Amani Ambayo Katika Hiyo Umoja wa Ulimwengu Unategemea
TAMAA ya kukomesha vita ni jambo la kusifika sana. Hakika tendo hilo lingeleta faraja kubwa. Lakini je! ingedumu? Hivi karibuni Israeli na Misri zimekuwa zikifurahia uhusiano ulio nafuu (mzuri) kupitia kwa mkataba wao. Walakini, je! chuki kati ya Waisraeli na Waarabu imeondolewa? Au, je! sikuzote kuna hatari ya kutokezwa vita? Vivyo hivyo katika nchi nyinginezo—kwa mfano, Ireland, Lebanon na Zimbabwe-Rhodesia—je! chuki ya tofauti za rangi, ya kidini na ya kutukuza taifa inaondolewa?
Ulizo jingine la kufikiria wakati wa kuchanganua mipango ya amani ni hili, Msingi wa adili wa amani ni nini? Mara nyingi katika mikataba ya mataifa yote kila nchi inayohusika hutafuta faida au ridhaa zote inazoweza kupata. Katika visa vingi, wakati mapatano au maafikiano yanapofanywa, ni jambo tu la “kuishi pamoja kwa amani,” kuvumiliana, bila upatano wa kweli. Kwa kawaida, mataifa yote mawili wakati ule ule yanaongeza lundo lao la silaha, ili kujilinda kutokana na nchi nyinginezo au moja na nyingine. Pamoja na hayo, wakati mapatano kati ya mataifa mawili au zaidi yanapofanywa, mataifa mengineyo yanakasirishwa na ushirika huo, yakiwa na maoni kwamba ni tendo la kuelekeza uwezo juu yao. Yanaanza kushuku au kuogopeshwa na mpango wa hila au shambulio halisi.
Basi, ni jambo gani linalokosekana katika jitihada hizo za amani? Ni hili: Hata jitihada za mataifa za kufanya amani ziwe za unyofu namna gani, iwapo hayajaiendea Biblia kupata mashauri, hayatafahamu mapenzi ya Mungu ni nini kwa habari ya mambo hayo, au kile anachoamua kuwa ndicho msingi wa amani. Kwa kukosa kufahamu jambo hilo, yanashindwa kufanya amani, kwanza kabisa, na Mungu. Hivyo, msingi unaofaa haujawekwa. Ikiwa hayapatani na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, yanawezaje kutazamia kuepuka yasitende kinyume cha mapenzi yake? Mataifa yanawezaje kutumainia kuingia katika hali yenye amani yasipokuwa na amani na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote?
MUNGU ANAWASIHI WATAWALA
Huenda wengine wakaona kuwa ni jambo lisilowezekana kwa mtu ye yote au taifa lo lote kumpendeza Mungu—kuwa katika amani naye. Walakini hiyo si kweli. Mungu humkaribisha mtu ye yote anayetaka uhusiano wenye amani pamoja naye. (Matendo 17:26, 27) Yeye atamwezesha mtu huyo afahamu namna amani hiyo inavyoweza kupatikana. Je! si jambo la akili kufahamu mapenzi ya Yule, ambaye, Biblia humsema kuwa, Mtawala katika ufalme wa wanadamu?—Dan. 4:25.
Mungu anawasihi hata watawala wa kitaifa, akisema hivi: “Na sasa, enyi wafalme, fanyeni akili, enyi waamuzi wa dunia, mwadibiwe. Mtumikieni [Yehova] kwa kicho, shangilieni kwa kutetemeka. [Mbusuni Mwana], asije akafanya hasira nanyi mkapotea njiani.”—Zab. 2:10-12.
Kutokana na usemi huo katika zaburi hiyo na kutokana na maandiko mengine mengi, twaweza kuona kwamba, ili mataifa yapate amani ya ulimwengu, kwanza lazima yafanye amani na Mungu. Ili kuwa na amani, jambo la kwanza la lazima ni upatano na umoja wa moyo pamoja na Muumba na Mwenye Enzi Kuu. Yeye anafahamu yaliyo ya lazima kwa uradhi na furaha ya wale ambao ameumba. Jambo hilo limekuwa wazi zaidi katika wakati wetu wa sasa wakati inapoonekana kwamba jitihada za wanadamu kwa habari ya uhusiano wa viumbe na mazingira yavyo wakati mwingi zimetokeza makosa ya kipumbavu na yenye pupa nayo yamekuwa jambo la kuhatirisha maisha ya starehe duniani.
Ombi hilo katika Zaburi ya pili, kwa wafalme na waamuzi wa dunia, linawapa watawala wa mataifa ya kisiasa nafasi ya kufanya amani pamoja na Mungu na Mwana wake. Walakini historia inaonyesha kwamba hakuna taifa lo lote zima ambalo limeweza kufanya hivyo, nao unabii unaonyesha kwamba hakuna taifa la kisiasa litakalofanya hivyo wakati wo wote. (Zab. 2:2, 3; Ufu. 16:13-16) Kwa hiyo, mataifa yenyewe hayatakuwa katika amani pamoja na Mungu au yenyewe kwa yenyewe wakati wo wote. Kwa sababu yamechukua msimamo huo, “dunia inapita, pamoja na tamaa zake.”—1 Yohana 2:17.
KUFANYA AMANI PAMOJA NA MUNGU
Hata tendo la mataifa liwe namna gani, Mungu ana uwezo wa kufikiliza mapenzi yake na kuleta amani. Walakini yeye haahidi amani ya kulazimishwa. Jambo hilo ndilo watu wengi wanaona kuwa tumaini la kweli peke yake. Wao wanafikiri kwamba, pengine mataifa, yatajipatia silaha za atomiki kwa kadiri ambayo yote yataogopa kuanzisha vita, yakifahamu kwamba kusingekuwa mshindi, bali ingekuwa tu kuharibiwa kwa ulimwengu. Wengine wanashikilia kwamba serikali isiyo ya kawaida, serikali ya ulimwengu au angaa mwungano wa serikali za kitaifa wa amani utaleta jambo hilo lenye kutamanika.
Hata hivyo, amani ya ulimwengu ambayo italetwa na Mungu itakuwa ya namna tofauti. Yeye anatuambia kwamba watu wenye tabia ya amani peke yao—ndio watakaoifurahia. “Wenye upole watairithi nchi,” ndivyo anavyotangaza mtunga zaburi, “watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zab. 37:11) Ahadi hiyo ilitangazwa na Yesu Kristo katika Mahubiri ya Mlimani. (Mt. 5:5) Yeye aliwafunza wafuasi wake kuomba hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wake uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” —Mt. 6:9, 10.
Ni serikali gani itakayotawala juu ya ulimwengu huo wa amani? Si yo yote yenye makao makuu katika mji wa kidunia. Baraza yake ya usimamizi itakuwa mbinguni. Yesu aliiita “ufalme wa mbinguni.” (Mt. 4:17) Hii ni serikali ya Mwana wa Mungu, ambaye nabii wa Mungu alimwita “Mfalme wa amani.” Kuhusu utawala wake, nabii huyo alisema hivi: “Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe, katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; kuuthibitisha na kuutegemeza kwa hukumu na kwa haki, tangu sasa na hata milele.”—Isa. 9:6, 7.
Kama vile unabii wa Isaya unavyotabiri amani chini ya utawala wa kimbinguni wa Yesu Kristo, mtunga zaburi Daudi anaulinganisha utawala wa Kristo na utawala wenye amani wa Mfalme Sulemani, wakati Sulemani alipotawala juu ya Nchi ya Ahadi kufikia mipaka yake iliyowekwa na Mungu. Mtunga zaburi huyo anasimulia namna ya amani anayotamani Mungu, akisema hivi: “Atawahukumu walioonewa wa watu, atawaokoa wahitaji, atamseta mwenye kuonea. . . . Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma [ikimaanisha kwa wakati usiojulikana, au milele]. Na awe na enzi toka bahari hata bahari, . . . Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima; . . . Na ahimidiwe [Yehova], Mungu wa Israeli, atendaye miujiza Yeye peke yake; Jina lake tukufu na lihimidiwe milele; dunia yote na ijae utukufu wake.”—Zab. 72:4-19.
Hatua za kufanya amani na Mungu ni zipi, na, kama matokeo, amani na wengine? Je! jambo hilo linaweza kufanywa duniani pote ili kwamba amani ya kweli ya ulimwengu iwe ndiyo matokeo? Ulizo hilo, lenye umuhimu sana kwa wote, ndilo kichwa cha mazungumzo katika makala inayofuata.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Biblia inaonyesha kwamba msingi wa amani ya ulimwengu lazima uwe ni amani pamoja na Mungu