Faraja Katika Wakati wa Huzuni
KIFO cha mpendwa kinaweza kuwa jambo la kufadhaisha zaidi ya mambo mengine yote maishani mwa mtu. Mwanamke mmoja kijana kutoka sehemu ya kusini ya Texas anaeleza hivi: “Nilipokuwa na mimba ya mtoto wangu wa pili, mume wangu aliuawa. Msiba huu mbaya ulishusha sana moyo wangu. Kuongezea maumivu yangu, mtoto wangu alizaliwa, akafa. Niliacha kusema na kila mtu, kutia na mtoto wangu mchanga. Lililonihangaisha hata zaidi ni kwamba, ingawa mwanangu mchanga alikuwa amepata umri wa kuweza kusema, hakuweza kusema hata neno moja. Wakati huu nilipokuwa nikijifikiria sana nisifahamu kwamba, ikiwa nisingemzungumzia, asingejifunza kusema daima.” Lo! namna mwanamke huyu alivyohitaji sana sana faraja! Furaha ni kwamba, alipata kutiwa moyo wakati mfanya kazi mwenzake alipoanza kumzungumzia juu ya Maandiko Matakatifu.
Ni tumaini gani linalotolewa na Biblia kwa watu wanaopata huzuni iletwayo na kifo? Maandiko yanaonyesha wazi kwamba hakuna sababu ya kuwa na wasiwasi juu ya waliokufa wala ya kujiachilia tushindwe kabisa na huzuni ya moyoni. Sababu ni kwamba, katika wakati wake Mungu, wapendwa waliokufa watarudishwa kwenye uzima. “Nina tumaini kwa Mungu,” akasema mtume Mkristo Paulo, “ya kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu.” (Matendo 24:15) Watakaofufuliwa kwenye uzima watapata faraja la kutopatwa tena na taabu, magonjwa au kifo. (Ufu. 21:3-5) Magonjwa yote yanayopata jamii ya kibinadamu yatasawazishwa kabisa na hali zilizobadilishwa zitakazokuwako baada ya ufufuo wao hata kwamba “mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.”—Isa. 65:17.
Kwa sababu Wakristo wa karne ya kwanza waliamini ufufuo, kifo cha wapendwa wao kilikuwa rahisi sana kuvumilia. Hawakuonyesha huzuni nyingi ya moyoni isiyozuilika inayoonyeshwa na watu wasio na tumaini lo lote. (1 The. 4:13) Lakini mtu anawezaje kuwa na uhakika kwamba kutakuwako na ufufuo?
Inafaa kuona kwamba, msingi wa tumaini la mtume Paulo ulikuwa juu ya imani yake katika Mungu. Kwa kuwa Mungu Mwenye Nguvu Zote Ndiye aliyeumba jamii ya kibinadamu, lazima vilevile awe na hekima na uwezo wa kufufua waliokufa, kuwaumba mara nyingine tena. Kwa kweli, tunayoambiwa na Biblia juu ya kuumbwa kwa mwanamume wa kwanza Adamu yanaweza kutusaidia tufahamu mwujiza wa ufufuo.
Adamu aliumbwa kutokana na chembe za ardhi. Ndiyo, chembe hizi hazina utu na hazina uwezo wa utendaji wenye akili au fikira. Hata hivyo, Mungu alipotengeneza chembe hizi zikawa mwili unaopatana na kuupa mwili huo nguvu kwa nguvu ya uhai, utu unaoweza kutofautishwa ulitokea—mwanamume mwenye uwezo wa kufikiri na kutumia akili na vilevile kupitisha uzima kwa kuzaa.—Mwa. 2:7.
Ebu angalia kwamba kilichomfanya Adamu awe mtu binafsi si vitu vilivyofanyiza mwili wake. Bali, alivyofanya Mungu kwa chembe za ardhi. Kwa hiyo, ufufuo hautegemei kuhifadhi au kutengeneza tena chembe zilizokuwa mwilini wa mtu kabla ya kifo chake. Hata wakati wa maisha yetu, chembe zinazofanyiza miili yetu zinaendelea kubadilika. Hivyo chembe zinazofanyiza mwili wako leo ni tofauti kabisa na zile za miaka saba hivi iliyopita. Hata hivyo, wewe ungali mtu yule yule. Vivyo hivyo, mtu akifufuliwa kwa uzima wa kibinadamu au wa kiroho, mwili wake utakuwa na sifa zote alizopewa na Mungu na kumfanya awe mtu yule yule aliyekufa. Atakuwa anafanana na alivyokuwa katika uzima wake wa kwanza.—1 Kor. 15:36-49.
Licha ya kutoa tumaini la ufufuo, Biblia inatoa msingi wa tumaini hilo. Kutokana na Maandiko tunajifunza kwamba kurudishwa kwa wafu kwenye uzima si jambo geni, jambo ambalo halijapata kutukia tena. Bali, Biblia inatoa mifano halisi ya wanaume, wanawake na watoto waliofufuliwa. (1 Fal. 17:21-23; 2 Fal. 4:32-37; Marko 5:41-43; Luka 7:11-15; Yohana 11:38-45; Matendo 9:36-42; 20:9-12) Ufufuo unaojulikana sana ni ule wa Yesu Kristo. Zaidi ya mashahidi 500 walimwona baada ya kufufuka kwake kutoka kwa wafu. (1 Kor. 15:6) Tukio hili lilihakikishwa vizuri sana hata kwamba mtume Paulo angaliweza kusema kwamba kukataa ufufuo huo kungalimaanisha kukataa imani ya Kikristo kwa ujumla. Tunasoma hivi: “Kama hakuna [ufufuo wa] wafu, Kristo naye hakufufuka; tena kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri kwetu ni bure na imani yenu ni bure. Naam, na sisi tumeonekana kuwa mashahidi wa uongo wa Mungu; kwa maana tulimshuhudia Mungu ya kuwa alimfufua Kristo, ambaye hakumfufua, ikiwa wafu hawafufuliwi. Maana kama wafu hawafufuliwi, Kristo naye hakufufuka. Na kama Kristo hakufufuka, imani yenu ni bure.”—1 Kor. 15:13-17.
Kwa mtume Paulo pamoja na mamilioni wengine, imani isiyotikisika katika ufufuo wa wafu ilikuwa ndiyo chanzo cha faraja isiyoshindwa. Na ndivyo ilivyo leo. Ni kweli, huenda wengine wakadhihaki wazo la ufufuo, wakisema kwamba ati hawajaona mtu ye yote akiinuka hata kidogo kutoka kwa wafu. Lakini kutoamini kwao kunawaweka katika hali bora zaidi kukabili (kukielekea) kifo? Kwa kukataa ushuhuda wa historia wa ufufuo uliopata kuwako, je! wanaweza kuwapa faraja gani waliofiwa? Wakati wao wenyewe wanapopoteza washiriki wa jamaa au rafiki wapendwa katika mauti, je! kutoamini kwao kunawasaidia wasiwe na huzuni nyingi ya moyoni? Mambo ya hakika yanajisemea.
Hivyo basi, katika nyakati za maombolezo, endelea kupata faraja kutokana na ahadi ya Mungu iliyo hakika ya ufufuo kama ilivyoandikwa katika Biblia. Hakuna tumaini jingine. Usiliache. Pia, pata uradhi katika kuletea wanaoomboleza faraja ya kweli kwa kushiriki pamoja nao ujumbe wa Biblia juu ya ufufuo.