Jionyeshe Kuwa Mwaminifu
“Inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu.”—1 Kor. 4:2.
1. Sababu gani imewapasa watumishi wa Mungu wawe wakijitahidi katika kusaidia wanadamu wenzao?
WOTE wanaomtumikia Yehova Mungu wakiwa wanafunzi washikamanifu wa Yesu Kristo wanayo hazina bora. (Linganisha 2 Wakorintho 4:1-7.) Wanayo maarifa ya lazima yanayoweza kumaanisha uzima kwa wale wanaoanza kuyatumia. (Yohana 17:3) Kwa kufaa, basi, imewapasa wafanye bidii sana katika kusaidia kiroho wanadamu wenzao. Vilevile, inawapasa wawe tayari kutoa msaada wa kimwili kwa wale wanaouhitaji. Utoaji huo wa kimwili unapatana na utoaji wa kiroho. Ni kwa sababu chakula, mavazi na nyumba ni vitu vya lazima kwa maisha, na, pasipo uhai, mtu hawezi kumsifu Yehova Mungu.—Zab. 30:9; 88:10-12.
2. Imewapasa wanafunzi wa Yesu wawe tayari kufanya nini kulingana na shauri lake katika Luka 12:33, 34?
2 Yesu Kristo aliwasihi wanafunzi wake hivi: “Uzeni mali zenu zote mkawape maskini. Jifanyieni mifuko isiyochakaa, na jiwekeeni hazina mbinguni ambako haitapungua. Huko wezi hawakaribii, wala nondo hawaharibu. Pale hazina yako ilipo, ndipo pia na moyo wako utakapokuwa.” (Luka 12:33, 34) Kwa hiyo, lazima iweko nia ya mtu kutumia wakati na mali zake kuwafaidi wengine. Kwa wazi, Yesu hakumaanisha kwamba wanafunzi wake wanapaswa wajifanye kuwa maskini kisha wategemee msaada kutoka kwa wengine. Lakini wanafunzi hao walipaswa wawe tayari kuacha mali zao ili wasaidie watu walio katika uhitaji kweli kweli wa kimwili au wa kiroho.
3, 4. (a) Ni shauri gani ambalo Timotheo alitakiwa awape Wakristo waliokuwa na mali? (b) Kupatana na shauri hilo, walipaswa waepuke maoni gani?
3 Maana ya shauri la Yesu inaonyeshwa vizuri na maagizo ambayo mtume Paulo alimpa Timotheo ili naye, apate kuwaambia Wakristo waliokuwa na mali. Tunasoma hivi: “Waamuru watu walio matajiri katika mambo ya maisha ya sasa, wasijivune, wasiweke tumaini lao katika mali isiyoweza kutegemewa; bali wamtegemee Mungu, ambaye kwa ukarimu hutupatia vitu vyote tuvifurahie. Waamuru watende mema, wawe matajiri katika matendo mema, na wawe wakarimu na walio tayari kuwashirikisha wengine mali zao. Kwa namna hiyo watajiwekea hazina ambayo itakuwa kwao msingi imara kwa wakati ujao. Hapo wataweza kujipatia uzima ambao ni uzima wa kweli.” (1 Tim. 6:17-19, Habari Njema kwa Watu Wote) Shauri hilo lina maana gani?
4 Wakristo waliokuwa matajiri hawakupaswa wajione kuwa watu bora kwa sababu ya mali zao. Wala haikuwapasa waweke tumaini lao katika mali. Kwa kuwa mali zinaweza kuibwa, kupotea au kuharibika, si msingi mzuri wa kutegemeza matumaini ya mtu juu yake. Lakini yule Mungu wa milele, Yehova, anastahili sisi tumtumaini kabisa. Kama isingalikuwa mipango yake ya ukarimu ambayo Yeye alifanya ili uhai uendelee kuwapo duniani, hakuna mtu ambaye angeweza kujiendeleza kuwa hai. (Matendo 14:16, 17; 17:25) Jinsi ungekuwa upumbavu, basi, kutokumfikiria Muumba na kutegemeza maisha juu ya vitu vya kimwili!
5. Imetupasa tuzitumieje mali zetu, na kwa sababu gani? (Luka 16:1-13)
5 Yehova ndiye Mwenye vitu vyote kwa sababu yeye ni Muumba. Basi, inafaa kabisa tumwabudu na kuzitumia mali zo zote tunazoweza kuwa nazo katika njia inayopendeza machoni pake. (Zab. 95:3-6) Hilo lamaanisha kutumia mali hizo tuwasaidie wengine kwa njia ya kiroho na ya kimwili. Wakristo waliokuwa matajiri waliombwa wafanye matendo mengi mema ambayo yangekumbukwa kama vile mali zao. Kwa kutumia mali walizokuwa nazo katika kusaidia wengine waliokuwa na taabu, wangekuwa wakijiwekea hazina mbinguni. Kwa kweli, Wakristo wote waliojitoa, kwa kuwa na bidii katika kusaidia watu wanaohitaji msaada wa kiroho na wa kimwili, wanajiwekea hazina mbinguni itakayoleta faida nyingi kwa namna ya zawadi zitakazotoka kwa Yehova Mungu.
6. Sababu gani imetupasa tuangalie tusiruhusu cho chote kituzuie kujiwekea hazina mbinguni?
6 Tofauti na mali za kimwili zinazoweza kuibwa au mavazi yanayoweza kuliwa na mende, kumbukumbu la matendo mema pamoja na Mungu haliharibiki. Basi, bila shaka imetupasa tujitahidi kuzuia mali za kimwili, mahangaiko ya kila siku wala anasa zisituzuie kujifanyia kumbukumbu jema pamoja na Yehova Mungu wakati tungali tunaishi. Sana sana hivyo, kwa kuwa hatuna hakika na muda wa maisha yetu, ni jambo la muhimu tuangalie tusivutwe kutoka katika shabaha yetu kubwa, yaani, kuendelea kuwa watumishi wenye kukubaliwa na Yehova Mungu na wanafunzi washikamanifu wa Bwana wetu Yesu Kristo. Lingekuwa sikitiko kama nini ikiwa mtu angepatwa na kifo, naye hakuwa ametumia vizuri nafasi zake ajiwekee hazina mbinguni!
7. Ni nini kinachoweza kutusaidia tukaze fikira juu ya kujiwekea hazina mbinguni?
7 Kwa hiyo, ni jambo la maana sana kwetu kukaza mioyo yetu juu ya kujitahidi kuongeza hazina yetu mbinguni. Jambo moja litakalotusaidia kufanya hivyo ni kutumia wakati wetu tufikirie kwa kuthamini mambo ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wametufanyia. Tunadaiwa na Yehova Mungu kwa sababu ya uzima wetu wenyewe. (Ufu. 4:11) Ijapokuwa wanadamu wengi sana wana nia ya kutoshukuru, Aliye Juu Zaidi ameendelea kuwaruhusu wote wafaidike na mipango yake ya ukarimu ya kuendeleza uhai. (Mt. 5:45) Halafu, katika kuonyesha upendo wake ulio bora, Yehova Mungu hakumhurumia hata Mwanawe, Yesu Kristo anayependwa kuliko wote asife kifo cha aibu katika mti. Hilo lilifanya iwezekane kwetu kukombolewa katika dhambi na kifo, na mwishowe tuwe watoto wa Mungu walio wakamilifu kwa umilele wote. (Rum. 5:8; 8:32) Naye Yesu Kristo alionyesha upendo wake mkuu kwa kutoa uhai wake kwa kupenda kwa ajili yetu. (1 Yohana 2:2) Je! upendo huo ambao tumeonyeshwa usituhimize tutumie kila nafasi tujionyeshe kuwa watu wa kushukuru kwa kusaidia wanadamu wenzetu kwa njia ya kiroho na ya kimwili?
UTUMIE WAKATI VIZURI
8. Ni nini kinachoweza kuonyesha kwamba mtu anatumia wakati mwingi mno katika kutafuta anasa?
8 Kwa kweli, kumpenda Yehova na Yesu Kristo kumepaswa kutuongoze tutumie wakati wetu vizuri. Je! tungekuwa tukifanya hivyo ikiwa anasa zingekuwa za maana sana hata kuonyesha kwamba hatuwezi kuishi pasipo hizo? Kwa wazi sivyo! Haitupasi kusahau hata kidogo kwamba, kwa kame nyingi, mamilioni na mamilioni ya watu wameishi bila radio, television, sinema, motokaa, michezo, safari ndefu za kujifurahisha na mengine kama hayo. Kwa kufaa, basi, je! si jambo la hekima kuviona vitu hivyo kuwa vyenye maana ndogo maishani mwetu? Kwa hiyo, mtu akiona anatumia wakati mwingi zaidi katika mambo ya anasa kuliko katika mambo yanayohusiana na ibada ya kweli, je! haionyeshi kwamba yeye amekuwa ‘mpenda anasa’? (2 Tim. 3:4) Je! hayuko katika hatari ya kuwa mtu asiye na matunda kabisa katika kulisifu jina la Mungu?—Luka 8:14.
9, 10. (a) Yakitegemea mfano wa Yesu Kristo, ni nini yaliyo maoni yaliyosawazika juu ya tafrija zinazofaa? (b) Yesu alikuwa na maana gani aliposema, “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake”?
9 Kwa kweli, watumishi wa Yehova Mungu waliojitoa wanaweza kufurahia kwa kufaa namna mbalimbali za starehe au tafrija zinazofaa. Hata Yesu Kristo alikubali mialiko ya vyakula na karamu, naye aliongeza furaha ya karamu ya arusi kwa kugeuza maji kimwujiza yawe divai bora kuliko zote. (Luka 5:29; 7:36; 14:1; 19:5, 6; Yohana 2:1-11) Lakini Yesu hakufanya anasa, kutia na vyakula na vinywaji kuwa vitu vya kwanza katika maisha yake. Siku moja aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.” (Yohana 4:34) Je! sisi vilevile tunapendezwa sana sana na kufanya mapenzi ya Mungu?
10 Yesu aliposema maneno hayo, alikuwa amechoka na kuwa na njaa. Walakini, kwa kuwa nafasi ilijitokeza ili atoe ushuhuda, alijitia sana katika kutoa ushuhuda huo hata akasahau na taabu aliyokuwa nayo. Ile furaha iliyotokana na kufanya mapenzi ya Mungu ilikuwa kama chakula cha Yesu Kristo. Bila shaka, sisi vilevile twataka iwe hivyo. Kwa hiyo, imetupasa tuzuie anasa zisije zikatufanya tusione furaha nyingi zaidi zinazotokana na kusaidia wanadamu wenzetu kiroho na kimwili.
11. Je! Wakristo wanastahili kutumia wakati ili wajipatie tu anasa zao wenyewe, nayo ni kanuni gani tunayoweza kupata katika Isaya 58:13, 14 itumiwe katika jambo hilo?
11 Ili tuepuke kuwa wenye choyo katika kutumia wakati wetu, inatupasa tuzidi kukumbuka kwamba wakati wenyewe ni zawadi kutoka kwa Yehova, ipate kutumiwa kupatana na mapenzi yake. Hatustahili kutumia wakati kwa anasa zetu wenyewe tu. Hilo linaonyeshwa vizuri na jambo ambalo Yehova Mungu alitazamia Waisraeli wafanye wakati wa siku ya Sabato. Alitangaza hivi kupitia kwa nabii wake Isaya: “Kama ukigeuza mguu wako usiihalifu sabato, usifanye anasa yako siku ya utakatifu wangu; ukiita sabato siku ya furaha, na siku takatifu ya [Yehova] yenye heshima; ukiitukuza, kwa kutokuzifanya njia zako mwenyewe, wala kuyatafuta yakupendezayo, wala kusema maneno yako mwenyewe; ndipo utakapojifurahisha katika [Yehova].” (Isa. 58:13, 14) Kwa hiyo, zaidi ya kuacha kufanya kazi, Waisraeli walipaswa kuiona Sabato kuwa siku iliyowekwa kwa pekee kwa kusudi la Yehova. Haikuwa siku tu ya kujitafutia wenyewe anasa bali wakati wa kufurahia kweli kweli kufanya mapenzi ya Mungu, wakitanguliza mambo ya kiroho. Kupatana na roho hiyo ya sheria ya Sabato, imewapasa Wakristo wa kweli wapendezwe na kutumia kila siku katika njia itakayotokeza sifa kwa Yehova Mungu.
UWE TAYARI KWA AJILI YA KURUDI KWA BWANA
12. (a) Kama inavyoonyeshwa katika Luka 12:35-40, ni sababu gani nyingine ya maana inayotufanya tuwe wenye bidii katika kazi ya Yehova? (b) Imetupasa tujitahidi kuwa katika hali gani kila siku, na kwa sababu gani?
12 Ipo bado sababu nyingine ya kuwafanya watumishi waliojitoa wa Bwana Yesu Kristo wasiwe wakitanga-tanga katika kufanya kazi ya Yehova. Hiyo inaonyeshwa katika mfano huu unaofuata ambao Mwana wa Mungu alitoa: “Muwe tayari kwa lo lote lile litakalotokea, na kanda zenu ziwe zimefungwa viunoni, na taa zenu ziwe zinawaka; muwe kama watumishi wanaomngoja bwana wao arudi kutoka arusini, ili atakaporudi na kubisha hodi, wamfungulie mara. Heri yao watumishi wale ambao bwana atakaporudi atawakuta wanakesha! Nawaambieni hakika, huyo bwana atajifunga ukanda kiunoni, atawakalisha mezani na kuwatumikia. Hata kama ni usiku wa manane au alfajiri, kama akiwakuta wako hivyo, heri yao. Muwe na hakika kwamba, kama mwenye nyumba angejua saa ambayo mwizi atakuja, angekesha, wala hangeiacha nyumba yake kuvunjwa. Na ninyi, hali kadhalika, jiwekeni tayari, maana Mwana wa Mtu atakuja saa ile ambayo hamuidhanii,” (Luka 12:35-40, Habari Njema kwa Watu Wote) Kama vile tusivyojua wakati uzima wetu unapoweza kwisha, vivyo hivyo hatujui wakati halisi Yesu Kristo atakapofika atekeleze hukumu, ijapokuwa twajua kwamba tukio hilo linazidi kukaribia sana. Hilo lamaanisha kwamba kila siku yapaswa itukute tuko tayari, tukingojea kurudi kwa Bwana wetu.
13. Katika mfano wa Yesu, wale watumishi walikuwa wakifanya nini wakati bwana wao hakuwapo? (b) Bwana wao anawapaje zawadi watumishi wake wenye kungojea?
13 Katika mfano huo, wale watumishi wanaonekana wakifanya ivyo hivyo. Kanzu ndefu hazitelemki chini sana bali zinakunjwa ziweze kufika katika mapaja yao na kufungwa kwa ukanda (mshipi). Wakiwa wamejifunga kanda hivyo, wanaendelea kutimiza kazi zao na huku taa zao zikitoa mwangaza unaohitajiwa. Ijapokuwa wakati wa kungojea unaendelea mpaka kuingia zamu ya pili (kama saa 3 za usiku mpaka usiku wa manane) na hata katika zamu ya tatu (usiku wa manane mpaka karibu saa 9 kabla ya alfajiri), watumishi hao waaminifu wanaendelea na bidii yao na kukesha. Mwishowe, bwana wao anaporudi na kuona bidii ya watumishi wake, anawalipa zawadi kwa njia isiyo ya kawaida. Anawakalisha mezani na kuanza kuwatumikia. Hawatendei kama watumwa, bali kama rafiki zake washikamanifu. Lo! wanapokea zawadi njema wee kwa sababu wameendelea kufanya kazi ya bwana wao usiku kucha wakiwa wanamngojea arudi!
14. Kwa sababu ya miaka mingi ambayo imepita tangu Yesu aliposema maneno hayo yaliyoandikwa katika Luka 12:35-40, ni maulizo gani yanayoweza kuulizwa?
14 Imepita miaka zaidi 1,900 tangu Yesu Kristo alipotoa mfano huo. Kwa hiyo wafuasi wake wamekuwa wakingojea kweli kweli muda mrefu arudi kuja kutekeleza hukumu juu ya ulimwengu usiomwogopa Mungu. Kwa wengi, huenda ikaonekana kana kwamba zamu ya pili imekwisha kupita na kwamba sasa tumeendelea sana katika zamu ya tatu. Lakini wengine kati yetu wanachoka sasa? Au, bado tumejifunga kanda kwa nguvu tufanye kazi? Je! tunaacha nuru zetu ziangaze kupitia kwa mwenendo mwema na kuhubiri kwa bidii wakati tunapotiwa bidii hiyo kwa kufuata utendaji wa roho ya Mungu? —Mt. 5:14-16; linganisha Zekaria 4:2-6.
15. Akirudi ili aje atekeleze hukumu, Yesu Kristo atatafuta kuona nini kati ya wale wanaojidai kuwa wanafunzi wake?
15 Bwana wetu atakaporudi kuja kutekeleza hukumu, atatafuta nini? Atajua kama wale wanaojidai kuwa watumishi wake ni watumishi wake kweli kweli. Je! wamekuwa waaminifu katika kutii amri ya “mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi”? (Mt. 28:19, 20, NW) Je! wana kumbukumbu jema la kazi zinazoonyesha kwamba wanahangaikia kwa bidii wale “wadogo” wa ndugu za Kristo? Wanapowaona ndugu hao wa Kristo wakihitaji kitu, je! wanalisha walio na njaa, wanawanywesha walio na kiu, wanakaribisha wageni, wanavika wale wenye kuvalia kimaskini, wanawapa msaada na kuwafariji wale walio wagonjwa na kuwatembelea wale wanaotiwa gerezani isivyo haki? (Mt. 25:35-40) Je! wameendelea kukesha kiroho, wasitiwe madoa na kazi za mwili zinazochafua? —Mt. 7:21-23; Luka 21:34-36; 2 Pet. 3:14.
16. Sababu gani imetupasa tufikiri kwa uzito sana juu ya namna tunavyofanya katika kujifanyia kumbukumbu la kazi njema pamoja na Mungu?
16 Imetupasa sote tufikiri kwa uzito sasa juu ya kusimama kwetu mbele za Mungu na Kristo. Hatuna wakati wa milele wa kujifanyia kumbukumbu la kazi njema. Pasipo kufikiria umri tulio nao sasa, ama kifo ama kurudi kwa Bwana wetu kutatufikia ghafula. Tusipotimiza madaraka yetu ya Kikristo, basi, mojawapo la matukio hayo mawili linaweza kutufikia ghafula kama vile mwivi. Basi, na tufanye bidii kila siku, tukiishi kana kwamba siku hiyo ndiyo siku yetu ya mwisho, tusiruhusu tamaa zetu wenyewe wala anasa zituzuie kumtumikia Yehova Mungu na Bwana wetu Yesu Kristo kwa uaminifu. Tukifanya hivyo, hatutasikitikia kamwe jinsi ambavyo tumetumia wakati wetu, nguvu zetu na mali zetu za kimwili. Hatutaogopa lo lote wakati tutakaposimama mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo atakapofanya maamuzi kwa ajili ya Baba yake. (2 Kor. 5:10) Basi, na tuonekane kuwa watu wenye kujiwekea hazina nyingi mbinguni.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Bidii ya kutoa msaada wa kiroho au wa kimwili kwa wale wanaouhitaji inaleta zawadi nyingi za kiroho