Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 5/1 kur. 8-13
  • Hazina Yako Iko Wapi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Hazina Yako Iko Wapi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUKADIRI MALI ZA KIMWILI KWA KUFAA
  • ANGALIA USIVUTWE NA MAHANGAIKO YA KILA SIKU
  • MANENO YANAYOTOKANA NA KINYWA CHA YEHOVA YANA NGUVU YA KUSAIDIA
  • Suala la Urithi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Suala la Urithi
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Yesu Atoa Ushauri Kuhusu Utajiri
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Jionyeshe Kuwa Mwaminifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 5/1 kur. 8-13

Hazina Yako Iko Wapi?

“Pale hazina yako ilipo, ndipo pia na moyo wako utakopokuwa.”​—⁠Luka 12:​34, Habari Njema kwa Watu Wote.

1. Wingi wa wanadamu wamekuwa wakihangaikia sana kitu gani? (Zab. 49:​6-11; 144:​12-14; Mt. 6:​31, 32)

KATIKA historia yote ya wanadamu, watu wengi wameweka maisha yao juu ya kujipatia mali nyingi​—⁠nyumba, dhahabu, fedha, mawe ya thamani, kondoo, mbuzi na ng’ombe nyingi, na mengine kama hayo. Watu wamefanya bidii nyingi ili waongeze mali yao, wakitumaini kwamba taabu zao zitafaidi watoto wao na wajukuu wao na hata vizazi vya wakati ujao. Lakini, je! mali za kimwili ndiyo hazina inayopaswa kushughulikiwa kwanza na watumishi wa Mungu?

2. Ikiwa Mkristo angekaza fikira zake zote juu ya miradi ya mali, angekuwaje kama “watu wa taratibu hii ya mambo”?

2 Kama Mkristo angejitumikisha sana katika kufuatia miradi ya mali, je! hangekuwa tofauti na watu wanaomtumikia Mungu? Angefanana sana na wale wanaosimuliwa na Daudi, mtunga zaburi aliyeongozwa na roho ya Mungu​—⁠“watu wa taratibu hii ya mambo, ambao fungu lao liko katika maisha haya, . . . wanaotosheka na wana wao na wanaowekea watoto wao akiba ya kile wanachoacha.” (Zab. 17:​14, NW) Hao “watu wa taratibu hii ya mambo” hawajui jambo jingine lililo bora sana zaidi ya kutosheleza tamaa zao wenyewe. Kwao maisha yana maana ya kupata utajiri, kuzaa watoto na kuwaachia urithi tu. Wao hawafikirii wajibu wao kwa Yehova Mungu.

3. Ni jambo gani lililokuwa lenye maana kuliko yote kwa Daudi? (Zab. 16:​5-8)

3 Lo! jinsi Daudi alivyokuwa na maoni tofauti juu ya maisha! Yeye alitangaza hivi: “Kwa habari yangu mimi, nitauona uso wako katika haki; nitatosheka wakati wa kuamka nilitazame umbo lako.” (Zab. 17:​15, NW) Ndiyo, jambo kubwa alilopendezwa nalo kuliko yote ni kuendelea kuwa mwenye haki apate kuona uso wa Mungu, yaani, aone kibali ya Mungu na baraka kana kwamba vikisimama mbele ya Muumba wake. “Wakati wa kuamka” apate uhakikisho kutoka kwa Mungu, Daudi angefurahia kuwapo kwa Yehova pamoja naye. Kweli kweli, moyo wa mtunga zaburi ulipendezwa sana na hazina za kiroho zinazoendelea muda mrefu.

4. Ni nini kinachoonyesha hazina yetu iliko?

4 Namna gani leo? Tukiamua kwa maoni yetu, maneno na matendo yetu, hazina yetu iko wapi? Je! ipo hapa duniani au iko mbinguni? Mahali ambapo hazina yetu ilipo panategemea njia ambayo katika hiyo mioyo yetu inatuelekeza. Yesu Kristo alisema hivi: “Pale hazina yako ilipo, ndipo pia na moyo wako utakapokuwa.” (Luka 12:​34, Habari Njema kwa Watu Wote) Kuchunguza na kufuata yo yote ambayo Mwana wa Mungu alisema wakati huo kunaweza kutusaidia sana tuweke mapendo yetu yanapopaswa kuwa.

KUKADIRI MALI ZA KIMWILI KWA KUFAA

5. (a) Sababu gani Yesu Kristo alikataa kujiingiza mwenyewe katika ugomvi wa urithi? (b) Ni onyo gani alilotoa wakati huo, na kwa sababu gani? (c) Ni mfano gani ambao alitoa ili akazie upumbavu wa kuona vitu vya kimwili kuwa vya maana sana?

5 Tunapochunguza vifungu vinavyozunguka au kutangulia maneno hayo ya Yesu, twafahamu kwamba kundi kubwa la watu lilikuwa likimsikiliza Mwana wa Mungu. Mmojawapo alisema hivi: “Mwalimu, mwambie ndugu yangu tugawane urithi aliouachia baba.” (Luka 12:​13, Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa kuwa sheria ya Musa iliweka katiba ya kwamba yule mwana mzaliwa wa kwanza ndiye angepokea sehemu mbili za urithi, bila shaka kusingalikuwako sababu ya kugombana. (Kum. 21:17) Inaelekea kwamba yule mtu aliyemwomba Yesu kuwapatanisha alitaka awe na kiasi kikubwa sana kuliko fungu alilostahili kupata. Alipoona jambo hilo, Mwana wa Mungu alikataa kujitia katika mambo hayo ila alilionya kundi hilo kubwa juu ya kutamani vibaya mali ya wengine. Akasema: “Jihadharini na kila aina ya tamaa; maana maisha ya mtu hayawi salama kutokana na wingi wa vitu alivyo navyo.” (Luka 12:​15, Habari Njema kwa Watu Wote) Hata mtu awe tajiri kiasi gani, hawezi kujifanya awe mtu wa kuishi milele. Atakufa tu kama anavyokufa mtu mwingine kisha aziache mali zake alizokusanya-kusanya. Yesu alizidi kukazia jambo hilo alipotoa mfano huu:

“Kulikuwa na mtu mmoja aliyekuwa na shamba lake ambalo lilizaa mavuno mengi sana. Huyo mtu akafikirifikiri moyoni mwake, akasema: ‘Nitafanya nini kwa vile sina mahali pa kuhifadhia mavuno yangu? Nitafanya hivi: nitabomoa ghala zangu na kujenga kubwa zaidi, na katika hizo nitahifadhi mavuno yangu yote na mali yangu. Hapo nitaweza kuiambia [nafsi] yangu: sasa unayo akiba ya matumizi kwa miaka na miaka. Ponda mali, ule, unywe na ufurahi.’ Lakini Mungu akamwambia: ‘Mpumbavu wewe; leo usiku [nafsi] yako itachukuliwa. Na vitu vile vyote ulivyojikusanyia vitakuwa vya nani?”’​—⁠Luka 12:​16-20, Habari Njema kwa Watu Wote.

6. Ni jambo gani ambalo tajiri yule katika mfano wa Yesu alikosa kuthamini, naye Yesu aliutumiaje mfano huo?

6 Tajiri huyo katika mfano huu hakufikiria namna ambavyo angeweza kutumia mali zake awasaidie wengine. Yeye alihangaikia tu starehe zake mwenyewe, akitumaini kujifaidi na mali zake alizoweka akiba miaka kwa miaka. Alisahau uhakika wa kwamba uhai wake ungekwisha upesi sana, akashindwa kutumia mali zake ili ajifanyie sifa nzuri pamoja na Yehova Mungu. Kwa hiyo, alipokufa, hakuwa na hazina yo yote ya namna ya kazi njema ambazo zingeweza kulipwa na Muumba wake. Kama Yesu alivyosema: “Ndivyo ilivyo kwa mtu anayejikusanyia utajiri kwa ajili yake mwenyewe, lakini si tajiri mbele ya Mungu.”​—⁠Luka 12:21, Habari Njema kwa Watu Wote.

7. Ni maneno gani ya mwanafunzi Yakobo yanayoonyesha kwamba huenda Wakristo wakanaswa katika mtego uliomnasa tajiri huyo wa mfano wa Yesu?

7 Ni jambo jepesi sana kwa wanafunzi wa Yesu Kristo kuangukia katika hatari ya kuwaza kwa njia ile ile kama tajiri huyo katika mfano. Kwa mfano, Yakobo, mwanafunzi Mkristo, aliona lazima alaumu vikali sana waamini fulani wenzake: “Basi, sasa sikilizeni ninyi mnaosema: “Leo au kesho tutakwenda katika mji fulani na kukaa huko mwaka mzima tukifanya biashara na kupata faida.” Ninyi hamjui hata maisha yenu yatakavyokuwa kesho! Ninyi ni kama ukungu unaotokea kwa muda mfupi tu na kutoweka tena. Mngalipaswa kusema: “Mungu akitujalia tutaishi na tutafanya hiki au kile.” Lakini sasa mwajivuna na kujigamba; majivuno ya namna hiyo ni mabaya.”​—⁠Yak. 4:​13-16, Habari Njema kwa Watu Wote.

8. Ni wakati gani ambapo ingekuwa kimbelembele kufuatia miradi ya mbele ya kutafuta mali, na kwa sababu gani?

8 Kwa kweli ni kimbelembele kabisa na kiburi mtu kusema kwamba anaazimia kufuatia mradi wa kukusanya mali ya kudumu muda mrefu, na kufanya hivyo pasipo kufikiria mapenzi ya Mungu. Hakuna njia ya kujulia hata yatakayoletwa na siku ya kesho. Huenda mipango iliyo bora ikakosa kutimizwa, au huenda kifo kikatokea ghafula, pasipo kutazamiwa. Maisha ya wanadamu ni dhaifu na yenye kubadilika kama ukungu, nayo si msingi unaotegemewa mtu kuweka matumaini yake juu yake. Kwa sababu hiyo, yule mtu anayejivuna juu ya jinsi atakavyotimiza mipango yake anakosa kujua kwamba inampasa kumtegemea Mungu, tena anadharau ule uhakika wa kwamba baraka ya kimungu yahitajiwa ili mtu afanikiwe. Kama alivyosema mwanafunzi Yakobo, tendo hilo lenye kiburi ni baya sana.

9. Twajifunza nini kutokana na 1 Timotheo 6:​9, 10 juu ya hatari ya kujitahidi kupata mali?

9 Mtu anayeendelea na mipango yake ya kukusanya mali pasipo kujali mapenzi ya Mungu, anaingia katika hatari kubwa ya kiroho. Paulo, mtume Mkristo alitoa onyo hili: “Wale wanaotaka kutajirika huanguka katika majaribu na kunaswa katika mtego wa tamaa nyingi mbaya za upumbavu, ambazo huwavuta mpaka kwenye uharibifu na maangamizi. Kwa maana kupenda sana fedha ni asili ya uovu wote. Watu wengine wametamani sana kupata fedha hata wakatangatanga mbali na imani, na wameivunja mioyo yao kwa huzuni nyingi.”​—⁠1 Tim. 6:9, 10, Habari Njema kwa Watu Wote.

10. (a) Imetupasa tufanye nini tunapofanya mipango kwa ajili ya wakati ujao, na kwa sababu gani? (b) Je! mali za kimwili zitumiwe kwa kutosheleza tu anasa za kipekee, nayo Maandiko yanasemaje juu ya hilo?

