Zaburi
Ni Nini Kilicho Bora Kuliko Uzima
KWA watu wengi, uzima—wenyewe tu—ndicho kitu cha thamani zaidi walicho nacho. Walakini sivyo ilivyo kwa watumishi wa kweli wa Mungu. Kuwa na uhusiano wa karibu na Baba yao wa kimbinguni wanaliona kuwa jambo lenye thamani kuliko kitu kinginecho, hata kuliko kuwa na uzima wenyewe pasipo Muumba wao. Ndivyo alivyoona Daudi, kama vile inavyoshuhudiwa na Zaburi 63. Kwa kuwa anajitaja mwenyewe kuwa ni “mfalme,” mambo yaliyoandikwa katika Zaburi hii yaweza kuwa yalitukia wakati ambapo aliukimbia Yerusalemu akapitia jangwa la Yudea, kwa sababu ya uasi wa Absalomu.—2 Sam. 15:13, 14, 23; kichwa cha Zaburi 63, tafsiri ya New World.
Katika jangwa hilo lenye vilima vitupu visivyomea kitu, hakuna mito wala vijito. Ebu wazia namna mtu anavyoweza kuona kiu katika sehemu kama hiyo! Akieleza matokeo ya yeye kuwa katika sehemu hiyo kavu isiyomea kitu, Daudi anasema juu ya namna alivyomtamani sana Mungu wake. Yeye analinganisha tamaa yake ya kushirikiana na Mungu wake na kutamani sana maji katika jangwa kavu. Twasoma hivi: “Ee Mungu, wewe ndiwe Mungu wangu, naendelea kukutafuta. Nafsi yangu yakuonea kiu. Kwa ajili yako nyama yangu imedhoofika kwa kutamani katika nchi kavu isiyo na kitu, mahali pasipo na maji.” (Zab. 63: 1, NW) Ni kwa sababu gani Daudi alitafuta Mungu wake? Yeye alitaka kibali ya Yehova, uongozi na Daudi alitamani sana kusaidiwa na kufarijiwa na Yehova hivi kwamba alisema tamaa hiyo kubwa ilikuwa ikimchosha na kumdhoofisha.
Kwa sababu ya kulazimika kuacha mahali pa makao ya Yehova ya mfano, Daudi alikumbuka wakati uliopita, alipokuwa na uhuru wa kwenda patakatifu kama alivyotaka. Alisema hivi: “Hivyo nimekuona katika patakatifu, kuona nguvu zako na utukufu wako.” (Zab. 63:2, NW) Katika patakatifu Daudi alikuwa na ufahamu wa pekee wa kuwapo kwa Mungu, kana kwamba alikuwa akimwona yeye Aliye Juu Zaidi. Hapo ndipo utukufu na nguvu za Yehova zilipoonekana. Maneno ya kusifu na kushukuru na kushangilia yaliyotolewa na waabudu yalimtukuza Aliye Juu Zaidi. Vilevile, yaliyosemwa na kufanywa yalimtukuza Yehova akiwa Mungu mwenye kufanya matendo ya kuokoa. Kupitia kwa maneno ya kutoka moyoni yaliyonenwa na waabudu waliojitoa, nguvu za Mwenye Nguvu Zote zilionekana.
Kisha Daudi anasema juu ya kumthamini Yehova kwa kuwa Mungu wake. Anaendelea kusema hivi: “Kwa sababu fadhili zako za upendo ni bora kuliko uzima, midomo yangu mwenyewe itakusifu. Hivyo nitakubariki wakati wa maisha yangu; kwa jina lako mimi nitainua mikono yangu. Kwa kuwa kwa sehemu iliyo bora zaidi, hata unono wenyewe, nafsi yangu imetoshelezwa, na kwa midomo yenye vilio vya shangwe kinywa changu chatoa sifa.” (Zab. 63:3-5, NW) Kwa habari ya Daudi, kusudi lake lote maishani lilikuwa kumsifu Yehova Mungu kwa kuonyeshwa upendo wa kimungu wenye fadhili au kwa kuhangaikiwa kwa huruma. Kwa mtunga zaburi huyo, fadhili za upendo za Yehova zilikuwa bora kuliko uzima wenyewe, kwa kuwa upendo mshikamanifu alioonyeshwa na Mungu ndio ulioyapa maisha yake maana. Ndiyo sababu Daudi alijiona kusukumwa aendelee kumsifu Yehova. Yeye alikuwa ameazimia kumbariki au kusema mema juu ya yeye Aliye Juu Zaidi kwa wakati wote uliobaki wa maisha yake. Akiinua mikono yake kana kwamba alikuwa akisali, Daudi alikuwa akimshukuru Yehova. Kwa sababu ya kuonyeshwa upendo na Mungu na kuangaliwa, Daudi alijisikia kutosheka kabisa. Yeye alikuwa amepokea sehemu iliyo bora kabisa. Kwa hiyo, midomo yake ingeendelea kumsifu kwa kumshangilia yeye Aliye Juu Zaidi.
Hata katika vipindi vya usiku alipokuwa macho, Daudi alikuwa akifikiri juu ya Mungu wake na mambo aliyomtendea. Twasoma hivi: “Ninapokukumbuka kitandani mwangu, wakati wa makesha ya usiku ninatafakari juu yako. Kwa kuwa umekuwa msaada wangu, nami ninashangilia chini ya uvuli wa mbawa zako.” (Zab. 63:6, 7, NW) Katika wakati wa Daudi, Waisraeli walikuwa na makesha matatu ya usiku. La kwanza lilianza saa 12 jioni mpaka saa 4 za usiku, la pili, kuanzia saa 4 mpaka saa 8 za usiku, na la tatu, kuanzia saa 8 za usiku mpaka saa 12 za asubuhi. Kwa kutumia vipindi hivi vya makesha ya usiku alipokuwa macho afikiri juu ya Yehova, mtunga zaburi huyo alionyesha bila shaka namna alivyothamini sana msaada aliopokea kutoka kwa Aliye Juu Zaidi alipolindwa kana kwamba alikuwa chini ya mbawa Zake.
Kwa kuwa alimpenda Yehova, yeye alijaribu kumwiga. Mtunga Zaburi huyo anaendelea kusema hivi: “Nafsi yangu imekufuata karibu-karibu.” Matokeo yalikuwa nini? “Mkono wako wa kuume,” asema Daudi, “wanishika sana.” (Zab. 63:8, NW) Ndivyo, Yehova alinyosha mkono wake wa kuume wenye kibali akamtegemeza mtumishi wake.
Iko tofauti kama nini kwa wale wanaopuza Muumba wao! Tunaambiwa hivi: “Kwa habari ya wale wanaoendelea kutafuta nafsi yangu waiharibu, wataingia kwenye sehemu za chini zaidi za dunia. Watapewa kwenye mamlaka ya upanga; watakuwa tonge tu la chakula cha mbweha.” (Zab. 63:9, 10, NW) Katika maneno hayo, Daudi alionyesha uhakika wa kwamba adui zake wangeshindwa na kutumbukia kwenye shimo la mauti. Wangeuawa kwa upanga, maiti zao zingekuwa chakula cha mbweha wala-nyama. Ni jambo linalostahili kuangaliwa kwamba Absalomu pamoja na wengi wa wafuasi wake walishindwa vitani katika njia yenye kuaibisha sana. Maelfu waliuawa.—2 Sam. 18:7, 8, 15-17.
Daudi hakuwa amemtumaini Yehova bure. Tumaini hilo linaonyeshwa vizuri sana katika mstari wa kumalizia wa Zaburi 63. Unasema hivi: “Naye mfalme mwenyewe atashangilia katika Mungu. Kila aapaye kwa yeye atajisifu, kwa kuwa vinywa vya wale wanenao uongo vitanyamazishwa.” (Mst. wa 11, NW) Kwa sababu ya yale ambayo Yehova angemfanyia, Daudi angeshangilia. Wengine, ambao kama vile Daudi, wangeapa katika jina la Yehova kwa unyofu wangejisifu au kulionea jambo hilo fahari. Sababu gani? Kwa sababu waliweza kufanya hivyo kwa kuwa walikuwa na uhusiano unaokubalika pamoja na yeye Aliye Juu Zaidi. Walakini wale wanaonena uongo katika jina la Mungu, ambao hawana uhusiano wenye kibali pamoja naye, vinywa vyao vitanyamazishwa katika mauti.
Kweli kweli, kama alivyosema Daudi, ‘fadhili za upendo za Yehova ni bora kuliko uzima.’ Kuweza kufurahia uhusiano wa karibu pamoja na Baba yetu wa kimbinguni tukiwa watumishi wake wenye kibali kunafanya maisha yawe na kusudi.