Nyakati Zetu ni za Haraka Kadiri Gani?
“Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu [Yesu]. Lakini atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”—Marko 13:13, Habari Njema kwa Watu Wote.
1. Ni mateso gani ambayo Yesu alitabiria watu wa Mungu, nayo yametimizwa juu ya nani, na namna gani?
KAMA SEHEMU ya unabii wake wa ajabu juu ya “mwisho wa taratibu ya mambo,” Yesu alisema: “Kisha watawatoeni ili mteswe na kuuawa. Mataifa yote yatawachukieni kwa ajili ya jina langu.” (Mat. 24:9, Habari Njema kwa Watu Wote) Maneno hayo yametimizwa juu ya watu gani katika nyakati hizi za sasa? Bila shaka, ni juu ya mashahidi Wakristo wa Yehova! Ni wao peke yao kati ya dini zote ndio wameteswa na wafuasi wa chama cha kisiasa cha Nazi, Wakomunisti, serikali za kijeshi zenye kutumia nguvu na hata nchi za kidemokrasi kuzunguka dunia yote.
2. Mashahidi wa Yehova katika Afrika wamevumiliaje mateso hayo? (Zab. 37:39)
2 Katika miaka ya karibuni, imani thabiti ya Mashahidi wa huko Malawi ambayo wameonyesha wakati wa kupatwa na mauaji, kulalwa kinguvu kwa wanawake, mapigo na vifungo, imewapatia heshima na kustaajabiwa si na ndugu zao za kiroho tu, bali vilevile na watu wanaopenda uhuru kila mahali. Ijapokuwa hali imekuwa afadhali kidogo katika Malawi, nchi nyingine za Kiafrika zinatoa ripoti juu ya mateso yanayoongezeka.
Taifa jipya moja limeamuru wananchi wake wote wavae vitambulisho vya kisiasa. Katika nchi nyingine, usiku wa Ukumbusho, “ndugu” mmoja ‘wa uongo alisaliti kundi zima, hivi kwa-mba polisi wakaja kupazunguka mahali pa kukutania, wakiweka vikosi vyao vya askari karibu na mlango wa nyuma, kwa sababu fulani. Filimbi ilipopigwa, hao Mashahidi walikuta mlango wa mbele hauna askari wa kuulinda, wakaponyoka wote na kutawanyika usiku, isipokuwa wawili tu. Wakristo hao wawili walipigwa kijeuri sana, lakini imani yao ilikuwa imara nao walitoa ushuhuda bora barazani.
Bado katika nchi nyingine, Mashahidi washikamanifu waliokataa kusema maneno ya kisiasa ya kutukuza nchi yao walipigwa na kufukuzwa katika vijiji vyao. Wengine walidhihakiwa na kuambiwa, “Mnaweza kwenda ko kote, hata kwa Yehova wenu.” Imezidi kuwa vigumu sana kusafiri huku, na waangalizi wanaosafiri wamekamatwa. Walakini, “chakula” cha kiroho hakikosi katika kambi za gereza. Mashahidi hao waliokamatwa wamekuwa wakitazamia hata kushiriki makusanyiko ya mwaka huu ya “Imani Ishindayo.”
Nchi nyingine ya Kiafrika inatoa ripoti kwamba Mashahidi 22 walikamatwa, wakapewa mashtaka ya uongo kwamba wanaendesha shughuli za kisiasa, walipigwa vibaya, wakavuliwa mavazi na kubaki na nguo za ndani, kisha wakafungwa gerezani kwa mwezi mmoja wakiwa katika hali hiyo ya kuwa karibu uchi. Bado katika nchi nyingine, watatu walipigwa mpaka wakafa, na wengine wengi walihukumiwa kufa kwa sababu ya kutoshiriki siasa; wameomba rufani ya hukumu hiyo. Vilevile katika nchi ya Kiafrika, kasisi mmoja wa kanisa la Kikristo la Kimisri alitoa mashtaka ya uongo ya kwamba wanajitia katika siasa za Mashariki ya Kati, hivyo akasababisha kufungwa kwa Mashahidi wanaume 13 na wanawake 20, mmojawapo alikuwa ana mimba na mwenzake alikuwa na binti mdogo.
