Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Je! Yehova Mungu alisema na Adamu moja kwa moja au kupitia kwa Malaika?
Inaelekea kwamba huenda ikawa Mungu alisema na Adamu kupitia kwa Mwanawe, ambaye baadaye akawa Yesu. Biblia inafunua kwamba mara nyingi Mungu alipokuwa akisema na wanadamu alifanya hivyo kupitia kwa malaika, ambaye hata huenda ikasemwa juu yake kama kwamba ni Yehova. (Mwa. 16:7-11; Amu. 2:1-4; 6:11-16; 13:15-22; linganisha Kutoka 3:2-4 na Matendo 7:30, 35.) Maandiko Yasema waziwazi kwamba Mungu alimpa Musa torati kupitia kwa malaika.—Gal. 3:19; Ebr. 2:2, 3.
Mnenaji mkuu wa Mungu alikuwa Mwanawe pekee, aliyeitwa “Neno.” Mungu alimtumia mara nyingi apashane habari na wanadamu. (Yohana 1:1) Kupitia kwake Mungu aliviumba vitu vingine vyote. (Yohana 1:3: Kol. 1:16) Hivyo, huenda Neno akawa ndiye aliyeambiwa na Yehova: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu.” Masimulizi juu ya kuumba yanaongeza kwamba Mungu “[aliwaambia Adamu na Hawa], Zaeni, mkaongezeke.” Kupatana na akili nzuri, Mungu aliwaambia Adamu na Hawa jambo hili na mengine mengi kupitia kwa “Neno” ambaye pia alishughulika na wanadamu.—Mwa. 1:26-28; 2:16; 3:8-13; Mit. 8:31.