Endeleeni Kuenenda Kama Watoto wa Nuru
“Zamani ninyi mlikuwa giza, bali sasa mmekuwa nuru.”—Efe. 5:8.
1, 2. (a) Katika mfano huo, sababu gani ni jambo la lazima mtu huyo aende kuelekeana na upepo? (b) Sababu gani inampasa Mkristo ajitahidi kuepuka kuenenda kama mataifa?
MWANAMUME huyo alishindana na upepo mkali. Akijikaza katika kila hatua, aliendelea kutembea mbele bila kusita. Sababu gani akajitahidi hivyo? Sababu gani hakugeuka tu na kutembea upande upepo ulikuwa ukielekea? Kwa sababu mwendo mfupi nyuma yake palikuwa na shimo kubwa refu lenye giza. Hakuwa na jambo jingine la kufanya iwapo alitaka kuishi. Si ajabu basi kwamba alijikaza akatembea kuelekeana na upepo huo mkali.
2 Leo, “roho ya ulimwengu,” iliyo kama upepo mkali, chini ya uongozi wa Shetani, inajaribu kuwafagilia wanadamu wote kwenye mwendo ambao bila shaka utaongoza kwenye “shimo kubwa” la uharibifu, wakati wa kuonyeshwa kwa hasira ya Mungu. (1 Kor. 2:12; Efe. 5:6) Ili Mkristo aepuke hasira hiyo lazima, ‘atembee kuelekeana na upepo.’ Ni lazima ajitahidi iwapo ataendelea kuenenda kama ‘mtoto wa nuru,’ wala si kama vile ‘mataifa waenendavyo’ au wanavyojiongoza wenyewe.—Efe. 4:17; 5:8.
NGUVU ZA NDANI ZAHITAJIWA
3. (a) Kulingana na Waefeso 3:16, ni lazima jitihada zetu zielekezwe wapi, kusudi tufaulu kuepuka kuenenda kama mataifa? (b) Tunatiaje nguvu ‘nyutu zetu za ndani’?
3 Jitihada zetu zinapaswa kuelekezwa wapi katika shindano hili? Paulo anajibu kwa kutusihi ‘kufanywa imara katika utu wetu wa ndani kwa nguvu kupitia kwa roho ya Mungu.’ Hii ndiyo sehemu tunayopaswa kufanyia kazi, yaani, ‘utu wa ndani,’ namna tulivyo ndani, katika ‘utu wa moyoni usioonekana.’ Huu unapaswa kutiwa nguvu. Namna gani? Tunajulishwa katika mstari unaofuata: “Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na . . . upendo.”—Efe. 3:16, 17; 1 Pet. 3:4.
4. (a) Ni nini linalohusika katika kuacha ‘Kristo akae katika mioyo yetu’? (b) Ni maulizo gani yenye kutufunua tulivyo tunayopaswa kuyafikiria sisi mmoja mmoja?
4 Ili ‘Kristo apate kukaa katika mioyo yetu’ ingemaanisha kwamba kwanza roho ya ulimwengu ingepaswa kuondolewa. Roho ya Kristo ingewezaje kuujaa ‘utu wa ndani’ ikiwa Shetani, ‘roho atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi,’ angali anatenda kazi ndani yetu au ameanza kutambaa ndani ya maisha zetu? (Efe. 2:2) Kwa hiyo jiulize mwenyewe hivi: “Katika moyo wangu ningali nafurahia roho ya Kishetani ya taratibu hii? Je! ninafurahishwa na mambo yanayoonyesha namna ambavyo imekosa adili?” Twaweza kwa urahisi kuwaonyesha wengine sura moja, hali, kwa kweli, ndani yetu, sisi ni watu tofauti kabisa. Kristo hukaa katika mioyo yetu kwa kuacha mfano wake na mafundisho yake yawe na matokeo juu ya maneno na matendo yetu. Kwa mfano, Yesu alisema kwamba wafuasi wake wa kiume wasitazame watu wa kike au wa kike kutazama wa kiume kwa kutamani. Katika mawazo yetu, je! tunatii maneno haya? Je! kwa bidii tunaepuka mambo ambayo yangeweza kuamsha maono kama hayo? Fikiria: Yesu angekuwa na roho ya namna ya kujifurahisha tunayofuatia? Je! tunayo roho yake si ile tu ya ‘kupenda haki bali pia kuchukia uasi wa sheria’? Ikiwa ndivyo, tunaacha roho ya Kristo izijaze nyutu zetu, tunayo ‘maelekeo yale yale ya akili’ aliyokuwa nayo Kristo. —Mt. 5:27, 28; Ebr. 1:9; 1 Pet. 4:1.