3. Watu wa Yehova wanaonyeshaje imani yao?
3 Ijapokuwa sana sana mambo yaliyotukia hivi karibuni katika Afrika yametajwa, nchi nyingine nyingi zilizo duniani zimekuwa zikiwakamata Mashahidi wa Yehova, hivi kwamba imekuwa vigumu zaidi kwao kuendesha utendaji wao wa kawaida na kutayarisha makusanyiko ya Kikristo. Wamisionari wamefukuzwa katika nchi fulani, na inazidi kuwa vigumu sana kutuma wamisionari katika mashamba mapya. Inakuwa sawasawa na vile Yehova alivyotangulia kusema kupitia kwa nabii wake Yeremia: “Nao watapigana nawe.” Hivyo ndivyo wanavyofanya hasa! lakini watu wa Yehova wanaendelea kutoa ushuhuda kamili, ijapokuwa maenezi makali na mateso wanayopata. Wanayaamini sana maneno haya ya ahadi: “Hawatakushinda; maana mimi [Yehova] nipo pamoja nawe . . . ili nikuokoe.”—Yer. 1:19.
“KAMA NYAKATI ZA NOA”
4. Ni kwa sababu gani Noa alivumilia? (Yak. 1:2-4)
4 Mzee Noa ndiye mtu aliyeishi katika nyakati za majaribu sana. Inaelekea kwamba kazi yake ya pekee ya kujitayarisha kwa ajili ya gharika iliendelea kwa muda wa miaka 60—kama muda ambao imetuchukua kuhubiri kusimamishwa kwa ufalme wa Mungu katika nyakati za kisasa. Ijapokuwa “dunia ikaharibika mbele ya Mungu . . . [nayo] ikajaa na jeuri,” Noa aliweza kuvumilia kwa sababu aliiamini kazi hiyo. Yeye aliendelea kutumika kwa bidii, akiwa “muhubiri wa haki” kama wanavyofanya Mashahidi wa Yehova wa nyakati hizi.—Mwa. 6:11; 2 Pet. 2:5, ZSB.
5, 6. (a) Tunaweza kuona ulinganifu gani kati ya siku za Noa na siku zetu? (b) Wakristo wamepaswa kujishughulisha na nini, na kwa sababu gani?
5 Walakini, wingi wa watu waliokuwako wakati huo, ulikuwa kama wanadamu wa leo. “Hawakujua kuna nini mpaka ile gharika ilipotokea, ikawachukua wote.” Kulingana na kifungu cha Luka cha maneno hayo ya Yesu:
“Watu waliendelea kula na kunywa, kuoa na kuolewa mpaka wakati ule Noa alipoingia katika safina. Tufani ikatokea na kuwaangamiza wote,”
Leo, ulimwengu mwovu na wenye nia kama hiyo, unakutana na “dhiki kubwa” ya uharibifu itakayoenea dunia yote!—Mat. 24:21, 37-35; Luka 17:26, 27, Habari Njema kwa Watu Wote.
6 Je! maneno hayo ya Yesu yaliyotangulia kutumiwa yanamaanisha kwamba ni vibaya Wakristo wanaoishi katika siku hizi za mwisho kula, kunywa na kuoa au kuolewa? Sivyo, Yesu hakumaanisha hivyo. Inafaa kujifurahisha chakula na kinywaji kizuri kwa kiasi. Vilevile, ndoa ni mpango ambao Mungu alifanyia wanadamu. Aliyokuwa akimaanisha Yesu ni kwamba haitupasi tuyaone mambo hayo kuwa ndizo shughuli (kazi) za maana kuliko zote katika maisha, tuziingilie kwa kadiri ya kusonga mambo ya kiroho. (1 Pet. 4:3; 1 Kor. 7:8, 29) Badala yake, imetupasa tupange maisha yetu vizuri ili tutangulize kazi ya maana ya ‘kuhubiri hii Habari Njema ya Utawala wa Mungu kama ushuhuda,’ kabla ya mwisho kufika.—Mat. 24:14, Habari Njema kwa Watu Wote.
“KAMA ILIVYOTOKEA WAKATI WA LOTI”
7. Ni haraka gani iliyotokea katika siku za Loti?
7 Wakati ule ambapo Ibrahimu na Loti walikuwa wakitumika kama mashahidi wa Mungu duniani, Yehova aliwaonya juu ya hukumu yake ambayo alikusudia kuileta juu ya Sodoma na Gomora. Hawakuweza kupatikana humo hata watu kumi wenye haki! Wakati malaika za Yehova walipokuwa wakijitayarisha kuuleta uharibifu uliokuwa umetabiriwa, Loti aliwasihi mara nyingi wanaume waliokuwa wamefanya uchumba na binti zake: “Amkeni! Tokeni mahali hapa, kwa sababu Yehova atauharibu mji huu!” Walakini, wale waliotazamiwa kuwa wakwe zake wa kiume, walilidharau onyo hilo la kimungu na kuliona kama mchezo tu. Lakini kulikuwa hakuna wakati wa kupoteza. “Hao malaika wakamharakisha Loti, wakisema: “Amka! Mchukue mke wako na mabinti wako wawili wanaopatikana huku, usije ukakumbwa katika uovu wa mji huu!’”—Mwa. 19:14, 15, NW.
8. (a) Ni “uovu” gani uliotokeza kuharibiwa kwa Sodoma na Gomora? (b) Sababu gani hilo limepaswa liwe jambo la kutuonya sisi leo?
8 “Uovu” huo ulikuwa nini? Ulitia ndani matendo ya uhanithi (matumizi mabaya ya ngono) ambayo katika ulimwengu wa sasa yamekuwa sehemu kubwa ya maisha, hata yanatukuzwa katika michezo na katika sinema na television. “Sodoma na Gomora, na miji ya kando kando yake . . . walifanya uzinzi na mambo yaliyo kinyume cha maumbile.” Vilevile, “waliendelea kula na kunywa, kununua na kuuza, kupanda mbegu na kujenga” pasipo kufikiria haki ya Mungu. Walijiingiza kabisa katika njia yao wenyewe ya maisha, ambayo ni njia ya choyo. Na lililowapata lilikuwa jambo gani? “Moto wa kiberiti ukanyesha kama mvua kutoka mbinguni na kuwaangamiza wote.” Yesu anaonya kwamba atatimiza hukumu inayofanana na hiyo wakati atakapofunuliwa, upesi, akiwa “Mwana wa Mtu.”—Mwa. 19:24-26, UV; Luka 17:28-30; Yuda 7, Habari Njema kwa Watu Wote.
9. Ni haraka gani inayotakiwa na sisi sasa, na tunawezaje kupata ulinzi?
9 Na tuwe kama Loti mwenye haki kwa kufanya haraka kuutoa ujumbe wa Yehova wa hukumu, unaotakiwa utolewe wakati wetu huu. Tusiwe kama mke wa Loti, bali, badala yake, tujilinde tusije tukatazama nyuma kwa kutamani faida za mali za ulimwengu huu uliohukumiwa kuangamizwa. (Luka 17:31, 32) Kujitia bidii kabisa katika kufanya mapenzi ya Mungu ambayo anataka yatimizwe wakati huu kutakuwa ulinzi wetu. Kumbuka, Petro alisema maneno haya kukamatana na kuokolewa kwa Loti: “Yehova ajua jinsi ya kuokoa watu wenye utawa katika jaribu, bali kuwaweka akiba watu wasio haki kwa siku ya hukumu wakatiliwe mbali.”—2 Pet. 2:6-9, NW.
KUTOA ‘USHUHUDA KAMILI’
10. (a) Kulikuwako na haraka gani wakati Yesu na mitume wake walipokuwa hapa duniani? (h) Yesu aliwazoezaje wanafunzi wake, na kwa kusudi gani?
10 Yesu na mitume wake walipokuwa hapa duniani, kulikuwa na haraka ya kwamba ushuhuda kamili utolewe wakati huo wa hukumu. Yesu mwenyewe aliweka mfano wa kufanya kazi hiyo, “alipita katika miji na vijiji akitangaza Habari Njema ya Utawala wa Mungu.” Mitume kumi na wawili pamoja na wengine, kutia na wanawake, walikwenda naye. Kwa kusudi gani? Ilikuwa kwa kusudi la kwamba apate kuwazoeza waweke maisha yao juu ya utumishi wa Mungu. Kwa njia hiyo wao vilevile wangeweza kushiriki kutoa onyo la uharibifu uliokuwa ukija juu ya “taratibu ya mambo” ya Kiyahudi, na kuwafariji watu walioonewa. Tena, wangesaidiwa wauvae utu wa Kikristo, wakionyesha katika maisha yao sifa zile zile za haki, na za ushikamanifu walizokuwa wameona Bwana wao akionyesha.—Mt. 9:35–10:15; Luka 8:1, 2, Habari Njema kwa Watu Wote; Luka 9:1-6; 10:1, 13-15; Efe. 4:24.
11. Wanafunzi hao walionyeshaje kwamba walikuwa wamejifunza vizuri somo lao?
11 Wanafunzi hao wa kwanza walijifunza vizuri somo lao. Walijitia katika utumishi wa bidii wa Ufalme, wakiwaendea watu kwa huruma po pote walipoweza kuwakuta—masokoni na mahali pengine pa kukutania watu wengi, katika masinagogi (kama ilivyokuwa desturi ya siku hizo) na nyumbani kwao. Hata walipotawanywa na mateso, waliendelea, “wakizitangaza habari njema za lile neno.”—Matendo 5:42; 8:4, NW; 16:13; 17:17.
12. Ni ushuhuda wa namna gani uliotolewa katika siku za mitume, na kwa matokeo gani?
12 Kuelekea mwisho wa miaka mingi ya kuhubiri kwa bidii, mtume Paulo aliweza kuwaambia wazee wenzake hivi: “Sikujizuia kuwaambia ninyi lo lote la mambo yaliyokuwa yenye faida wala sikujizuia kuwafundisha waziwazi na nyumba kwa nyumba. Lakini nilitoa ushuhuda kikamilifu kwa wote Wayahudi na Wagiriki juu ya toba kwa Mungu na kumwamini Bwana wetu Yesu.” (Matendo 20:20, 21, NW) Maneno haya “kamili” na “kikamilifu” yanaonekana mara nyingi katika kitabu cha Matendo kuambatana na ushuhuda wa haraka uliotolewa na mitume na wafanya kazi wenzao. (Matendo 2:40; 8:25; 10:42; 20:24; 23:11; 28:23, NW) Yalikuwa matokeo gani ya ushuhuda huo ulio “kamili”? Makundi ya waamini yalitokea na kusitawi kila mahali ambako “habari njema” zilihubiriwa. Na waangalizi wanaosafiri walipotembelea waamini hao ili wa-watie moyo katika utumishi wao, makundi yalitiwa nguvu. “Yalizidi kuwa imara katika imani, na idadi ya waamini ikaongezeka kila siku.”—Matendo 15:36, UV-16:5, Habari Njema kwa Watu Wote.
13. Ni hukumu gani ambayo Yehova alitimiza katika karne ya kwanza, lakini sababu gani kundi hilo la Kikristo liliokolewa?
13 Katika kutimiza lile onyo lililotolewa na Yesu na wanafunzi wake, Yehova katika wakati wake aliileta hukumu juu ya ‘kizazi chenye ukaidi’ cha Wayahudi, kizazi kilichokuwa kimemwua “Mkuu wa uzima,” Bwana Yesu Kristo. (Matendo 2:40; 3:15) Lile kundi la Kikristo—kile kikundi kilichokuwa kimefanya haraka sana kutii amri ya Bwana wao ya kutaka ‘habari njema ya ufalme ihubiriwe katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda,’ lilikuwa hali gani? Mwisho ulipofika, imani yao yenye bidii iliwaokoa. Uvumilivu wao ulilipwa.—Mt. 24:13-16.
SISI TUKO WAPI KULINGANA NA MAMBO YANAYOTUKIA?
14. Kwa kulinganisha, “habari njema” zimehubiriwa leo kwa kadiri gani, na kwa matokeo gani?
14 Tena, mwishoni mwa kizazi hiki, “habari njema” ‘zimehubiriwa katika kuumba kote kuliko chini ya mbingu.’ (Kol. 1:23, NW) Lakini shamba la kuhubiri ndani yake leo, linatia “ulimwengu wote,” pamoja na makao ya “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini,” na vilevile nchi nyingine nyingi katika Afrika, bara ya Amerika, Asia, nchi za Australia na visiwa vya bahari. Kazi ya kutoa ushuhuda huo wa kuzunguka dunia yote imeweza kufanywa kwa uwezo tu wa roho ya Yehova katika muda mfupi sana wa miaka kama 60 hivi. Na bado wapya wanaendelea kuja makundi makundi kwenye tengenezo la Yehova! Eneo la kazi hiyo limekuwa kubwa sana kuliko katika siku za mitume, ilipochukua punde kuliko miaka 40 kuwapa Wayahudi waliotawanyika onyo la mwisho.
15. Sababu gani zile “pepo nne” za Ufunuo 7 zimezuiwa?
15 Lakini, sisi tuko wapi kulingana na mambo yanayotukia? Ufunuo sura ya 7 unatuambia. Mtume Yohana ‘akawaona malaika wanne wamesimama katika pembe nne za dunia wakishika pepo nne za dunia.’ Hizo ni pepo za uharibifu, kwa maana baadaye, zinapaswa ‘ziiharibu nchi na bahari na miti.’ Lakini kwanza, “watumishi wa Mungu wetu” wanapaswa wapigwe muhuri katika vipaji vya nyuso zao. Huko nyuma katika mwaka 1914, wakati ‘utawala juu ya ulimwengu ulipogeuka kuwa wa Bwana wao [Yehova] na wa Kristo wake,’ watumishi hao walitamani sana mwisho ufike, wapate kukusanywa kwa Bwana wao mbinguni. Lakini sivyo—bado Yehova alikuwa amekusudia kuwapa kazi ya kufanya hapa duniani. Vile-vile, iliwapasa wao wenyewe wasafishwe kuwekwa tayari kufanya utumishi wa ukuhani wakati ujao katika ufalme wa Kristo wa miaka 1,000. Basi, zile “pepo nne za dunia” zilizuiwa kwa muda.—Ufu, 7:1-4; 11:15, Habari Njema kwa Watu Wote.
16. Ni kikundi gani kingine ambacho kimependelewa kwa vile malaika hao wangali ‘wakizishika sana pepo’ hizo, nao wana tumaini gani?
16 Kwa wingi wa rehema na fadhili zake za upendo, Yehova amewatumia “watumishi” hao wa Israeli wa kiroho, “Israeli wa Mungu,” katika kazi ya maana ya kusaidia kukusanya kikundi kingine—“umati mkubwa wa watu . . . wa kila taifa, ukoo, jamaa na lugha.” Washiriki wote wa 144,000 watakapokwisha kuingia katika utumishi wao katika mbingu, ule ‘utawala wa Bwana wetu na wa Kristo wake’ utaendelea kuwatawala wanadamu hapa duniani. Huo “umati mkubwa wa watu” ulianza kutokea tangu mwaka 1935, hivi kwamba leo watu zaidi ya milioni mbili wanatazamia kutumikia sikuzote wakiwa raia za kidunia za Ufalme huo. Hao ndio kiini (msingi) wa “dunia mpya,” jamii yenye haki ya wanadamu watakaoishi milele chini ya enzi kuu ya Yehova Mungu. (Ufu. 7:9, 10; 21:1, 3-5; 2 Pet. 3:13, Habari Njema kwa Watu Wote) Walakini, malaika hao bado wangali “wakishika pepo nne za dunia.” Kwa sababu gani?
17. Malaika wanaendelea ‘kuzuia pepo hizo’ kwa sababu gani?
17 Inaweza kuwa tu kwamba Yehova ana kazi zaidi hapa duniani ambayo anataka mashahidi wake wafanye. Kuna wengi zaidi wa huo “umati mkubwa wa watu” wanaotakiwa kukusanywa. Mamilioni ya watu wanaohudhuria mwadhimisho wa Ukumbusho katika miaka ya karibuni, pamoja na Mashahidi wanaoendelea kuongezeka daima katika nchi nyingi za Kiasia, visiwa vya bahari na nchi za Ulaya za Kikatoliki, wanaonyesha kwamba ile kazi ya kukusanya haijamalizika bado. Ni jambo la haraka kwamba watu wote wa Yehova wajitie bidii katika utumishi wake mpaka mwisho wa taratibu hii mbovu.—Marko 13:10; Efe. 5:15, 16.
18. (a) Inaonekana sasa kuna uchunguzi gani unaoendelea? (b) Sababu gani imetupasa tuliangalie sana onyo la Paulo katika 2 Wakorintho 13:5?
18 Vilevile, kama vile kulivyokuwako na kazi kubwa ya kuwachunguza-chunguza mabaki waliotiwa mafuta katika muda wa miaka kumi uliofuata mwaka 1914, yaonekana kwamba sasa kazi hiyo ya kuchunguza-chunguza wale wengine wanaojidai kuwa watu wa “umati mkubwa wa watu” inaendelea. Maneno ya mtume Paulo yanatuhusu sana sisi sote tunaoishi katika nyakati hizi za hatari: “Jichunguzeni ninyi wenyewe mpate kujua kama kweli mnayo imani. Jichungueni ninyi wenyewe.” (2 Kor. 13:5, Habari Njema kwa Watu Wote) Je! kweli tunathamini kujiweka kwetu wakf kwa Yehova—uhusiano wetu wa karibu sana tulio nao pamoja na yeye, na ambao umewezeshwa na dhabihu ya Yesu? Je’ tunathamini umoja tulio nao pamoja na Baba huyo na Mwana huyo katika kazi ya maana ambayo tumependelewa tushiriki wakati huu? Je! tunatumikia katika kumpenda Yehova na kumpenda jirani yetu? Au, nia yetu imekuwa kujiokoa wenyewe tu katika pigano la Har–Magedoni? Tukiwa washiriki wa “umati mkubwa wa watu,” je! tutaendelea kumtumikia Mungu “mchana na usiku” mpaka “dhiki kubwa”? Au, tutalegeza ulinzi wetu, tumruhusu Shetani atushinde kupitia kwa anasa, mambo yasiyo ya adili au masumbufu ya maisha?
19. (a) Sababu gani tunaweza kufurahi kwa vile malaika hao ‘wamezishika sana hizo pepo’ mpaka wakati huu? (b) Kama inavyoonyeshwa na 2 Wakorintho 13:11, tunawezaje leo kusonga pamoja na tengenezo la Mungu linalosonga mbele?
19 Wale malaika wanne hawataendelea ‘kuzishika sana’ pepo nne za dunia sikuzote. Tunaweza kufurahi kwa vile wamefanya hivyo mpaka wakati huu, na ya kwamba matokeo yake yatakuwa wokovu kwa mamilioni ya wanadamu. Lakini wakati unamalizika. Yatupasa tukeshe, tuwe macho, tuzidi kusonga mbele pamoja na tengenezo la Mungu duniani. Tuna furaha kama nini kwa vile tuko upande wa udugu wa ulimwenguni pote, ambao peke yake ndio wenye amani, nao umeungana katika kusifu jina la Yehova katika nyakati hizi za hatari! Inatupasa nyakati nyingine tugeuze nia au maoni yetu ya kipekee ili tusonge mbele pamoja. Lakini na tujiweke tayari kwa unyenyekevu kufanya hivyo nyakati zote, ili tutumikie kwa haraka na kuendelea katika furaha ile tunayoshiriki pamoja na watu wote wa Mungu. Kama Paulo alivyoshauri: “Hatimaye, ndugu, endeleeni kufurahi, kutengenezwa upya, kufarijika, kufikiri kwa upatano, kuishi kwa amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja na ninyi.”—2 Kor. 13:11, NW.
[Picha katika ukurasa wa 8]
‘HAWAJUI KUNA NINI’ Kama katika siku za Noa na za Loti, leo watu wengi wanashughulika sana na mambo ya kila siku ya maisha hata wanapuza haraka ya nyakati