Kuendeleza Uhusiano Unaofaa
“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.
1, 2. (a) Yehova ni mtoaji mkarimu kwa njia gani? (h) Mtu anayeshuku yuko katika hatari gani, na hii inaweza kuepukwaje? (c) Je! imani inaweza kukua, na je! ni zaidi ya kukua kwa akili?
YEHOVA ni mtoaji mkarimu. Tumekwisha jifunza kutokana na masimulizi ya Luka kwamba Yehova hujibu maombi ya wale wanaodumu katika sala na wanaoendelea kukesha. Na waandikaji wengine wa Biblia pia waliongozwa kwa roho watoe mashauri yenye kutumika maishani juu ya mambo yanayohusiana sana na sala na imani.
2 Kwa mfano, mwanzoni mwa barua yake, Yakobo anatukumbusha kwamba inatupasa ‘kuendelea kumwomba Mungu’ atupe hekima katika kuelekeana na kuvumilia majaribu mbalimbali. Anasihi na kuonya hivi: “Na aombe kwa imani, pasipo shaka yo yote.” Mtu anayeendelea kuwa na mashaka ni “wa nia mbili [Kigiriki, “nafsi mbili”]” na hapati cho chote kutoka kwa Yehova. Mahali pake, twataka imani yetu iwe na sifa anayotaja Yakobo: ‘Sifa hii iliyojaribiwa ya imani yenu huleta uvumilivu.’ (Yak. 1:3-8)a Ingawa, huenda mwanzoni imani yetu isiwe nyingi kama ile ya Ibrahimu, inaweza kukua na ni lazima iwe ya kweli wakati wote, isiwe nusu-nusu. Acheni isemwe juu yetu kama alivyoandika Paulo: ‘Onyesha imani katika moyo wako.’ Twapaswa kuwa na nia nzuri, ikitokeza kazi njema.—Rum. 4:20; 10:9, 10; 2 The. 1:3.
3. Kwa kutofautisha, fikira zetu zinavutwa kwa kweli gani katika Yakobo 4:7, 8?
3 Katika kuthibitisha yanayotangulia, baadaye Yakobo aliandika hivi: “Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili.” Ili afikie kwenye jambo hili, Yakobo alitoa tofauti fulani, kama alivyofanya Yesu, ili kuthibitisha kweli zilizohitaji kukaziwa: “Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yak. 4:7, 8.
4. (a) Ili kumkaribia mtu inahitaji tendo la namna gani, likitokezwa na nini? (b) Je! Mungu anatoa zaidi ya ukaribishaji kwa hawa, na ni mipango gani ambayo imekwisha kufanywa kwa ajili ya faida ya wote?
4 Lo! namna inavyotia moyo kuwa mwenye nia moja katika njia inayofaa, namna inavyochangamsha moyo mwishowe! Mtu anaweza kuwa na nia moja na mwenye kustahimili kwa sababu ni wajibu, walakini kumkaribia mtu kunataka jambo kubwa zaidi. Kwapaswa kutoka moyoni, kukimsukuma mtu ajitoe na kuwa tayari kujinyima kusudi apate na kufurahia uhusiano unaotamanika wa kipekee. Angalia kwamba Yakobo hasemi kwamba tukimkaribia Mungu, basi yeye, atakuwa amejikalia kitako tu akingojea kutukaribisha. Mahali pake, iwapo tunachukua mwendo fulani wa kibinafsi katika kumkaribia Mungu, basi vilevile naye atachukua mwendo unaofanana na huo. Yeye anafanyaje hivyo? Tayari amekwisha kutoa mipango fulani mizuri kutia na Neno lake na zawadi ya Mwana wake Mkombozi wetu, hata kwamba wanadamu wote wanaotaka waweza kuitumia wajifaidi wakiwa na kusudi lenye unyofu wa moyo na kweli.
5. Mara nyingi watumishi wa Mungu waliojiweka wakf wanatumiwaje katika kusaidia wale ambao wanataka ‘kumkaribia Mungu’?
5 Hata hivyo, je! Yehova anafanya jambo fulani la kibinafsi la moja kwa moja? Katika habari nyingi, ni jambo gani linalogusa na kuvuta moyo wa mtu anayetafuta kweli? Zaidi ya maarifa ya kweli, je! vilevile si kupendezwa na mtu binafsi kweli kweli na kwa uchangamfu kunakoonyeshwa na yeye anayetumiwa kama mhudumu wa Mungu? (1 Kor. 3:5) Mtu anayetafuta kweli anapohudhuria mkutano wa kwanza wa Mashahidi wa Yehova, huenda asifahamu sana yanayosemwa, walakini tena anavutiwa sana na mazingira (hali) ya urafiki wenye unyofu wa moyoni unaoonyeshwa na wote, licha ya kuangaliwa na kukaribishwa kibinafsi. Katika njia hii anaona kwamba, katika kujibu jitihada zake mwenyewe za kutafuta kweli pamoja na Mtoaji wa hiyo kweli, sasa Mungu anamkaribia. Kadiri anavyofanya maendeleo, anaona ushuhuda wa uongozi na baraka za Mungu, kwa kuwa Yeye anatoa ‘kwa ukarimu na pasipo kukemea.’—Yak. 1:5.
6. Ni kwa njia gani peke yake hili lafanywa liwezekane, na jambo gani lapaswa kukumbukwa?
6 Kadiri mtu anayetafuta kweli anavyoongozwa hatua kwa hatua katika njia ya haki, anakuja kuthamini namna lilivyo pendeleo kutumiwa na Yehova kama mmoja wa wawakilishi wake katika kusaidia wengine. Kumwagwa kwa roho yake katika mioyo yetu kunawezesha hili, ili kwamba tuweze kuonyesha tunda la roho hiyo na kuiga upendo wa kweli kama wa Mungu.—Gal. 5:22, 23; 1 Yohana 4:11.
UKESHE, NA UWE THABITI
7. Namna barua ya Yakobo ilivyo kwa ujumla inaonyesha nini?
7 Yakobo alikuwa akiandikia Wakristo waliojiweka wakf na ambao walikuwa wamekwisha kuchukua hatua za kutubu na kugeuka. Walikuwa wamegeuka na kuacha mwendo wao wa kwanza wa dhambi, na sasa walikuwa wamejiweka wakf kabisa kwa Yehova kusudi wayafanye mapenzi yake tangu wakati huo. Kama vile barua ya Yakobo inavyoonyesha kwa ujumla, wengi hawakuwa wakiishi kulingana na masharti ya kujiweka kwao wakf. Walipuza uhitaji wa kuendeleza uhusiano huo na Yehova katika hali nzuri.
8. (a) Ni kwa sababu gani uhusiano hauwezi kuchukuliwa vivi hivi tu? (b) Yakobo alitamani sana kusaidia wale waliokuwa wakirudi nyuma kuhusiana na jambo gani?
8 Ni mara chache, zikiwako, ambazo uhusiano unakaa mahali pale pale. Hauwezi kuonwa vivi hivi. Ama unakua, hata iwe unakua polepole, na kama vile mti, unaimarika, au unaharibika na kuanza kunyauka. Kama matokeo matunda na maua yanaharibika. (Zab. 1:1-3) Hilo ndilo jambo lililotukia kwa taifa la Israeli wa mwili. Kabla haijakuwa kuchelewa mno, Yakobo alikuwa anahangaika kusudi awaeleze Waisraeli wa kiroho ambao nao vilevile walikuwa wakirudi nyuma. Kwa hiyo, aliliweka jambo hili mbele yao kwa wazi sana, akitofautisha namna mbalimbali za hekima zilizo za kweli na zilizo za uongo, vilevile urafiki, kama inavyoelezwa katika Yakobo 3:13-18 na Yakobo 4:1-6. Kisha anawasihi kama ilivyotajwa hapo juu katika Yakobo 4:7, 8. Inafanana na namna Yehova alivyowasihi Israeli wa mwili, kama tusomavyo katika Isaya 55:6, 7 na Malaki 3:6, 7.
9. (a) Ni njia gani ya kushambulia inayotumiwa na Ibilisi, na hii inatumiwaje katika siku hizi? (b) Petro alitoaje shauri lenye kutia moyo kuhusiana na hilo?
9 Je! hali iyo hiyo ipo leo, kwa kiasi fulani? Pasipo shaka “nyakati za hatari” zilizotabiriwa zipo sasa na mikazo na hatari za namna zote zinazoongezeka zikiwasonga watu kila mahali, sana sana juu ya Wakristo wa kweli ambao wamo kwenye ‘barabara nyembamba inayoongoza kwenye uzima.’ (Mt. 7:14; 2 Tim. 3:1-5) Ibilisi anazo njia mbili kubwa za kushambulia. Nyakati nyingine, kama alivyoandika Petro, yeye hutenda “kama simba angurumaye . . . akitafuta mtu ammeze” baada ya kututisha na kutuondoa kwenye njia hiyo. (1 Pet. 5:8) Yeye huleta hali zenye kuogopesha, ama juu ya taifa zima ama juu ya mtu binafsi, akiwa na kusudi la kutulazimisha turidhiane, ikiwa si kutuachisha kabisa msimamo wetu unaohusu dhamiri ya Kikristo na kanuni za Biblia. Ndiyo sababu Petro aliendelea kusihi hivi: “Nanyi mpingeni huyo (Ibilisi), mkiwa thabiti katika imani . . . Na Mungu wa neema yote . . . mkisha kuteswa kwa muda kidogo, yeye mwenyewe atawatengeneza, na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu.”—1 Pet. 5:9,10.
10, 11. (a) Ni njia nyingine gani inayotumiwa na Shetani, nayo inafananishwaje leo, ikiongoza kwenye hatari gani? (b) Kwa hiyo twapaswa kuwa macho na thabiti jinsi gani?
10 Njia ile nyingine ya kushambulia ya Ibilisi ni yenye hila zaidi. Vilevile Shetani “hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru.” Yeye hutenda kama nyoka, si kwamba aogopeshe, bali ili ashawishi na kuvuta, kama vile ‘nyoka alivyomshawishi mwanamke kwa ujanja wake.’ (2 Kor. 11:3, 14) Kama ushuhuda wa njia hii ni kwamba, kuna jambo moja Shetani analojua asilotaka wewe ujue, na jambo hilo ni kwamba wakati wake ni mfupi. Kama matokeo ya vita mbinguni, kufuatia kuzaliwa kwa ufalme wa Kimasihi katika mwaka 1914, W.K., yeye, joka mkubwa, ‘alivurumishwa chini duniani, . . . akiwa na ghadhabu nyingi, akijua ana wakati mfupi.’ (Ufu. 12:1-12) Ikiwa anaweza kuwashawishi sana sana wale “wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu” kwamba ‘wakati wa mwisho’ si mfupi sana, basi ameshinda nusu ya vita. (Ufu. 12:17) Wengi wangepoteza hali ya kuona uharaka na kushindwa kukesha. Twaweza kuhangaikia sana mapendezi ya kawaida ya maisha ya kila siku kwa vyepesi. Hakika katika habari hii inatupasa kujifunza namna ya kuyaona mambo kama ayaonavyo Yehova na kujaribu kuthamini namna yeye anavyohesabu wakati, tukikumbuka maneno ya Petro: “Lakini mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili, mkeshe katika sala.”—1 Pet. 4:7; 2 Pet. 3:8, 9.
11 Waandikaji wote wawili wa Biblia, Yakobo na Petro, walisema mengi yanayotusaidia na kututia moyo kuwa wenye kukesha na kuwa thabiti katika njia inayofaa, tukiwa na moyo mzuri na kuzingatia sala na imani.
WAOMBEENI WALIO NA UHITAJI
12. (a) Mwishowe Yakobo anatoa maelezo zaidi namna gani juu ya sala? (b) Waangalizi na walio na uhitaji wanasaidiwaje?
12 Mwishoni mwa barua yake, Yakobo anaeleza habari ya sala kuhusiana na imani hata zaidi na kwa njia tofauti. Hata hali iweje, tuwe ‘tunapatwa na mabaya’ au ‘tunachangamka,’ inatupasa kumjia Mungu katika sala na katika kumsifu. Kisha anazungumza juu ya kuwaombea wale walio na uhitaji. Mtu aliye mgonjwa, kwa wazi akiwa ni mgonjwa kiroho na kupatwa na matokeo mabaya akilini na moyoni, anaambiwa “awaite wazee wa [kundi]; nao wamwombee.” Huu ni wonyesho wa imani upande wake na kwamba anafahamu anapopaswa kwenda ili kupata msaada. Mtu hamwiti daktari asipokuwa na kiasi fulani cha imani katika daktari huyo. Sasa angalia matokeo mazuri ya kuchukua mwendo kama huo: “Na kule [kusali] kwa imani [kutamponya] mgonjwa yule, na [Yehova] atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.” (Yak. 5:13-15) Bila shaka hili linatoa uongozi mzuri kwa wale walio na uhitaji na kwa waangalizi ambao wanapaswa kuwa tayari na kuwa na nia ya kutumikia kama chombo katika kutimiza mahitaji hayo.
13. Yakobo anamtumiaje Eliya kama mfano wenye kutokeza katika habari hii?
13 Yakobo anaeleza zaidi jambo hili na, akiwa anawafikiria waangalizi na ndugu wengine waliokomaa, anasema kwamba “kuomba kwa mtu wa haki, kunapotenda kazi, kuna nguvu nyingi.” Akiunga hili mkono, anataja kisa chenye kutokeza cha kujibiwa kwa sala za Eliya, kwanza ‘kusinye,’ na kuwa hivyo kwa kipindi cha miaka mitatu na miezi sita, na kisha mvua ianze kunya tena. Na Eliya hakuwa mtu asiye wa kawaida. Yeye ‘alikuwa mwanadamu kama sisi.’—Yak. 5:16-18, NW.
14. Katika maneno ya kumalizia, Yakobo anatoaje kitia-moyo?
14 Akimalizia, huku akitutia moyo zaidi tuwe macho kusaidia, ikiwezekana, hata wale ‘wanaopotoshwa kutoka katika kweli,’ yeye anasema kwamba ye yote “anayemrudisha mwenye dhambi kutoka katika kosa la njia yake ataokoa nafsi yake kutoka katika mauti na atafunika wingi wa dhambi.” (Yak. 5:19, 20, NW) Lo! namna ulivyo mwisho wenye kufariji! Lo! namna inavyofanana na namna Yehova mwenyewe anavyojieleza—“Mungu mwenye rehema na neema, asiye mwepesi wa hasira na mwingi wa fadhili za upendo na kweli, . . . mwenye kusamehe makosa na uasi na dhambi.”—Kut. 34:6, 7, NW.
15. Vivyo hivyo, Yuda anataja njia gani mbili za kusaidia walio na uhitaji?
15 Kwa kupendeza, Yuda anamalizia barua yake katika njia yenye kufanana na hiyo juu ya “kujijenga wenyewe juu ya imani yenu iliyo takatifu zaidi sana, na kusali kwa roho takatifu.” Yeye pia anakazia uhitaji wa kuwa macho kusaidia wale walio na uhitaji katika njia ya fadhili hata hivyo yenye uharaka: “Endeleeni kuonyesha rehema wengine wenye mashaka; waokoeni kwa kuwanyakua kutoka motoni. Walakini endeleeni kuonyesha wengine rehema, mkifanya hivyo kwa woga, huku mkilichukia hata na vazi la ndani lililochafuliwa na mwili.” (Yuda 20-23, NW) Kwa hiyo hapa tena wale waliokomaa wanasihiwa. Iwapo unawajua wengine walio na mashaka au ambao wameangukia kwenye uchafu, usiwapuze mara moja, bali wanyakue kutoka motoni, ikiwezekana, ukijihadhari mwenyewe usichomeke au kuchafuliwa kwa njia yo yote.
‘ANGALIA SANA. . . FIKIRIA SANA’
16, 17. Katika kitabu cha Waebrania, Paulo anatoa ufanani mwingi juu ya msingi gani, ukiongoza kwenye kukata uamuzi gani?
16 Mtume Paulo alitumiwa kama mwandikaji wa nyingi za barua katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Barua yake kwa Wakristo Waebrania inatoa msaada unaotumika maishani na uongozi katika kusitawisha imani ya kweli na yenye nguvu, ikiongoza kwenye uhusiano wa karibu sana na Yehova na Kristo Yesu.
17 Kwa hiyo, katika barua hiyo mara nyingi Paulo anafananisha Wayahudi walio washiriki wa Israeli wa mwili, na wale Wayahudi ambao walikuwa washiriki wa kwanza wa kundi la Kikristo walio washiriki wa Israeli wa kiroho, na ambalo watu wa Mataifa waliongezwa baadaye. Msingi wake ukiwa ufanani huu, Paulo anaonyesha namna Wakristo Waebrania walivyofurahia faida nyingi kuliko zile za Israeli wa mwili, walakini hili pia lilileta madaraka makubwa zaidi. Wakristo wote wa kweli leo, bila kujali msingi wao ni nini, vivyo hivyo wanaweza kutumia mambo aya haya maishani mwao na hivyo kujifaidi.
18. Ni onyo gani katika barua hii linalorudiwa juu ya kutoa udhuru (sababu), na msingi wake katika historia ya Israeli ni nini?
18 Mwanzoni Paulo anataja kwamba ikiwa neno lililonenwa kupitia kwa malaika wakati Sheria ilipopewa Israeli lilipaswa kuheshimiwa sana, basi “sisi je! tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii? ambao kwanza ulinenwa na Bwana” wetu Yesu? (Ebr. 2:1-3; Gal. 3:19) Onyo kama hilo linatolewa kuelekea mwisho wa barua hiyo. Baada ya kusimulia yaliyotukia katika Mlima Sinai, Paulo anaandika hivi: “Maana ikiwa hawakuokoka wale waliomkataa yeye aliyewaonya juu ya nchi, zaidi sana hatutaokoka sisi tukijiepusha na yeye atuonyaye kutoka mbinguni.”—Ebr. 12:25.
19. Kwa hiyo, ni maelezo gani ya wazi na yenye kusaidia yaliyotolewa katika Waebrania 3:12-15; 12:25-29?
19 Hapa ndipo imani yetu inapaswa kuwa ya kweli ili kuwa na sifa iliyojaribiwa inayotakiwa. Moyo unahusika. Baada ya kutaja maelezo ya Mungu juu ya Israeli kwamba “sikuzote ni watu waliopotoka mioyo yao,” Paulo anatoa onyo kali kwa ajili ya faida yetu: “Angalieni ndugu zangu, [usisitawi] katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye haki.” Hatuwezi kusimama mahali pale pale. Iwapo ‘hatumkaribii Mungu’ kwa imani yenye kuendelea kukua kadiri tunavyomthamini kwa ukamili zaidi, basi kuna hatari ya kwamba tutafanywa wagumu “kwa udanganyifu wa dhambi,” na kuanza kujitenga, bila kutambua kinachotukia. Twapaswa kusaidiana kwa habari hii ‘na kuendelea kutiana moyo kila siku.’ Uhakika huu thabiti, imani hii isiyotikisika, inapaswa kuendelezwa ili turithi “ufalme usioweza kutetemeshwa” na baraka zake.—Ebr. 3:10-14; 12:28.
20. Licha ya kukazia imani, katika barua yake, Paulo anatutiaje moyo kuhusiana na sala?
20 Vilevile Paulo anatutia moyo kuhusiana na sala, na ‘kumtazama sana Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu. . . . Hakika mfikirieni sana yeye aliyevumilia mazungumzo yenye kupinga kutoka kwa wafanya dhambi ambayo ni kinyume cha faida zao, ili kwamba msichoke na kujiuzulu katika nafsi zenu.’ Kwa sababu ya yote aliyovumilia anaweza kutuhurumia udhaifu wetu, ijapokuwa mwenyewe hana dhambi, na kupitia kwake twaweza kufikia ‘kiti cha fadhili zisizostahilika’ na kupata msaada wakati unaofaa.—Ebr. 4:15, 16, NW; 12:2, 3.
21. Ni wapi na kwa njia gani Paulo anashikamanisha sana sala na ‘silaha za vita’ zinazotolewa na Mungu, ikiongoza kwenye uamuzi gani?
21 Mwishowe, kama vile Paulo alivyowaandikia Waefeso, kumbuka kwamba ‘kusali kila wakati katika roho’ kunafungamanishwa karibu na kuvaa ‘silaha zote za vita za Mungu.’ Na, kama Paulo, twapaswa kujiombea na kuombea wengine ili kwamba tupewe ‘uwezo wa kusema ili tuzijulishe siri takatifu za habari njema, kwa ujasiri.’—Efe. 6:10-20. —Kutoka The Watchtower May 15, 1979
[Maelezo ya Chini]
a Tazama Mnara wa Mlinzi, Desemba 15, 1978, kur. 13-16, kwa mazungumzo juu ya Yakobo 1:1-12.