Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 7/15 kur. 5-7
  • Je! Mungu Ana Jina?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Mungu Ana Jina?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • BASI, JINA LA MUNGU NI JINA GANI?
  • JINA HILO LAPATIKANA WAPI?
  • SABABU GANI “YAHWEH”?
  • “YEHOVA” LAJULIKANA ZAIDI SANA
  • Yehova
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • A4 Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kiebrania
    Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
  • Jina la Mungu
    Amkeni!—2017
  • Jina la Mungu Lilipatwa na Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 7/15 kur. 5-7

Je! Mungu Ana Jina?

HUENDA watu wengi wakasema: ‘Je! jina la Mungu lina maana? Kuna mmoja tu Aliye Mkuu Zaidi.’ Kwa mfano, kiongozi mmoja wa kidini katika Canada alisema hivi wakati mmoja: “Vilevile jina ambalo watu humpa Mungu si la maana.” Mwanadini huyo alishikilia kwamba hakuna tofauti yo yote mtu akitumia “Alah,” kama wafanyavyo Waislamu, au “Manitou,” kama wafanyavyo Wahindi fulani wa Amerika ya Kaskazini. Wengine wa viongozi wa kidini wana maoni ayo hayo.

Lakini ebu tufikirie: Sababu gani sisi hutumia majina? Jina ni nini?

Kwanza kabisa, majina hutumiwa kwa ajili ya kutambulisha watu. Vilevile mara nyingi yanahusianishwa sana na mambo aliyofanya mtu au sifa yake. Kwa mamilioni, majina kama vile Aleksanda Mkuu au Ghandi mara moja humkumbusha mtu mambo waliyofanya wanaume hao.

Walakini sababu gani jina la Mungu ni la lazima? Kwa sababu, ingawa watu wengi humwamini Mungu mmoja tu wa kweli, wengine wengi wasiohesabika huabudu miungu mingi. Mabanyani wana mamilioni ya miungu. Katika sehemu nyingine za Asia na katika Afrika, mamilioni ya watu huabudu babu zao. Wengi huabudu Serikali, viongozi wa kisiasa au “mabingwa” wa sinema. Na juu ya wengine, inasemekana kwamba “mungu wao ni tumbo.”​—Flp. 3:19.

Kumtofautisha Aliye Mkuu Zaidi na miungu hiyo mingi, yeye ana jina la pekee na la kibinafsi kabisa. Nalo jina hilo, kama tutakavyoona, ni la maana kwa ajili ya kumtambulisha na vilevile kwa maana linashikamanishwa na sifa yake. Yeye amejifanyia mwenyewe jina.

BASI, JINA LA MUNGU NI JINA GANI?

Je! jina la Mungu laweza kuwa “Allah”? Hasha. Kama vile kamusi yo yote nzuri itakavyokuonyesha, “Allah” ni ufupisho wa neno la Kiarabu linalomaanisha “mungu.” Kwa wazi, hilo si jina.

Namna gani “Bwana”? Vilevile hilo si jina. ‘Iko miungu mingi na mabwana wengi,’ yasema Biblia. (1 Kor. 8:5) Neno la Kispania la “Bwana,” linalotumiwa mara nyingi katika tafsiri za Kispania za Biblia, ni Señor, ambalo wakati mwingi linamaanisha “bwana” au “maulana.” Hilo lingewezaje kuwa jina la binafsi, jina pekee la Aliye Mkuu Zaidi?

Huenda wengine wakasema: “Je! Yesu si ndilo jina la Mungu?’ Wakati Mariamu alipotangaziwa kuzaliwa kwa Yesu, mjumbe wa kimbinguni au malaika alimwambia hivi: “Jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu.” (Luka 1:30-32) Kwa hiyo Yesu ni jina la Mwana wa Mungu, si lile la Aliye Mkuu Zaidi. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Baba ni mkuu kuliko mimi.”​—Yohana 14:28; linganisha Mithali 30:4.

Akiwa Mwana wa Mungu, Yesu hufurahia uhusiano wa karibu sana pamoja na Babaye. Naye Yesu alionyesha wazi kwamba Babaye ana jina. Wakati Kristo alipowafunza wanafunzi wake Sala ya Kielelezo inayojulikana sana, ambayo wakati mwingine huitwa “Sala ya Bwana,” maneno yake ya kwanza kabisa yalikuwa haya: “Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe.” (Mt. 6:9) Katika sala ya baadaye kwa Babaye, Yesu alisema hivi: “Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa. . . . Nami naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo.”‏ (Yohana 17:6, 26) Hivyo, Yesu aliwafunulia maana kamili ya jina la Baba.

Kwa kupendeza, namna ya Kiebrania ya jina “Yesu” ni “Yehoshua,” ambalo ni kifupi cha “Yehova-yeshua,”‏ linalomaanisha ‘Yehova ni wokovu.” Basi ndivyo hivyo​—jina la Baba, Aliye Mkuu Zaidi, ni YEHOVA. Na inafaa kama nini kwamba Yesu, akiwa wakili wa Yehova wa wokovu, jina lake lapaswa kutokana na la Babaye!

JINA HILO LAPATIKANA WAPI?

Jina “Yehova” lapatikana katika maandishi mengi na katika sehemu nyingi. Walakini chanzo kikuu cha jina hilo ni maandishi ya zamani ya Kiebrania yaliyomo katika Biblia. Huenda ukasema, ‘Ee, mimi sijapata kuona jina hilo katika Biblia yangu.’ Ni kweli kwamba Biblia nyingine hazitumii jina la Mungu. Lakini kumbuka mambo yaliyomo katika Biblia ni tafsiri, nao watafsiri hutofautiana katika kutafsiri maandiko ya awali. Hiyo inakuwa hivyo kwa Biblia na vilevile kwa kitabu cho chote au makala inayotafsiriwa na watu tofauti tofauti.

Kwa mfano, tafsiri ya New World Translation of the Holy Scriptures, inayotumiwa sana katika gazeti hili (katika Kiingereza), inalo jina “Yehova” mara elfu nyingi. Walakini katika tafsiri inayojulikana sana ya King James au (Union Version ya Kiswahili) linapatikana mara chache tu. Iwapo una nakala ya Biblia hiyo, fungua kitabu cha Kutoka, sura ya 6, mstari wa 3, nawe utapata maneno haya; “Nami nilimtokea Ibrahimu, Isaka, na Yakobo, kama Mungu Mwenyezi, bali kwa jina langu YEHOVA sikujulikana kwao.”

Pengine unapendelea tafsiri ya Kikatoliki. Nyingi hazina jina la Mungu. Walakini ikiwa una nakala ya The Jerusalem Bible, tafsiri ya kisasa ya Kikatoliki, na iwapo wataka kufungua mstari uliotangulia kutajwa, utaona kwamba inatumia jina “Yahweh” mahali pa “Yehova.” Sababu gani hivyo?

SABABU GANI “YAHWEH”?

“Yahweh” (wakati mwingine “Jahveh”) ni jaribio tu la kulionyesha jina la Mungu katika namna inayokaribia zaidi Kiebrania cha awali. Katika kuandika Kiebrania cha kale, ni herufi bubu (konsonanti) tu zilizotumiwa, bila vokali. Jina la Mungu katika hati za kale zaidi za Kiebrania linaonyeshwa kuwa הוה (YHWH au JHVH), nao wafafanuzi wa Biblia huziita herufi hizo “Tetragrammaton,” maana yake “herufi nne.”

Karne zilivyokuwa zikipita, matamshi sahihi ya jina hilo la kimungu katika Kiebrania yalisahauliwa. Hivyo, hakuna uhakika juu ya vokali zinazopaswa kutumiwa ili kulikamilisha jina hilo. Kwa kuunganisha ishara za vokali za maneno mawili ya Kiebrania Adonay’ (Bwana) na Elohim’ (Mungu) pamoja na zile herufi nne, matamshi Yehowah’ yalitokezwa Mwishowe, katika namna ya Kilatini, ikawa “Yehova.” Hata hivyo, wanafunzi wengi wa Kiebrania husema kwamba “Yahweh” ni sahihi zaidi. Lakini Rudolph Kittel, mhariri kitabu Biblia Hebraica, anaweka vokali katika zile herufi nne kuwa “Yehwah,” katika chapa zake zote.

“YEHOVA” LAJULIKANA ZAIDI SANA

Hata hivyo, jina “Yehova,” lajulikana na kutumiwa zaidi sana. Kwa karne nyingi sana, limetumiwa katika tafsiri za Biblia na vitabu vya namna zote.a Vilevile linaonekana katika maandishi mbalimbali. Kwa mfano, maandishi ya Kilatini juu ya bendera ya silaha ya baraza ya mji wa Plymouth, England (Uingereza), yasema Turris Fortissima Est Nomen Jehova, maana yake: “Jina Yehova ndilo ngome imara kabisa.”‏ (Tazama Mithali 18:10.) Hivyo, jina “Yehova” linaonekana hata katika bas za huko.

Sasa ebu tufanye “matembezi” mafupi kwenye kisiwa cha Minorca katika Bahari ya Kati, kando ya pwani ya Spania. Hapa, katika mji mkuu wa Mahon, Zile Herufi Nne zaonekana ukutani mwa soko la mboga la watu wote, uliokuwa ukuta wa kanisa wenye matao hapo zamani. Karibu na hapo, katika mji mdogo wa San Luis, herufi za Kiebrania za jina la Yehova zimeandikwa juu ya mnara wa kanisa la mahali hapo.

Sasa ebu tutazame ndani ya Kanisa linalojulikana sana la Toledo, mji wa zamani wa kidini wa Spania. Angalia sanamu nzuri iliyochorwa darini mwa chumba kikuu cha kuvalia nguo. Ni mchoro wa Lucas Giordano, mchoraji Mwitalia mwenye kujulikana sana wa karne ya 17. Hapo, katika mahali penye kutokeza sana, pana zile herufi nne za Kiebrania za jina la Mungu.

Pengine lenye kujulikana zaidi la makanisa yote ya Jumuiya ya Wakristo ni kanisa la St. Peter’s Basilica katika Mji wa Vatican (Italia). Hapo, kuna mchoro wa kuhani mkuu wa Israeli akiwa na zile herufi nne juu ya vazi lake la kichwa, unaopamba kaburi la Papa Pius wa Kumi (1835-1914). Vilevile zinapatikana mshipini kwenye kipaji cha uso cha sanamu inayopamba kaburi la Papa Clement wa Kumi na Tatu (1693-1769).

Wapenda muziki wenye maana wanafahamiana vizuri na “Itikio la Wimbo Haleluyah lililoko katika utenzi wa kidini wa Handel unaojulikana sana, Masihi. Mamilioni ya watu yamesikia ukiimbwa tangu ulipochezwa mara ya kwanza mwaka 1743. Lakini ni wangapi wamefahamu kwamba “Haleluyah” (au, “Aleluyah”) maana yake ni “Msifuni Yehova”?

Mwanamuziki mwingine mwenye kujulikana sana, Franz Schubert, alitunga muziki wa wimbo uitwao “Mwenye Nguvu Zote” (Kijeremani, Die Allmacht), kichwa chake kikiwa: “Yehova ni Mkuu, aliye Bwana!”

Jina la binafsi la Mungu linaheshimiwa na kuonyeshwa katika sehemu nyingine na vikao vingine vingi visivyohesabika. Vilevile uchunguzi mdogo unathibitisha kwamba JHVH (YHWH) ndilo JINA la Aliye Mkuu Zaidi, kama inavyoonyeshwa katika Biblia ya Kiebrania. Jina hilo takatifu linaonekana humo mara ngapi? MARA ELFU SITA NA MIA TISA NA SITINI (6,960)! Je! si ni wazi kabisa kwamba jina hilo la kimungu HALIKUKUSUDIWA LIONDOLEWE?

Na hata hivyo tafsiri nyingi za Biblia zimeliondoa jina la Mungu. Sababu gani? Kabla ya kujibu, ebu na tulichunguze jina la Mungu katika historia.

[Maelezo ya Chini]

a Kitabu Webster’s New International Dictionary (1955) chasema hivi kuhusiana na “Yehova”: “Aliye Mkuu Zaidi; Mungu; Mwenye Nguvu Zote . . . Namna Na Kikristo ya Tetragrammaton (zile herufi nne).”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mnara wa kanisa Menorca, Spania

Bas za mji Plymouth, Uingereza

Sanamu juu ya kaburi la Papa Clement wa Kumi na Tatu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki