Kufanya Kazi ya Yehova Katika Njia ya Yehova
“Basi, wengi wetu tuliokomaa, na tuwe wenye nia ii hii; na . . . kwa kadiri tulivyofanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika kawaida ii hii.’’—Flp. 3:15, 16, NW.
1, 2. Ni utendaji gani wenye sehemu mbili unaotakiwa kufanywa na Wakristo waliojiweka wakf leo, kama maandiko yanavyoonyesha?
NI KAZI gani ya Yehova wanayopaswa kuifanya wale ambao wamejiweka wakf wafanye mapenzi yake na kuzifuata nyayo za Yesu Kristo, Mwana wake? Ni kazi yenye sehemu mbili ambayo Yesu Kristo alitabiri na kuamuru ifanywe.
2 Alitabiri hivi: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14, NW) Kwa hiyo, kushiriki kazi ya kuzihubiri habari njema hizi za Ufalme, bila shaka, ni sehemu ya maana ya kufanya mapenzi ya Yehova leo. Yesu aliongeza kuamuru wanafunzi wake wa kwanza hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mt. 28:19, 20, NW) Leo Wakristo wanapaswa si kuhubiri tu, bali vilevile kufundisha watu mambo ambayo wao wenyewe wamefundishwa. Imewapasa wasaidie wengine wafanye mambo ambayo Yesu mwenyewe aliamuru mitume na wanafunzi wake wa kwanza wafanye.
3. Maandiko yanaonyesha nini kwa habari ya namna kazi ya Mungu inavyopaswa ifanywe?
3 Kazi ya Yehova Mungu inapaswa ifanywe namna gani? Je! kila Mkristo afanye kazi hiyo kama anavyotaka tu kuifanya au kama anavyofikiri tu imepaswa ifanywe? Sivyo kabisa. Badala yake, Neno la Mungu linaamuru jinsi tunavyopaswa tuifanye. Kanuni hiyo ilionyeshwa zamani sana katika siku za Musa, maana tunasoma hivi katika Kumbukumbu la Torati 12:8: “Msifanye kwa kufuata mambo yote tuyafanyayo hapa leo, kila mtu kama aonavyo vema machoni pake.” Tofauti na hivyo, inatupasa tufanye kama inavyoamriwa katika Kumbukumbu la Torati 6:18: “Fanya yaliyo sawa, na mema, machoni pa [Yehova]; ili mpate kufanikiwa.” Mtume Paulo anaonyesha kwamba kanuni hizo zinahusu vilevile kundi la Kikristo: “Basi ndugu, nawasihi, . . . kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja.” (1 Kor. 1:10) Na, katika Wafilipi 3:15, 16, Paulo anaonyesha kwamba kufikiri, kusema na kufanya kazi kwa umoja ni alama ya Wakristo waliokomaa. Umoja huo wa kusudi na tendo ni wa lazima katika kufanya kazi ya Yehova Mungu katika njia yake.
KUITANGULIZA KAZI YA MUNGU
4. (a) Kazi ya Mungu imepaswa iwe na sehemu gani maishani mwetu? (b) Ni mambo gani yanayoweza kudai mali zetu kwa haki?
4 Basi ni kama mambo gani fulani yanayotiwa katika kufanya kazi ya Yehova katika njia ya Yehova? Kwanza, inatupasa tuifanye iwe ya kwanza maishani mwetu. Kama Yesu alivyosihi: “Kwa hiyo, zingatieni kwanza Utawala wa Mungu na matakwa yake.” (Mat. 6:33, Habari Njema kwa Watu Wote) Tunao wakati huo tu, nguvu hizo tu za mwili na za akili na mali hizo tu za ulimwengu huu. Kuna mambo mengi sana yanayodai wakati wetu kwa haki. Kwa mfano: inampasa baba apatie jamaa yake riziki, ya kiroho na ya kimwili vilevile, na kupanga wakati fulani wa kuwa na tafrija pamoja nao. Mambo hayo yote, anatakiwa ayafanye.—Linganisha 1 Timotheo 5:8.
5. (a) Mkristo anaweza kutangulizaje kazi ya Mungu kwa habari ya kazi yake ya kimwili? (b) Baba mmoja alipataje matokeo mazuri kwa kufanya hivyo?
5 Walakini, hata katika wajibu huo kuna mambo fulani tunayoweza kuchagua. Kwa mfano, ili tutangulize ufalme wa Mungu maishani mwetu, tunaweza kuchagua kazi ya kimwili inayoweza kutuachia wakati wa kushiriki kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi na kutimiza mambo ya kiroho ya jamaa zetu. Baba mmoja aliyekuwa akifanya kazi ya ufundi katika chumba cha kuvumbua dawa aliacha kazi hiyo, akajiandika mwenyewe, akaanza kufanya kazi zo zote za vivi hivi tu, ili aweze kutumia wakati zaidi katika kutimiza mambo ya kiroho ya wanawe wanne na binti mmoja. Matokeo? Watoto wake wakakua vilevile wakawa wafanya kazi wazuri wa Kikristo.
6. Inatupasa tufanye uchaguzi gani kwa habari ya matumizi ya wakati wetu wa kupumzika?
6 Halafu habari ya wakati wetu wa kupumzika. Sote twahitaji wakati wa tafrija, lakini ya kadiri gani? Je! tunatanguliza tafrija maishani mwetu? Je! tunafanya mno tafrija tunayopenda hata tunaacha na mambo yetu ya kiroho? Au, tunatimiza kwanza mahitaji yetu ya kiroho kisha, wakati unapopatikana, tunafurahia tafrija fulani? Mara nyingi jambo linalotakiwa ni kuchagua, maana jambo la kawaida si hili NA lile, bali ni hili AU lile. Je! tunaona kazi ya Mungu ya kuhubiri na kueneza “habari njema” kuwa ndilo jambo la kwanza maishani mwetu na mambo mengine kuwa ya pili? Au, bila akili tunatanguliza anasa, nguvu na mali zetu, na kuifanya kazi ya Mungu kuwa jambo la pili? Tukifanya hivyo, je! tunajifanya kuwa watu “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu”?—2 Tim. 3:4.
USAWA NA KUPANGA WAKATI
7, 8. (a) Kufanya kazi ya Yehova katika njia ya Yehova kunatutaka tufanye nini juu ya jinsi tunavyo-shiriki “habari njema’’ pamoja na wengine? (b) Juu ya jinsi tunavyopanga wakati?
7 Yesu alisema kwamba hakufanya jambo linalotokana na yeye mwenyewe tu. Yeye alifuata sana agizo alilopewa na Baba yake. (Yohana 14:10) Hivyo, yatufaa tuuchunguze sana mfano wake na kufanya kazi ya kuhubiri “habari njema” katika njia alizofanyia. Kwa njia hiyo tutakuwa tukifanya kazi ya Yehova katika njia ya Yehova. Yesu hakungojea watu waje kwake, wala hakuhubiri “habari njema” kwa watu aliokwisha kujuana nao peke yao. Yeye “alikuwa akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.” (Luka 8:1) Kwa kufuata mfano wake, wanafunzi wake walianza kuwafikia watu wengine wakiwa na “habari njema”; waliwahubiri watu wengi katika masoko na mahali pengine ambapo watu walikusanyika makundi makundi. (Matendo 16:13-15; 17:17-21) Leo, Mashahidi wa Yehova wanafuata kanuni zile zile. Walionyesha nia ya kushiriki “habari njema” pamoja na wengine, wawe ni watu waliojuana nao au wageni. Wanapofanya kazi za maisha ya kila siku, wanakutana na watu wao wa ukoo na jirani, katika biashara na shuleni; nao wanajaribu kutumia nafasi hizo washiriki kweli ya Biblia pamoja na wengine katika njia zinazofaa. Lakini si kila mtu ambaye angezisikia “habari njema” ikiwa tungehubiria watu hao tu. Kuna watu fulani ambao hatungewaona ikiwa tusingewatembelea katika nyumba zao. Kwa vile wanao upendo unaopanuka na kufikia aina zote za watu, Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kumfikia kila mtu wakiwa na ujumbe wa Ufalme. Je! kushiriki kwako utendaji huo kunaonyesha kwamba unayo maoni hayo ya Kikristo yaliyosawazika?—Mt. 5:46-48; 1 Tim. 2:3, 4.
8 Jambo linalohusiana sana na usawa ni kupanga wakati. Kwa kweli kuna ‘wakati uliowekwa kwa kila jambo chini ya mbingu.’ (Mhu. 3:1-8) Kupatana na kanuni hiyo, tunapohudhuria mkutano wa kundi na mhudumu. Mkristo anatoa hotuba, huo sio wakati wa kusinzia, kunong’onezana na mtu wingine wala kusoma jambo lisilohusiana na mazungumzo yanayoendelea wakati huo. Vilevile, zile jioni za mikutano sio wakati wa kwenda kufanya ziara za kurudia wala kufanya kazi nyingine za Kikristo zinazoweza kufanywa wakati mwingine. Yaonekana kwamba sana sana wazee wanahitaji kuwa waangalifu sana katika jambo hili la kupanga wakati. Huenda mara nyingi wakashawishwa kushughulika na mambo ya kundi wakati mikutano inapoendelea. Walakini, mambo hayo yanaweza kufanywa wakati mwingine ikiwa kuna mpango bora.
KUFANYA KAZI YA MUNGU KWA AMANI, KWA FURAHA
9, 10. (a) Sababu gani imetupasa tufanye kazi ya Yehova kwa amani? (b) Sababu gani mara nyingine hilo m tatizo?
9 Yesu aliwashauri mitume wake hivi: “Mkakae kwa amani ninyi kwa ninyi.” (Marko 9:50) Ingawaje, je! Yehova siye “Mungu wa amani,” na Mwanawe “Mfalme wa amani”? (Flp. 4:9; Isa. 9:6) Na je! Yesu hakusema wale wenye amani, yaani, wenye kufanya amani, ni wenye furaha? (Mt. 5:9, Kingdom Interlinear Translation) Hilo linamaanisha kwamba imetupasa tupendezwe sana na kujitahidi kuwa na amani katikati yetu.
10 Ni kwa sababu gani mara nyingine kufanya kazi pamoja na kwa amani kunaleta tatizo? Bila shaka sababu moja ni kwamba sote tuna nyutu (tabia) mbali-mbali. Basi, je! haitupasi tuwe tayari kusamehe tofauti za kufikiri na kutenda, tuwe wenye ufahamu badala ya kuwa wenye kulaumu? Sababu nyingine inayofanya kutunza amani kuwe tatizo nyakati nyingine ni kwa vile tunatamani sana kuona kazi ya Mungu ikifanywa katika njia iliyo bora sana, nasi tunadhani njia yetu ndiyo njia bora. Huenda ikawa hivyo mara nyingine. Lakini mara nyingi, jambo laweza kufanywa katika njia nyingi zinazokubalika kuliko katika njia moja. Inapokuwa hivyo, ni jambo la maana sana kwetu kufanya kazi pamoja tukiwa na amani kuliko kutaka jambo fulani lifanywe katika njia inayofaa zaidi kushinda zote.
11. Imempasa mzee awe na nia ya kufanya nini kwa kupenda amani?
11 Sana sana inawapasa wazee wakumbuke ubora wa kutunza amani wakati wanapokutana pamoja wafikirie mambo yanayohusu kundi. Ikiwa hakuna kanuni ya lazima iliyovunjwa, na ni shauri tu la kupendeza au shauri la kupunguza gharama, mwenye hekima atamkubalia yule anayesisitizia jambo hilo, ili amani iendelezwe. Tukizidi kusema kwa nguvu sana jambo lifanywe katika njia yetu, huenda tukatokeza maoni ya uchungu na hata kuwatenganisha ndugu zetu. Je! hapo kushinda kwetu kutakuwa kumefaa hasara hiyo? Hata kidogo! Basi kufanya kazi ya Yehova katika njia yake, kunamaanisha vilevile kuifanya kwa amani, tukikumbuka maneno ya Zaburi 133:1: “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja.”
12. Sababu gani kufanya kazi ya Yehova kwa furaha ni takwa la kiasi sana?
12 Bado jambo jingine la maana la kufanya kazi ya Yehova ni kwamba tuifanye kwa furaha. Kama vile mke asiye na furaha asivyompendeza sana mume wake, ndivyo na sisi tungekuwa, tukimtumikia Mungu pasipo furaha. Mtume Paulo anaamuru kwa kufaa sana hivi: “Furahini katika Bwana sikuzote; tena nasema, Furahini.” (Flp. 4:4) Lo! jinsi Wakristo leo walivyo na sababu nyingi za kufurahi! Bila shaka ‘kweli imewaweka huru’ (Yo-hana 8:32); wanao msamaha wa dhambi (Matendo 13:38); wanaona maarifa ya kweli yakizidi kuongezeka (Dan. 12:4); wanashirikiana vizuri wao kwa wao (Rum. 1:11, 12); wanaona furaha nyingi zaidi zinazotokana na kutoa (Matendo 20:35); wanafurahia baraka za paradiso ya kiroho (2 Kor. 12:4); na kwa kushika ukamilifu wanajua kwamba wanaufurahisha hata moyo wa Mungu wao mkuu, Yehova.—Mit. 27:11.
KUFANYA KAZI YA MUNGU KWA MIKONO SAFI
13. Mara nyingi Waisraeli wa kale walikuwa wakishindwa katika jambo gani, ikamfanya Yehova awaamuru wafanye nini?
13 Jambo moja la kufanya kazi ya Yehova katika njia yake ni kule kuifanya kwa mikono safi, yaani, kwa adili njema. Si wachache tu ambao wameshindwa katika jambo hili. Huenda tukawa na bidii sana katika kufanya kazi ya Yehova, lakini ni kazi bure tusipofuata kanuni za Biblia juu ya mwenendo mwema. Yehova Mungu alikazia jambo hilo alipokuwa akiwaambia watu wake wa kale, yaani, Waisraeli. Aliwaambia kwamba ameona namna zao mbalimbali za kuabudu kuwa zenye kuchukiza sana, kisha akasema: “Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya.”—Isa. 1:13-16.
14. Paulo alijonyeshaje kuwa mfano mzuri katika mwenendo, kupatana na amri gani ya kale?
14 Yehova Mungu ni mtakatifu, safi na mwenye haki, naye anaamuru watumishi wake wawe wata-katifu na safi vilevile. “Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.” (1 Pet. 1:16) Sote ni watu wenye makosa na, kwa hiyo, inakuwa vigumu kwetu kuwa watakatifu na safi. Huenda mara nyingine tukajiona kama mtume Paulo alipoandika kwamba mambo aliyotaka kufanya, hakuyafanya, na mambo ambayo hakutaka kufanya, akayafanya. (Rum. 7:19) Yeye hakuacha hata kidogo kupigana na udhaifu aliorithi, maana aliandika hivi: “Nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.” (1 Kor. 9:27) Wale Wayahudi waliokuwa wakirudi kutoka Babeli wa kale waliamriwa hivi: “Iweni safi ninyi mnaochukua vyombo vya [Yehova].” Ijapokuwa labda amri hiyo ilihusu kwanza usafi wa kidini, kanuni hiyo inahusu vilevile usafi wa adili (mwenendo mwema).—Isa. 52:11.
15. Kuna sababu gani nyingine ya kutaka tuangalie mwenendo wetu?
15 Yatufaa sana tuwe safi, si kwa sababu tu ya kwamba ule ujumbe tunaochukua ni safi, bali vilevile ili tusiwakwaze wengine. Yesu alionya kwamba ni jambo zito sana sana kumkwaza mmojawapo wa wadogo wake. (Luka 17:1, 2) Paulo alikuwa mwangalifu katika jambo hilo, na maneno yake yanaonyesha wazi: “Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe; bali katika kila neno tujipatie sifa njema, kama watumishi wa Mungu; katika saburi nyingi, . . . katika kuwa safi, . . . katika upendo usio na unafiki.” Kweli kweli kufanya kazi ya Yehova katika njia ya Yehova maana yake ni kuangalia kuifanya kazi ya Yehova kwa mikono safi, tusije tukaleta suto juu ya Yehova na juu ya kundi lake, tukawakwaza wengine.—2 Kor. 6:3-10.
KUFANYA KAZI YA YEHOVA PASIPO CHOYO
16. Mfalme Daudi alimwomba Mungu amfanyie nini, ikiwa na maana gani?
16 Zaidi ya yote, kufanya kazi ya Yehova hakutatufaidi kitu isipokuwa tunaifanya katika upendo, pasipo choyo, kwa moyo safi. Mfalme Daudi alithamini ubora wa hilo, na ndiyo sababu alisali hivi: “Unifundishe mimi, Ee Yehova, njia yako. Mimi nitatembea katika kweli yako. Unganisha moyo wangu ili niogope jina lako.” (Zab. 86:11, NW) Kutumikia kwa moyo uliogawanyika kungemaanisha kuachilia choyo kiingie. Kungeonyesha kusudi baya. Ndiyo maana tunaamriwa tumpende Yehova Mungu kwa moyo wetu wote, nafsi yote, akili na nguvu zetu zote.—Marko 12:29-31.
17. Sababu gani si jambo rahisi mtu kuangalia makusudi yake?
17 Hilo si jambo jepesi kulifanya. Kila wakati Waisraeli walikuwa wakishindwa jambo hilo. Kwa sababu gani? Kwa sababu mioyo mibaya ya wanadamu ni yenye udanganyifu na hila nyingi sana, kama tunavyosoma katika Yeremia 17:9. Na, kama Yeremia anavyoendelea kuonyesha, ni Yehova Mungu peke anayeweza kuufahamu sana moyo huo. Ndiyo sababu kujifunza Neno lake kutatusaidia tufahamu maelekeo au mipango yetu ya choyo, tupigane nayo na kuyashinda. Ndiyo, maelekeo mabaya ya mioyo yetu yanatokea kila wakati ili yaharibu kazi zetu njema. Makusudi mabaya ndiyo yaliyosumbua viongozi wa dini waliokuwa katika siku za Yesu, na. kwa sababu hiyo walimpinga sana Yesu. Ndivyo ilivyo na mapadre wa leo wa Jumuiya ya Wakristo. Wanaonekana kuwa wanamtumikia Mungu, kumbe wanahangaikia sana faida zao wenyewe.—Mt. 23:13-33.
18. Mtume Paulo alikaziaje uhitaji wa kumtumikia Yehova Mungu pasipo choyo?
18 Lo! jinsi mtume Paulo anavyoeleza ubora wa kusudi zuri: “Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu.”—1 Kor. 13:1-3.
19. Ni shauri gani zaidi linalotolewa na Maandiko juu ya aina ya upendo tunaopaswa kuonyesha?
19 Kwa hiyo, Paulo anatushauri kwa kufaa sana hivi: “Mambo yenu yote na yatendeke katika upendo.” (1 Kor. 16:14) Lakini je! Paulo anamalizia apo hapo tu? Sivyo, akifahamu namna mioyo yetu mibaya ilivyo na hila, anasema hivi: “Pendo lenu lisiwe na unafiki.” (Rum. 12:9) Jinsi ilivyo vyepesi kutoa maonyesho ya upendo usiotokana kweli na moyo unaoongozwa na kusudi zuri! Ndiyo sababu Paulo alijitahidi kujipendekeza kuwa mmoja wa wahudumu wa Mungu kwa kuwa na “upendo usio na unafiki.” (2 Kor. 6:6) Ndiyo, upendo wetu wapaswa uwe “upendo utokao katika moyo safi”; na, kama mtume Petro alivyosema, upendo wetu wapaswa uwe “upendano wa ndugu usio na unafiki.” —1 Tim. 1:5; 1 Pet. 1:22.
20. Kwa kifupi, kufanya kazi katika njia ya Yehova kunataka nini kwetu, kwa kutuletea matokeo gani?
20 Lo! jinsi kufanya kazi ya Yehova katika njia ya Yehova kulivyo na mambo mengi! Yehova Mungu anataka tuitangulize katika maisha yetu, tuifanye kwa hekima, kwa amani, kwa furaha, kwa mikono safi na kwa moyo safi. Tukifanya hivyo, tunaweza kuwa na furaha nyingi sasa na kupata kibali yake na uzima usio na mwisho katika taratibu yake mpya ya mambo, inayokaribia sana. —Kutoka The Watchtower, Nov. 1, 1978.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Utumishi wa upendo wa kumtolea Mungu, uliopangwa vizuri, kutanguliza faida za Ufalme nyakati zote, unaweza kutokeza furaha nyingi sasa na siku za usoni