“Kikombe” Ambacho Mataifa Yote Watalazimika Kunywea Mkononi Mwa Mungu
1. Kwa sababu ya wakati ujao wenye msiba, tunachochewa kuuliza maulizo gani juu ya kinywaji wanachopewa wanadamu wanywe?
LO! NAMNA ambavyo katika kizazi chetu hali ya mambo ya ulimwengu imechukua sura mbaya! Kulingana na ambavyo watu wenye ufahamu wanasema juu ya mwendo wa mambo ya ulimwengu, kule wanakoelekea mataifa si jambo la kupendeza kufikiria. Bila shaka kitakuwa kinywaji kichungu kwa wanadamu kunywa. Kwa sababu ya kushindwa kwenye kuendelea kwa jitihada za kibinadamu zisizo na tumaini za kuzuia msiba wa ulimwengu, twaona sababu ya kuuliza, Je! mtu mwenye Akili zaidi, ndiyo, Mungu, anahusika katika jambo hili?
2. Kichwa cha Zaburi 75 na mistari yacho ya saba na nane inatajaje kitu chenye maana kwetu leo?
2 Hapa usemi wenye maana katika wimbo wa zamani unakuja katika fikira. Kulingana na kichwa cha wimbo huo uliimbwa chini ya kichwa, “Usilete kwenye Uharibifu.” Taifa la Israeli ambalo mwenye kutunga wimbo huo alitoka halikwenda kwenye uharibifu wa kudumu pamoja na mataifa jirani, walakini, chini ya Uongozi wa Kimungu, liliinuka tena. Hivyo tunao wimbo wenye kufaa kwa ajili ya nyakati zetu, mistari ya saba na nane ambayo sasa inatupendeza, kwa sababu inasema hivi: “Kwa kuwa Mungu ni hakimu. Anamshusha huyu, na kumwinua yule. Kwa kuwa kuna kikombe mkononi mwa Yehova, nayo divai inatoa pofu, kimejaa mchanganyiko. Na bila shaka urojorojo wake utamwagwa kutoka ndani yacho; waovu wote wa dunia wataufyonza, na kuunywa.”—Zab. 75:7, 8, NW, na maneno ya juu; tazama pia The Jerusalem Bible.
3. Kulingana na kinywaji ambacho mataifa wanalazimishwa kunywa, Yehova anawahukumu kuwa nini nasi twawezaje kuepuka kunywa pamoja nao?
3 Kikombe” ambacho mataifa yote watanywea katika wakati ujao unaokuja kinacho kinywaji kichungu zaidi ambacho watakuwa hawajapata kukinywa wakati mwingine. Masomo ambayo twaweza kupata kutoka kwa historia ya zamani na ya sasa yanaonyesha jambo hilo. Uhakika wa kwamba mataifa yote wana lazima ya kunywa kinywaji hicho chenye kunyamazisha unahakikisha kwamba Mungu, ‘Mfalme wa mataifa,’ anawahukumu kuwa “waovu.” (Zab. 75:8; Yer. 10:7) Kwa hiyo, mkononi mwake, watalazimishwa kunywa urojorojo ule ule unaotoka katika “kikombe” chenye divai yenye kutoa povu, iliyokolezwa sana. Walakini namna gani sisi ambao tunatumainia wakati ujao wenye furaha? Twaweza kuepukaje tusinywe pamoja na mataifa yaliyohukumiwa maangamizi kinywaji hicho chenye kutokeza kifo kinachotoka katika “kikombe” hicho? Ni jambo la akili kwamba, twahitaji kusikiliza shauri lo lote linalotolewa na Yule ambaye atawapa mataifa “kikombe” hicho katika wakati wake uliowekwa na kisha tutende mara moja kwa kupatana na shauri hilo. Je! tutafanya hivyo?
4. Hali yenye kuongopesha ya siku za Yeremia ilihusu sehemu gani ya dunia?
4 Hali ya ulimwengu leo inafanana na ile ambayo zaidi ya mataifa 20 yalijipata ndani yake wakati wa miaka ya mwisho mwisho ya Yeremia. Wakati huo sehemu ya dunia iliyohusika ilikuwa katikati ya bara za Afrika, Asia na Ulaya. Leo katika sehemu hiyo twapata mataifa yenye kutoa mafuta ya Mashariki ya Kati. Kama vile katika wakati wa Yeremia sehemu hii ingali yenye kushindaniwa.
5. Tarehe ya unabii wa Yeremia, sura 25, inatajwaje kwetu?
5 Huko nyuma mtu mmoja ambaye ulimwengu waweza kuita “mtu wa msiba” alijitokeza kwenye mambo ya ulimwengu. Jina lake refu, Nebukadreza, linamaanisha “Nebo Ni Mwenye Kulinda Kutokana na Msiba [au, mpaka].” Mwanamume huyu wa msiba, mwana wa Nabopolasa, alipata kuwa mtawala wa Babeli katika mwaka 625 K.W.K. Katika mwaka uo huo unabii wenye kuogopesha sana ulitolewa juu yake. Haukutolewa na mnajimu katika nchi hiyo ya zamani ya watu wenye kutazama nyota, bali na Muumba wa nyota, Yehova, Mungu wa nabii Yeremia. Tarehe ya unabii huo imetolewa kwetu katika Yeremia 25:1, 2: “Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, katika habari za watu wote wa Yuda, katika mwaka wa nne wa Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda; mwaka ule ndio mwaka wa kwanza wa Nebukadreza, mfalme wa Babeli; ambalo Yeremia, nabii, aliwaambia watu wote wa Yuda, na wenyeji wote wa Yerusalemu.” Mwaka wa nne wa kutawala kwa Yehoyakimu ulikuwa mwaka 625 K.W.K.
6. Unabii wa Yeremia 25:8-14 ulitoa msingi gani kwa njozi ya vikapu vya tini?
6 Kwa kweli unabii huu ulikuwa miaka 8 mbele ya njozi ya Yeremia ya vikapu vya tini kwenye hekalu katika Yerusalemu. (Yer. 24:1-3) Unabii huo wa kwanza uliipa njozi hiyo msingi gani, nao ulisema nini?
“Basi [Yehova] wa majeshi asema hivi, Kwa kuwa hamkuyasikiliza maneno yangu, angalieni, nitapeleka watu na kuzitwaa jamaa zote za upande wa kaskazini, asema [Yehova], nami nitatuma ujumbe kwa Nebukadreza, mfalme wa Babeli, mtumishi wangu, nami nitawaleta juu ya nchi hii, na juu yao wakaao ndani yake, na juu ya mataifa haya yote yaliyopo pande zote; nami nitawaangamiza kabisa, na kuwafanya kitu cha kushangaza, na kitu cha kuzomewa, na ukiwa wa daima. Tena, nitawaondolea sauti ya kicheko, na’ sauti ya furaha, sauti ya bwana arusi, na sauti ya bibi arusi, sauti ya mawe ya kusagia, na nuru ya mishumaa. Na nchi hii yote pia itakuwa ukiwa, na kitu cha kushangaza; nayo mataifa haya watamtumikia mfalme wa Babeli miaka sabini.”
“Na itakuwa miaka hiyo sabini itakapotimia, nitamwadhibu mfalme wa Babeli, na taifa lile, asema [Yehova], kwa sababu ya uovu wao, nayo nchi ya Wakaldayo pia; nami nitaifanya kuwa ukiwa milele. Nami nitaleta juu ya nchi ile maneno yangu yote niliyoyanena juu yake, naam, yote yaliyoandikwa ndani ya kitabu hiki, aliyotabiri Yeremia juu ya mataifa haya yote. Kwa maana mataifa mengi na wafalme wakuu watawatumikisha; naam, hao pia; nami nitawalipa kwa kadiri ya matendo yao, na kwa kadiri ya kazi ya mikono yao.”—Yer. 25:8-14.
“NEBUKADREZA, MFALME WA BABELI, MTUMISHI WANGU”
7. Ni jina la nani leo lipaswalo kuogopewa kama lile la Nebukadreza, nao mataifa wataliogopa wakati gani?
7 Je! leo jina la mwanamume ye yote linaogopewa na mataifa yote kama vile ambavyo jina Nebukadreza lilivyoogopewa na mataifa yote huko nyuma, kuanzia na baada ya mwaka wa 23 wa kutabiri kwa Yeremia? (Yer. 25:3) Sivyo! Hakuna mwanamume ye yote wa karne hii ya 20 atakayeandikwa katika historia ya kisasa kuwa afanana na Mfalme Nebukadreza wa zamani. Ni kweli kwamba, katika Warumi 13:1, 6, NW, mtume Paulo asema kwamba Wakristo wenye kutii sheria hulipa kodi zao kwa “mamlaka zilizo kuu” kwa sababu ni “watumishi wa Mungu kwa watu wote [Kigiriki, leitourgoi] wakati wote wakitumikia kusudi ili hili.” Walakini leo hakuna mwanasiasa mmoja ye yote awezaye kuitwa kiunabii na Yehova Mungu kuwa “mtumishi wangu.” (Yer. 25:9; 27:6) Mtu wa pekee awezaye kuitwa “mtumishi” katika utimizo wa unabii huu kupitia kwa Yeremia ni mtumishi wa Yehova aliye mkuu kupita wote katika ulimwengu wote. Huyu ndiye Mwanawe aliyekwezwa sasa, Yesu Kristo, ambaye amempa jina lililo juu zaidi ya kiumbe kingine cho chote mbinguni na duniani. (Isa. 42:1; Flp. 2:5-11) Ijapokuwa watawala wa ulimwengu hawamwogopi leo kama vile Nebukadreza, watafanya hivyo katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” inayokuja kwenye Har–Magedoni,—Ufu. 16:13-16.
8. Sababu gani Yehova alimwita Nebukadreza “mtumishi wangu,” nalo ni jambo gani kuhusiana naye linalopaswa kuonwa kuwa mfano unaotuhusu leo?
8 Sababu gani Yehova alimwita Mfalme Nebukadreza “mtumishi wangu?” Sababu Alimtumia kuadhibu watu wa Yuda kwa ajili ya kukataa kwao kuwasikiliza manabii Wake. Adhabu kupitia kwa mfalme wa Babeli ilifikia nchi jirani ambazo ziliwatumia vibaya watu wa Yehova zikiwa na nia ya kuwadhuru kwa sababu ya kumdharau Yeye. Hata hivyo, hii maana yake si kwamba Nebukadreza alikuwa mfano wa Yesu Kristo, ambaye alimwabudu Yehova peke yake kama Mungu. Mahali pake, kazi ya kuangamiza ambayo; Nebukadreza alifanyia Yehova juu ya mataifa yenye hatia ndiyo yenye kufanana, Inafananisha kimbele kazi ya kushinda ulimwengu ambayo Yesu Kristo akiwa Afisa Mkuu wa Kuangamiza wa Yehova atatekeleza wakati wa “dhiki kubwa” inayokaribia, ambayo katika hiyo mataifa yote yaliyo adui yatageuzwa kuwa mavumbi chini ya nyayo za Mtumishi mkuu zaidi wa Yehova. Hivyo mataifa haya (kutia ndani yale ya Jumuiya ya Wakristo) ndiyo mfano wa kisasa wa mataifa hayo ya zamani ambayo yaliangushwa na Mamlaka ya Ulimwengu ya Babeli. Hiyo ndiyo sababu jambo hili ni lenye kuhangaikiwa sana nasi leo.
9. Ni kipindi gani kingine kilichoanza, wakati wa kuanza kwa “miaka sabini” ya kufanywa ukiwa kabisa kwa Yuda, nacho kipindi hicho cha wakati hakikukatizwaje wakati wo wote?
9 Jeshi lenye kuponda-ponda la Kibabeli lilileta ukiwa kwa nchi ya ufalme wa Yuda kwa miaka 70. (Yer. 25:11, 12; 29:10; Dan. 9:1, 2; 2 Nya. 36:17-21) Ukiwa, huo ulio kamili wa nchi ya Yuda na Yerusalemu kwa makumi saba ya miaka ulianza katika mwezi wa vuli wa Tishri wa mwaka 607 K.W.K. Tukio hilo lenye msiba linashikamanishwa na mwaka wenye msiba zaidi wa 1914 W.K. Namna gani hivyo? Kwa sababu katika vuli wa mwaka huo “nyakati saba” za Mataifa zilizoanza na kufanywa ukiwa kwa Yuda katika mwaka 607 K.W.K. zilimaliza mwendo wazo wa miaka 2,520. (Luka 21:24; Dan. 4:16, 23, 25, 32) Hizo ‘nyakati za mataifa yasiyo ya Kiyahudi zilizowekwa,’ au Majira ya Mataifa, zilichukua kipindi cha wakati, wakati ambapo Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Yehova aliruhusu Mataifa watawale ulimwengu duniani bila kukatishwa na ufalme wake wa Kimasihi. Baada ya Nebukadreza kuuharibu Yerusalemu katika mwaka 607 K.W.K., ufalme wa Mungu wa halisi duniani haukupata kurudishwa tena kwenye Yerusalemu wa kidunia, mikononi mwa nyumba ya kifalme ya Daudi, kusudi usikatishe kutawalwa kamili kwa dunia na mamlaka za ulimwengu za Mataifa.
10. Ijapokuwa Koreshi alipindua nasaba ya Nebukadreza katika mwaka 539 K.W.K., Yuda na mataifa mengine walimtumikiaje mfalme wa Babeli miaka 70?
10 Mshindi wa Babeli Mwajemi, Koreshi Mkuu, hakurudisha ufalme wa jamaa ya Daudi huko Yerusalemu. Ni kweli kwamba alishinda Babeli ya kimataifa katika mwaka 539 K.W.K., au yapata miaka miwili kabla ya “miaka sabini” ya kukaa ukiwa kwa nchi ya Yuda kumalizika. Alijitangaza mwenyewe kuwa “mfalme wa Babeli” na kwa mara ya kwanza hakubadili maongozi ya nasaba ya Kibabeli ya Mfalme Nebukadreza. Hivyo mataifa yaliyotiishwa na Nebukadreza yaliendelea kumtumikia “mfalme wa Babeli” miaka 70. Kwa mara ya kwanza katika mwaka wa 70 wa kufanywa ukiwa kwa Yuda ndipo Koreshi Mkuu alipowaweka huru Wayahudi waliopelekwa uhamishoni kutokana na utumwa wa moja kwa moja kwa mfalme wa Babeli na kuwaruhusu warudi nyumbani ili wakaijenge upya nchi yao iliofanywa ukiwa na mji wao mkuu wa taifa Yerusalemu na hekalu lake. (Ezra 1:1 mpaka 3:2) Katika njia hii Wababeli walimtolea Yehova hesabu kwa sababu ya “uovu wao” ambao walikuwa wamemfanyia Mungu wa Israeli.—-Yer. 25:12.
KUWAPA MATAIFA YOTE “KIKOMBE” HICHO
11. Mambo hapa duniani hayajapata kuwa sawa tena tangu mwaka 1914 W.K. kwa sababu ya matukio gani mbinguni?
11 Kwa kuwa sasa Nyakati za Mataifa zilimalizika katika mwaka 1914, twafahamu kwamba siku ya mataifa ya kumtolea Yehova hesabu kwa sababu ya “uovu wao” lazima iwe imekaribia sana. Ulimwengu haujapata kuwa sawa tena tangu mwaka 1914. Wanahistoria wa kilimwengu hawawezi kuieleza sababu ya jambo hili. Walakini sababu ni kwamba tu yapata Oktoba 4/5, mwaka 1914, au miaka 2,520 tangu kufanywa ukiwa kwa Yuda na Yerusalemu baada ya ushindi wa Kibabeli, Nyakati za Mataifa za kutawala ulimwengu pasipo kukatizwa zilimalizika. wakati huo Yehova hakusimamisha katika Yerusalemu wa kidunia ‘kiti cha enzi cha Yehova’ kusudi mrithi wa kidunia wa Mfalme Daudi akalie, hivyo arudishe ufalme wa halisi wa kidunia wa Mungu. (1 Nya. 29:23) Mahali pake, kwa kuwa “ufalme wa dunia” sasa ulikuwa umekuwa ufalme wa Bwana Mungu, Yehova alitokeza kuzaliwa kwa ufalme wake kutoka kwa tengenezo lake la kimbinguni na kumkalisha Mwanawe, Yesu Kristo Mrithi wa Daudi, kwenye mkono wake wa kuume juu ya kiti cha enzi cha mbinguni. (Ufu. 11:15; 12:1-5) Tangu wakati huo mzao huyu wa kifalme wa Mfalme Daudi amejiunga na Yehova Mungu katika utawala wa ulimwengu kati-kati ya adui zake kabla hajawakanyaga-kanyaga mpaka kufa.
12. Jamii ya Yeremia imekuwa ikiwapaje mataifa “kikombe” hicho?
12 Kama matokeo ya jambo hili, kunabaki “kikombe” kwa Mataifa kunywea mkononi mwa Mungu. Sana sana tangu mwaka 1919 jamii ya Yeremia imekuwa ikivuta fikira za mataifa kwenye “kikombe” hiki. Kwa kuwapa mataifa taarifa hiyo ya kimbele, jamii ya Yeremia kwa njia ya mfano imekuwa ikiwapa mataifa kikombe cha Yehova. Jambo hili lilionyeshwa kiunabii katika Yeremia, sura 25. Hapo nabii huyu alisema hivi:
“Maana [Yehova], Mungu wa Israeli, aniambia hivi, Pokea kikombe cha divai ya ghadhabu hii mkononi mwangu, ukawanyweshe mataifa yote, ambao nitakupeleka kwao; nao watakunywa, na kulewa-Iewa, na kufanya wazimu, kwa sababu ya upanga nitakaoupeleka kati yao.”
“Ndipo nikakipokea kikombe kile mkononi mwa [Yehova], nikawanywesha mataifa yote, ambao [Yehova] alinipeleka kwao; yaani Yerusalemu, na miji ya Yuda, na wafalme wake, na wakuu wake, ili [kuifanya miji hiyo] kuwa ukiwa, na ajabu, na mazomeo, na laana; vile vile kama ilivyo leo.”—Yer. 25:15-18.
13. “Upanga” ambao Yehova angepeleka kati ya mataifa ungekuwa nini?
13 “Upanga” ambao Yehova angepelekea mataifa yote yanayotajwa katika Yeremia 25:18-26 ulikuwa nini? Ilikuwa vita ya kushinda ambayo alimruhusu “mtumishi” wake, Nebukadreza, kupiga juu ya hayo mataifa yote.
14. “Upanga” huo ulipiga nini kwanza, nayo matokeo yake yalipata wafalme gani, na namna gani?
14 “Upanga” wa mfano kwanza ulipiga ufalme wa halisi wa Mungu katika nchi ya Yuda. (Yer. 25:29) “Wafalme” wa Yerusalemu ambao walisikia mapigo ya “upanga” walikuwa ni (1) Yehoyakimu mwana wa Yosia; (2) Yehoyakini (Yekonia) mwa wa Yehoyakimu; na (3) Sedekia mwana wa Yosia na Amu wa Yehoyakini. Pigo la kwanza, juu ya Mfalme Yehoyakimu katika mwaka 620 K.W.K., miaka minne baada ya unabii wa Yeremia juu ya ule “upanga” na kile “kikombe,” lilimfanya kuwa mfalme kibaraka aliyeapa chini ya Nebukadreza. Pigo la pili la upanga lilipigwa katika mwaka 617 K.W.K. likamtoa Yehoyakini kijana kutoka kwa ufalme wake juu ya Yerusalemu likampeleka uhamishoni katika Babeli. Pigo la tatu na la mwisho liliharibu Yerusalemu na hekalu lake katika mwaka 607 K.W.K. na kumpeleka uhamishoni Mfalme Sedekia mwenye kuvunja kiapo mpaka Babeli afie kule kama mfungwa kipofu, asiye na mwana. Kufikia katikati ya mwezi wa Tishri wa mwaka 607 K.W.K., Yerusalemu na miji ya Yuda ilipata kuwa ukiwa.
15. Ni nani vilevile wangekinywea “kikombe” hicho mkononi mwa Yehova, naye ni nani angekinywea baada ya hawa wote?
15 Yerusalemu usingekuwa peke yake katika kunywa kinywaji kichungu kutoka kwa Mungu. Katika Yeremia 25:19-26 nabii huyo anataja zaidi ya wafalme 20 au falme ambao anawapa “kikombe cha divai ya ghadhabu.” Anaanza na Farao wa Misri na watumishi wake na kisha anataja orodha ya watawala wa kitaifa na kumalizia kwa kusema hivi: “Na mfalme wa Sheshaki atakunywa baada yao.” Wanafunzi huliona “Sheshaki” kuwa jina la fumbo la Babeli (Babiloni). Mfalme wake aliyehukumiwa maangamizi alipata kuwa wa mwisho wa nasaba ya Nebukadreza, yaani, Nabonidasi, pamoja na mwanawe aliye msaidizi wake Belshaza. Belshaza huyu alilazimishwa kunywea “kikombe” cha Yehova katika mwaka 539 K.W.K., alipouawa baada ya Koreshi Mwajemi kuangusha Babeli. Kwa kutumia maandishi ya fumbo Sheshaki, Yeremia aliepuka kutaja Babeli moja kwa moja wakati huo.
16. Wengine wanaweza kukataaje kukinywea “kikombe” hiki, walakini Yeremia alipaswa kusema nini?
16 Nyingine za falme hizo zinazotajwa huenda zilitokeza upinzani kwa Nebukadreza mwenye uadui kusudi zizuie amri ya Yehova isitekelezwe. Walakini kwa ajili ya kuwashauri nabii Yeremia aliambiwa aseme hivi: “[Yehova] wa majeshi asema hivi, Lazima mtakunywa. Maana, angalieni, ninaanza kutenda mabaya katika mji [Yerusalemu] uitwao kwa jina langu, je! mtaachiliwa msiadhibiwe?” Akijibu ulizo lake mwenyewe, Yehova asema: “Hamtaachiliwa msiadhibiwe; kwa maana nitauita upanga [wa ushindi wa kijeshi wa Babeli] ule uwapige wote wakaao katika dunia, asema [Yehova] wa majeshi.”—Yer. 25:28, 29.
17. Mataifa wameonyeshaje kukataa kwao kukinywea “kikombe” hicho, walakini jambo hili limefaulu kadiri gani?
17 Tangu mwaka 1919 W.K. mataifa wamekataa kunywea “kikombe” cha mfano cha ujumbe wa Yehova wa ghadhabu ya kimungu mkononi mwa jamii ya Yeremia. Kwa hiyo wamechukua hatua juu ya Mashahidi wa Yehova, wote wawili wa jamii ya Yeremia na “mkutano mkubwa” wa wenzi wenye kushirikiana nao, hata kuwapiga marufuku na kuzuia kuenezwa kwa ujumbe wao wa Biblia uliochapwa. Walakini yote haya yamekuwa bure! Wakichochewa na roho ya Yehova, mashahidi wake watiifu wanaendelea kufanya mikutano yao na kuhubiri kichini-chini. Hivyo wanamtii Mungu kuliko wanadamu wanaompinga Mungu. (Matendo 4:19; 5:29) Katika wakati ujao ulio karibu wapinzani hao wa kisiasa watajifunza kwamba kuwafanya Mashahidi wa Yehova waende kichinichini hakutazuia kamwe watawala wa ulimwengu wasinywee kile “kikombe” mkononi mwa Mungu mwenyewe katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye mahali paitwapo kwa mfano Har–Magedoni.—Ufu. 16:13-16.
18. Siku hiyo itakuwa “kuu” kwa nani, na kwa hiyo jamii ya Yeremia inakataa kufanya nini?
18 Siku hiyo itakuwa “kuu” kwa Yehova. Itakuwa pindi yenye furaha kwake, kwa sababu wakati huo atapigana kwa ajili ya kusudi la enzi yake kuu ya ulimwengu wote. Akiwa Amiri-Jeshi Mkuu atamtuma Mwanawe Yesu Kristo mwenye kushinda ulimwengu kwenye vita, ili apate ushindi unaozidi sana ushindi wo wote uliopatwa na Mfalme Nebukadreza wa zamani wa Babeli. (Ufu. 19:11-21) Hii itampa Yehova sababu ya kuinua sauti kwa shangwe zaidi kupita wafanyavyo wale wakanyagaji wenye furaha wa shinikizo la mvinyo wanapotayarisha divai ambayo itafurahisha moyo wa Mungu na mwanadamu. (Ufu. 19:11-15; Amu. 9:12, 13) Jamii ya Yeremia inao uhakika juu ya ushindi wa Yehova kwenye Har–Magedoni. Kwa hiyo wanakataa kunyamaa juu ya kutukuzwa huku kunakokuja kwa enzi kuu ya Yehova, hata ingawa watawala wa mataifa ya ulimwengu wanakasirishwa na kinywaji hicho kichungu.
19. Kwa ujasiri jamii ya Yeremia inachapisha mambo kadiri gani ya yale wanayoambiwa na Yehova?
19 Kwa ujasiri jamii ya Yeremia leo inatii amri iliyopewa nabii huyo huko nyuma katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Mfalme Nebukadreza juu ya Babeli: “Basi, tabiri wewe [Yeremia] maneno haya yote juu yao, na kuwaambia, [Yehova] atanguruma toka juu, naye atatoa sauti yake toka patakatifu pake; Atanguruma sana juu ya zizi lake; Atapiga kelele kama mtu akanyagaye zabibu, juu ya wenyeji wote wa dunia.”—Yer. 25:30.
KINYWAJI KINACHOFANYA MATAIFA KUTENDA ‘KAMA WATU WENYE WAZIMU’
20. Je! jamii ya Yeremia inapaswa kuitwa ‘watu wenye kupiga yowe tu msiba’ kwa sababu ya ambacho ushindi wa Yehova utamaanisha kwa mataifa?
20 Sauti ya ushindi ya Yehova itasikika mbinguni na duniani pote. Jamii ya Yeremia na wenzi wao wanaendelea kuonyesha jambo hili kimbele, ujapokuwa ushindi kwa Yehova unamaanisha msiba kwa mataifa yote. Kwa hiyo je! jamii ya Yeremia yapaswa kuitwa ‘watu wenye kupiga yowe tu msiba’? Hasha! Ama sivyo, Yehova Mungu, ambaye anawapa ujumbe wao, apaswa kuitwa vilevile mpiga yowe msiba. Katika onyo lenye rehema yeye asema hivi: “[Yehova] wa majeshi asema hivi, Tazama [msiba] utatokeo toka taifa hata taifa: na tufani kuu itainuliwa toka pande za mwisho za dunia. Na waliouawa na [Yehova] siku ile watakuwapo, toka upande mmoja wa dunia hata upande wa pili; hawataliliwa, wala kukusanywa, wala kuzikwa; watakuwa samadi juu ya uso wa nchi.”—Yer. 25:32, 33.
21. Sababu gani kwa haki Yehova angeweza kuchukua daraka kwa wale waliochinjwa kwa sababu ya Nebukadreza kupanua milki yake?
21 Katika lugha hiyo Yehova alitabiri mwendo wa Nebukadreza kwenye ushindi juu ya mataifa ambayo yangefanywa kuwa sehemu ya Milki ya Babeli. Kwa hiyo yeye angemruhusu Nebukadreza afagie taifa baada ya taifa, akiondoa upinzani wote kwa upanga wa kuangamiza ambao Yehova aliweka mkononi mwake. Kwa sababu hiyo Yehova alichukua daraka la wale waliochinjwa na washindi wa Babeli. Yeye mwenyewe aliwaita hawa waliouawa kutokana na uadui wa Kibabeli ‘waliouawa na Yehova.’ Yeye Ndiye aliyewafanya mataifa wanywe kutokana na kile “kikombe” kinywaji ambacho kiliwafanya watende ‘kama watu wenye wazimu.’ Wanadamu wawe wanampa Yehova sifa kwa ajili ya jambo hili au sivyo, historia ya kibinadamu iko kwa wingi kuonyesha kwamba Mfalme Nebukadreza aliipanua Milki ya Babeli katika eneo lililokuwa kubwa zaidi kuliko la mamlaka za ulimwengu zilizotangulia. Yehova alihusika katika jambo hilo, kwa kuwa, katika mwaka wa kwanza kabisa wa utawala wa Nebukadreza, Yeye alitabiri kupanuliwa huko kwa Milki ya Babeli.—Yer. 25:1, 2; 32:1, 2; 52:29; 2 Fal. 25:8; Yer. 52:12; Dan. 2:37, 38; 4:20-25.
22. Sababu gani tusingetaka kuwa kati ya wale wanaouawa na Yehova katika “dhiki kubwa” inayokuja?
22 Namna gani, sasa, juu ya ‘wale waliouawa na Yehova’ katika “dhiki kubwa” inayokaribia ambayo itamalizikia katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni? Je! twataka kuwa kati yao? Hasha! Kwa kuwa kuchinjwa naye kutamaanisha hukumu ya kuangamizwa naye.
23. Ilionyeshwaje kwa njia ya kutananisha sehemu ya taratibu hii ya mambo ambayo ingeangamia kwanza katika “dhiki kubwa,” na sababu gani hiyo kwanza?
23 Wakati wa kuanza kwa “dhiki kubwa” mataifa yote yaliyohukumiwa maangamizi yatakuwa upande mmoja kumpinga Mungu wa jamii ya Yeremia. Upande huo utatia ndani mataifa ya Jumuiya ya Wakristo, kwa kuwa yako kati ya wapinzani na watesi wa Mashahidi wa Yehova. Jumuiya ya Wakristo itakuwa sehemu ya kwanza ya taratibu hii ya mambo kuangamia, kwa kuwa ndiyo mfano wa kisasa wa ufalme wenye kuasi wa Yuda na Yerusalemu. Ili kufananisha hilo, ufalme wa Yuda ndio uliofanywa unywee kwanza kile “kikombe” ambacho ndani yake mlikuwa “divai ya ghadhabu.” Yehova alisema kwamba angeanza na “mji uitwao kwa jina [lake]” katika kuleta msiba wa taifa zima. (Yer. 25:29) Jumuiya ya Wakristo isiyo kama Kristo ndiyo sehemu ya kidini yenye kutakiwa kutoa hesabu kubwa zaidi mbele za Mungu na Kristo, na kwa hiyo ni kutoka kwake msiba wa ulimwengu utaanza, kama kwamba ni katika tendo lenye kufuatana. Itakuwa “tufani” ya mfano ambayo haiwezi kuanuliwa (kuondolewa) na ndege zenye kunyunyiza mawingu.
24. Kutokezwa kwa tufani hiyo kutoka “katika pande za mwisho wa dunia” kunaonyesha nini, nao watakaouawa watakuwa wangapi?
24 “Tufani” hii yatoka “katika pande za mwisho wa dunia,” kwa kuwa itatolewa nje ya makao ya mataifa yaliyohukumiwa; maangamizi. (Yer. 6:22) Katika utimizo wa kisasa, jambo hili lamaanisha, kwa kweli, kutoka Chanzo kisichoonekana, cha kimbinguni, hata kwamba kwa hakika litakuwa ‘tendo la Mungu.’ Ikikumba kuzunguka dunia yote, kama vile tu gharika ya siku za Nuhu ilivyogharikisha dunia yote, bila shaka, itakusanya waliouawa na hiyo “tufani” toka upande mmoja wa dunia mpaka ule mwingine. Jamii ya Yeremia yenye kuokoka na “mkutano mkubwa” wa wenzi wao wangewezaje kuwazika wote? Yehova atapaswa kutumia uwezo wake kuziondoa maiti hizo.—Ufu. 19:11-21.
25. Kwa sababu ya Yeremia 25:34-38, ni afadhali kuwa wapiga “yowe” wa namna gani?
25 Katika hiyo “siku ya kisasi ya Mungu wetu,” itakuwa afadhali mtu angekuwa kati ya wale ambao wenye kudhihaki waliita ‘wenye kupiga yowe msiba’ kuliko kuwa kati ya wale watakaopiga yowe kwa sababu ya “dhiki iliyo kuu.” (Isa. 61:2; Ufu. 7:14, 15; Mt. 24:21-30) “Pigeni yowe, enyi wachungaji, na kulia;” asema Yehova kupitia kwa Yeremia. “Na kugaagaa katika majivu, enyi mlio hodari katika kundi; maana siku za kuuawa kwenu zimetimia kabisa, nami nitawavunja vipande vipande, nanyi mtaanguka kama chombo cha anasa. Nao wachungaji watakuwa hawana njia ya kukimbia, wala walio hodari katika kundi hawataokoka. Sauti ya kilio cha wachungaji, na sauti ya kupiga yowe kwao walio hodari kati kundi, kwa maana [Yehova] anayaharibu malisho yao. Na mazizi yenye amani yamenyamazishwa, kwa sababu ya hasira kali ya [Yehova]. Ameacha mahali pake pa kujificha, kama simba; maana nchi yao imekuwa kitu cha kushangaza, kwa sababu ya ukali wa upanga uoneao, na kwa sababu ya hasira yake kali.”—Yer. 25:34-38.
26. Katika unabii huo, “wachungaji” nao “walio hodari katika kundi” ni nani?
26 Je! unabii huo unatufanya tufikiri juu ya viongozi wa kidini ambao wameitwa makasisi au wachungaji wa kiroho na makundi yao ya kanisa ambayo yameitwa “makundi”? Inaelekea ndivyo, walakini hapa Yehova hazungumzi na viongozi wa kidini wa mataifa. Katika Maandiko ya Kiebrania watawala wa kisiasa wanatajwa kama wachungaji na watu au raia zao wanaitwa makundi yao. Kwa hiyo “walio hodari katika kundi” ni wakuu au wenye kibali ya kifalme wa kundi hilo la kitaifa. Lazima iwe hivyo kwa habari ya Yeremia 25:34-38, kwa kuwa ni wapi katika sura yote mnapotajwa makuhani na Walawi? Wale ambao Yeremia anaamriwa awape “kikombe” cha Yehova wanasimuliwa kama “wafalme,” “wakuu,” na “falme.” (Yer. 25:18-26) “Msiba” na tufani” ya ulimwengu inayokaribia itapiga, si viongozi wa kidini peke yao, lakini vilevile, mwishowe, sehemu za kisiasa na za kiserikali za taratibu hii ya mambo.
27. Ni mwakilishi gani wa Sheshaki atakayenywea “kikombe” hicho baada ya wote?
27 Kwa hiyo ni “mfalme wa Sheshaki” atakayekinywea “kikombe” baada ya hao wote. Unabii ulioandikwa katika Yeremia 51:41 unalitaja jambo hili kama kwamba tayari limekwisha kufanywa, ukisema, hivi: “Jinsi Sheshaki alivyotwaliwa! Naye sifa ya dunia yote alivyoshambuliwa! Jinsi Babeli alivyokuwa ukiwa katikati ya mataifa!”—Yer. 25:26; 27:7.
28. “Wachungaji” hao “walio hodari” wanahangaikia nani zaidi, na malisho yao yanaharibiwaje?
28 Kwa sababu zilizo za kichoyo “wachungaji” na hao ‘watu hodari’ watapiga “yowe,” ndiyo, watagaagaa mchangani. Wakati Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova atakapofanya hesabu wakati wa “dhiki kubwa,” kwa hofu watatambua kwamba siku imewafikia wapate kuchinjwa na kutawanywa. Iwapo pangekuwa njia ya kuepukia au mahali pa kukimbilia, pengine wasingekuwa na maelekeo ya kupiga “yowe.” Wao hawajali sana jambo litakalopata ‘makundi’ yao ya kitaifa, walakini wanahangaikia kuangamizwa kwao wenyewe. Kazi zao zenye mshahara mnono na vyeo vyao vya juu lazima vitoweke! “Mazizi” yao, taratibu ya mambo ambayo kupitia kwayo walinyonya makundi yao ya kitaifa, inaharibiwa, inaangamizwa. Mahali ambapo palikuwa makao yao ya “amani” kwa ajili ya kujifurahisha kuishi kwa faida yao wenyewe—pamefanywa kuwa pasipo uhai. Kimya cha kifo kinatulia juu ya mazizi ya ‘makundi’ yao.
29. Wakati huo Yehova atakuwaje kama simba, nao “upanga” utainuliwa kwa matokeo gani?
29 Ili kutokeza hicho “kitu cha kushangaza” ulimwengu mzima ni lazima hasira ya Yehova iwe inawaka kweli kweli. Wakati huo asingekuwa tena kama simba wa bonde la mto aliyelazimishwa kutoka pangoni mwake na maji yenye kugharikisha ya Mto Yordani. Hasha, walakini ‘Yehova wa majeshi’ ni lazima wakati huo awe kama simba mwenye ujasiri anayeacha “mahali pake pa kujificha” ashambulie wajapokuwapo wachungaji wa kondoo wa sehemu za malisho. Kupitia kwa Mwanawe-Mtumishi, Yesu Kristo, yeye ainua “upanga” wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” (Yer. 25:30, 38) Kutokana na mapigo ya “upanga uoneao” wake wachungaji wa kilimwengu hawatapona tena!
30. Kwa sababu ya tunayosikia kwa sikio la imani katika unabii wa Yehova, twapaswa kufanya nini sasa?
30 Sikiliza! Kwa sikio la imani unabii wa Yehova, je! unasikia sauti yake ikiongezeka zaidi na zaidi? Kupitia kwa ukumbi huu wa kunasia sauti wa “wakati wa mwisho,” twasikia likija, kutoka kwa wakati ujao uliotabiriwa, yowe la “wachungaji” wote wa kitaifa, pamoja na vilio vya “walio hodari” wa makundi ya wanadamu wenye mfano wa kondoo. Tufanyeje, basi, sisi wasikilizaji? Hivi: Maadamu njia ya kuponyokea ingali wazi na maadamu kungali mahali pa kukimbilia, ebu na tuchukue hatua! Ebu na tupate kimbilio letu la usalama na kuhifadhiwa katika ufalme wa Yehova kupitia kwa Mchungaji wake aliyewekwa, Yesu Kristo.—Eze. 34:23, 24; Yer. 23:5, 6.
(Mfulilizo huu wa makala juu ya unabii wa Yeremia utanendelezwa tena katika toleo la Aprili 15 la Mnara wa Mlinzi.)
—Kutoka The Watchtower Sept. 15, 1979.
[Picha katika ukurasa wa 12]
Kupitia kwa jamii ya kisasa ya Yeremia, kwa rehema Yehova anaonya juu ya “tufani” ya duniani pote inayokuja