5, 6. (a) Sababu gani funzo la pekee pamoja na kutafakari ni mambo ya lazima ili kutia nguvu ‘nyutu zetu za ndani’? (b) Je! maarifa ya akilini ndiyo jawabu kamili; ikiwa sivyo, ni jambo gani jingine linalohitajiwa?
5 Basi, funzo la pekee na kutafakari Biblia ni mambo ya lazima iwapo ‘tutaimarishwa na kusimamishwa juu ya msingi,’ “ili tupate kufahamu pamoja na watakatifu wote jinsi ulivyo upana, na urefu, na kimo, na kina” cha kweli ya Neno la Mungu, na sana sana kwa kuwa linahusu mfano wa upendo uliowekwa na maisha pamoja na mafundisho ya Yesu Kristo. Kilicho na mizizi iliyoingia ndani sana hakiwezi kuondoshwa kwa urahisi. Kwa hiyo inatupasa kuweka ‘mizizi na msingi’ wa kiroho ukiwa na nguvu kwa kuacha maarifa ya Kristo yabubujike ndani ndani kwenye ‘utu wetu wa ndani’ tulio nao. —Efe. 3:17, 18.
6 Walakini, usiwe hata kidogo na maoni ya kwamba kuwa na Kristo akikaa katika moyo wako kunamaanisha tu kujaza mambo mengi ya hakika ya Kibiblia kwa kusoma sana. Mtume Paulo alifahamu vizuri sana hatari ya imani yenye kujengwa juu ya msingi wa maarifa ya akili peke yake, na kwa hiyo aendelea kusema hivi: “Na kuujua upendo wake Kristo, upitao ufahamu kwa jinsi ulivyo mwingi, mpate kutimilika kwa utimilifu [anaotoa] Mungu.” Jambo jingine zaidi ya elimu ya akili linahitajiwa. Ni kweli kwamba kadiri unavyoshirikiana na mtu sana, ndivyo ufahamuvyo fikira zake. Hata hivyo huwezi kujua kweli kweli anavyoona mtu huyo mpaka uanze kumwiga katika njia yake ya kuwatendea wengine au kuiga mwendo wake wa maisha. Vivyo hivyo, pia, mtu hawezi kuufahamu upendo wa Kristo kwa kusoma vitabu tu, walakini wakati mtu anapokuwa kama Kristo, basi, kwa kushiriki kwa huruma katika maono ya wengine, mtu anaweza kufahamu yale ambayo ‘yanazidi maarifa.’—Efe. 3:19.
7. Kweli au uongo?—Kwa kuwa Kristo alikuwa mkamilifu kututaka tuwe kama yeye ni kutazamia mengi mno. Sababu ya Kimaandiko ya jibu lako ni nini?
7 Lo! namna ulivyo mradi wa juu! Namna ulivyo mfano wa juu wa kufikia! Ni kweli, huenda likaonekana kuwa jambo kubwa ajabu, walakini kwa msaada wa Mungu linawezekana, ujapokuwapo uwezo wetu usiokamilika, kwa kuwa Paulo asema kwamba Mungu aweza “kufanya mambo ya ajabu mno kuliko yote tuyaombayo au tuyawazayo.” Ulizo ni hili, Je! sisi tunafanya sehemu yetu?—Efe. 3:20; angalia pia 1 Petro 2:21 na 1 Wakorintho 11:1.
‘VUENI UTU WA KALE PAMOJA NA TAMAA ZAKE ZENYE KUDANGANYA’
8. Kulingana na Paulo, ni namna gani za tamaa zinazoweza kukawia-kawia katika “utu wa zamani”? (b) Wengine wameteteaje uchaguzi wao wa namna fulani za tafrija zenye kushusha adili, na je! kuwaza huko kwafaa kulingana na Maandiko?
8 Ndivyo alivyosihi mtume Paulo katika Waefeso 4:22. Hapana, usiweke kiraka juu ya utu wa kale, walakini ‘uvue,’ utupilie mbali. (Kol. 3:9) Sababu gani? Kwa sababu ‘tamaa zake zenye kudanganya,’ zinazokawia-kawia katika mioyo yetu yenye ‘kudanganya,’ zaweza ‘kuharibu’ au kufanya utu wa kale uendelee kuwa mbaya zaidi. (Yer. 17:9) Ili kutetea upendeleo wao wa tafrija ambazo kwa wazi ni mbaya, Wakristo wengine wametoa sababu wakisema hivi: ‘Haisumbui dhamiri yangu, kwa hiyo kuna ubaya gani?’ Je! yaweza kuwa kwamba dhamiri zao ni mbaya nazo tamaa za mioyo yao zinawadanganya? Uhakika wa kwamba dhamiri yetu haitusumbui hauhakikishi kwamba mwendo wetu ni mzuri. Hata mtume Paulo alikubali hivi: “Maana sijui sababu ya kujishitaki nafsi yangu, lakini sihesabiwi haki kwa ajili hiyo; ila ani[chunguza]ye mimi ni [Yehova].” (1 Kor. 4:4) Dhamiri za wengi katika kundi la Kikristo zilikuwa zimekufa ganzi hivi kwamba waliruhusu uasherati katikati yao, hata kujivunia huo. Lo! namna zilivyokuwa dhamiri zilizoongozwa vibaya!—1 Kor. 5:1, 2, 6; Tito 1:15; 1 Tim. 4:2.
9. Ni ripoti gani yenye kushtua inayoonyesha namna dhamiri zinavyoweza kubadilishwa polepole?
9 Ni rahisi kuacha dhamiri zetu zichafuliwe polepole na ‘tamaa zenye kudanganya.’ Kutoka kwa afisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi ya Ulaya tunapata ripoti hii yenye kushtua:
“Ni hakika kwamba yapata miaka 10 iliyopita ndugu zetu wasingetazama nyingi za sinema zinazoonyeshwa sasa, kwa sababu hali yao ya kuona uhitaji wa adabu imebadilika. Hakuna shaka kwamba kwa kadiri fulani maelekeo ya ulimwengu huu yamevuta wengine wa ndugu zetu.”
10. (a) Kukubalika kwa michezo ya kupigana kwa panga au na wanyama mpaka kufa kulifikilizwaje katika karne ya kwanza? (b) Twaweza kujifunza nini kutokana na jambo hili?
10 Kwa njia ya polepole sana Shetani hujitahidi kufanya kanuni zake mbovu zikubalike. Wakati michezo ya kupigana kwa panga au kupigana na wanyama mpaka mmoja auwawe ilipoanzishwa katika Palestina, kwanza ilipokelewa kwa “woga mwingi” na watu ‘wasiozea kuona mambo hayo,’ kulingana na mwanahistoria wa karne ya kwanza Livy, anaongeza hivi:
‘Ndipo kwa kurudiwa-rudiwa, wakati mwingine kuruhusu wapiganaji waumizane tu . . . alifanya watu wenye kuona mambo hayo wayazoee hata kupendezwa nayo, naye aliamsha katika vijana kuona furaha katika kutumia silaha.’
Hatua kwa hatua woga mwingi ulipunguzwa. Baada ya muda kupita hawakuogopa tena walakini wakawa washiriki wenye furaha. Njia za Shetani hazibadiliki sana; kwa hiyo uwe macho kwamba hali yako ya Kikristo ya ‘kuwa na adabu’ haibadilishwi polepole. Tua ufikiri: Dhamiri yako imekuruhusu ufanye mambo kadiri gani? Je! ni kupita kiasi? Kwa habari ya tafrija, je! mwendo wako ni tofauti kidogo na ule wa watu ambao ‘wamekwisha kufa ganzi’?
HAKIKISHA YANAYOKUBALIKA KWA BWANA
11, 12. (a) Ni kwa sababu gani shauri katika Waefeso 5:10, 17, ni la maana sana leo, nalo laweza kutumiwaje? (b) Je! uhakika wa kwamba tafrija zilizopotoka zaweza kuwa na sehemu nzuri unazifanya zikubalike kwa Mkristo?
11 Mengi ambayo yameoza kiadili huwekwa mbele yetu kana kwamba yanafaa kabisa. Hiyo ndiyo sababu inatupasa ‘kuendelea kuhakikisha yanayokubalika kwa Bwana.’ “Kwa sababu hiyo [kwa sababu siku ni mbovu] msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya [Yehova].”—Efe. 5:10, 17.
12 Kwa hiyo juu ya tafrija inayotolewa na ulimwengu, jambo la maana ni kuchagua. Akitoa mfano wa hili, mtu mmoja alisema hivi: “Sehemu kubwa ya sinema ni nzuri sana, walakini sikuzote sinema nyingi zinakuwa na tamasha za ngono, kwa hiyo iwapo unataka kuona sehemu nyingine inayobaki inakupasa kutazama ngono.” Walakini kutazama sehemu kubwa ya sinema iliyo “nzuri sana” kwafaa kukufanya uharibu adili yako kutokana na “tamasha za ngono”? Tamasha hizo zinazoonyesha yale yanayofanywa sirini sasa zinaonyeshwa watazamaji. Ikiwa Paulo alisema, “yanayotendeka kwao [mataifa] kwa siri, ni aibu hata kuyanena” maoni yetu yanapaswa kuwa nini kuhusu kutazama sehemu yo yote ya tafrija ya namna hiyo? (Efe. 5:12) Mahali pa kutazama orodha ya amri za kitabu cha Wayahudi cha mafundisho, inampasa Mkristo atumie ‘uwezo wake mwenyewe wa kupambanua’ na ‘kuacha kuwa mjinga [Kigiriki: “kutokuwa na ufahamu, kukosa ujuzi wa adili”].’ (Ebr. 5:14) Huenda ikamaanisha kwetu kuepuka kabisa sinema au maonyesho fulani ya television ambayo kwa upande mwingine huenda yakawa na mambo yenye kufurahisha. Mwandikaji mmoja aliyedai kuwa Mkristo katika kame ya kwanza alitoa jambo zuri sana katika maandishi yake The Shows:
‘Hata iwe kwamba kule [kwenye sinema] kuna mambo yaliyo mazuri, mambo yanayofaa na yasiyo na mabaya; hata mambo mengine yaliyo mazuri kabisa. Hakuna mtu anayepunguza ukali wa sumu kwa nyongo [kiunga kichungu] . . . kitu kilicholaaniwa kinawekwa kwenye viunga vilivyokoleshwa vizuri na vya ladha tamu.’—Tertullian.
13. Mtu anaweza kumsaidiaje mtu ambaye, kwa “maneno yasiyo na maana,” anadharau shauri la Biblia?
13 Namna ilivyo vizuri wakati sisi mmoja mmoja twaweza kutiana moyo kusudi tufuatie mwendo ‘unaokubalika kwa Bwana’! Usemi wa kijana mmoja ni wenye kusifika kweli kweli: “Nadhani vijana waliokomaa kiroho wanajitahidi sana kuepuka sinema za uasherati na vilevile kuwatia moyo wengine waziepuke.” Hata hivyo, Paulo alionya kundi kwamba wengine wangedharau shauri lililo wazi la Maandiko wakati aliposema hivi: “Mtu asiwadanganye kwa maneno yasiyo na maana; kwa kuwa sababu ya hayo [uasherati uchafu, usemi mchafu, na mengineyo] hasira ya Mungu huwajia wana wa uasi.” (Efe. 5:6) ‘Wanaozungumza maneno yasiyo na maana’ wanaweza kuwa uongozi mbaya kwa wengine. Kuhusiana na watu wanaoendelea kuenenda bila utaratibu, mtume Paulo anashauri hivi:
“Lakini ikiwa mtu ye yote hatii neno letu . . . , mwangalieni mtu huyu, acheni kushirikiana na yeye, ili apate kuaibishwa. Hata hivyo msimwone yeye kama adui, bali endeleeni kumwonya kwa upole kama ndugu.”—2 The. 3:14, 15; NW.
Kweli usimtendee kama “adui,” walakini acha kushirikiana naye katika mambo ya kirafiki kama atakavyo. Huenda akapata ufahamu kwamba inampasa kurekebisha fikira zake.
WATOTO WA NURU WANA MAMBO YA KUFANYA YALIYO TOFAUTI
14, 15. (a) Katika karne ya kwanza, watu wengi wa mataifa walifanyaje ili kujifurahisha tafrija maishani mwao? (b) Ni mambo gani mengine yaliyo tofauti ya kufanywa na Wakristo yanayotajwa katika Waefeso 5:18, 19, nayo yangeonwaje na watu wa mataifa?
14 Watu wote, vijana na wazee, wanatamani kichocheo fulani, kiburudisho fulani, badiliko la mwendo, la kuwachangamsha zaidi ya hali ya kawaida ya kila siku. Jambo lililokuwa la kawaida kwa watu wa ulimwengu katika karne ya kwanza lilikuwa kupata msisimko au “kiburudisho” kwa kulewa. Mara nyingi vikusanyiko vyao vya kirafiki viligeuka kuwa ‘mashindano ya ulevi.’ Lo! namna ilivyowapasa Wakristo kuwa tofauti! Walikuwa na chanzo kizuri cha kuburudisha. Kilikuwa nini? Mtume Paulo anatuambia hivi “Tena msilewe kwa mvinyo, ambamo mna ufisadi; bali mjazwe [r]oho.” Uongozi wa roho ya Mungu waweza kutokeza furaha iliyo kubwa zaidi kwa Wakristo. Kwa hiyo, vikusanyiko vyao vya kirafiki kwenye karamu visingeonyesha “ufisadi” au “kuishi kiwazimu” (tafsiri ya Beck) kwa wasioamini. Kwa kuwa roho takatifu ya Mungu ilijaza mioyo yao, yale ambayo yanatoka vinywani mwao yanatofautiana sana na yanayotoka vinywani mwa watu ‘waliojazwa’ kwa kileo. Mahali pa kujiingiza katika nyimbo zisizo na adabu, mara nyingi zikifuatiwa na kucheza ngoma za uasherati, ambazo kwazo mataifa walijulikana sana, Wakristo wangefuata shauri la Paulo lenye kujenga: “Endeleeni . . . mkisemezana wenyewe kwa zaburi na sifa kwa Mungu na nyimbo za kiroho, kuimba na kufuatana wenyewe kwa muziki katika mioyo yenu kwa Yehova.” Hawa wangefurahishwa kindani.—Efe. 5:18, 19, NW; 1 Pet. 4:3.
15 Lo! namna jambo hili lilivyoonwa na mataifa kuwa lenye kuchosha! Walakini hao “watoto wa nuru” wa kwanza walikuwa wenye furaha, kwa sababu walikuwa na roho tofauti kweli kweli. Walitenda kama jamaa moja yenye uchangamfu, ‘nyumba ya Mungu,’ huku kila mmoja akitumia “kipawa” chake kwa ajili ya kulijenga kundi lililo kama jamaa.—Efe. 2:19; 4:7.
16. (a) Uchangamfu kama wa jamaa utakuwa na matokeo gani katika kundi, na ni kwa sababu gani shauri katika Yakobo 1:27, lapaswa kukumbukwa? (b) Ni hatari gani inayopaswa kuepukwa katika vikusanyiko fulani vya kirafiki? (c) Tafrija za Wakristo wanaokuwa na vikusanyiko vya kirafiki zapaswa kuwa na jambo gani?
16 Kwa hiyo leo kundi likiwa na uchangamfu kama huo wa ‘kijamaa,’ litakuwa na tamaa ya asili ya kukutana pamoja kwa mikutano, na vilevile vikusanyiko vya kirafiki, kwa ajili ya kujengana mmoja na mwenzake. Upendo wa kweli utawaongoza wote, vijana kwa wazee, wahangaikiane kutoka kwa moyo, na sana sana wale ambao ni “yatima na wajane.” (Yak. 1:27) Walakini vikusanyiko vya kirafiki havipaswi kuruhusiwa kuharibika, kama ilivyotokea katika kisa kifuatacho:
“Ilikuwa imekuwa sherehe yenye kupendeza ya ndoa, yenye mashauri mazuri ya Kimaandiko kutoka kwa mhudumu aliyetoa hotuba ya ndoa. Kisha, watu hao wawili waliooana, pamoja na wengine mia kadha, wakaenda kwenye jumba lililokuwa karibu kwa karamu. Walakini namna hali ilivyokuwa tofauti! Kikundi cha wacheza muziki wenye kulipwa kilikuwa kikicheza, kikicheza muziki usio na kiasi, wenye kuamsha tamaa za mwili kwa sauti ya juu sana hata kwamba wageni kadha wakaomba waruhusiwe kuondoka. Vileo vilikuwa vikitelemshwa kwa wingi sana. Kucheza dansi kulionyesha roho ya kutojizuia. Wageni wengi waliuliza, Mbona kuharibu ndoa yenye furaha ya kitheokrasi kwa kuuleta ulimwengu uizunguke?”
Ni nini kinachoweza kufanywa katika pindi ambazo Wakristo wanastarehe au kufanya tafrija? Mambo mengi yenye kujenga! Jambo la maana ni kwamba linalofanywa lapaswa kuonyesha kwamba sisi ni “watoto wa nuru,” na kwamba tunaongozwa na roho ya Mungu, wala si “roho ya ulimwengu.”—1 Kor. 2:12.
WOTE WATUMIA MAONGOZI YA WEMA
17. Wazee na wengine walio na ‘sifa za kiroho’ wanaweza kusaidiaje wale ambao huenda wakawa wanachukua ‘hatua ya uongo’ kwa upande wa tafrija?
17 Kwa kuwa mkazo wa ulimwengu unaongezeka, kuwa macho ni kwa lazima ili kushinda roho yake katika kundi. Maongozi ya wazee’ yanapaswa yasaidie ili roho ya Mungu iendelee kumiminika kundini. Nyakati nyingine hii inaweza kumaanisha ‘kutengeneza upya’ fikira za wengine ambao wanakosa usawa. Mzee mmoja aliyehangaikia sana kupenya kwa uulimwengu kwenye kundi aliandika hivi: “Tukiwa wazee ni lazima tushiriki lawama kwa sababu wengine wetu tunakuwa wadhaifu kunapokuwa uhitaji wa kutoa shauri linapohitajiwa na kutoshikilia yaliyo haki.” Walakini, si wazee tu, bali wote ‘walio na sifa za kiroho [“walio wa kiroho,” Tafsiri ya Kingdom Interlinear] wapaswa kuwa na nia ya ‘kumtengeneza upya mtu huyo anayechukua hatua ya uongo katika roho ya Upole.’ Shauri hilo la upole laweza kuzuia ‘hatua moja ya uongo’ isiwe mwendo mpotovu wenye kuendelea, unaoelekeza kwenye msiba.—Efe. 4:11-14; Gal. 6:1, NW.
18. Sababu gani usawa unahitajiwa?
18 Wote wanapaswa kutambua kwamba tafrija zinazopendelewa na kuchaguliwa na watu zatofautiana. Mahali pa kuwa wenye kulaumu kupita kiasi, pengine kukaribia kuwa ‘wenye haki kupita kiasi,’ tuwatie moyo wengine wafanye yanayotakiwa. Tutumie kanuni zilizowekwa katika Biblia. Turuhusu uwezo wa Neno la Mungu uvute mioyo ya wale wanaochukua ‘hatua ya uongo,’—Mhu. 7:16.
19. Wazazi wanaweza kutumiaje uongozi wao kwa ajili ya faida ya watoto wao?
19 Sana sana wazazi wako katika hali nzuri ya kusaidia watoto wao. Mtume huyu anawaamuru akina baba: “Msiwe mkiwaudhi watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika adabu na rekebisho la akilini la Yehova.” Neno la Kigiriki lililotafsiriwa ‘kuwalea’ linatia ndani wazo la kuchangamkia mtoto, kwa kuwa neno la asili laweza kutumiwa kuhusu ‘mama mlezi awatunzaye’ watoto wake.—Efe. 6:4, NW; 1 The. 2:7.
20. (a) Kwa sababu gani kuna uhitaji wa adabu? (b) Kutokana na maelezo ya kijana mmoja, inawapasa wazazi wafanye nini, na hili litathaminiwaje baadaye na watoto wao?
20 Kuhangaika huko kutazuia wazazi wasiwe na ubaridi kuelekea namna ya tafrija anayochagua mtoto wao. Upendo mwingi kwa mtoto utamfanya mzazi kuwa thabiti nyakati nyingine, ‘kumlea mtoto katika adabu.’ Sana sana kwa sababu mkazo unaoletwa na watoto wa rika lao mtoto aweza kukataa vizuizi vingine anavyowekewa na wazazi wake, pengine kwa upande wa tafrija. Mhubiri mmoja wa wakati wote mwenye umri wa miaka 21 ambaye alilelewa na wazazi wenye kumwogopa Mungu aliikumbuka miaka yake ya utineja, akisema:
“Baada ya miaka mingi ndipo tu nilitambua mazoezi niliyopata yalikuwa kwa ajili ya faida yangu, ingawa wakati huo nilidhani ya kuwa mimi ndiye niliyekuwa nikipata hasara. Kwa habari ya wazazi, huenda wakaona kama kwamba wanampoteza mtoto wao kwa kuwa thabiti. Hawampotezi. Wanapaswa kuyaona mambo kulingana na vile yatakavyokuwa wakati mrefu ujao. Wajua inakuwa jambo la kuogopesha wazazi wakati mtoto wao anaposema, ‘Ah, mama, Susana anafanya hivyo na yungali katika Kweli, kwa hiyo ni nini, kinachokufanya ufikiri ninatoka katika Kweli?’ Ni vigumu sana kwa wazazi kusema, ‘Hapana.’ Walakini baada ya kuwa na umri mkubwa zaidi, miaka mingi baadaye, na unaangalia nyuma, ndipo tu unaweza kusema, ‘Asante, Yehova, kwamba wazazi wangu walikuwa na ujasiri wa kushikilia waliyosema.’ “
21. Inawapasa wazazi wasaidie watoto wao wasitawishe uhusiano gani wenye kutamanika? Kwa sababu gani?
21 Walakini nguvu za nje au adabu siyo jawabu kamili. Mtume Paulo alizungumza juu ya “rekebisho la akilini la Yehova.” Kwa halisi, maneno ya awali yanamaanisha kuweka akili ya Yehova ndani kama nguvu zenye kuongoza au uvutano wenye kuongoza. Jitahidi kusaidia mtoto wako asitawishe uhusiano na Mungu ili kwamba apate kukataa namna za tafrija mbaya pamoja na mwenendo wote mbaya. Kama vile kijana mmoja aliyesitawisha uhusiano huo alivyosema: “Kwa kadiri kubwa si kati yangu mimi na wazazi wangu walakini kati yangu mimi na Yehova.”
22. Kwa kuendelea kuenenda kama watoto wa nuru, twaweza kuwa na tumaini gani?
22 Kwetu sote, ni kati yetu sisi na Yehova. Kwa hiyo mtu ye yote wa Yehova asisahau wao ni akina nani, yaani, “watoto wa nuru.” Endelea kuenenda kama kimulikaji sana, ukifurahia maisha yenye furaha na yenye kuridhisha, na kuwa na taraja la furaha ya milele katika taratibu mpya itakayoonekana karibuni yenye kuchochea adili yenye kung’aa.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Kuwa na ‘Kristo akikaa mioyoni mwetu’ kungemaanisha kwanza roho ya ulimwengu lazima ifukuziwe mbali.