Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 11/1 kur. 10-15
  • Kuendeleza Usafi Wakati wa Kuleta Zawadi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuendeleza Usafi Wakati wa Kuleta Zawadi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUJIFUNZA JUU YA DHABIHU ZINAZOKUBALIKA KUTOKANA NA MIPANGO MINGINE YA TORATI
  • KUJALI KWINGI ANAKOTUJALI YEHOVA
  • Watu Waliosafishwa kwa Ajili ya Kazi Zilizo Bora
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Kufukiza Uvumba—Je, Kunahitajiwa Katika Ibada ya Kweli?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Kumtolea Yehova Vilivyo Bora Zaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Jinsi ya Kumkaribia “Msikiaji wa Sala”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 11/1 kur. 10-15

Kuendeleza Usafi Wakati wa Kuleta Zawadi

‘‘Mpeni [Yehova] utukufu wa jina lake, leteni [zawadi] mkaziingie nyua zake. Mwabuduni [Yehova] kwa uzuri wa utakatifu.”​​—⁠Zab. 96:8, 9.

1, 2. Kwa sababu gani lazima watu wa Mungu wawe safi, na jambo hili lilikaziwaje kwa Waisraeli?

UTAKATIFU, utakato au usafi wa Yehova unawataka watu wake waendelee kuwa safi. (1 Pet. 1:14-16) Uhakika huu ulikaziwa kwa Waisraeli kwa mipango iliyotolewa katika torati ya Musa. Iliwapasa waendelee kujitenga na mazoea ya uasherati na yenye kushusha adili ya mataifa waliowazunguka, na ikiwezekana, waepuke kugusa maiti au kitu kingine cho chote ambacho kingewachafua.​​—⁠Law. 11:4-8, 10-20, 24, 25; 18:3-24.

2 Walipokuwa kwenye safari za kivita, Waisraeli waliamriwa wadumishe usafi katika kambi zao. Sheria ilisema hivi: “Na kiwe kitakatifu kituo chako; asije akaona [Yehova] kitu kwako kisichokuwa najisi mpaka jioni.’ acha.” (Kum. 23:14) Iwapo Mwisraeli alichafuliwa kwa njia fulani, ilimpasa ‘kufua nguo zake, naye aliendelea kuwa najisi mpaka jioni.’ (Law. 11:40) Hata kule kuosha hakukutosha. Mpaka siku nyingine ilipofika wakati wa machweo kulingana na namna ya Kiebrania ya kuhesabu siku, ndipo mtu angeweza tena kuwa na msimamo unaofaa kwa Yehova. Wakati wa kipindi cha kutangatanga jangwani cha Waisraeli, wakati kambi yao ilipokuwa na watu milioni nyingi, kuendeleza kanuni ya kimungu ya usafi halikuwa jambo rahisi.

3. Kwa habari ya mambo ya usafi, makuhani wa Kiharuni walikuwa na daraka gani?

3 Ili kutoa dhabihu yenye kukubalika, ilimpasa Mwisraeli kuwa safi kwa ajili ya sherehe hiyo. (Law. 15:31) Lilikuwa daraka la makuhani kuendeleza kanuni ya Mungu ya usafi, kudumisha usafi wao wenyewe na kusaidia Waisraeli wenzao kuwa katika hali yenye kukubalika ili kutoa matoleo ambayo yangekubaliwa na Mungu.​​—⁠Mal. 2:7.

4. Yehova alizionaje dhabihu za Waisraeli ambao hawakutimiza matakwa yake?

4 Waisraeli walipodharau matakwa ya kimungu ya mwenendo unaofaa, si kwamba tu dhabihu zao hazikufaa kitu bali zilimchukiza Yehova Mungu. Maandiko yanatuambia hivi: “Sadaka ya mtu mbaya ni chukizo kwa [Yehova]; bali maombi ya mtu mnyofu ni furaha yake.” (Mit., 15:8) “Yeye achinjaye ng’ombe ni kama yeye amwuaye mtu; na yeye atoaye dhabihu ya mwana-kondoo ni kama yeye avunjaye shingo ya mbwa; afukizaye uvumba ni kama yeye abarikiye sanamu; naam, wamezichagua njia zao wenyewe, na nafsi zao zafurahia machukizo yao.”​​—⁠Isa. 66:3.

5. Kwa sababu gani inatupasa leo kuhangaikia msimamo wetu na Mungu?

5 Kanuni za haki zilizotiwa katika sheria ya Mungu kwa Israeli hazijabadilika. Zinatumika wakati wote, katika hali zote na chini ya hali zote. Ndiyo sababu mashahidi Wakristo wa Yehova leo wanapaswa kufikiria msimamo wao mbele za Mungu kwa akili timamu. Kila mtu aweza kujiuliza mwenyewe hivi: ‘Je’. mimi ninajitahidi kudumisha usafi wangu wa akili, adili, mwilini na kiroho? Je! mimi binafsi nashiriki katika kulifanya kundi la Kikristo kuwa safi​—⁠usafi unaolifanya lionekane tofauti kabisa na kizazi hiki kiovu na kichafu? Je! njia ambayo katika hiyo mimi naitunza na kuitumia nyumba yangu na mali nyingine, kutia na mwili wangu, inaonyesha kwamba mimi naifuata sana njia ya Yehova? Je! ndivyo ilivyo njia yangu yote ya maisha? Jibu letu​—⁠ndiyo​—⁠kwa maulizo hayo litakuwa wonyesho wa kwamba tunajitahidi kutii ombi hili lililoongozwa na Mungu la kujilinda na “uchafu wa mwili na roho.”​​—⁠2 Kor. 7:1.

KUJIFUNZA JUU YA DHABIHU ZINAZOKUBALIKA KUTOKANA NA MIPANGO MINGINE YA TORATI

6. Torati ilisema nini juu ya mafuta ya kutiwa watu?

6 Takwa linalopasa mafuta ya kutiwa watu yanayotajwa katika sheria ya Musa linaonyesha vilevile ubora wa kushikilia kanuni ya Mungu ya utakatifu. Alipopata maelezo ya pekee ya kufanyiza mafuta, Musa alipata amri kali zilizohusu matumizi ya mafuta hayo. Twasoma hivi: “Haya yatakuwa ni mafuta matakatifu ya kutiwa kwa ajili yangu mimi katika vizazi vyenu vyote. Hayatamiminwa katika kiwiliwili cha binadamu, wala msifanye mengine mfano wa haya kama yalivyoungwa kwa viungo vyake; ni matakatifu, na kwenu ninyi yatakuwa matakatifu. Mtu awaye yote atakayetia mafuta haya juu ya mgeni, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake.” (Kut. 30:31-33) Kutoliheshimu kusudi takatifu la mafuta ya kutiwa watu kulikuwa kosa lenye kustahilisha kifo.

7. Twaweza kupata masomo gani ya maana kutokana na amri za kimungu juu ya mafuta ya kutiwa watu?

7 Hii inatupa masomo ya maana sana. Biblia inafunua kwamba mafuta haya yalifananisha roho takatifu ya Yehova. (Linganisha Zekaria 4:2-6.) Kuhani Mkuu Yesu Kristo hakutiwa mafuta kwa mafuta, bali kwa roho takatifu. (Mt. 3:16-17; Luka 4:18; Ebr. 1:8, 9) Kwa hakika, basi, twataka kuiheshimu sana roho ya Mungu, tukifanya yote tuwezayo kufuata uongozi wake. Hii inatia ndani kudumisha dhamiri njema ili kwamba tusiichukize au ‘kuihuzunisha roho hiyo.’ (Efe. 4:30) Zaidi ya hayo, kwa kuwa Yehova analijenga kundi la Kikristo kupitia kwa roho yake, inatupasa kujiangalia tusiwape watu sifa kwa ajili ya yale yanayotimizwa. (1 Kor. 3:5, 6) Imani yetu thabiti katika unabii ulioongozwa kwa roho hii pia ni uhakikisho wa kwamba tuna maoni yanayofaa kuelekea roho hii iliyotokeza unabii huo. (1 Pet. 1:21) Je! maneno na matendo yetu yaonyesha kwamba tunazingojea “mbingu mpya na dunia mpya” na kwamba twataka watu wengi iwezekanavyo wajifunze juu ya tumaini hili kuu?​​—⁠2 Pet. 3:13, 14.

8. Torati ilitoa maagizo gani juu ya uvumba?

8 Kama vile ilivyokuwa kwa habari ya mafuta ya kutiwa watu, sheria ya Mungu kwa Israeli ilitoa maagizo kuhusu uvumba. Baada ya kuvitaja viungo na namna ya kutayarisha uvumba, Biblia inasema hivi: “Yatakuwa kwenu matakatifu sana. Na uvumba utakaofanya, hamtajifanyia uvumba wenye viungo sawasawa na uvumba huo; utakuwa mtakatifu kwa ajili ya [Yehova]. Mtu ye yote atakayefanya mfano wa huo, ili kuunusa, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake.” (Kut. 30:34-38) Katika njia hii, matumizi mabaya ya uvumba mtakatifu yalikatazwa vikali. Twaweza kujifunza nini kutokana na hayo?

9. (a) Tunajifunza jambo gani kutokana na Zaburi 141:2 na Ufunuo 5:8 juu ya kilichofananishwa na uvumba? (b) Twaweza kuonyeshaje kwamba sisi tunathamini pendeleo la sala?

9 Uvumba ulikuwa ukifananisha sala zenye kukubalika zilizotolewa na watumishi waaminifu wa Mungu. Ukweli huu ulitajwa katika Zaburi 141:2; “Sala yangu ipae mbele zako kama uvumba, kuinuliwa mikono yangu kama dhabihu ya jioni.” Vilevile, katika kitabu cha Ufunuo (5:8), twasoma kwamba manukato “ni maombi ya watakatifu.” Ni jambo la maana kama nini kwamba tuthamini pendeleo la sala! Twaweza kuonyesha kuthamini kwa kuomba kwa ukawaida, tukifanya maombi yetu kupatana na mapenzi ya Mungu. (1 Yohana 3:21, 22; 5:14, 15) Sala za kichoyo, zenye makusudi mabaya zaweza kufananishwa na kutumia vibaya uvumba, haziwezi kusikiwa na kupendelewa na Baba yetu wa mbinguni.​​—⁠Yak. 4:3.

10. Ni shauri gani linalotolewa na Maandiko juu ya mtu anayeweza kuliwakilisha kundi katika sala?

10 Kwa sababu sala ni sehemu ya maana sana ya ibada ya kweli, wanaume wanaowakilisha kundi katika sala wanapaswa kuwa mifano bora. Mtume Paulo alielekeza shauri hili lililoongozwa na Mungu kwa Timotheo: “Nataka wanaume wasalishe kila mahali, huku wakiinua mikono iliyotakata pasipo hasira wala majadiliano.” (1 Tim. 2:8) Pasipo waa lenye kutokana na matendo ya kutokuwa washikamanifu kwa Mungu na kwa wanadamu, pamoja na kutokuwa na maoni ya uadui, wanaume kama hao wangewakilisha kundi ifaavyo. Kwa kuuendeleza uzito wa sala, tungejitahidi kuweka akili zetu bila kutanga-tanga wakati wengine wanapomwomba Mungu kwa niaba yetu.

11, 12. (a) Nadhiri ni nini? (b) Kulingana na Torati, kushindwa kutimiza nadhiri kulikuwa jambo zito kadiri gani?

11 Mpango mwingine ulioshikamana sana na mpango wa torati wa kutoa sadaka ni ule wa kuweka nadhiri. Waisraeli waliamriwa hivi: “Inawapasa ninyi kufanya toleo [la kuteketezwa] kwa moto kwa Yehova, toleo lililoteketezwa au dhabihu ili kufanya nadhiri ya pekee.” (Hes. 15:3, NW) Nadhiri nyingi zilifanywa kama ombi la kibali na msaada wa Mungu. Mradi Aliye Juu Zaidi alitimiza ombi hilo, yule aliyefanya nadhiri hiyo alijifanya mwenyewe kwa hiari kuwa na wajibu wa kufanya jambo la pekee au kutofanya jambo fulani ambalo kama sivyo angekuwa na haki ya kulifanya.

12 Hivyo, nadhiri ilikuwa na uzito kama vile kiapo. Kushindwa kutimiza nadhiri kulikuwa jambo zito, kama inavyoweza kuonwa kutokana na usemi ufuatao katika Torati: “Utakapoweka nadhiri kwa [Yehova], Mungu wako, usiwe mlegevu katika kuiondoa; kwa kuwa [Yehova], Mungu wako, hataacha kuitaka kwako; nayo hivi itakuwa dhambi kwako. Lakini ukijizuia usiweke nadhiri, haitakuwa dhambi kwako.”​​—⁠Kum. 23:21, 22.

13. Kulingana na sheria ya Mungu juu ya nadhiri, maneno yetu tukiwa Wakristo yanapaswa kuwaje?

13 Kanuni ambayo twaweza kujifunza kutokana na hili ni kwamba Baba yetu wa mbinguni anatutazamia tuwe wanyofu na wenye haki katika sehemu zote za maisha. Tamaa yetu yapaswa kuwa kama ile ya mtunga zaburi Daudi: “Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee [Yehova] mwamba wangu, na mwokozi wangu.” (Zab. 19:14) Inapokuwa hivyo, tutakuwa tukitii onyo la upole la mwanafunzi Yakobo: “Ndiyo yenu na iwe ndiyo, na siyo yenu iwe siyo, msije mkaangukia hukumu.” (Yak. 5:12) Ndiyo, maneno yetu yapaswa kuwa kama hati iliyotiwa sahili. Wengine wanapaswa kuwa na uhakika kwamba maneno yetu yanategemeka, yanaaminika. Kwa kuwa Yehova anatazamia watumishi wake ‘kusema kweli kila mtu na mwenzake,’ mtu asiye mwaminifu au asiye mnyofu hawezi kutazamia hata kidogo Aliye Juu Zaidi azikubali zawadi zake.

14, 15. (a) Torati ilitoa mipango gani kwa ajili ya sikukuu? (b) Je! sikukuu hizo zina ufanani wo wote na makusanyiko ya Kikristo leo, nalo andiko la 1 Wakorintho 5:7, 8 linafunua nini kuhusiana na jambo hili?

14 Kungali na sehemu nyingine ya utendaji wa Kikristo ambayo tutafanya vema kuchunguza ambayo Torati iliagiza. Yehova aliamrisha watu wake Israeli kuadhimisha sikukuu tatu za kila mwaka. Kila mwanamume Mwisraeli alitakiwa kuzihudhuria. (Kum. 16:16) Kwa wengi, hii ilimaanisha kusafiri mwendo mrefu, wakipata shida kwa kuwa mbali na nyumbani. Leo twaweza kuhudhuria makusanyiko mawili au matatu kila mwaka, nako kuhudhuria kwetu kwaweza kutia ndani kujinyima kwa kadiri fulani. Je! sisi tunajitahidi kuhudhuria makusanyiko kwa sababu ya kutaka kufurahia ushirika na ndugu zetu na kupata chakula cha kiroho kinachotolewa kwa ukarimu?

15 Ni wazi kwamba, mengi zaidi ya kuthamini tu makusanyiko ya watu wa Mungu yanahusika. Kwa sababu gani: Kwa sababu hatujawekewa kipimo cha kuadhimisha siku fulani pamoja na sikukuu kama vile Waisraeli. (Kol. 2:16, 17) Mtume Paulo aliandika hivi: “Basi, jisafisheni, mkatoe ile chafu ya kale, mpate donge jipya, kama vile mlivyo hamkutiwa chachu. Kwa maana [mwana-kondoo wetu wa Sikukuu ya Kupitwa] amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo; basi na tuifanye karamu, si kwa chachu ya kale, wala kwa chachu ya uovu na ubaya, bali kwa yasiyochachika, ndio weupe wa moyo na kweli.” (1 Kor. 5:7, 8) Yesu Kristo akiwa sura yenyewe ya mwana-kondoo wa Sikukuu ya Kupitwa, alitolewa dhabihu mara moja tu. Kwa hiyo, mwendo wetu wa maisha kama Wakristo unaweza kufananishwa na sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu. Je! tuna nia ya kutaka kuondoa kilicho dhambi ili kudumisha usafi wa kibinafsi na wa kundi? Kutii matakwa ya haki ya Mungu ni kwa lazima kabisa ili utumishi wetu ukubaliwe naye.

KUJALI KWINGI ANAKOTUJALI YEHOVA

16. (a) Yehova alitoa onyo lenye nguvu lakini la upole kupitia kwa nani katika karne ya tano K.W.K.? (b) Wakati huo hali zilikuwaje kwa habari ya utawala?

16 Kwa kuwa mwaliko wa Yehova wa kuleta matoleo si kwa ajili ya faida yake, bali kwa ajili ya hali njema yetu ya milele, twafanya vema kuangalia maonyo yake yenye fadhili juu ya yale yanayofanya zawadi zetu zikubalike. Katika karne ya tano K.W.K., Yehova Mungu alitoa onyo kali lakini la upole kupitia kwa nabii wake Malaki juu ya jambo hili kwa wale waliokuwa wakidai kumwabudu Yeye. Wakati huo Mamlaka ya Ulimwengu ya Uajemi ilikuwa ikitawala. Sehemu ambazo wakati mmoja zilikuwa chini ya uongozi wa falme ndogo-ndogo zilikuwa chini ya uongozi wa maliwali waliotawala mikoa wakimwakilisha mtawala wa Uajemi. Ili kuwezesha maliwali kudumisha utawala wa kifalme na kukusanya kodi kwa ajili ya hazina ya kifalme, maafisa hawa walipewa uwezo juu ya raia za mikoa yao wa kumruhusu mtu aishi au kustahili kufa. Kwa sababu ya mamlaka nyingi ya liwali, wengi wa raia walikuwa wakilipa kodi na hata kumletea liwali zawadi za ziada. Hawakutaka kumkasirisha na kuhatirisha maisha zao wenyewe.

17. Katika wakati wa Malaki, watu wa Israeli na makuhani wao walikuwa wakishindwaje katika kutoa zawadi zenye kukubalika kwa Yehova?

17 Tukiwa na msingi huu wa mambo, twaweza kufahamu namna neno la Yehova kupitia kwa Malaki linavyofaa. Aliye Juu Zaidi aliwagombeza Waisraeli. Kupitia kwa Malaki, alionyesha namna ilivyokuwa dhambi kwao kuleta wanyama vipofu, waliolemaa na wagonjwa-wagonjwa kama dhabihu na makuhani kukubali matoleo hayo yenye mawaa. Ndipo ulipokuja mwito huu: “Haya! mtolee liwali wako; je! atakuwa radhi nawe? (Mal. 1:7, 8) Waisraeli hawakuhitaji kufikiri sana ili wafahamu matoleo yasiyotamanika ya mwendo kama huo katika kushughulika na liwali wa kibinadamu. Hivyo, basi, wangetazamiaje kupata kibali ya Mfalme mkuu Yehova? Wasingeweza kutazamia hivyo. Ilikuwa kwa faida yao bora watende kulingana na kipa-moyo cha Malaki: “Ni sawa, nawasihi, ombeni fadhili za Mungu, ili atupe neema.” (Mal. 1:9) Wangetazamia kupata tena kibali ya kimungu kwa kuishi tu kulingana na matakwa ya Yehova.

18. Wakristo wanawezaje kuwa na hatia ya kushindwa kama vile Waisraeli wa wakati wa Malaki?

18 Lazima leo tuhakikishe kwamba tunapata faida kutokana na mifano yenye kushauri iliyoandikwa katika Maandiko Matakatifu. (Rum. 15:4) Isingetufaa kujifanya kwamba tunatoa zawadi kwa ukarimu, kama walivyofanya Hanania na Safira hali kwa kweli tunafuata faida za kichoyo. (Matendo 5:1-11) Isingefaa kutumia nguvu zetu, mali na uwezo kwa kadiri kubwa sana kwa ajili ya anasa zetu hata kwamba tunaachwa bila kitu cha kusaidia wengine kimwili na kiroho. Hii ingekuwa sawa na kumwambia Yehova: ‘Mimi hapa nakutolea nilichobakiza.’ Je! huko kusingekuwa kumdharau? Je! kweli tunaweza kumtazamia aukubali utumishi unaotolewa hivyo? Namna ilivyo wazi kwamba njia yetu yote ya maisha, maisha yetu ya kila siku, maoni yetu na makusudi, yamefungamanishwa na matoleo yetu kwa Yehova! Ni lazima tudumishe usafi katika kila njia.

19. Ni kitu gani kinachoweza kutusaidia kuamua kama tunatoa vitu vyetu vilivyo bora zaidi?

19 Kama vile ilivyokuwa kwa Waisraeli, ndivyo ilivyo kwetu, ‘zawadi ya kila mtu na iwe kwa kadiri ya baraka ya Yehova.’ (Kum. 16:17) Na tuhesabu baraka ambazo Baba yetu wa mbinguni ametupa, bila kuacha hata moja. Kisha tunaweza kuamua kila mtu binafsi kama tunamtolea Yehova kulingana na zawadi alizotupa. Lo! namna lilivyo jambo zuri kwamba anajua uwezo wetu na hali yeye hasemi kitu chenyewe ambacho kila mmoja wetu anapaswa kumtolea! Yeye anaturuhusu tuonyeshe kuthamini kwetu kutoka moyoni. Na je! twataka kumtolea anachostahili, yaani, vitu vyetu vilivyo bora zaidi? Cho chote kisichokuwa bora kabisa hakingestahili. Basi, na tumtolee vitu vyetu vilivyo bora zaidi yeye ambaye ametupa vitu vyote tulivyo navyo! ​—⁠Kutoka The Watchtower May 1, 1979.

[Picha katika ukurasa wa 13]

MAFUTA (roho ya Yehova)

UVUMBA (sala zinazokubalika)

TOLEO LA KUTEKETEZWA (kujitoa kabisa)

MIKATE ISIYOTIWA CHACHU (mwendo wa maisha wa usafi)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki