Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 6/1 uku. 22
  • Maswali Kutoka Kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Habari Zinazolingana
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Jinsi Wema Utakavyoshinda Uovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Je! Wema Utapata Kuushinda Uovu Wakati Wowote?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 6/1 uku. 22

Maswali Kutoka Kwa Wasomaji

● Sababu gani torati ya Musa ilitoa adhabu ya kifo kwa mtu ye yote aliyelaani wazazi wake?

Sheria ya Mungu ilisema hivi: “Kwa maana kila mtu amlaaniye baba yake au mama yake hakika atauawa; amemlaani baba yake na mama yake; damu yake itakuwa juu yake.” (Law. 20:9) Mtu kuwalaani wazazi wake, kutaka msiba mbaya uwapate, kungeonyesha maelekeo yenye chuki, ya uuaji. Kungekuwa kukosa vibaya sana shukrani kwa ajili ya ulinzi na uangalizi aliopewa na wazazi wake. Ingawa mwenyewe hakutumia silaha kuwapiga, mtu huyo, alitamani moyoni kwamba wafe kwa njia nyingine. Machoni pa Mungu, roho hiyo ya ukatili ni uuaji. (Linganisha Mathayo 5:21, 22; 1 Yohana 3:15) Kwa hiyo, katika sheria yake kwa Israeli, Aliye Juu Zaidi alitoa adhabu ile ile kwa kutukana wazazi kama vile kuwaua halisi.

● Andiko la Danieli 12:1 linamtaja Mikaeli kama ‘akisimama’ kabla ya wakati wa taabu isiyo na mfano wake. Je! Mikaeli amekwisha ‘simama’ tayari, au jambo hilo litatokea muda mfupi tu kabla ya “dhiki kubwa”?

Vionyesho vinaonyesha kwamba Mikaeli amekwisha ‘simama.’

Danieli sura ya kumi na moja linatoa unabii wenye kuendelea juu ya mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini. Twafahamu kwamba unabii huo unasimulia matukio ya kihistoria tangu wakati wa Danieli mpaka wakati huu.a Kisha sura ya 12 inaanza hivi: “Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo.”​—Dan. 12:1.

Mikaeli ‘alisimamaje,’ nalo jambo hilo lingetukia wakati gani?

Mara kadha wa kadha kitabu cha Danieli hutumia tendo la ‘kusimama’ kusimulia kuchukua kwa mtu mamlaka au uweza. Kwa mfano unabii fulani juu ya Aleksanda Mkuu akijitwalia mamlaka unasema hivi: “Na mfalme hodari atasimama, atakayetawala kwa mamlaka kubwa, na kutenda apendavyo.” (Dan. 11:3; linganisha Danieli 11:7, 21; 8:22, 23.) Kwa hiyo, ‘kusimama’ kwa Mikaeli kungemaanisha kutwaa kwake mamlaka au kuanza kutawala.

Baada ya kufufuliwa kwake Yesu Kristo, ambaye kutokana na Maandiko twamfahamu kuwa Mikaeli malaika mkuu, alipaswa ‘kuketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu’ mpaka ufike wakati wake wa ‘kwenda akishinda katikati ya adui [zake].’ (Zab. 110:1, 2, NW: Ebr. 10:12, 13) Mara nyingi Mashahidi wa Yehova wameonyesha kutoka katika Biblia na utimizo wayo katika historia kwamba kipindi cha Yesu cha ‘kuketi’ kilimalizika wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza yenye kuendelea kwa ukali katika vuli ya mwaka 1914 W.K. Kisha ukafika wakati wake wa ‘kusimama’ au kukubali utawala wa Ufalme mbinguni, ambao unatajwa katika sehemu ya kwanza ya Danieli 12:1.

Mstari huo unaendelea kusimulia jambo lile jingine ambalo lingetokea. Kungekuja “wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa.” Katika Mathayo 24:21, Yesu aliiita “dhiki kubwa.”

Wakati wa kipindi cha katikati tangu ‘kusimama’ kwa Mikaeli, mataifa yamekuwa na nafasi ya kukubali na kutii utawala wa Ufalme. Walakini yamekataa kufanya hivyo na hata yamewatesa Wakristo wanaotangaza kwamba Yesu ndiye mtawala mwenye ruhusa wa ‘ufalme wa dunia.’ (Ufu. 11:17, 18) Kukusanyika pamoja kwa vikundi vya kitaifa juu yake na watu wake hakujamfanya Mikaeli auache utawala wake. Hasha, ameendelea kudumu katika huo. Matokeo ya mwendo wa mataifa yatakuwa yenye msiba kwao. Utawaongoza kwenye mwanzo wa ile “dhiki kubwa,” ambayo katika hiyo watavunjwa, vipande vipande kama vile nyungu ya mfinyanzi iwezavyo kuvunjwa kwa fimbo ya chuma. (Zab. 2:1, 2, 8, 9) Kwa kufurahisha, Danieli 12:1, 2 linaonyesha kwamba watu wa Mungu kama kikundi wataokoka huo “wakati wa taabu” na kuingia kwenye Taratibu Mpya ambamo hata watu wenye haki waliokufa watafufuliwa.​—Matendo 24:15.

● Ikiwa Petro hakupata kamwe kuwa katika Korintho, sababu gani wengine huko wakadai kuwa ‘ni wa Kefa (Petro),’ na sababu gani habari hiyo imo katika Biblia?

Ni kweli kwamba Biblia haitoi kionyesho cho chote kuonyesha kwamba mtume Petro alipata kuwa katika Korintho wakati wo wote. Hata hivyo, mtume Paulo aliliandikia kundi hilo hivi: “Kila mtu wa kwenu husema, Mimi ni wa Paulo, na Mimi ni wa Apolo, na, Mimi ni wa Kefa, na, Mimi ni wa Kristo.”​—1 Kor. 1:12.

Paulo alikuwa amesikia kwamba wengine huko walikuwa wakileta mgawanyiko, wakijipanga pamoja na majina ya Wakristo mashuhuri. Wote wawili Paulo na Barnaba walikuwa wamekuwa huko Korintho. Kwa hiyo wengine huko huenda wakawa walitetea mmoja wao na wengine mwingine kwa sababu ya kuwa walikuwa wamejifunza mengi kutoka kwao, kwa sababu ya utu wao au kwa sababu ya uwezo wao wa kufundisha.

Lakini sababu gani wengine wao waseme kwamba wao walikuwa wa Petro, na hali kwa wazi yeye hakupata kamwe kuwa katika Korintho? Si jambo lisilowezekana kwamba wengine wao walikuwa wamejifunza juu ya Petro na namna alivyotumia zile “funguo za ufalme wa mbinguni.” (Mt. 16:18, 19) Hivyo, wengine huko Korintho huenda wakawa walikuwa wamelichukua jina la Petro kama kwamba maoni yake ya Ukristo yalikuwa yanakaribiana na yale ya dini ya Wayahudi na kama yaliyotofautiana na yale ya Paulo, ambaye alikazia kwamba Wakristo hawamo chini ya torati ya Musa. (Gal. 2:15-21; 4:8-11) Petro alikuwa amepata kujulikana sana wakati wa kufungulia Wayahudi pamoja na waongofu (wafuasi wa dini ya Wayahudi) njia kwenye Ukristo kabla Wasamaria na watu wa Mataifa hawajafunguliwa Njia. Na katika wakati mmoja huko Antiokia alikuwa ameonyesha kuhangaikia isivyofaa maoni ya Wakristo Wayahudi, Paulo akalazimika kumsahihisha. (Gal. 2:11-14) Hivyo, wakati wa mgawanyiko uliokuwako huko Korintho, huenda wengine walijipanga katika upande wa Kefa kama kwamba Ukristo wake ulikuwa namna ya Ukristo uliotofautiana na ule wa wale waliochukua jina la Paulo.

Kwa kufaa, akiwa chini ya uongozi wa roho ya Mungu, Paulo alilaumu mgawanyiko wa namna hiyo. Aliwasaidia Wakristo wa Korintho waone sababu ya uhakika wa kwamba Kristo hawezi kuwa amegawanyika. Ijapokuwa sana sana Paulo ‘aliaminishwa habari njema kwa wale wasiotahiriwa naye Petro kwa wale waliotahiriwa,’ Paulo akielekeza sana sana mahubiri yake kwa watu wa Mataifa na Petro kwa Wayahudi, kwa msingi, ujumbe wao ulikuwa ule ule. (Gal. 2:7, 8; Efe. 4:4-6) Wao hawakuwa wamegawanyika katika mafundisho yao wala katika kusudi lao. Wote wawili Paulo na Petro walikuwa wameshiriki katika mkutano huko Yerusalemu (49 W.K.), ulipofanyiwa uamuzi wa kwamba watu wa Mataifa waliogeuka hawakuwa na lazima ya kutahiriwa na kushika Torati. (Matendo 15:7-14) Na hata Petro alimwita Paulo “ndugu yetu mpenzi” ambaye maandiko yake yalikuwa ya maana pamoja “na maandiko mengine” yote. (2 Pet. 3:15, 16) Hivyo, hakukuwa na sababu yo yote nzuri ya kuwako mgawanyiko huo katika Korintho.

Habari hii ilitiwa ndani ya Biblia ikiwa kama shauri lenye onyo. Leo, pia, vikundi vidogo vidogo vyaweza kutokea katika kundi. Kwa mfano, wengine kundini huenda wakawa na maoni ya kutaka uhuru zaidi na hivyo washirikiane zaidi na wale wenye maoni kama yao au na mzee Mkristo wanayemwona kuwa na maoni kama yao. Huenda wale wengine wakaonwa na kile kikundi cha kwanza kuwa wasiopendelea mabadiliko katika mambo, au wakitafuta shauri na kufuata maoni ya mzee wanayempendelea. Huenda hali kama hiyo ikaleta roho mbaya ya mgawanyiko na faraka. Mara nyingi sana wanadamu wasiokamilika wanaelekea sana kupendelea wale wanaotekenya masikio yao. Walakini shauri la Mungu ni kwamba hekima ina wingi wa washauri, ambao wanapaswa kushirikiana katika kutumia ujuzi wao wa Neno la Mungu pamoja na mambo ambayo wamepata kuona.​—Mit. 15:22.

[Maelezo ya Chini]

a Tazama “Your Will Be Done on Earth” (1958), kur. 220-307.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki