Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 11/15 kur. 3-6
  • Je! Wewe Unamtumaini Mungu . . . Au Mwanadamu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Unamtumaini Mungu . . . Au Mwanadamu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MSIBA HUKO JONESTOWN
  • “WONYESHO WENYE KUCHUKIZA”
  • Kuwatumaini Wengine Ni Muhimu kwa Maisha Yenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Fanya Yehova Awe Itibari Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Tunaweza Kupata Wapi Uongozi Bora?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Unaweza Kuwatumaini Ndugu Zako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 11/15 kur. 3-6

Je! Wewe Unamtumaini Mungu

. . . Au Mwanadamu?

BILA SHAKA kichwa cha habari za magazeti chenye kugutusha zaidi katika mwaka wa 1978 kilikuwa ule msiba katika Jonestown, Guyana. Ulifananishwa na ule wa Wayahudi 960 wenye kushika sana dini huko Masada ambao walipendelea kufa kuliko kukubali kushindwa na kujitolea kuwa watumwa wa Warumi; vilevile unafananishwa na raia Wajapan 1,000 waliojitupa kutoka kwenye genge katika Saipan wakati majeshi ya Amerika yalipoteka kisiwa hicho. Msiba huu wa Guyana ulitangazwa kila siku katika njia za mawasiliano ulimwenguni pote. Kwanza, hesabu ya waliokufa ilikuwa 400, kisha 500, kisha ikawa juu kufikia 780 na kisha: “IDADI YA WALIOKUFA GUYANA YATAJWA KUWA 900 NA U.S., KUKIWA NA WATOTO 260 KATI YA WALIOKUFA KATIKA JAMII HIYO.” (Gazeti New York Times, Novemba 26, 1978) Mwishowe, idadi hiyo ilipanda kufikia 913.

Msiba huu unahusiana moja kwa moja na ulizo “Je! wewe unamtumaini Mungu au mwanadamu?” Pengine utajibu: ‘Bila shaka, ni jambo la hekima kuweka tumaini langu katika Mungu mahali pa kuliweka katika mwanadamu.’ Na ndivyo ilivyo, kwa sababu Biblia inaonya hivi: “Usiweke tumaini lako katika viongozi wa kibinadamu; hakuna mwanadamu anayeweza kukuokoa.” (Zab. 146:3, Today’s English Version) Mungu anaweza kukuokoa kwa sababu “jina la [Yehova] ni ngome imara; mwenye haki huikimbilia akawa salama.” (Mit. 18:10) Hata hivyo, ili mtu aweze kumtumaini Mungu anahitaji zaidi ya kusema tu. Anahitajiwa awe na matendo, kwa sababu “imani pasipo matendo imekufa.” Mtu anayemtumaini Mungu ataishi kulingana na kanuni za Biblia, akipenda yale ambayo Mungu anapenda na kuchukia yale ambayo Mungu anachukia.​​—⁠Yak. 2:26; Ebr. 1;9.

Yanayopatana na shauri la mtunga zaburi la kutoweka tumaini letu katika viongozi wa kibinadamu ni maneno ya Yesu: “Msimwite mtu ye yote hapa duniani ‘Baba,’ kwa sababu mna Baba mmoja tu mbinguni. Wala hampaswi kuitwa ‘Kiongozi,’ kwa sababu kiongozi wenu wa pekee ndiye Masihi.”​​—⁠Mt. 23:9, 10, TEV.

Hata hivyo, kwa karne zote 19 tangu Yesu ayaseme maneno haya kwa mara ya kwanza, watu ambao wanadai kuwa wafuasi wake wamefanya jambo ilo hilo. Si kwamba tu wamewapa watu vyeo “baba” au “kiongozi,” bali pia wamekuwa wafuasi wa watu wenye kuabudiwa, kama vile Konstantino Mkuu, Charlemani, Napoleon na Hitler. Watu elfu nyingi, ndiyo, milioni nyingi, wameweka tumaini lao katika mwanadamu, hata kuwa tayari kumfuata mpaka kufa. Kuhusu uvutano aliokuwa nao Hitler, mtu mmoja aliyeishi Ujeremani wakati huo aliandika hivi, hivi karibuni: “Ijapokuwa mwisho wa vita ulikuwa tayari umeonekana, Wajeremani wengi hawakutaka kuamini kwamba Hitler angewakatisha tamaa nao waliziamini ahadi zake za zana za vita zisizo za kawaida, ambazo zingeleta ushindi kamili.” Wale walioweka tumaini lao katika watu kama hao walipata kuhuzunika, na mara nyingi hata kufa. Walishindwa kuweka tumaini lao katika Mungu.

Ni kwa sababu gani watu wengine wamekuwa wenye uvutano juu ya wengine? Ni kwa sababu ya kile ambacho leo kinaitwa “majaliwa ya kuongoza,” na ambayo yaelezwa kuwa ‘uvutano wa mtu wa kuongoza ukiwafanya watu wengi wawe na ushikamanifu au shauku ya pekee sana kwa kiongozi wa nchi au wa kijeshi.’ Mfano wenye kutokeza wa hili ni ule wa Napoleon. Baada ya kutoroka kutoka kwenye kisiwa cha Elba akiwa na kikundi cha wanajeshi 1,000, alipata elfu nyingine nyingi baada ya muda mfupi wa kutoa amri. Walipofika Grenoble nalo jeshi lake likakabiliwa na jeshi la watu 6,000, Napoleon aliliamuru jeshi lake lisimame huku yeye akipanda farasi kuelekea jeshi la adui. Alipolikaribia alishuka kutoka juu ya farasi akatembea kwa miguu kuelekea umati huo wa wanaume. Kiongozi wao akawaamuru wampige risasi. Wanaume hao wakainua bunduki zao na kuzilenga, walakini kwa kumwogopa sana kiongozi huyu aliyekuwa mbele yao hakuna hata mmoja wao aliyepiga risasi ambayo ingemkomesha asirudi na kuchukua utawala katika Ufaransa. Basi, wakati mmoja Napoleon aliweza kusema hivi: “Uwezo usio wa kawaida wa kuvuta na kuamuru watu umepewa Aleksanda, Charlemani na mimi. Walakini kwa habari yetu sisi imetupasa kuwapo katika mwili.” Halafu akalinganisha uwezo wao na ule wa Yesu Kristo ambaye anaweza kuonyesha uwezo wake ijapokuwa hayupo katika mwili.

MSIBA HUKO JONESTOWN

Mwanamume ambaye habari zake zimekuwa zikisikika sana hivi karibuni katika mwaka 1978 na ambaye alikuwa na haya yanayodaiwa kuwa majaliwa ya kuongoza watu alikuwa James Warren Jones. Kasisi Mkatoliki ambaye ameacha kufanya kazi kwa sababu ya uzee na ambaye alitumikia pamoja na Jones kwenye Baraza ya Haki za Kibinadamu ya San Francisco alisema hivi: “Yeye alikuwa na uwezo usio wa kawaida juu ya watu, na uwezo wa namna hiyo unaelekea kurusha akili.” Watu elfu nyingi walikusanyika alipokuwa akihubiri kwenye jumba liitwalo People’s Temple nao watu mia nyingi walimfuata kwenye ujamii alioanzisha katika Guyana na ambao aliuita “Jonestown” (“Mji-wa-Jones”). Si kwamba tu walimfuata kwenda mahali hapo bali pia mwishowe wengi wao walijiua alipowaamuru wafanye hivyo. Kwa kutiwa moyo na askari wake wakatili wenye kubeba silaha, yeye mwenyewe alijiua baada ya kuwafanya wengine 909 wafanye vivyo hivyo. Ulikuwa msiba ulioshtua ulimwengu.

Lo! namna ulivyo mfano wenye kutokeza na mbaya sana wa yale yanayoweza kutokea wakati watu, mahali pa kumtumaini Mungu na kufuata Kiongozi wake Yesu Kristo aliyemweka, wanaweka tumaini lao katika kiongozi wa kibinadamu, mtumiaji nguvu asiyeongozwa na kanuni! Lo! namna tofauti hizi zinazofuata zinavyoonyesha upumbavu wa kufanya hivyo!

Yesu Kristo pamoja na ujumbe wake alikuwa akielekeza watu kwenye uzima: “Mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele,” ndiyo, “uzima wa milele.” (Yohana 10:10; 3:16) Tofauti na hilo, “Kasisi” Jones alikuwa akielekeza watu kwenye mauti. Alikuwa “amefanya mkataba wa kujiua na kila mshiriki wa madhehebu yake,” ndivyo tunavyoambiwa. Vilevile, alisifu “ubora wa kifo, uzuri wa kufa.” Kwa kweli, mara nyingi alifanya mazoezi ya sherehe ambayo katika hiyo wafuasi wake walikuwa wakionyesha ushikamanifu wao kwake kwa kunywa kinywaji chenye sumu, ingawa kwenye mazoezi hayo hakikuwa na sumu. Walakini, mara ya mwisho iliyoleta msiba, kilikuwa nayo.

Twaendelea kusoma kwamba Yesu aliwapenda watoto. Huku wanafunzi wake wakiona kwamba Yesu hapaswi kusumbuliwa na watoto, yeye aliona vingine, kwa maana twasoma kwamba Mwana wa Mungu alisema hivi: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu, msiwazuie.” Kisha Yesu “akawakumbatia, akaweka mikono yake juu yao akawabariki.” (Marko 10:13-16) Tofauti yake, Jones aliwaadhibu watoto kwa kuwaweka katika chumba chenye giza na kwa kuamuru kwamba ncha zenye nguvu ya umeme ambazo ziliwapiga kwa umeme zifunganishwe nao. Au alikuwa akiamuru kwamba watelemshwe ndani ya kisima chenye maji mara nyingi, iwapo hawakupiga yowe kwa sauti kubwa kutosha. Wakati huo wa mwisho wenye msiba, watoto 200 walilazimishwa kunywa kinywaji hicho chenye sumu, au kilinyunyizwa kupitia kwa koo zao kwa sindano.

Yesu alihubiri amani na kutotumia nguvu, akionya kwamba “wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.” (Mt. 26:52) Hata hivyo, “Kasisi” Jones alikuwa na wanaume wakatili ambao si kwamba tu walitumia nguvu bali pia walimwua mwanabunge wa United States na waandishi watatu wa magazeti ambao aliogopa kwamba wangepeleka habari zenye kuharibu sifa ya ujamii huo wake. Zaidi ya hayo, alipokuwa akiwakusanya watu wake wote wajiue, alikuwa na kundi la wanaume wakatili wenye silaha wakiogopesha wale ambao hawakutaka kunywa kinywaji hicho chenye sumu.

Yesu Kristo alileta uhuru na faraja kutokana na yale yaliyowalemea watu. Basi, aliweza kusema hivi: “Njoni kwangu, nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:28-30) Vile-vile, “ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:31, 32) Katika Guyana, Jones alifanya mji wake wa Jonestown kuwa kambi ya mateso, kwa kuwafanya watu wake wote kuwa wafungwa kwa kuchukua vyeti vyao vya kusafiria. Yeye alihakikisha kwamba walitumika kama watumwa asubuhi sana mpaka jioni sana katika jua lenye joto kali. Chakula chao kikaendelea kupungua polepole mpaka wakaanza kupata wali (mchele uliopikwa) na mchuzi peke yake mara tatu kwa siku. “Hii ni hell” akasema mmoja wa washiriki wa madhehebu hiyo aliyetaka kutoroka.

Juu ya Yesu, twaambiwa hivi: “Alikuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake.” (2 Kor. 8:9) Walakini Jones alikuwa na tamaa kubwa sana ya fedha hata kwamba alikuwa akiomba-omba, na kubembeleza-bembeleza na hata kuwalazimisha wafuasi wake watoe mali zao, hata fedha zao za malipo ya uzeeni, hivi kwamba wakati wa kufa kwake alikuwa na fedha kati ya shilingi milioni 76 (Z24.6 milioni) na shilingi milioni 114 (Z34.6 milioni).

Kristo Yesu Mwana mkamilifu wa Mungu hakuwa na dhambi. Basi aliweza kuwauliza wapinzani wake hivi: “Nani miongoni mwenu anishuhudiaye ya kuwa nina dhambi?” (Yo-hana 8:46) Alikuwa “mtakatifu, asiyekuwa na uovu, asiyekuwa na waa lo lote.” (Ebr. 7:26) “Hakutenda dhambi.” (1 Pet. 2:22) Ingekuwa vigumu kuwazia tofauti iliyo kubwa zaidi kati ya Yesu na kiongozi huyu wa kidini Jones. Kulingana na ripoti juu yake, “kila mwanamke aliyekuwa karibu na Jones alitakiwa afanye ngono naye kwa ukawaida,” naye alikuwa na suria na mke vilevile. Bila kutosheka na hayo inaripotiwa vilevile kwamba alikuwa na hesabu fulani ya wapenzi wanaume.

Yesu Kristo aliikubali Biblia kuwa Neno la Mungu, aliitumia kama uongozi akitaja maneno yake naye alisema hivi juu yake: “Neno lako ndiyo kweli.” (Mt. 19:4-6; Yohana 17:17) Achia mbali kuikubali Biblia, Jones alitumia mahubiri yake kuishambulia Biblia. Hata pindi moja alitupa nakala ya Biblia sakafuni, akilalamika hivi: “Watu wengi sana wanaitazama hii badala ya kunitazama mimi.”

Tofauti nyingi zaidi zaweza kutolewa kati ya Kiongozi aliyetumwa na Mungu na mwanadamu Jones, mwanadamu mwenye kujifanya mwenyewe kuwa masihi, walakini nyingine moja itatosha. Yesu Kristo hajapata kudai hata wakati mmoja kwamba ndiye “Alfa na Omega,” Mungu Muumba wa ulimwengu wote. Dai lake peke yake lilikuwa: “Mimi ni Mwana wa Mungu.” (Yohana 10:36; Ufu. 1:8) Namna gani Jones? Kama alivyosema mmojawapo wa washiriki wake: “Jim aliacha kujiita Yesu aliyezaliwa upya akaanza kujiita Mungu. Alisema kuwa yeye ndiye Mungu mwenyewe ambaye aliumba mbingu na dunia.” Vilevile, huko kwenye ujamii wake wa Guyana alikuwa akipiga mayowe mara nyingi hivi: “Mimi ndiye Alfa na Omega!”

“WONYESHO WENYE KUCHUKIZA”

Hakuna shaka kwamba msiba wa Jonestown ulikuwa matokeo ya kipofu kuongoza kipofu na wote wakatumbukia shimoni. (Mt. 15:14) Kisa (tukio) hicho chote kinathibitisha hekima ya amri ya Yesu ya kutokweza watu. Bila shaka wengi wa wale ambao walimfuata Jones wakati mmoja walikuwa washiriki wa mojawapo ya madhehebu ya Jumuiya ya Wakristo. Walakini walishawishwa na masihi huyu wa kujifanya ambaye aliona njozi ya paradiso ya ujamii. Kwa kufaa, basi, kisa hiki kimeelezwa kuwa ‘wonyesho wenye kuchukiza wa namna kiongozi mwenye majaliwa ya kuongoza watu anavyoweza kupotoa akili za wafuasi wake kwa mchanganyiko wa kishetani wa dai la kupenda wengine kuliko kujipenda mwenyewe na ukatili wa kutumia akili.’

Hata hivyo bado mtu aweza kustaajabishwa na ujinga wa watu waliodanganywa na Jones. Inasemekana kwamba 80 kwa mia walikuwa weusi, ambao sana sana walikuwa katika hali ya kimaskini. Wengine, weupe kwa weusi, walioongozwa na hali ya kupendezwa na hali njema ya wengine, walijiunga naye kwa sababu ya mkazo alioweka juu ya usawa wa watu wa rangi mbalimbali na kwa sababu ya mipango ambayo hapo kwanza aliidhamini kwa ajili ya faida za kibinadamu. Hata hivyo mtu anakuwa na shaka juu ya kujitoa kwao kwa kanuni za haki. Kwa kuruhusu na kushiriki katika mambo yote machafu ambayo Jones mwenyewe alifanya na aliyosababisha, bila shaka wao walionyesha kwamba tumaini lao halikuwa katika Mungu, wala hawakutaka kumfuata Yesu Kristo.

Wangewezaje kujitoa kipumbavu hivyo na kuwa washikamanifu kwa mtu ambaye ‘alijionyesha kuwa na uwezo juu ya watu na kuwalazimisha kutosheleza tamaa yake ya fedha, ya kujipenda pamoja na nyege zake’?

Kwa wazi hakuna mtu ye yote anayemtumaini Mungu wa Biblia angeweza kudanganywa na mtu mwovu sana hivyo na ambaye kwa uchoyo, na kwa upotovu, alitumia vibaya uwezo wake wa kuvuta wengine, mtu ambaye kwa ukatili, alitumia vibaya sana tumaini la ujinga la wengine. Wakristo wa kweli wanalindwa na matokeo mabaya ya kumtumaini mwanadamu wa kawaida. Neno la Mungu, Biblia, si kwamba tu linawaelekeza kwenye dini ya kweli, bali pia linatambulisha waziwazi namna ya dini ambazo zapaswa kuepukwa, madhehebu ambazo mara nyingi msingi wake ni kukweza kiongozi fulani wa kibinadamu au madhehebu yenye kufanywa na mwanadamu.

Mtume Paulo aliwataja watu wapotovu mfano wa “Kasisi” Jones alipoandika hivi: “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinizi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi.” (1 Kor. 6:9, 10) Maandiko yaonyesha kwamba “kiongozi” wa Jonestown alikuwa mengi ya mambo haya yanayotajwa. Na wengi waliongozwa vibaya.

Kwa habari ya mtumiaji nguvu huyu wa kidini​—⁠na wengine wenye kufanyiza madhehebu kama yeye​—⁠“matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo.” Ndivyo anavyoandika mtume Paulo kama ‘onyo la kimbele’ kuhusu Wakristo wa kujifanya, wengi ambao wametokea katika miaka ya karibuni, na tena anaongeza hivi: “Watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.” Kwa upande mwingine, asema Paulo, wale wanaourithi Ufalme na baraka zake ni wale ambao wanasitawisha “tunda la [roho] . . . upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi.”​​—⁠Gal. 5:19-23.

Tunda hili halipatikani katika kambi ya watu wenye wazimu wa maoni ya moyoni wa madhehebu yenye kuabudu mwanadamu. Mahali pake, linapatikana kati ya wale ambao ‘wanamwambia Yehova: “Ndiwe kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, nitakayemtumaini.’”​​—⁠Zab. 91:2.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Kumtumaini Mwanadamu huleta Msiba

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kumwamini Mungu kunaleta uzima wa milele

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki