Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Je! Yehova Mungu alinena kwa Adamu moja kwa moja, au alinena kupitia Neno, yule Mwana mzaliwa pekee wa Mungu?
Biblia haitupi jibu la wazi kabisa kwa swali hili. Ingawa Mungu angaliweza kuwa alinena moja kwa moja kwa mwana wake mkamilifu wa kibinadamu katika Edeni, yaelekea Yeye aliwasiliana na Adamu kupitia Neno.
Mara nyingi Biblia hunena juu ya Mungu akifanya mambo na hali kwa kweli aliyafanya kupitia malaika mmoja au zaidi. Mathalani, Mwanzo 1:1, ZSB, hutuambia hivi: “Katika mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Kama hayo tu ndiyo yangalikuwa maneno ya pekee ambayo Biblia ilisema juu ya asili ya ulimwengu wote mzima, tungekata shauri kwamba Mungu aliiumba moja kwa moja, kana kwamba kwa mikono yake mwenyewe. Hata hivyo, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hupanua uelewevu wetu. Twasoma hivi: “Katika yeye [Mwana wa Mungu] vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana . . . Vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake.” (Wakolosai 1:16, 17) Maandiko mengine huthibitisha sehemu ya Mwana katika kuumba ulimwengu wote mzima. (Yohana 1:3, 10; Waebrania 1:1, 2) Na bado, sehemu yake ilikuwa kuwa mfanya kazi mwenye cheo cha chini kuliko Yehova, ambaye ndiye mwenye kuanzisha asili ya uumbaji, kuutia nguvu, na kuuelekeza.—Zaburi 19:1.
Mungu alisema hivi kwa mwanadamu wa kwanza: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula [mpaka ushibe, NW].” (Mwanzo 2:16, 17) Yehova hakuhitaji kifaa fulani cha kimashine au chenye kutegemea nguvu-umeme, kama megafoni au redio ya mawimbi mafupi. Kama vile Mnara wa Mlinzi wa Agosti 1, 1989, ulivyosema: “Mwanadamu huyo hakumwona yeyote mwenye kunena hivyo. Sauti ile ilitoka katika makao yasiyoonekana nayo ilikuwa ikimwambia yeye. Ilikuwa sauti ya Mfanyi wa mwanadamu, Muumba wake! . . . Ili asikie sauti hiyo ya kimungu mwanadamu huyo hakuhitaji chombo chochote cha sayansi ya ki-siku-hizi cha kupokelea mawimbi ya redio. Mungu aliongea naye moja kwa moja.”
Je! Mungu alinena kupitia malaika, labda Logosi, ambaye alikuja kuwa Yesu? Yawezekana sana. Bila kushikilia mambo kwa ushupavu usio wa kiakili, C. T. Russell aliandika hivi: “Labda Yesu ndiye aliyekuwa Mwakilishi wa Mungu katika Bustani ya Edeni pamoja na Adamu.” (The Watch Tower, Februari 1, 1915) Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu alitumikia kwa muda mrefu katika cheo kilichokwezwa cha kuwa “Neno” la Baba yake, au Mneni, kwa malaika na wanadamu. (Yohana 1:1; 12:49, 50; Ufunuo 1:1, 2) Kwa hiyo hata ikiwa usimulizi wa Mwanzo hutoa wazo la kwamba Mungu alinena moja kwa moja kwa Adamu mkaa pekee, hiyo haikanushi kunena Kwake kupitia malaika, kutia na yule Neno, Mwana wa kimbingu wa Yehova. Hasa ndivyo ingekuwa ifikiriwapo kwamba hata pale mwanzoni Yehova alimtumia Logosi kuumba mwanadamu, na huyu ‘alipenda sana mambo yanayohusu wana wa wanadamu.’—Mithali 8:22, 31, NW; Yohana 1:3.
Kwa kielelezo, fikiria pindi ambapo Musa alienda juu ya Mlima Sinai. Kutoka 19:21-24 husimulia hivi: “Ndipo BWANA [Yehova, NW] akamwambia Musa . . . Musa akamwambia BWANA [Yehova, NW] . . . BWANA [Yehova, NW] akamwambia.” Halafu usimulizi wa kutolewa kwa Amri Kumi wafanyiwa utangulizi hivi: “Mungu akanena maneno haya yote.” (Kutoka 20:1) Je! hiyo yasikika kana kwamba Mungu alinena kibinafsi maneno hayo ya Sheria? Maoni hayo yangeweza kupata uungaji mkono katika jambo la kwamba twaambiwa Mungu alinena kwa Musa “uso kwa uso.”—Kutoka 33:11.
Na bado, tuna ufunuo zaidi juu ya jambo hili. Mtume Paulo aliandika hivi juu ya Sheria: “Iliamriwa kwa utumishi wa malaika kwa mkono wa mjumbe.” (Wagalatia 3:19) Baadaye, Paulo alitofautisha waziwazi maagizo ambayo Mungu aliandaa katika Sheria na mambo ambayo Wakristo walipokea kupitia Yesu: “Ikiwa lile neno lililonenwa na malaika [kupitia malaika, NW] lilikuwa imara, na kila kosa na uasi ulipata ujira wa haki, sisi je! tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii? ambao kwanza ulinenwa na Bwana [Yesu], kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia.” (Waebrania 2:2, 3) Kwa hiyo Mungu hakunena maneno ya Sheria kwa sauti yake mwenyewe ya kibinafsi, wala hakumtumia Logosi. Bali, alichagua kutumia malaika wengine.
Ingawa hivyo, wazo la msingi ni nini? Mara nyingi tusomapo juu ya Mungu akinena kwa wanadamu, sisi huona kwamba alifanya hivyo kupitia viumbe roho watiifu walionena kwa ajili yake. (Linganisha Mwanzo 18:2, 3, 33; 19:1; Kutoka 3:2-4; Waamuzi 6:11, 12, 20-22.) Mtajo wa cheo cha Yesu kuwa Neno hudokeza kwamba yeye alikuwa mmoja ambaye Mungu alitumia mara nyingi kuwasiliana na viumbe wake wengine. Je! hiyo ilitia ndani Adamu mwana mkamilifu wa Mungu? Yaelekea sana kuwa hivyo.—Luka 3:38.
Ni kweli kwamba Logosi alipokuwa duniani baadaye, Baba alinena mara tatu kwa kusikika ili huyu “Adamu wa mwisho” aweze kusikia. (1 Wakorintho 15:45; Mathayo 3:16, 17; 17:1-5; Yohana 12:28-30) Katika pindi hizi, kwa nini Mungu anene kupitia malaika kama mjumbe ili kutoa habari zenye kumwelekea au zenye kumhusu Mwana huyu mwenye thamani kubwa? Kiakili zaidi, Yehova angenena moja kwa moja; Mwana wake mkamilifu, na hata wanadamu wasiokamilika waliokuwa karibu, walisikia sauti ya Mungu mwenyewe. Kwa hiyo Adamu yule mwanadamu mkamilifu alipoumbwa, Baba yake mwenyewe upendo angaliweza kuwa alishughulika moja kwa moja na uumbaji mpya huu ulio mkamilifu. Hata hivyo, kulingana na yaliyotangulia, yaelekea kwamba alimtumia Neno.