Ushuhuda wa Kuwako kwa Muumba
EBU chukua darubini yenye nguvu kupita zote, uutazame ukubwa wa mbingu. Tazama kwa darubini ya kisasa yenye kuona vitu vilivyo vidogo zaidi kama vile chembe. Nawe waona nini? Hili—kwamba katika vile vilivyo vikubwa zaidi, pamoja na vile vilivyo vidogo zaidi, ndiyo, katika ulimwengu wote ulio mkubwa mno wenye kuonekana—kunao utaratibu, uzuri na mpango. Napo tunapouona mpango, tunafikia mkataa gani? Je! Biblia haionyeshi jibu, katika Waebrania 3:4, HNWW?—“Kila nyumba hujengwa na mjenzi fulani—na Mungu ndiye mjenzi wa vitu vyote.”
Namna gani juu ya utaratibu? Bwana Isaac Newton, mwanasayansi mwenye kumwogopa Mungu ndiye aliyekuwa wa kwanza kufahamu kwamba vitu katika ulimwengu wote ulio mkubwa mno vilikuwa vikiendelea kutoka kwenye utaratibu kuingia kwenye hali isiyo na utaratibu. Jambo hilo liliongoza kwenye kukata maneno kwamba, isipokuwa nguvu fulani yenye kutoka nje iingilie jambo hilo kwa kusudi, kila tendo la kubadili vitu vinavyoonekana katika ulimwengu unaotuzunguka litafuatwa na hali ya kupoteza mpango. Ule mpango wa kwanza unaharibika. Kwa hiyo, lazima iwe kwamba Mtu fulani alikusudia, akaumba na kupanga vitu katika utaratibu fulani. Isipokuwa Mkusudiaji huyo aingilie hali hiyo, utaratibu utaendelea kuharibika.
Kwamba Mkusudiaji mwenye akili aliutokeza ulimwengu ulio mkubwa mno ni wazo linalopatana na wazo la wanasayansi la kwamba ulimwengu wote ulio mkubwa mno ulitokea mabilioni ya miaka iliyopita kwa sababu ya mlipuko wa kitu kimoja. Katika miaka ya karibuni kisio hilo limependelewa zaidi ya lile linalodai kwamba ulimwengu wote ulio mkubwa mno umekuwako nyakati zote, maana yake, hauna mwanzo. Walakini si lazima tutegemee makisio ya sayansi ya kisasa yenye kubadilika-badilika ili kuthibitisha kwamba yuko Muumba. Kwa kuwa Muumba huyo mwenyewe anaonyesha wazi yeye ni nani na ni nini: “[Yehova], . . . asema hivi; . . . Mimi nimeiumba dunia, [nimemwumba] mwanadamu juu yake; Mimi, naam, mikono yangu mimi, imezitanda mbingu, na jeshi lake lote nimeliamuru.” (Isa. 45:11, 12) Ushuhuda wa yeye kuwa Muumba unaonekana na kustaajabiwa katika vitu vingi, vingi sana tunavyoviona vikituzunguka.
“MIMI . . . [NIMEMWUMBA HATA] MWANDAMU”
Bila shaka, katika nyakati mbalimbali, sisi sote tumecheza-cheza na vidole vidogo sana vya mtoto—vyororo, vilivyoumbwa vizuri sana, vyenye thamani kubwa—vilivyotengenezwa vizuri kuliko vidole vya wanyama! Na bila shaka tumepata kuwaza namna uhai mdogo sana wa mtoto huyo ulivyoanza kutokana na mbegu ya mama yake yenye ukubwa kama wa ncha ya sindano, kwa kuungana na shahawa ya baba iliyo ndogo sana isiweze kuonekana kwa jicho la kawaida. Ndiyo, sisi sote tulikuwa na mwanzo mdogo sana, katika chembe ya mbegu iliyojigawanya, ikajigawanya, ikiendelea kujigawanya, mpaka mwishowe zile chembe zaidi ya 10,000,000,000,000 zinazoufanyiza mwili wa mtu mzima ‘zikajua’ wakati wa kuacha kujigawanya.
Mfuatano wote wa mambo, mtungo wa mimba na ukuzi wenye kuchagua ni wenye kustaajabisha sana tusiweze kuufahamu. Walakini si jambo asiloweza kufahamu Mungu, kwa kuwa ndiye aliyeuanzisha. Ni kama vile Mfalme Daudi aliyosema: “Mifupa yangu hukufichwa wewe wakati nilipoumbwa kwa siri. . . . Macho yako yaliona hata mwanzo wa mimba yangu, na sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa kwa mwandiko katika kitabu chako.” Ndiyo, tuliumbwa kulingana na ‘mambo yaliyoandikwa’ na Muumba mwenye upendo, tukapewa mwili mzuri sana pamoja na sifa zenye adili zilizokusudiwa zitusaidie kuendeleza usawa maishani mwetu na kuyafanya maisha yafurahishe wakati wote. Kwa hiyo tuna kila sababu ya kuungana na Daudi katika maneno ya wimbo wake aliouimba miaka 3,000 iliyopita: ‘‘Ee Yehova, umenichunguza mimi, nawe wanijua. . . . Uliendelea kunificha katika tumbo la mama yangu. Nitakusifu wewe kwa sababu kwa njia yenye kutia hofu nimeumbwa kiajabu. Kazi zako ni za ajabu, kama nafsi yangu inavyojua sana.”—Zab. 139:1, 13-16, NW.
Hakuna mwisho wa maajabu ambayo yametiwa katika kiumbe cha Mungu, mwanadamu. Wengine wanaweza kudaije kwamba uhai ulianza kwa bahati tu, na kwamba mwanadamu aligeuka-geuka kutokana na chembe ndogo sana kwa mfululizo wa matukio yasiyokusudiwa? Katika chembe iliyo ndogo sana ya mwanadamu mna visehemu vidogo sana vinavyofanana na ngazi vinavyoitwa DNA, kila kimojawapo kikiwa na habari juu ya mtu yule yule tu, habari zile zile juu ya uhai zikiwa zimeandikwa katika kila chembe yenye kujigawanya. Habari hizo zaonyesha ni chembe zipi zinazopaswa kufanyiza macho, pua, ulimi, masikio, meno, ngozi, viungo, na sehemu zote nyingine za mwili. Zinahakikisha kwamba “aina” hiyo ni ya kibinadamu kabisa, si nyani, au mbwa au mnyama mwingineyo. Zinaonyesha tabia zinazoweza kurithiwa za mtu huyo. Sehemu zilizofanyizwa kipekee sana zinazotokana na mfululizo huo wa ukuzi zinaonyesha kweli kweli kwamba yuko Muumba mwenye akili sana!
AKILI YA MWANADAMU
Bila shaka sehemu inayostaajabisha zaidi ya kiumbe hicho cha kidunia cha Mungu, mwanadamu, ni ubongo, ilimo akili. Ubongo unakua kwa haraka sana, ukifikia robo tatu za uzito wake wa ule wa mtu mzima katika miaka miwili ya kwanza ya kuishi. Si ajabu kwamba vitoto vyetu vichanga vinakuwa na maulizo mengi sana na hamu ya kutaka kujua: ‘Ni nani aliyeumba mbingu? ndege? paka? maua? Ni nani aliyeniumba mimi?’ Kwani, hata katika umri huo wa mapema, mtoto huyo amekwisha tambua kwamba vitu vinavyomzunguka vina wale walioviumba. Kwa hiyo, anakata maneno kwamba, vitu vyote vilikuwa na Yeye aliyeviumba. Ni kwa sababu gani watu wengi sana wazima wameacha kufikiri katika njia hiyo yenye akili?
Ubongo wenyewe unastaajabisha kwa vile ulivyo kama chembe ndogo za umeme zenye uhai. Kwa halisi maelfu ya wanasayansi huenda wakafanya kazi kwa miaka mingi ili watokeze na kutia habari kwenye kompyuta inayofaa kufanya kazi ya namna fulani. Hata hivyo wanalazimika kukubali kwamba, ikiwa wangeweza kutokeza kompyuta yenye eneo la kuwekea habari na uwezo wa kufanya mambo ya namna mbalimbali kama ubongo wa kibinadamu, wangehitaji jengo refu sana na lenye vyumba vingi sana la kuiweka. Hata hivyo ubongo wa kibinadamu wenye uzito wa ratli tatu (karibu kilo moja na nusu) wenye ukubwa mdogo hivi kwamba waweza kuushika kwa mkono mmoja, umepewa uwezo kabisa wa kujipangia habari wenyewe, na kushughulika na kila hali iliyo ya lazima kwa maisha ya kibinadamu. Na zaidi, unapokusanya habari zake wenyewe kutoka kwa fahamu za kuona, kusikia, kugusa, kuonja na kunusa, na kuanzisha usemi na matendo ya mwenyeji, unafanya kazi kwa kadiri ambayo hakuna kompyuta yenye kufanyizwa na mwanadamu itakayoweza kufikia. Nayo ni kompyuta gani itakayofanya kazi kutokana na moyo wenye kuonyesha upendo, fadhili za kibinadamu, shukrani, na kuthamini? Ni kompyuta gani itakayofikiri, itoe sababu, maelezo, au imwabudu mwenye kuifanyiza?
Tunapofikiria namna mwanadamu ameumbwa kiajabu, na ulimwengu wote ulioumbwa unaotuzunguka, kwa habari ya kazi za Mungu zinazoonekana, twaweza kusema pamoja na Ayubu hivi: “Tazama, hivi ni viunga tu vya njia zake; na jinsi yalivyo madogo manong’ono tusikiayo katika habari zake!” (Ayubu 26:14) Walakini haitupasi kutosheka na kusikia manong’ono tu kuhusu Muumba wetu. Tukilichunguza Neno lake, Biblia, tutajifunza mengi, wala si juu ya kuumba kwake tu, bali pia juu ya kusudi zuri sana la kuviumba vyote hivyo.