Maswali kutoka kwa Wasomaji
● Je! 2 Yohana 7 halionyeshi kwamba Yesu angerudi katika mwili?
Hapana, mstari huo hausemi juu ya kurudi kwa wakati ujao katika mwili.
Ebu angalia namna ya kiarifa hasa ambacho kimetumiwa katika tafsiri ya The New English Bible pamoja na tafsiri nyinginezo za kisasa: “Wadanganyaji wengi wametoka wakaingia katika ulimwengu, ambao hawakubali Yesu Kristo kama ajaye katika mwili. Hao ndio watu wanaoelezwa kuwa Mpinga Kristo.”—2 Yohana 7.
Mtu mmoja aweza kusoma katika mstari huu wazo la kwamba unasema kuhusu wakati ujao (kama kwamba unasomwa, “Yesu Kristo kama angali atakuja katika mwili”). Lakini mtu mwingine anaweza kushikilia kwamba ulikuwa ukisema juu ya tukio la wakati uliopita. Kwa hiyo tafsiri ya Good News Bible inautafsiri hivi: “Yesu Kristo alikuja kama mwanadamu.” Nazo tafsiri nyinginezo zinautafsiri hivi, “Yesu Kristo amekuja katika mwili.” (New International Version; Zaire Swahili Bible) Hata hivyo kwa kweli mtume Yohana alitumia namna ya kiarifa cha wakati uliopo, ambacho kinatafsiriwa kwa usahihi zaidi katika Kiingereza (au Kiswahili) katika maana ya wakati usio na mwisho, kwa mfano, “yuaja katika mwili.”—Union Version; New World Translation; The New American Bibie.
Katika barua yake, ya kwanza, Yohana alisema vilevile juu ya ‘kuja’ kwa Yesu walakini katika habari hiyo mtume huyo alitumia namna ya kiarifa cha jambo ambalo limekwisha tukia, ambacho kinatafsiriwa kwa usahihi hivi: “Mwayapata maarifa ya usemi ulioongozwa kwa roho ambao umetoka kwa Mungu kwa njia hii: Kila usemi ambao umeongozwa kwa roho unaokiri kwamba Yesu Kristo amekwisha kuja katika mwili watokana na Mungu.” (1 Yohana 4:2, NW) Hapo anasema kwamba Yesu alikuwa amekuja kama mwanadamu katika mwili.
Alipokuja mara ya kwanza, Yesu hakupata kuwa mwanadamu tu wa nyama na damu. Alipata vilevile kuwa Kristo, mtiwa mafuta wa Mungu. Chini ya uongozi wa roho ya Mungu, Yohana alijua kwamba kulikuwako na kungekuwako na watu wenye kueneza mafundisho ya uongo juu ya jambo hilo. Huenda wengine wangekana wakisema kwamba Yesu hakupata kuishi wakati wo wote. Huenda wengine wangekubali kwamba kulikuwako mwanadamu aitwaye Yesu aliyeishi wakati mmoja, walakini hawakubali kwamba yeye alikuwa ametiwa mafuta kwa nguvu zipitazo zile za binadamu kwa roho takatifu ili apate kuwa Kristo tena aendelee kuwa Kristo. Mawazo kama hayo yenye kudanganya yangepunguza cheo cha Yesu Kristo kama mkombozi pamoja na cheo chake cha kimbinguni cha wakati huu na cha wakati ujao. Yohana angeweza kuwatambulisha kwa kufaa kuwa wadanganyaji wale watu “wasiokiri ya kuwa Yesu Kristo yuaja katika mwili.”—2 Yohana 7.
Kwa habari ya ‘kuja’ kwa wakati ujao, Yesu mwenyewe alisema waziwazi kwamba katika wakati wa kuja kwake kwa mara ya pili yeye hangekuwa katika mwili, aonekane na wanadamu. Yeye alifufuliwa kama roho, asipate tena kuwa mwanadamu wa nyama na damu. (Yohana 14:18-22; 1 Pet. 3:18, NW; 1 Kor 15:45) Kwa sababu hiyo, Yesu aliwaambia wafuasi wake kuhusu ushuhuda mwingi uonekanao ambao kwa huo wangeweza kutambua kuwapo kwake kusikoonekana.—Mt. 24:3-14.
● Kabla ya kujifunza Biblia mimi na mke wangu tulikuwa tumetalikana, si kwa sababu ya uasherati bali kwa sababu hatukusikilizana. Sasa nimekwisha kuwa Mkristo. Kulingana na Biblia, je! niko huru kuoa tena?
Kama mtu aliye katika ‘hali unayoieleza angekuwa huru kuoa tena kulingana na Maandiko hilo lingetegemea kama ndoa hiyo ilimalizika machoni pa Mungu.
Ndoa yako ilimalizwa kisheria kabla hujawa Mkristo, pengine kwa msingi wa kisheria wa kutofaana. Jambo hilo lilimaliza ndoa hiyo kwa maoni ya serikali. Walakini kwa kufaa wewe unataka kujua kama Mtoa-sheria wa Ulimwengu Wote angali anakuona wewe pamoja na mke wako wa kwanza kama “mwili mmoja.”—Mwa. 2:22-24.
Yesu alisema jambo linalotusaidia hapa. Baada ya kukubali kwamba talaka zilikuwa zimefanywa kwa sababu mbalimbali, aliongeza hivi: “Kila mtu atakayemwacha [atakayemtaliki, NW] mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati [Kigiriki, porneia,] akaoa mwingine, azini.” (Mt. 19:9; 5:32) Kwa hiyo, sababu peke yake ya Kibiblia ya talaka ambayo ingempa mtu uhuru wa kuoa tena ni “uasherati” au porneia, inayotia ndani uzinzi pamoja na mwenendo mwingineo mpotovu.
Kwa hiyo, kama mkeo alikuwa na hatia ya kufanya uzinzi, ungalikuwa na msingi wa Kimaandiko wa kupata talaka. Kama ungefanya hivyo kwa msingi wa uzinzi au kwa sababu nyingineyo ya kweli ya kisheria hamngekuwa tena “mwili mmoja.” Vivyo hivyo, kama wewe ungekuwa na hatia ya kufanya uzinzi naye mke wako asitake kukusamehe, awe amepata talaka, nyote wawili mngekuwa huru kulingana na Maandiko.
Walakini, wewe wasema kwamba, uasherati haukuwa umefanywa kabla ya talaka. Kwa hiyo, kulingana na aliyosema Yesu, kungekuwa na sababu gani ya kuamini kwamba talaka hiyo iliimaliza ndoa hiyo machoni pa Mungu? Ijapokuwa mtu anapokuwa Mkristo aweza kumwomba Mungu amsamehe dhambi za wakati uliopita, hiyo haimaanishi kwamba wajibu wote wa wakati uliopita pamoja na mapatano yanaondolewa. (1 Yohana 1:7; 1 Kor. 6:9-11) Kwa mfano: Huenda ukawa ulikuwa umekopa fedha kwa rafiki, ukaahidi kulipa deni hiyo kwa ukawaida. Kisha ukapata kuwa Mkristo. Je! jambo hilo lingeifuta deni hiyo? Hata kidogo. Kwa kujifunza maoni ya Mungu juu ya kulipa deni, pengine ungeliona daraka lako kwa uzito zaidi. (Zab. 37:21; 15:4; 112:5) Inaweza kuwa vivyo hivyo kuhusiana na ndoa. Ulipooa, Mungu alianza kuwaona ninyi wawili kama “mwili mmoja.” Hivyo jiulize mwenyewe hivi: Je! Mungu ana msingi wo wote wa kuacha kuwaona hivyo?
Anaweza kuwa nao. Jambo fulani laweza kuwa lilitokea baada ya kufanya talaka ambalo lingeweza kumaliza ndoa hiyo machoni pa Mungu. Twaweza kujua sababu gani iko hivyo kwa kulifikiria jambo hilo kulingana na aliyosema Yesu katika Mathayo 19:9. Ijapokuwa wewe hukuwa umefanya uasherati, ikiwa mke wako alikutaliki na baadaye ukafanya “uasherati,” ndoa hiyo inaweza kuonwa kuwa ilimalizika. Yeye alikukataa, nao ulikuwako ule msingi wa baadaye wa Kibiblia wa ninyi kutokuwa “mwili mmoja” tena. Kwa upande mwingine, pengine yeye ndiye aliyekuwa na hatia ya kufanya “uasherati” baada ya talaka. Kama vile alivyokubali Yesu, chini ya hali hizo ndoa hiyo yaweza kuonwa kuwa ilimalizika machoni pa Mungu, kwa kuwa kulikuwako talaka, na sasa wewe, mwenzi asiye na hatia, umethibitisha kwamba amekuwa mwasherati.
Kwa hiyo, katika habari ya kisa kama hicho unachotokeza, jambo ambalo limetokea au ambalo halikutokea tangu ilipofanywa talaka laweza kuwa ndilo jambo la kuamulia kama machoni pa Mungu ninyi wawili mngali “mwili mmoja” au sivyo.
Ukiamua kwamba kulingana na maoni ya Mungu wewe hauko huru kuoa tena kulingana na Maandiko, waweza kufanya nini? Uwezekano mmoja ni kujaribu kushiriki kweli za Biblia unazojua pamoja na mwenzi wako ambaye kwa sasa umetalikana naye. Huenda ukaweza kumsaidia kuona kwamba Biblia inaweza kugeuza watu ambao hapo kwanza maisha zao zilikuwa na matatizo na kuwaletea furaha. Walakini ikiwa ninyi wawili mtachagua kuishi pamoja tena, ingefaa mwoane kisheria ili kifungo chenu kiheshimike mbele ya wote.—Ebr. 13:4.
Ikiwa kwa wakati huu hakubali mpatane tena, endelea kuishi maisha safi ya adili, kama vile kwa wazi umekuwa ukifanya. (Yak. 3:17; 1 The. 4:3-5) Mtume Paulo alieleza kwamba wale wanaoishi bila mwenzi wa ndoa wana nafasi ya ’kutumia wakati na uhuru wao katika njia bora kwa kuifuatia ibada ya kweli.a (1 Kor. 7:29-35) Kwa kuendelea kushirikiana na kundi la Kikristo pamoja na kuendelea kuwa na kazi nyingi katika kuhubiri na kufundisha Neno la Mungu utapata uradhi mwingi pamoja na baraka nyingi.
[Maelezo ya Chini]
a Tazama Awake! ya Desemba 8, 1972, kur. 5-8, na Mnara wa Mlinzi wa Septemba 15, 1977, kur. 411-415.