Vijana Wanaomkumbuka Muumba Wao
KICHWA cha kipindi cha Ijumaa alasiri katika “Imani Ishindayo” makusanyiko ya mataifa yote zaidi ya 100 ya Mashahidi wa Yehova wakati wa mwaka 1978 kilikuwa “ENYI VIJANA, MWE VIELELEZO KATIKA IMANI.” Wakati wa sehemu hii ya programu yenye kichwa “Vijana Wanaomkumbuka Muumba Wao,” vijana wa kiume na wa kike waliojiweka wakf walizungumza juu ya maisha yao kama watumishi wa Yehova. ‘Yafuatayo ni mambo yaliyoonwa ambayo wali-simulia.
Utaona kwa hesabu fulani ya vijana waliohojiwa waliamua kutumia wakati wao wote katika kuhubiri “habari njema hizi za ufalme.” (Mt. 24:14, NW) Baadhi yao wanafanya hivyo kama “mapainia wa pekee,” wakitumia zaidi ya saa 140 kila mwezi katika utendaji huu. Wengine wamekuwa “mapainia wa kawaida,” wanaotumia saa zisizopungua 1,000 kila mwaka katika kutangaza “habari njema.” Ebu na tufikirie baadhi ya mambo haya yaliyosemwa na vijana hawa Wakristo.
Katika kusanyiko mjini New York, kijana mwanamke alisimulia hivi: ‘Najua kwamba vijana wengine wanasita juu ya kuwa na wajibu kwa Yehova Mungu. Hata wengine waliobatizwa hawatangulizi faida za kiroho. Nazungumza kutokana na mambo niliyoona, kwani ndivyo mimi nilivyojisikia. Walakini kanuni za Maandiko, kama ile ya Malaki 3:10 ambapo tunaambiwa tumlipe Mungu kile tunachodaiwa, zilinisaidia kubadili moyo wangu. Nawatia moyo nyie vijana wote katika wasikilizaji mtangulize faida za kiroho. Ye yote ambaye ana umri wa kutosha kwenda kwenye karamu au kufanya uasherati au kutumia dawa za kulevya ana umri wa kutosha kuweka maisha yake wakf kwa Yehova pia.’
KUFURAHIA “UTUMISHI WA SHAMBANI”
“Shamba ni ulimwengu,” akasema Yesu. (Mt. 13:38) Ndiyo sababu Mashahidi wa Yehova wanauita utendaji wao wa kuhubiri “utumishi wa shambani.” Katika kusanyiko la New York, msichana mmoja alizungumza juu ya yale yaliyomaanishwa na utumishi wa shambani kwake:
‘Utendaji wangu wa kushiriki kweli za Biblia pamoja na wengine ulianza nilipokuwa na umri mdogo sana. Nilipokuwa nikienda pamoja na wazazi wangu nyumba kwa nyumba, nilikuwa nikimsalimia mwenye nyumba na kutabasamu na kumpa ujumbe uliochapwa. Muda si muda niliweza kuzungumza na watu juu ya vichwa vya Biblia. Nilifurahi kujua kwamba hesabu fulani ya wale niliozungumza nao walitaka kupata msaada wa kuifahamu Biblia. Niliwatembelea kwa ukawaida nami nilifurahi sana kuona wakifanya maendeleo katika maarifa ya Mungu na kuona wakiacha mazoea machafu, na pia kuonyesha tamaa ya kushiriki mambo yenye msingi wa Biblia waliyopata kuamini. Kushiriki utumishi wa shambani kwa ukawaida kumeitia imani yangu nguvu juu ya taratibu mpya ya Mungu inayokuja ambayo itarudisha paradiso ya duniani pote. (Ufu. 21:l-5) Ikiwa nitasadikisha wengine juu ya tumaini hilo, ni lazima kwanza liwe lenye nguvu ndani yangu.’
Shahidi kijana aliyezungumza na wenye kuhudhuria kipindi cha Kiingereza katika Montreal, Canada, alisimulia hivi: ‘Utumishi wangu wa shambani ulianza wakati wa utoto wangu wa mapema sana. Nilikuwa nikiandamana na wazazi wangu katika utendaji wa kuhubiri. Nilipokuwa na umri wa miaka mitano nilianza kutoa mahubiri mepesi mlango kwa mlango.
‘Wakati wa miaka hiyo ya mapema utumishi wa shambani ulikuwa jambo la kuchezea. Hata hivyo, baada ya muda fulani nilipata kufahamu kwamba shuleni nilikuwa tofauti kabisa na wengine wote. Ndipo lilipoanza kuwa jambo gumu kuzungumza na wanafunzi wenzangu juu ya kweli. Wakati wa kuhubiri nyumba kwa nyumba, nilikuwa nikiogopa wazo la kukutana na mtu ninayejua shuleni. Ninapokumbuka wakati huo, naona kwamba kwa habari yangu tatizo langu lilikuwa kumwogopa mwanadamu, ambako Biblia inasema “huleta mtego.’”—Mit. 29:25.
‘Baada ya kumaliza masomo shuleni, niliamua kujaribu kupainia kwa muda. Kama matokeo, kuhubiri kulianza kunipendeza kuliko wakati mwingine wo wote. Sikuuona tena kuwa utendaji wa kuchezea wala haukuwa mzigo. Kwa kuona wanafunzi wangu wakifanya maendeleo katika kweli, nilifurahia uradhi mwingi sana kwa kuona ushuhuda wa kwamba Yehova Mungu alikuwa akitegemeza jitihada zangu. Sasa nimekuwa nikipainia kwa muda wa miaka miwili na nusu. Nikikumbuka nafasi nilizokuwa nazo za kuchagua kazi nyingine, maoni yangu ni kama yale ya mtume Paulo, aliyeandika hivi: “Nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo.”—Flp. 3:8.
KULITHAMINI KUNDI
Je! vijana wanafurahia kushirikiana na kundi la Kikristo? Dan, anayetumikia kama painia katika Quebec, Canada, anasimulia haya aliyoona yeye mwenyewe: ‘Nilibatizwa tangu mwaka 1975 tu, na maisha yangu kabla ya kuijua kweli ya Biblia yalikuwa yasiyo na adili na yasiyo ya Kikristo. Nilitafuta msisimuko, nilikuwa nikilewa mara nyingi. Wakati hili lilipoacha kunifurahisha, nilianza kuvuta bangi. Nilipokuwa na umri wa miaka 17 nilikuwa nikivuta bangi karibu kila siku.
‘Walakini furaha niliyodhani kuwa nilikuwa nayo wakati huo ilikuwa si kitu ikilinganishwa na furaha ambayo nimepata tangu nianze kushirikiana na watu wa Yehova. Mkutano wangu wa kwanza kwenye Jumba la Ufalme ni jambo linalofaa kukumbukwa. Jambo lililonivutia zaidi ni kwamba baada ya mkutano watu mbalimbali walinijia na kujijulisha kwangu katika jitihada za kunifanya nijisikie kustarehe. Tangu wakati huo nimehudhuria kwa ukawaida mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Kabla ya kujifunza kweli, sikuwa na tamaa ya kushirikiana na watu walio wazee, kwani hakukuwa na jambo ambalo tungeshiriki pamoja. Walakini nimepata rafiki wengi wazuri wa umri wote kati ya Wakristo wenzangu.’
MWENYE UMRI WA MIAKA 10 ATAFUTA MSAADA
Katika kusanyiko la Munich, Ujeremani, kijana wa kiume alitoa jambo hili lililoonwa katika kipindi cha lugha ya Kigiriki katika kusanyiko hilo: ‘Nilipokuwa katika shule ya msingi, wazazi wangu waliacha kushirikiana na kundi la Kikristo. Nina furaha kuwaambia kwamba, ijapokuwa nilikuwa mtoto, nilifaulu kuendelea kushirikiana na kundi kwa njia fulani.
‘Nilipokuwa na umri wa miaka 10 nilianza kumwomba Yehova msaada. Kwa kuwa wazazi wangu hawakuniruhusu kushirikiana na Mashahidi wa Yehova waziwazi, niliona kwamba njia ya pekee ya kusaidia kazi ya kuhubiri ni kuchanga fedha. Kwa hiyo nilianza kukusanya fedha nilizopewa na wazazi za matumizi yangu ya kipekee. Kwa muda wa miaka miwili nilikusanya drachma 500 (fedha za Kigiriki). Kwa furaha nilitoa hizi kwa kundi. Miaka mingi baadaye nikaenda katika nchi ya ugeni kwa ajili ya masomo yangu ya shule. Hata hivyo, nia yangu ya kweli, ilikuwa kuwa huru niweze kuhudhuria mikutano ya kundi.
‘Wazazi wangu waliposikia hayo, yakawa na matokeo mazuri juu yao. Kwa mara nyingine tena wakaanza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme na sasa baba yangu anatumikia katika cheo chenye madaraka kunduni. Kwa habari yangu mimi, sasa ninafurahia kutumikia kama painia wa kawaida nalo hilo ndilo ninalotakia vijana wote.’
Ni jambo linalopendeza kweli kweli kusikia habari za vijana wengi ambao wamefanya ibada ya Yehova kuwa jambo kubwa maishani mwao. Tunatumaini kwamba mambo haya yaliyoonwa yataamsha wengine waitii hii amri ya Maandiko: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako.”—Mhu. 12:1.