Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 5/15 kur. 17-24
  • Kuzaa Matunda Kunakomtukuza Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuzaa Matunda Kunakomtukuza Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MATUNDA
  • KUKAA NDANI YA “MZABIBU”
  • “MKUTANO MKUBWA” WA UFUNUO 7:9-17
  • Mzabibu Unaotoa Divai Inayofurahisha Mungu na Mwanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Kuonea Shangwe Uhusiano wa Karibu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • ‘Utunze Mzabibu Huu’!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Kuzaa Matunda Kama Matawi na Kuwa Rafiki za Yesu
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 5/15 kur. 17-24

Kuzaa Matunda Kunakomtukuza Mungu

1. Kwa maneno yake katika Ezekieli 15:1-5, Yehova alionyesha kusudi la msingi la mzabibu kuwa kusudi gani?

KWA kweli, kusudi la mzabibu ni kusudi gani? Zamani sana Mpanzi wa mzabibu wa kwanza alimwuliza nabii wake Ezekieli ulizo hilo, katika maneno haya “Mwanadamu, mzabibu una sifa gani kuliko mti mwingine, au tawi la mzabibu liliokuwa kati ya miti ya msituni? Je! mti wake waweza kutwaliwa, ili kufanya kazi yo yote? watu waweza kufanya chango kwa huo, ili kutundika chombo cho chote? . . . Tazama, ulipokuwa mzima, haukufaa kwa kazi yo yote.” (Eze. 15:1-5) Kwa wazi, basi, kusudi la pekee la mzabibu ni kuzaa matunda, zabibu tamu ambazo kutoka hizo divai hutolewa.​—Amu. 9:13.

2. Kulingana na kusudi hilo la mzabibu, Yesu alisema katika Yohane 15:16 kwamba wazo lake katika kuyachaguwa “matawi” hayo ya kimtume lilikuwa wazo gani?

2 Divai ilitumiwa katika mwadhimisho wa Sikukuu ya Kupitwa ya mwisho ya Yesu na mitume wake. Baada ya chakula hicho cha jioni alitoa mfano wake wa “mzabibu wa kweli” na “matawi” yake. Akiukumbuka huo yeye angeweza kuwaambia mitume kumi na mmoja waaminifu hivi: “Ninyi hamkunichagua mimi; mimi niliwachagueni na kuwatuma mwende mkazae matunda, matunda yadumuyo, naye Baba [Mpanzi wa mzabibu] apate kuwapa ninyi cho chote mumwombacho kwa jina langu [kwa sababu ninyi mnazaa matunda].”​—Yoh. 15:16, Habari Njema kwa Watu Wote.

3. Kwa sababu gani mzabibu unaondolewa matawi yasiyozaa kila wakati, nalo hilo lapaswa kutoa somo gani kwa kila “tawi” lenye kuthamini katika huo “mzabibu wa kweli”?

3 Ili upate kuzaa matunda kikamilifu, mzabibu huo unaondolewa matawi yasiyozaa kila wakati. Iko kama Yesu ambaye ndiye “mzabibu” wa kiroho alivyosema: “Yeye huliondoa ndani yangu kila tawi lisilozaa matunda. . . . Mtu ye yote asipokaa ndani yangu hutupwa nje kama tawi litupwavyo nje hata likakauka. Watu huliokota tawi la namna hiyo na kulitupa motoni liungue.” (Yoh. 15:2, 6, Habari Njema kwa Watu Wote) Hivyo, basi, jambo hilo latupa somo gani sisi? Basi, ikiwa ye yote kati yetu ni “tawi” katika “mzabibu” huo wa kiroho naye anathamini pendeleo lake, yeye hatataka kuondolewa. Hivyo inamlazimu kuzaa matunda​—mengi sana!

MATUNDA

4. “Matunda ni yapi, kama inavyoonyeshwa katika Isaya 5:7?

4 Hata hivyo, matunda ni yapi? Matunda, zabibu, hazifananishi wanafunzi wa Kristo. Matawi ndiyo yanayofananisha wanafunzi waliozaliwa kwa roho. Maandiko yanaonyesha ni matunda yapi yanayozaliwa na matawi. Kwa mfano, wakati Yehova alipofananisha Israeli na shamba la mizabibu, alitaja matunda aliyokuwa akitazamia. Alisema hivi: “Shamba la mizabibu la [Yehova] wa majeshi ndilo nyumba ya Israeli na watu wa Yuda ni mche wake wa kupendeza; akatumaini kuona hukumu ya haki, na kumbe! aliona dhuluma; alitumaini kuona haki, na kumbe! alisikia kilio [kama kile cha Sodoma wa kale].”​—Isa. 5:7; Mwa 18:21; 19:13.

5. Katika siku za Yesu, ni mambo gani mazito zaidi ya sheria ya Mungu ambayo viongozi wa dini walikuwa wakikosa kujali, nao walikuwa wakifundisha mambo gani?

5 Kwa hiyo, kama sehemu ya matunda ya hilo “shamba la mizabibu” la mfano la Israeli, Yehova akiwa Mpanzi wake alikuwa akitazamia hukumu (ya haki) pamoja na haki, kinyume cha uvunjaji wa sheria na mwenendo mpotovu. Hukumu na haki ilikuwa haipatikani katika Israeli katika siku za Yesu. Muda mfupi tu kabla ya kuuawa kwake huko Yerusalemu kwa sababu ya imani yake aliwaambia waandishi na Mafarisayo wanafiki hivi: “Mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili na rehema, na imani.” (Mt. 23:23) Kwa habari ya kuvunja Sheria ya Mungu, Yesu aliendelea kusema hivi: “[Ninyi Mafarisayo na waandishi mmelitangua] neno la Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu.” “Wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.”​—Mt. 15:6, 9.

6, 7. (a) Kama ilivyokuwa kwa habari ya Israeli wa asili, ni matunda gani yanayopaswa kutazamiwa kutoka “matawi” ya ule “mzabibu wa kweli,” nayo hiyo inapasawa kuonyeshwaje? (b) Katika siku za Yeremia, Israeli walikuwa wakifanyaje uzinzi katika njia mbili?

6 Hukumu ya haki, rehema, uaminifu, haki, kushika Sheria ya Mungu wala si kuipotoa yalikuwa baadhi ya matunda ambayo Yehova alitazamia kuona kutoka katika hilo “shamba la mizabibu” la mfano la Israeli. Kwa kupatana, je! yeye anapaswa kutazamia matunda yaliyo tofauti na hayo yote kutoka katika “matawi” ya “mzabibu wa kweli” wake? Hata kidogo! Matunda ambayo Yeye anatamani kuona yakipamba hayo “matawi” ni sifa za utu kama wa Kristo. Walakini kuna mengi zaidi ya utu usiotenda.

7 Wonyesho unaotenda wa sifa za utu unahitajiwa pia. Kwa mfano, katika siku za nabii Yeremia, Yehova alilalamikia matunda aliyokuwa akitolewa na “shamba la mizabibu” la mfano la Israeli. Alisema hivi: “Juu ya kila kilima kirefu, na chini ya kila mti wenye majani mabichi, umejiinamisha, ukifanya mambo ya ukahaba. Nami nalikuwa nimekupanda, mzabibu mwema sana, mbegu nzuri kabisa; umegeukaje, basi, kuwa mche usiofaa wa mzabibu-mwitu machoni pangu? . . . Wawezaje kusema, Sikutiwa unajisi, sikuwafuata Mabaali?” (Yer. 2:20-23) Hivyo, sehemu nyingine ya matunda aliyoyatazamia Yehova kutoka katika “mzabibu” wa mfano wa Israeli yalikuwa usafi wa adili pamoja na ibada yake ya pekee. Walakini, badala ya kupata matunda ya namna hiyo katika matawi, Yehova alipata uasherati na uzinzi kati ya Waisraeli mmoja mmoja, na vilevile uzinzi wa kiroho kwa habari ya taifa zima kwa kufanya mapatano ya kirafiki na mataifa ya kipangani yaliyowazunguka.​—Linganisha Yakobo 4:4.

8. Waisraeli walikosaje kumtolea Yehova ibada ya pekee?

8 Zaidi ya hayo, badala ya kumwabudu Yehova peke yake akiwa Mungu wao wa agano, taifa hilo lilikuwa likifuatia sanamu za Baali na kuziabudu. Ilikuwa kana kwamba, “zabibu” za “mzabibu” wa mfano wa Israeli zilikuwa ‘zabibu za Sodoma,’ hivi kwamba “vichala” vyao vilikuwa vichungu. Hivyo, matunda ya “mzabibu” wa Israeli yalitia ndani kulalana wanaume kwa wanaume kama kule kwa Sodoma wa kale. (Kum. 32:32) Matunda hayo yasiyotamanika yanatofautiana sana na yale anayotaka Mungu.

9. “Matawi” ya “mzabibu wa kweli” yanapaswa kujiepushaje na uzinzi wa kiroho, hata ijapokuwa wachukiwe na ulimwengu?

9 Mungu huyo asiyebadilika hataki matunda ya namna hiyo katika “matawi” ya “mzabibu wa kweli” wake, Yesu Kristo. Kwa hiyo jamii ya Ufalme wa Waisraeli wa kiroho lazima wajiweke wenyewe safi kwa habari ya adili. Hawapaswi kufanya uzinzi wa kiroho kwa kufanya urafiki na ulimwengu huu. Wanahitajiwa kumwabudu Yehova peke yake akiwa Mungu. Wao hawajali ikiwa ulimwengu utawachukia kwa sababu ya kuzaa matunda ya namna hiyo. “Kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia.” Ndivyo Yesu alivyowaambia wale mitume kumi na mmoja waaminifu katika usiku ule aliposalitiwa na Yuda Iskariote.​—Yohana 15:19.

10. (a) Lazima “matawi” ya “mzabibu wa kweli” yazae matunda ya namna gani ya kujitenga na kutokuwa na madoa, nalo hilo linawataka wachukue hatua gani? (b) Kwa sababu ya kukosa kuzaa matunda ya namna hiyo, taifa la Israeli lilipata hasara gani?

10 Kwa kutokuwa sehemu ya ulimwengu huu kwa kujiepusha na siasa zake na vita vyake wanaonyesha matunda ya usafi na kutokuwa na madoa kutokana na ulimwengu huu. Matunda hayo lazima yaonyeshwe na wote walio katika tengenezo la Yehova kama vile linavyowakilishwa na Mwanawe, aliye “mzabibu wa kweli,” Yesu Kristo. Lazima waonyeshe kwamba wanashikamana kabisa na ufalme wake chini ya Yesu Kristo. Hiyo inawahitaji kumkiri na kumkubali waziwazi Mwana wa Mungu kuwa Masihi au Kristo aliyeahidiwa muda mrefu uliopita. Yesu aliye Masihi hakutolewa matunda ya namna hiyo na “mzabibu” wa mfano wa Israeli wa asili. Ulishindwa kuzaa “matunda” ya ufalme wa Mungu. Matokeo yake yalikuwa hasara kubwa sana kwao, kwa kuwa ufalme wa Mungu uliondolewa kwao na kupewa taifa jingine ambalo lingezaa matunda yaliyohitajiwa, Israeli wa kiroho. (Mt. 21:43) Taifa hili jipya linaundwa kwa “matawi” yanayoonyesha kwamba yanashirikiana na “mzabibu wa kweli” kwa kutomkataa Yesu aliye Masihi kama lilivyofanya taifa la Kiyahudi lakini wanamkubali waziwazi na kufuata nyayo zake.

11. (a) Kwa sababu ya unabii wa Mathayo 24:14, ni jambo gani linalohusika zaidi ya ‘kumpokea Yesu moyoni mwa mtu’? (b) Ni hali gani inayohusiana na “mzabibu wa kweli” ambayo ni wajibu kwa “matawi” ya mzabibu huo?

11 Kwa hiyo, hii inatia ndani mengi zaidi ya kumkiri na kumkubali Masihi moyoni mwa mtu, ‘kumpokea Yesu moyoni mwa mtu,’ kama wasemavyo wahubiri wa injili wa Jumuiya ya Wakristo. Lazima hilo lithibitishwe na lidhihirishwe kwa matendo ya hadharani. (Rum. 10:10) Lazima kuweko kushiriki kwa kibinafsi katika utimizo wa unabii wa Yesu: “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14, NW) Ikiwa “tawi” lo lote katika “mzabibu” wa Kristo lililo wakf na kubatizwa, na kutiwa mafuta kwa roho halishiriki katika kazi hiyo iliyotabiriwa, lingewezaje kuwa linazaa matunda ya ufalme wa Mungu? Wajibu kuhusu jambo hili ni kwamba wao ni “matawi” katika yule aliyekuwa wa kwanza katika kutiwa mafuta kwa roho ya Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu ili kuzihubiri habari njema za Ufalme. (Isa. 61:1-3; Luka 4:16-21) Kama ilivyo kwa habari ya shina, ndivyo inavyopaswa kuwa kwa “matawi” yenye kunywa maji ya mti!

12. Tangu mwaka 1914, lazima Mathayo 24:14 litimizwe kwa kadiri kubwa namna gani, nao ni nani walio na daraka la kuona kwamba “habari njema hizi” zimehubiriwa kwa kadiri hiyo?

12 Unabii wa Mathayo 24:14 ulikuwa na utimizo mdogo katika karne ya kwanza W.K., kuanzia na wakati Yesu alipopaa mbinguni na kuonekana mbele za Mungu mpaka mwaka 70 W.K., wakati Warumi walipouharibu Yerusalemu. Lakini utimizo huo ulifananisha tu utimizo ulio kamili zaidi wa unabii huo katika wakati huu tangu mwaka 1914 na kuendelea. Mwishoni mwa Majira ya Mataifa katika masika ya mwaka huo, ufalme wa Mungu wa Kimasihi ulizaliwa huko mbinguni. Leo, zaidi ya karne 19 baada ya “mzabibu” wa Kristo kuanza kutokeza “mtawi,” kuna baki dogo tu la “matawi” hayo walio hai bado na wanaozaa “matunda” ya ufalme wa Mungu, kwa kuwa “matawi” hayo yalipaswa yawe yasiyozidi 144,000 warithi washirika pamoja na Yesu Kristo. (Ufu. 7:4-8; 14:1-3) Baki hili ndilo lililo na daraka la kuona kwamba “habari njema hizi za ufalme” zimehubiriwa duniani pote ili mataifa yote yapate kusikia.

13. Kwa hiyo Baba ya Yesu ametukuwa duniani pote kwa sababu ya mabaki ya “matawi” ya mzabibu kuzaa “matunda” gani?

13 Kuzaa matunda ya kuitii amri ya kuhubiri kumekuwa na matokeo ya kumtukuza Yehova Mungu. Iko kama vile Yesu alivyowaambia “matawi” yake ili kuwatia moyo: “Baba yangu hutukuzwa kama mkizaa matunda mengi na kuwa wanafunzi wangu.” (Yoh. 15:8, Habari Njema kwa Watu Wote) Katika wakati huu wa utimizo wa mwisho wa unabii wa Mathayo 24:14, je! mabaki ya “matawi” hayo yamezaa “matunda mengi”? Tukiangalia maandishi yanayopatikana kwa kipindi kilichoanzia na mwaka 1919 W.K., lazima tuseme Ndiyo! Kwa kuzaa “matunda” kama hayo Yehova Mungu ametukuzwa ulimwenguni pote.

KUKAA NDANI YA “MZABIBU”

14. Katika Yohane 15:4-6, Yesu ameonyeshaje kwamba kukaa ndani yake pasipo kutoka kulikuwa kwa lazima ili mabaki ya hayo “matawi” yaweze kuzaa matunda mengi namna hiyo?

14 Imekuwa lazima “matawi” yakae ndani ya “mzabibu” wa Kristo bila kutoka ili yaweze kuzaa matunda mengi namna hiyo katika nyakati hizi zenye msukosuko tangu itokee Vita ya Kwanza ya Ulimwengu katika mwaka 1914. Bila shaka maneno ya Yesu yametumika juu ya mabaki ya “matawi” yenye kuzaa matunda: “Kaeni ndani yangu [mzabibu wa kweli], nami nikae ndani yenu. Kama vile tawi haliwezi peke yake kuzaa matunda lisipobaki katika mzabibu, hali kadhalika na nyinyi hamwezi kuzaa matunda msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu, nanyi ni matawi. Akaaye ndani yangu, nami nikiwa ndani yake, huyo huzaa matunda mengi, maana bila mimi hamwezi kufanya cho chote. Mtu ye yote asipokaa ndani yangu hutupwa nje kama tawi litupwavyo nje hata likakauka. Watu huliokota tawi la namna hiyo na kulitupa motoni liungue.”​—Yoh. 15:4-6, Habari Njema kwa Watu Wote.

15. (a) Kama mitume hawakushikamana naye, Yesu hangewaweka hata kidogo washirikiane naye katika kitu gani? (b) Kwa sababu gani mabaki hawangeunga mkono Ushirika wa Mataifa na waendelee kukaa ndani ya “mzabibu wa kweli”?

15 Yesu Kristo hawezi kuwekea “matawi” haya ufalme katika ushirika pamoja naye mbinguni wasiposhikamana naye hata katika wakati wa magumu. (Luka 22:28-30) Ili wadumishe utiwa mafuta wao kwa roho ya Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu, lazima waendelee kukaa ndani yake yeye aliye shina la “mzabibu.” Ama sivyo, taraja lao la kushiriki katika ufalme wa mbinguni lingeondolewa kwao. Kwa hiyo, wakati Nyakati za Mataifa zilipokwisha katika mwaka 1914 na ikafunuliwa kwamba ufalme wa Mungu wa Kimasihi ulikuwa umezaliwa mbinguni, mabaki ya “matawi” yaliyotiwa mafuta yalikuwa na wajibu wa kufanya nini? Wamshangilie Yesu Kristo aliyetukuzwa kwa ushikamanifu kuwa ndiye Mfalme wa Mungu wa Kimasihi aliyetawazwa na kukalia kiti cha enzi! Ili waendelee kukaa ndani yake, wao hawangemkana na kupendelea kitu kingine kilichofanyizwa na wanadamu badala ya ufalme ulio na haki ya kutawala dunia yote, kama vile Ushirika wa Mataifa. Kwa kuwa waliendelea kukaa ndani yake, yeye naye hakuacha kukaa ndani yao.

“MKUTANO MKUBWA” WA UFUNUO 7:9-17

16. (a) Vita ya Pili ya Ulimwengu ilileta matokeo gani katika uhusiano kati ya “mkutano mkubwa” na mabaki ya “matawi” ya ule mzabibu? (b) Kwa habari ya Umoja wa Mataifa, “mkutano mkubwa” ulijiweka upande wa nani, na kwa sababu gani?

16 Katika wakati wa miaka minne ya muda wa Ushirika wa Mataifa likiwa tengenezo la kuhifadhi amani “mkutano mkubwa” uliotabiriwa ulianza kutokea ukiwa na wanaume na wanawake waliofurahishwa na matunda ya Ufalme yaliyotolewa na matawi ya ule “mzabibu wa kweli.” Magumu yenye ukatili pamoja na majaribu waliyoyapata wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu kwa sababu ya kushirikiana na mabaki ya watiwa mafuta hayakuwashinda na kuwafanya waache kushirikiana na wazaaji hao wa “matunda” ya Ufalme. Walijua kwamba ili wawe washikamanifu kwa Mfalme aliyetawazwa na kukalia kiti cha enzi ambaye ndiye “mzabibu wa kweli,” iliwapasa kuwa washikamanifu kwa “matawi” yake, ndugu zake za kiroho. (Mt. 25:31-40) Wakiwa pamoja na “ndugu” za Kristo, walikataa kulikubali tengenezo lililofufuliwa la kuhifadhi amani na usalama likiwa Umoja wa Mataifa. Badala ya kukubali kitu hiki kilichokuwa badala ya ufalme wa Kimasihi wa Yehova, wao waliendelea kuhubiri wakiwa pamoja na mabaki ya warithi wa Ufalme wakiwa Mashahidi wa Yehova.

17. (a) Kwa habari ya kukaa chini ya “mzabibu” katika njia ya mfano, “mkutano mkubwa” wanapendelea kukaa chini ya “mzabibu” gani duniani? (b) Kabla ya hapo walikuwa wakikaa chini ya “mzabibu” gani?

17 Kwa habari ya kukaa salama duniani chini ya mzabibu na mtini wa mtu mwenyewe katika njia ya mfano, huo mkutano mkubwa unapendelea jambo gani? Unapendelea kukaa chini ya “mzabibu wa kweli” pamoja na “matawi” yake kwa kuwa ndio wanaowakilisha ufalme wa Yehova chini ya Kristo. (Mik. 4:1-4) Kabla ya kujifunza habari njema ya ufalme wa Yehova uliokuwa ndiyo umezaliwa ukiongozwa na Yesu Kristo aliye “mzabibu wa kweli,” walikuwa wakikaa chini ya mzabibu mwingine​—“mzabibu wa nchi.” (Ufu. 14:19) Huo ni “mzabibu” wa namna gani? Hilo ni tengenezo la kisiasa ulimwenguni pote ambalo katika hilo watawala wanadamu hujaribu kwa ukaidi kushikilia utawala wa dunia, na kwa njia hiyo kushindana na ufalme wa Yehova wa Kimasihi.

18. Ni kwa sababu gani “matawi” ya ule “mzabibu wa kweli” yamekuwa yakiwahimiza wale wa “mkutano mkubwa” watoke chini ya “mzabibu wa nchi”?

18 “Matawi” yenye kuzaa matunda ya “mzabibu” alioupanda Yehova yamewasihi wale wa “mkutano mkubwa” watoke chini ya “mzabibu wa nchi.” Hawapaswi kuendelea kutumia zabibu na divai yake yenye sumu na yenye kuleta kifo. Namna gani hivyo? Kwa sababu “mzabibu” huo umehukumiwa kuangamizwa, kama ilivyotabiriwa katika Ufunuo 14:18-20;

“Na malaika mwingine akatoka katika ile madhabahu, yule mwenye mamlaka juu ya moto; naye akamlilia kwa sauti kuu yule mwenye mundu ule mkali, akisema, Tia mundu wako mkali, ukachume vichala vya mzabibu wa nchi, maana zabibu zake zimeiva sana. Malaika yule akautupa mundu wake hata nchi, akauchuma mzabibu wa nchi akazitupa zabibu katika shinikizo hilo kubwa la ghadhabu ya Mungu. Shinikizo lile likakanyagwa nje ya mji, damu ikatoka katika shinikizo mpaka kwenye hatamu za farasi, kama mwendo wa maili mia mbili.”

Hapa mzabibu mmoja unashindana na mzabibu mwingine, kwa kuwa Yesu Kristo aliyetukuzwa ambaye ndiye “mzabibu wa kweli,” anauponda mzabibu adui, “mzabibu wa nchi.” “Farasi wanaotumiwa kukanyaga shinikizo hilo lenye kina kikirefu lenye urefu wa maili 200 ni wale farasi wa vita wa Yesu Kristo na majeshi yake ya kimalaika.​—Ufu. 19:11-15.

19. (a) Kwa sababu gani hakuna “shinikizo” la ghadhabu ya Mungu lililowekwa tayari kwa ajili ya “shamba la mizabibu” lake la kiroho? (b) Kwa sababu gani linaweza kuwa jambo lenye kuwadhuru “mkutano mkubwa” wakiingiza vitu kama vile “miiba na mibigili” katika shamba hilo la mizabibu?

19 “Shinikizo” hilo la “ghadhabu” ya Mungu limewekwa tayari kwa ajili ya “mzabibu wa nchi” usio wa Kikristo. Kwa upande mwingine, tangu Mungu awarudishe mabaki ya Waisraeli wa kiroho kwenye kibali yake katika mwaka uliofuata baada ya vita wa 1919, yeye hana “ghadhabu” yo yote juu ya hili “shamba la mzabibu” la mfano au la kiroho. Yeye ameliangalia hili “shamba la mizabibu” la Israeli wa kiroho ili alifanye lizae kwa ajili ya utukufu wake. Ndani yake hamna nafasi ya vitu kama miiba na mibigili ya kuzuia hili “shamba la mizabibu” lisizae matunda. (Luka 6:44) Kwa hiyo, “mkutano mkubwa” unaoshirikiana sasa na “shamba la mizabubu” la Yehova hawapaswi watake kuleta vitu visivyofaa kama vile miiba na mibigili ndani ya “shamba la mizabibu” lenye kuzaa matunda. Hiyo ingewadhuru “mkutano mkubwa,” kwa kuwa Yehova, kwa kutaka kutimiza kusudi lake lisilobadilika la kulifanya “shamba la mizabibu” lake la kiroho lizae kikamilifu, angepigana na “mibigili na miiba” ya namna hiyo. Angeikanyaga ili aiponda-ponde kisha aiteketeze kana kwamba kwa moto.​—Isa. 27:4.

20. “Mkutano mkubwa” wanapaswa kutafuta kuwa na uhusiano wa namna gani na Yehova, nao wanapaswa kushiriki katika kuliimbia “shamba la mizabibu” lake wimbo gani?

20 Huu ndio wakati wa “mkutano mkubwa” kufanya amani na Yehova Mungu na kukishika kisima cha nguvu zake ili watiwe nguvu waweze kufanya yampendezayo. Huu ni wakati unaofaa kwao kuyakumbuka maneno ya wimbo unaoimbiwa sasa “shamba la mizabibu” lake la Israeli wa kiroho: “Katika siku hiyo; Shamba la mizabibu la mvinyo, liimbieni. Mimi, [Yehova], nalilinda, nitalitia maji kila dakika, asije mtu akaliharibu; usiku na mchana nitalilinda. Hasira sinayo ndani yangu; kama mibigili na miiba ingekuwa mbele zangu, ningepanga vita juu yake, ningeiteketeza yote pamoja. Au azishike nguvu zangu, afanye amani nami; naam, afanye amani nami. Siku zijazo Yakobo atatia mizizi; Israeli atatoa maua na kuchipuka; nao watajaza uso wa ulimwengu matunda.”​—Isa. 27:2-6.

21. (a) Lazima mabaki ya Yakobo, au Israeli wa kiroho wazae matunda kadiri gani? (b) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Yehova amelifanya shamba liwazalie matunda?

21 Hii ndiyo “siku” ya mabaki ya Waisraeli wa kiroho ya kuzaa matunda kwa kuujaza uso wa dunia matunda yenye kuendeleza uhai. Yehova amelifanya shamba lizae matunda kuizunguka dunia yote, kwa kuwa mamia ya maelfu wameitikia ushuhuda wa Ufalme unaotolewa na mabaki nao wametokea katika nchi zaidi ya 200 wakawa washiriki wa “mkutano mkubwa” unaomshangilia Yehova Mungu akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote na Yesu Kristo akiwa ndiye ambaye sasa amepewa mamlaka ya kuitawala dunia yote akiwa mfalme.​—Ufu. 7:9-17.

22. Kuzaa matunda kwa mabaki ya “matawi” ya ule “mzabibu wa kweli” pamoja na kule kwa “mkutano mkubwa” kumekuwaje na matokeo kwa habari ya Mungu?

22 Kuzaa matunda kwa “matawi” ya “mzabibu wa kweli” kumemtukuza Yehova Mungu kweli kweli, akiwa ndiye Mkulima. Kwa sababu ya kazi yao ngumu ya Kikristo ule “mkutano mkubwa” unamtukuza Mungu huyu aliyeupanda na kuulimia “mzabibu” huu wa kifalme pamoja na “matawi” yake, wale wa “mkutano mkubwa” wanajiepusha vivyo hivyo na hali yo yote ya kutozaa na kutafuta kuwa wenye kuzaa katika kusitawisha sifa zote za utu wa kimungu na kuzionyesha katika matendo kwa utukufu Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 21]

MABAKI YENYE KUZAA MATUNDA PAMOJA NA “MKUTANO MKUBWA” WATALINDWA WAKATI MALAIKA AVUNAPO “MZABIBU WA NCHI”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki