Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 4/1 kur. 8-11
  • Wakati Watoto Wanapokuwa Wapotovu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakati Watoto Wanapokuwa Wapotovu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UBORA WA MAZOEZI YANAYOFAA
  • WAKATI WAZAZI WAMEKOSA KUJALI
  • UASI YAJAPOKUWA MAZOEZI YA MAPEMA
  • KUDUMISHA NIA INAYOFAA
  • Kufurahisha Mioyo ya Wazazi Wako
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Hadithi ya Mwana Mpotevu
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Mwige Yehova Unapowazoeza Watoto Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kuendelea Kupashana Habari
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 4/1 kur. 8-11

Wakati Watoto Wanapokuwa Wapotovu

TINEJA (kijana wa miaka 13-19) mwenye nguvu na afya amekaa kilegevu kitandani katika nyumba moja mjini New York. Mama yake amwita mara nyingi aamke amsaidie na kazi ngumu lakini kijana hamsikilizi. Mama anapozidi kumkaza, kijana huyo anawaka kwa hasira kali. Anang’oa simu ukutani, na kuvunja viti na meza na kufuli ya mlango wa nje wa nyumba. Wakati huu wote akiwa anapiga kelele: “Nitakuua!” Mwishowe hasira isiyozuilika inapoa.

Kijana huyu mpotovu haheshimu baba yake wala mama yake. Kwa kweli, yeye haheshimu mamlaka yo yote anapozunguka-zunguka mabarabarani mjini na wahuni wengine, huku wakibeba bastola wasiyoruhusiwa.

Wazazi wengi walio katika hali kama hiyo wanauliza: ‘Hili lilitokeaje? Tulikosea wapi?’

UBORA WA MAZOEZI YANAYOFAA

Nyakati nyingine huenda kushindwa kwa wazazi kukahusika. Ikiwa wazazi wanakosa kufunza watoto wao kwa maneno na mfano, hawawezi kutazamia kupata matokeo mazuri. Biblia inasema:.“Fimbo na maonyo hutia hekima; bali mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye.” (Mit. 29:15) Mazoezi yanayofaa yanapaswa yaanze mapema iwezekanavyo, tangu utotoni. Kwa sababu alipata mafunzo ya mapema, Daudi angaliweza kusema hivi katika mojawapo ya zaburi zake: “Kwako [Yehova] nalitupwa tangu tumboni, toka tumboni mwa mamangu ndiwe Mungu wangu.” (Zab. 22:10) Vivyo hivyo, Timotheo aliyafahamu maandishi matakatifu “tangu utoto.” Tangu yale ya mwanzo-mwanzo aliyokumbuka maishani, yeye hakuweza kufikiria wakati wote ambapo hakufahamiana vizuri na Neno Takatifu.​—2 Tim. 3:15.

Kadiri watoto wanavyoendelea kukua, jitihada ya kweli inahitajiwa ili kuwasaidia wapate kuthamini ya kwamba utii kwa kanuni za juu za Maandiko huongoza kwenye maisha yaliyo mazuri zaidi. Ndivyo ilivyo sana sana katika hizi “siku za mwisho” zenye magumu. (2 Tim. 3:1, 2) Kitabu cha Biblia cha Mithali chaweza kusaidia wazazi kweli kweli katika kutoa mashauri yenye kutia moyo. Si kwamba tu kitabu hiki kinaonya juu ya hatari ya mashirika yaharibuo, uasherati, ulafi, utumiaji mbaya wa vileo, na yanayofanana na hayo, bali pia kinatia moyo kufuata mwendo ufaao. (Mit. 1:10-19; 4:14-27; 5:3-14; 7:1-27; 23:20-35) Namna ya kutia moyo ambako wazazi wanaweza kutia ndani wanapotoa mafunzo ya adili kwa watoto walio wakubwa zaidi inaonyeshwa kwa mfano katika maneno ya Mithali 3:1-6;

“Mwanangu, usiisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri zangu. Maana zitakuongezea wingi wa siku, na miaka ya uzima, na amani. Rehema na kweli zisifarakane nawe; zifunge shingoni mwako; ziandike juu ya kibao cha moyo wako. Ndivyo utakavyopata kibali na akili nzuri, mbele za Mungu na mbele ya mwanadamu. Mtumaini [Yehova] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yake.”‏

WAKATI WAZAZI WAMEKOSA KUJALI

Bila shaka, ikiwa hapo mwanzoni kumekuwako kutojali au kushindwa kwa wazazi, huenda wakaliona kuwa jambo gumu sana kujaribu kutoa mafunzo ya adili. Huenda ikawa lazima wazazi waeleze watoto wao sababu gani wanajali sana juu ya kufanya yale waliyokosa kufanya hapo kwanza. Huenda hii ikatia ndani kukubali kwa unyenyekevu makosa yao ya awali. Kisha, wakati na subira utahitajiwa ili wapate kutumainiwa na wana na mabinti zao wakubwa, kuwahakikishia upendo wa kweli wa wazazi na kwamba wanapendezwa nao kweli kweli. Huenda mwanzoni matokeo yakawa yenye kukatiza tamaa sana, hata yenye kuvunja moyo. Lakini wazazi hawapaswi kushindwa upesi, kwa kuwa hii itatilia shaka kule kupendezwa na kujali kwao. Kijana anaweza kuwaza hivi: ‘Ikiwa kweli bado wazazi wangu wanijali, wangekuwa wakijaribu kunisaidia.’ Hivyo, wazazi wanapoacha jitihada zao za kwanza zikatizwe na kutoitikia kwa watoto wao, huenda wakashiriki kuleta kutokuaminiwa na wana na mabinti zao. Ndiyo sababu ni jambo la maana sana kwa wazazi kuvumilia. Kujali kwa wazazi huenda kukaamsha dhamiri ya mtoto, na kutokeza sifa zake zilizo bora. Marta, aliyekuwa akiongoza kikundi cha wasichana wahalifu, alikubali hivi; “Niliumia sana kuona mama yangu akinihangaikia sana, lakini singemwonyesha hivyo hata kidogo na kuacha afahamu nilivyojisikia moyoni.”

Mara nyingi mfano mwema unakuwa na matokeo yenye nguvu sana kwa watoto waasi kuliko maneno mengi. Ingawa ni lazima uthabiti wa yaliyo haki udumishwe, wazazi wanapaswa waangalie wasipoteze kujiweza kwao na kuanza kupiga kelele au kutumia usemi wa kutukana. Maandiko yanashauri hivi: “Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya.”​—Efe. 4:31.

Hata ikiwa kuzoeza watoto kumeachiliwa kwa miaka mingi, pengina pangali pana tumaini. Kijana mmoja wa Mexico anasimulia hivi:

“Nilipokuwa na umri wa miaka saba, niliwaacha wazazi wangu. Kandokando ya njia, magari yaliyoachwa, au nyakati nyingine, magari ya kubeba shehena za reli na barabara yakawa ndiyo nyumbani kwangu. Nikishirikiana na vijana wengine nilianza kuiba. Pindi nyingi tulikamatwa na polisi na kuwekwa gerezani. Tulipoulizwa waliko wazazi wetu, tulisema kwamba sisi hatukujua. Nilipokuwa na miaka 10, tulijiunga na kikundi cha wasafirishaji wa kichini-chini wa dawa za kulevya. Mara nyingi nilikaribia kupoteza maisha yangu. Nilipokuwa na miaka 12, tulienda United States kinyume cha sheria na kuendelea na utendaji wetu ulio kinyume cha sheria. Siku moja kiongozi wa kundi letu alitisha kuniua kwa sababu ya kukosa kugawanya mali niliyokuwa nimeiba. Nilipigwa naye akachukua kutoka kwangu pesos 28,000 (fedha za Mexico).

“Nilihuzunika sana nikataka kurudi nyumbani au kujiua. Ndipo nilipokumbuka nyanya yangu aliyeishi Ciudad Judrez, lakini sikujua mahali penyewe. Nilianza kumtafuta. Mwishowe nilipompata, alikuwa akijitayarisha kuhudhuria kusanyiko moja la Mashahidi wa Yehova, akanikaribisha niende pamoja naye.”

Kwa msingi wa aliyosikia kusanyikoni kijana huyu, alianza kufikiria maisha yake kwa uzito. Akaanza kujifunza Biblia na, kwa furaha ya wazazi wake, akageuza tabia zake na kurudi nyumbani.

UASI YAJAPOKUWA MAZOEZI YA MAPEMA

Lakini namna gani ikiwa watoto wanakuwa wapotovu yajapokuwako mazoezi ya mapema? Wazazi wanaweza kupata faraja kutokana na uhakika wa kwamba waliifuata dhamiri yao katika kutimiza daraka lao. Vilevile wanaweza kuwa na tumaini kwamba katika wakati ujao jitihada za mazoezi bora zitawarudishia watoto waliopotoka akili zao. Tumaini hili laweza kuwa la kutia moyo sana.

Bila shaka mazoezi yanayofaa yanaweza kuwa na matokeo ya kudumu juu ya watoto. Biblia inasema hivi: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mit. 22:6) Ijapokuwa kwa kawaida watoto waliofunzwa vizuri hawawi watu waliopotoka, wengine wanapotoka lakini wanarudiwa na akili zao tena. Yanayowapata yanaweza kulingana na yale ya mwana mpotovu katika mfano alioutoa Yesu Kristo. Tunasoma hivi:

“Mtu mmoja alikuwa na wana wawili; yule mdogo akamwambia babaye, Baba, nipe sehemu ya mali yangu inayoniangukia. . . . Hata baada ya siku nyingi, yule mdogo akakusanya vyote, akasafiri kwenda nchi ya mbali; akatapanya mali zake huko kwa maisha ya uasherati. Alipokuwa amekwisha tumia vyote, njaa kuu iliingia nchi ile, yeye naye akaanza kuhitaji. Akaenda akashikamana na mwenyeji mmoja wa nchi ile; naye alimpeleka shambani kwake kulisha nguruwe. Akawa akitamani kujishibisha kwa maganda waliyokula nguruwe, wala hakuna mtu aliyempa kitu. Alipozingatia moyoni mwake, alisema, Ni watumishi wangapi wa baba yangu wanaokula chakula na kusaza, na mimi hapa ninakufa kwa njaa. Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena; nifanye kama mmoja wa watumishi wako.”​—Luka 15:11-19.

KUDUMISHA NIA INAYOFAA

Baba huyo alifanyaje? Kwa kuwa hakuwa ameanza kuweka nia mbaya moyoni kuelekea mwanawe, alitenda kwa huruma na kwa upendo wenye rehema. Mfano wa Yesu unaendelea hivi:

“Alipokuwa angali mbali, baba yake alimwona, akamwonea huruma, akaenda mbio akamwangukia shingoni, akambusu sana. Yule mwana akamwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena. Lakini baba aliwaambia watumwa wake, lileteni upesi vazi lililo bora, mkamvike; mtieni na pete kidoleni, na viatu miguuni; mleteni ndama yule aliyenona mkamchinje; nasi tule na kufurahi; kwa kuwa huyu mwanangu alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana. Wakaanza kushangilia.”​—Luka 15:20-24.

Kulingana na roho ya mfano huu, wazazi wanapaswa kujilinda wasiwe na uchungu na maoni ya ukatili kuelekea mwana au binti mpotovu. Ama sivyo, inaweza kuwa vigumu sana kwa mtoto kubadilika, kama alivyofanya yule mwana mpotovu wa mfano wa Yesu.

Matokeo mema ya upendo na fadhili yanaonyeshwa vema na mfano wa msichana mmoja katika Ohio (U.S.A.) ambaye wazazi wake ni Mashahidi wa Yehova. Akiamini kwamba hakupewa uhuru wa kutosha, Vickie mwenye umri wa miaka 15 alianza kuasi mamlaka ya wazazi. Mwishowe, akiwa na miaka 17, alihamia nyumba yake mwenyewe katika mji walimoishi watu wa jamaa ya mama yake. Ingawa watu hawa wa ukoo hawakukubaliana na aliyokuwa akifanya Vickie, walijaribu kumtia moyo. Ikawaje mwishowe? Msichana huyo anasimulia hivi:

“Nilishuka moyo sana, hata karibu nijiue, na nilichukizwa na ulimwengu na waliomo ndani yake. Kwa hiyo nilihamia kwa watu wa ukoo wa mama yangu. Hawakunilaumu wala kunisumbua hata kidogo. Niliogopa sana kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, lakini nilihudhuria. Upendo na fadhili ambazo kila mtu alionyesha zilikuwa nyingi sana. Hawatafahamu namna nilivyothamini, na namna walivyofanya iwe rahisi zaidi kwangu kuacha njia yangu mbaya ya maisha.”

Basi, watoto wanapokuwa wapotovu, wazazi hawapaswi kupoteza tumaini haraka. Ingawa wanachukia uovu, wanapaswa kuepuka kuwa washupavu na wenye uchungu kuelekea watoto wao. Lililo la maana zaidi, wazazi wanapaswa kujitahidi kuweka mfano bora na kuendeleza imani yenye nguvu katika Mungu.

Hivyo ndivyo alivyofanya Mfalme Daudi. Alitaabika sana kwa sababu ya matatizo (magumu) ya jamaa yake. Mwanawe mmoja alimgeuka akitafuta kiti chake cha enzi na kutaka kumwua. Lakini Daudi hakuruhusu hilo limvunje moyo aache kumtumikia Mungu. Kwa kweli, alipokuwa mzee na dhaifu, alimtia moyo mwanawe Sulemani hivi: “Mjue Mungu wa baba yako, ukamtumikie kwa moyo mkamilifu, na kwa nia ya kumkubali; kwa kuwa [Yehova] hutafuta-tafuta mioyo yote, na kuyatambua mawazo yote ya fikira; ukimtafuta ataonekana nawe; ukimwacha atakutupa milele.”​—1 Nya. 28:9.

Hata ikiwa watoto wa mtu watakosa kutii, Yehova Mungu hatawaacha watumishi wake waliojitoa. Kama vile alivyomtegemeza Daudi wakati wa majaribu na huzuni, ndivyo anavyotia nguvu watu wake leo wapate kuvumilia taabu, kutia na uchungu unaotokea watoto wanapokuwa waasi. Kwa kweli, ikiwa vifungo vyote vya upendo wa asili vingevunjika, bado mtu asingekuwa peke yake, ameachwa pasipo tumaini. Daudi alisema hivi: “[Hata] baba yangu na mama yangu [wakiniacha], . . . [Yehova] atanikaribisha kwake.”​—Zab. 27:10.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki