanyia wanadamu wenzetu mema hata wasiposhukuru.​—⁠Mt. 5:44-48.

17. Upendo ‘unaamini mambo yote’ katika maana gani?

17 Tuyafahamuje maneno, ‘upendo huamini yote’? Bila shaka hii haimaanishi kwamba tutakuwa wajinga, tushindwe kufahamu yaliyo mabaya kweli kweli. Mahali pake, maana yake ni kwamba upendo hauna mashaka. Kwa hiyo, ijapokuwa ndugu zetu Wakristo huenda wakafanya na kusema mambo ambayo yanatuumiza, hatutaamua mara moja kwamba wanataka kutuumiza. Tunapouona mwenendo wa wengine, hatutawafikiria vibaya mara moja bali tutajaribu kuuona katika njia ifaayo. Tutawapa ndugu zetu Wakristo nafasi, bila kufikiri kwamba wana makusudi mabaya.​—⁠Mhu. 7:​21, 22.

18. Kwa habari ya tumaini na uvumilivu, upendo utatusaidia kufanya nini?

18 Vivyo hivyo, upendo unatumaini kwamba mambo yatakuwa mazuri. Hii haimaanishi kwamba upendo ni ujinga. Bali, unatazamia, ndiyo, unaomba matokeo yawe mema. Upendo unatumaini mema. Kwa hiyo, tunapotembelea watu katika eneo lenye watu wasioitikia, tunaweza, kwa mfano, kufanya hivyo tukitumaini kwamba, baada ya muda kupita, wengine wataigeukia kweli. (Linganisha Warumi 9:1-3.) Vilevile, mwenzi wa ndoa anayeamini anatumaini kwa kufaa kwamba hatimaye (baadaye) asiyeamini atakubali “habari njema.” (1 Pet. 3:​1, 2) Upendo unapotusaidia kutumaini matokeo mema, vilevile unatusaidia kuvumilia kila namna ya mateso, majaribu, matukano na kusingiziwa.

19. Sababu gani hatutajuta hata kidogo kwa sababu ya kuonyesha upendo?

19 Katika hali zo zote, kuonyesha upendo kutatusaidia sikuzote. Hatutasahau hata kidogo kwamba tulionyesha upendo. Upendo wa kweli, upendo wa kujinyima, haujafanya hata kidogo hali mbaya iwe mbaya zaidi. Basi, je! sisi hatuna sababu nzuri ya kumwiga Baba yetu wa mbinguni ambaye sifa yake kuu ni upendo?​—⁠1 Yohana 4:​7, 8.

20. (a) Kama inavyoonyeshwa katika 1 Wakorintho 13:8-13, njia ya upendo itaendelea kuwa “njia iliyo bora” kwa muda gani? (b) Ijapokuwa karama za mwujiza za roho zimekoma; bado wanafunzi wa kweli wa Kristo wanaweza kujulikanaje?

20 Si katika taratibu hii ya mambo tu, bali kwa umilele wote, upendo utaendelea kuwa njia iliyo bora. ‘Hautapungua neno’ wakati wo wote, au kufika mwisho. Mtume Paulo alionyesha hivyo aliposema: “Ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika. . . . Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo.” (1 Kor. 13:​8-13) Historia ya kundi la Kikristo inathibitisha kwamba karama za mwujiza zilikoma, kwa wazi kufikia karne ya pili W.K. Hata hivyo, wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo wanaweza kujulikana, mpaka hivi leo, kwa sababu ya upendo walio nao kati yao.

21. Kwa kuwa upendo ni wa maana sana, tunaweza kujiuliza maulizo gani?

21 Namna gani sisi mmoja mmoja? Je! sisi tunapanua upendo tulio nao kwa ndugu zetu Wakristo? Je! sisi tunafanya maendeleo katika kuonyesha upendo kama vile mtume Paulo alivyoufafanua? Bila shaka hivyo ndivyo tunataka kufanya. Kwa kuwa upendo ni tunda la roho ya Mungu, je! sisi tunaomba roho hiyo ili tuonyeshe upendo zaidi katika maisha zetu? (Gal. 5:22) Upendo na uendelee kuwa na matendo katika maisha zetu ili tuendelee kuishi, ndiyo, tuendelee kuonyesha upendo kwa umilele wote tukiwa watumishi washikamanifu wa Mungu mwenye upendo, Yehova.​—⁠1 Yohana 4:​20-5:3. ​—⁠Kutoka The Watchtower Sept. 15, 1978.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ili tuonyeshe upendo katika mikutano ya Wakristo tunapaswa kuangalia watoto

[Picha katika ukurasa wa 13]

Upendo katika matendo unaonyeshwa kwa kuwasaidia wengine

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki