Zaburi
Yehova, Kimbilio Lenye Kutegemeka
UNAWEZA kufanya nini kunapokuwa uvunjaji mbaya sana wa sheria na utengemano inapoelekea hakuna uwezekano wa kupata haki ya hukumu? Unaweza kwenda wapi? Mtunga zaburi Daudi wakati mmoja alielekeana na hali kama hiyo. Aliweka tumaini lake lote katika Aliye Juu Zaidi, akasema hivi: “Nimefanya kimbilio langu katika Yehova.” (Zab. 11:1, NW) Walakini je! jambo hilo lilifaa?
Wengine hawakudhani hivyo. Walimshauri Daudi na washiriki wake wakimbilie milimani, pengine wafanye kimbilio katika pango, wafanye hivyo haraka kama anavyofanya ndege anapokuwa hatarini. Walakini mtungaji huyo wa zaburi alikataa kufanya hivyo, bila shaka kwa sababu hali wakati huo zilikuwa zile ambazo kukimbia kungeonyesha kukosa kumwamini Yehova kuwa mtoaji wa usalama. Aliwaambia hivi washauri wake: “Mnaweza kuthubutuje ninyi watu kuiambia nafsi yangu [mimi]: ‘Kimbia kama ndege kwenye mlima wenu [wingi, kwa wazi kuhusu Daudi na washiriki wake!]’”—Zab. 11:1, NW.
Sababu gani watu fulani walikuwa wakimshauri Daudi hivyo? Wazo lao lilikuwa hili: “Kwa maana, tazama! waovu wenyewe wanapinda upinde wao, wanatayarisha mshale wao kwenye kamba ya upinde, wapige gizani wale walio wanyofu katika moyo. Misingi yenyewe inapoangushwa chini, mtu ye yote aliye mwenye haki anapaswa kufanya nini?” (Zab. 11:2, 3, NW) Kulingana nao, waovu walikuwa na upinde wao wakiwa tayari kupiga watu wenye haki, wakifanya hivyo “gizani,” wakifichwa na giza. Hawakuwa wamekamata upinde tu bali tayari walikuwa na mshale kwenye kamba ya upinde, ukiwa umelengwa kuwaelekea wale walio wanyofu moyoni. Kwa sababu hiyo, washauri wa Daudi wangeweza kuendelea kubisha hivi: ‘Misingi inayotegemeza jamii—haki ya hukumu, sheria na utengemano—imeangushwa chini. Kwa hiyo, mtu mwenye haki ana uchaguzi gani ila kukimbia tu? Hawezi kubadili mambo; hawezi kutendewa kwa haki.’
Daudi alijibuje? “Yehova yu katika hekalu lake takatifu. Yehova—kiti chake cha enzi ki katika mbingu. Macho yake mwenyewe hutazama, macho yake mwenyewe yenye kung’aa huchunguza wana wa watu. Yehova mwenyewe humchunguza mwenye haki na mwovu pia, na ye yote anayependa jeuri hakika nafsi Yake inamchukia. Atanyesha juu ya waovu mitego, moto na kiberiti na upepo wenye kukausha, kuwa fungu la kikombe chao. Kwa kuwa Yehova ni mwenye haki; anapenda vitendo vya haki. Wanyofu ndio watakaouona uso wake.”—Zab. 11:4-7, NW.
Daudi alikuwa na uhakika kwamba kumtegemea Yehova kama kimbilio lake kusingekuwa kwa bure. Alijua kwamba Aliye Juu Zaidi, Yeye ambaye ndiye kiti chake cha enzi ki katika mbingu zilizo juu zaidi, anatazama. Macho ya Yehova yanapenya mpaka ndani kabisa ya vitu. Hakuna lo lote linalokosa kuonwa naye. Kwa kuwa macho ya Yehova yako juu ya wenye haki, anajua wanayohitaji na, kwa hiyo, anaweza kuja kuwaokoa. Kwa upande mwingine, Aliye Juu Zaidi anachukia watu wenye jeuri na, hivyo, kuwachunguza kunafanya msiba wao uwe jambo la hakika. Lazima wakati utakuja wakati waovu watakapolazimishwa kunywa kinywaji chenye kuua cha hukumu za Yehova, zinazofananishwa na mitego, moto, kiberiti na upepo wenye kukausha unaokausha majani. Hakutakuwako kuponyoka kufikilizwa kwa hukumu za Mungu. Itakuwa kama kwamba mitego inaanguka chini kama mvua kutoka juu ya anga. Kwa sababu Yehova mwenyewe ni mwenye haki na anapenda vitendo vya haki, wanyofu watapata wokovu ulio bora sana. Itakuwa kama kwamba uso wa Mungu umegeuzwa kuwaelekea kwa kuwaonyesha upendo na kibali. Kwa hiyo wataona uso wa Mungu kama watu wenye kufurahia baraka na kibali yake.
Kweli kweli, maneno ya mtunga zaburi yanaweza kuwa chanzo cha kweli cha faraja kwetu nyakati za magumu. Bila shaka kwa hekima kuna nyakati tunapoikimbia hatari, kama alivyofanya Daudi alipokuwa akiondoka Yerusalemu kwa ajili ya uasi wa Absalomu. (2 Sam. 15:14) Hata Yesu Kristo aliwaagiza wafuasi wake hivi: “Wakati wanapowatesa ninyi katika muji huu, kimbieni kwa muji mwingine.” (Mt. 10:23, ZSB) Maneno ya mtunga zaburi, hata hivyo, yanatutia moyo tuepuke kuchukua tendo la haraka-haraka lenye kuonyesha kukosa imani kwa Yehova. Kuendelea kwetu kumtegemea Aliye Juu Zaidi kama kimbilio letu kutatupa kibali yake. Hatakosa kuwa mwaminifu kwetu.—Rum. 8:38, 39.