10 Kwa upande mwingine, mioyo yetu ikituongoza vizuri, hatutasahau kwamba maisha yanageuka. Tutakumbuka vilevile kwamba yatupasa tumtegemee sana Yehova Mungu. Kisha, wakati wo wote tufanyapo mipango kwa ajili ya wakati ujao, tutafikiria kwa sala namna mipango hiyo inavyopatana na kusudi la Mungu. Jambo hilo litatuzuia tusijiingize mno katika shughuli za kutafuta mali hata tukose wakati wa kutosha kujenga imani yenye nguvu. Kufikiri hivyo kwa njia ya sala kutatusaidia vilevile tuone kwamba hatukusanyi mali za kimwili kwa kusudi tu la kutosheleza anasa zetu wenyewe, bali zitumiwe katika kufaidi wanadamu wenzetu walio na taabu. Kutumia fedha kwa njia hiyo pasipo choyo, ndilo jambo ambalo mtu anatakiwa kufanya ili awe Mkristo wa kweli. Maandiko yanatuambia hivi: “Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe, apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji.” (Efe. 4:28) “Dini iliyo safi na isiyo na hitilafu mbele ya Mungu Baba ni hii: Kuwasaidia yatima na wajane katika shida zao, na kujilinda mwenyewe usichafuliwe na ulimwengu huu.”​—⁠Yak. 1:​27, Habari Njema kwa Watu Wote.

ANGALIA USIVUTWE NA MAHANGAIKO YA KILA SIKU

11. Ni shauri gani ambalo Yesu alitoa juu ya maoni yanayofaa juu ya kuhangaikia mambo ya kila siku ya maisha?

11 Ijapokuwa Wakristo wengi wanafahamu upumbavu wa kulundika mali nyingi kwa ajili ya anasa na faida yao wenyewe tu, huenda wasifahamu kwamba mahangaiko ya kila siku yanaweza kuwavuta vyepesi wasijitoe kwa nafsi yote wamtumikie Yehova Mungu. Hiyo ndiyo maana hasa ambayo Yesu alionyesha alipokaza fikira zake kwa wanafunzi wake, akisema:

“Kwa sababu hiyo nawaambieni, msiwe na wasiwasi juu ya chakula mnachohitaji kwa kuishi, wala juu ya nguo mnazohitaji kwa ajili ya miili yenu. Kwa sababu uzima ni bora kuliko chakula, na mwili ni bora kuliko mavazi. Chukueni, kwa mfano, kunguru: hawapandi, hawavuni wala hawana ghala yo yote. Hata hivyo, Mungu huwalisha. Ninyi ni bora zaidi kuliko ndege! Ni nani kati yenu kwa kuwa na wasiwasi anaweza kuongeza urefu wa maisha yake? Basi, kama hamwezi kufanya jambo dogo kama hilo, kwa nini kuwa wasiwasi juu ya yale mengine? Angalieni maua jinsi yanavyomea. Hayafanyi kazi wala wala hayasokoti. Hata hivyo, nawahakikishieni kwamba Solomoni mwenyewe na fahari zake zote hakupata kuvikwa vizuri kama na mojawapo. Lakini, kama Mungu hulivika vizuri jani la shambani ambalo leo liko na kesho latupwa motoni, je, hatafanya zaidi kwenu ninyi? Enyi watu walio na imani haba! Basi, msivurugike akili, mkihangaika daima juu ya mtachokula, au mtakachokunywa. Kwa maana hayo yote ndiyo yanayohangaikwa na watu wasiomjua Mungu. Baba yenu anajua kwamba mnahitaji vitu hivi. Shughulikieni kwanza Utawala wa Mungu, na hayo yote mtapewa kwa ziada.” ​—⁠Luka 12:22-31, Habari Njema kwa Watu Wote.

12. Sababu gani ni upumbavu kuhangaikia mno chakula na mavazi na kuanza kulegea katika shughuli za kiroho?

12 Inatufaa tuyafikirie sana maneno haya ya Yesu sana sana wakati wa ukosefu wa fedha, au fedha inapopungua thamani na bei za vitu zinazidi kuongezeka. Wasiwasi wote, masumbuko na mahangaiko yaliyo katika ulimwengu hayatafanya hali yetu iwe bora. Chakula cha mwili hakiwezi kuendeleza maisha yetu milele, wala hakiwezi kutupatia jina zuri pamoja na Yehova Mungu. Kwa sababu hiyo, mtu anayesumbukia chakula hata anaacha kumtumikia Mungu, bila shaka angekuwa akiona chakula cha mwili kuwa bora sana kuliko uhai wake. Vivyo hivyo, mtu anayesumbukia mno mavazi yake, na kuanza kulegeza utafutaji wa mambo ya kiroho, angekuwa akiona mavazi kuwa bora sana kuliko mwili wake. Kusumbukia mno mahitaji ya kila siku ni kukosa imani ya kwamba Mungu ana uwezo wa kulisha na kuvika watumishi wake.

13. Sababu gani mambo ambayo Yehova ametendea kunguru na maua ya shambani yamepaswa yatutie moyo sisi?

13 Kwa vile kuna mifano isiyolinganika kuonyesha kwamba Yehova ni Mtoaji wa riziki na mavazi, hakuna sababu ya kumfanya mtu ye yote akose imani. Kama Yesu alivyoonyesha, wale kunguru hawahangaikii watakakopata chakula chao kingine, wala maua hayasumbukii mno mapambo yao. Hata hivyo, kunguru hao, kwa kutafuta chakula, wanapata cha kutosha kuwasaidia, nayo maua yanamea na kuwa na mapambo yenye rangi za kupendeza ajabu, hivi kwamba hata Mfalme Solomoni hakuweza kushindana nayo kwa mavazi yake mazuri. Ndiyo, Yehova Mungu amepanga mambo kwa njia ya kwamba kunguru wanaweza kuona chakula wanachohitaji, nayo mimea (mboga) yaweza kupambwa kwa maua yenye uzuri wa ajabu. Basi, tunaweza kudhani kwamba Yehova Mungu angeacha watumishi wake wafe njaa au wawe wakitembea bila kuwa na mavazi ya lazima, hata asijali (asiangalie)? Hata kidogo. Kwa hiyo, kama ilivyo kawaida, Wakristo wa kweli wanaweza kutumaini kwamba, ikiwa hawaruhusu mahangaiko ya maisha yawazuie kumtumikia Mungu, watapata mambo ya lazima ambayo wanahitaji. Kwa kweli wao watakuwa bora kuliko watu wa ulimwengu, ambao wako katika taabu ile ile ya ukosefu wa fedha. Afadhali Wakristo, kwa sababu wao hawapotezi mali zao katika michezo ya kamari, kuvuta tumbako, kulewa pombe wala mambo yaliyo kama hayo.

MANENO YANAYOTOKANA NA KINYWA CHA YEHOVA YANA NGUVU YA KUSAIDIA

14. Bila Yehova kuwapa Waisraeli msaada wa moja kwa moja, je! wangalisalimika jangwani, nayo maneno ya Musa yanafunua nini katika jambo hili?

14 Ebu yafikirie, vilevile, mambo ambayo Yehova Mungu alitendea Waisraeli katika jangwa. Musa aliwakumbusha hivi: “Nawe utaikumbuka njia ile yote [Yehova], Mungu wako, aliyokuongoza miaka hii arobaini katika jangwa, . . . akakutweza, akakuacha uone njaa, akakulisha kwa mana, usiyojua wewe wala baba zako hawakuijua; apate kukujulisha ya kuwa mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila litokalo katika kinywa cha [Yehova].” (Kum. 8:​2, 3) Katika jangwa hilo lisilolimwa, Waisraeli karibu milioni tatu hawangeweza kupona kwa muda wa miaka 40. Kwa kweli, Yehova Mungu aliwaruhusu waingie katika hali ambayo walidhani kwamba kwa hakika wangekufa njaa. Walimlilia Musa na Haruni: “Mmetutoa huko na kututia katika bara hii, ili kutuua kwa njaa kusanyiko hili lote.” (Kut. 16:3) Pasipo njia ya kawaida ya kuendeleza uhai, yaani, chakula, Waisraeli hao walidhani kwamba walikusudiwa kufa.

15. Sababu gani Yehova aliwaruhusu Waisraeli waone njaa, na ni katika maana gani ile mana ilikuwa maneno ya kinywa chake?

15 Yehova kweli aliwanyenyekeza kwa kuwaruhusu wajione kuwa katika hali hiyo ya kutoweza kitu. Kusudi lake kufanya hivyo lilikuwa kuwafundisha wajue kwamba, wakati chakula cha kawaida kinapokosekana, maneno ya kinywa cha Yehova yanaweza kumsaidia mwanadamu. Ile mana ya mwujiza ilikuwa wonyesho huo, kwani Yehova alitoa amri nayo mana ikatokea. Kwa kuwa Yehova Mungu alisaidia taifa zima liendelee kuwa hai katika jangwa muda wote wa miaka 40, tunaweza kutumaini sana kwamba maneno ya kinywa chake yanaweza kutusaidia sisi leo vilevile.

16. Ni maneno gani ambayo Yehova amesema juu ya kusaidia watumishi wake kwa kuwapa riziki? (Zab. 37:​3, 4, 23-26; 145:​14-19)

16 Ni maneno gani ambayo Yehova ametoa juu ya kusaidia watumishi wake? Mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu aliandika hivi: “[Yehova] hatawatupa watu wake.” (Zab. 94:14) Naye Yesu Kristo alisema hivi: “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? . . . kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”​—⁠Mt. 6:​31-33.

17. Huenda maneno ya kinywa cha Yehova yakawa kwa njia gani inayoonekana ukija wakati wa kuendeleza uhai wa watumishi wake?

17 Kwa hiyo, wote wanaotafuta kweli kweli ufalme wa Mungu na haki yake kwanza, wataangaliwa naye kwa upendo. Wajapokuwa katika hali zinazoonekana kuwa bila tumaini, maneno ya kinywa cha Yehova yatawasaidia. Kama vile mana ilivyokuwa wonyesho unaoonekana kutoka katika kinywa cha Yehova, ikawafanya Waisraeli waendelee kuwa hai katika jangwa, vivyo hivyo leo ahadi ya Yehova ya kusaidia watumishi wake kwa kuwapa riziki itaonekana wazi. Kwa mfano, nyakati fulani Yehova ameongoza waamini wenzao au hata wasioamini wawasaidie watumishi wake walio na shida. Kwa kuwa kusumbukia mno mambo ya kila siku ya maisha kunaweza kuharibu maoni yetu ya kiroho, inatufaa tuzidi kuwa wenye nguvu katika kuamini kwamba Yehova anao uwezo wa kutupatia riziki.​—⁠Ebr. 13:​5, 6.

18. (a) Sababu gani imetupasa tufikiri kwa uzito kama tunaweka hazina mbinguni? (b) Tunaweza kujiuliza maulizo gani ili tujue mahali ilipo hazina yetu ya kweli?

18 Shauri hili la kuweka hazina mbinguni lisionwe kwa mchezo. Baraka zote za wakati ujao na matumaini ya uzima yanalitegemea. (Linganisha Luka 12:​45-48.) Kwa sababu hiyo, inamfaa kila mmoja ajichunguze kwa kuuliza hivi: Je! kweli faida za Ufalme zinatangulizwa katika maisha yangu? Je! natumia wakati wangu, nguvu zangu na mali zangu katika njia inayotokeza kulisifu jina la Mungu na kwa kuwafaidi wanadamu wenzangu? Je! naweza kuona kwamba vitu vya kimwili si vya maana sana maishani mwangu, bali kwamba furaha nyingi kuliko zote zinatokana na kumtumikia Yehova Mungu? Hazina yetu ikiwa mbinguni, hapo tu ndipo tunapoweza kuyajibu maulizo hayo, tukisema Ndiyo.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mana, wonyesho kutoka kwa Yehova, ilisaidia taifa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki