Jina la Mungu Katika Historia ya Kale
MUNGU, Nguvu inayotegemeza ulimwengu, ni Mtu halisi. Pamoja na hayo, tumeona kwamba ana jina la pekee, la binafsi—Yehova (au, Yahweh—katika Kiebrania, YHWH).
Lakini namna gani juu ya msingi wa kihistoria wa jina hilo? Historia yaweza kueleza jambo gani juu ya jina hilo la kimungu?
MSINGI WA KIHISTORIA WA KALE
Ebu turudi kwenye karne ya 16 K.W.K. Waisraeli wako Misri wakiteseka chini ya utawala wenye ukatili wa Farao. Musa apewa mgawo na Yehova aombe Israeli wawekwe huru. Ili kuonyesha Musa apaswa kutenda na kusema kwa jina la nani, Mungu amwambia hivi: “Waambie wana wa Israeli maneno haya, [Yehova], Mungu wa baba zenu . . . amenituma kwenu; hili ndilo jina langu hata milele.”—Kut. 3:15.
Walakini baadaye Farao mwenyewe akataa kusikiliza, akisema hivi: “[Yehova] ni nani . . . ? Mimi simjui [Yehova].” (Kut. 5:2) Baada ya mapigo kadha, Mungu amwambia Farao hivi: “Nilikusimamisha wewe kwa sababu ii hii, ili nikuonyeshe uweza wangu, tena kwamba jina langu litangazwe katika dunia yote.”—Kut. 9:16.
Vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, ambavyo vina maandishi ambayo yametangulia kutajwa, vimejaa mitajo ya jina la Mungu la binafsi. Katika maandiko ya Kiebrania ya Kumbukumbu la Torati peke yake linaonekana mara 550. Jina hilo halikutumiwa na makuhani na Walawi peke yao. Musa aliandika hivi: “Sikiza, Ee Israeli; [Yehova], Mungu wetu, [ni Yehova] mmoja. nawe mpende [Yehova], Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa [nafsi] yako yote, na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” (Kum. 6:4-7) Bila shaka, jina tukufu la Mungu lilitumiwa sana katika ibada ya jamaa katika siku zile.
UTAWALA WA MFALME DAUDI
Katika utawala wa Mfalme Daudi, jina la Yehova lilitumiwa na likatukuzwa zaidi. Chini ya uongozi wa kimungu, Daudi aliandika zaburi nyingi zenye kupendeza, au nyimbo za sifa, kwa Yehova. Vilevile Daudi alitayarisha kundi kubwa la wacheza muziki hekaluni na itikio la wimbo lenye kutia ndani maelfu ya waimbaji na wachezaji. Kwa ukawaida walicheza na kuimba nyimbo nzuri, zenye kuchochea za kumsifu Yehova, ‘kulisifu jina lake.’—Zab. 68:4.
Je! Yehova alikasirishwa na matumizi hayo yote ya jina lake katika jamaa na mbele ya watu wote? Je! alimlaani Daudi na rafiki zake kwa msingi wa amri ya tatu: “Usilitaje bure jina la [Yehova]”? (Kut. 20:7) Bila shaka sivyo! Daudi alibarikiwa sana na Mungu na utawala wake ulifanikiwa sana.
MAONI YALIYOBADILIKA
Karne tano hivi baadaye, nabii mwaminifu wa Yehova Malaki aliitumia Tetragrammaton (herufi nne za Kiebrania za jina la Mungu) mara 48 katika sura zile fupi nne za unabii wake. Katika sehemu moja, neno la Yehova lililonenwa kupitia kwa Malaki lilikuwa hili: “Kwa maana tokea mawio ya jua hata machweo yake jina langu [litakuwa] kuu katika Mataifa.” Nalo jambo hilo linarudiwa ili kukazia—“Jina langu [litakuwa] kuu katika Mataifa, asema [Yehova] wa majeshi.”—Mal. 1:1, 11.
Angalia vilevile aliyoandika Malaki kuhusiana na makuhani fulani wa siku zake: “Mwana humheshimu baba yake, na mtumishi humcha bwana wake; basi kama mimi ni baba yenu, heshima yangu iko wapi? na kama mimi ni bwana wenu, kicho changu ki wapi? [Yehova] wa majeshi awauliza ninyi, enyi makuhani, mnaolidharau jina langu.”—Mal. 1:6.
Vifungu vya maneno vinavyozunguka vyaonyesha kwamba makuhani hao hawakuwa na hatia ya kukosa kutumia jina la Mungu bali walikuwa wanaonyesha kutoliheshimu kwa kutoa dhabihu zisizokubalika. Maandiko ya Kiebrania na maandishi mengine ya kipindi hicho yanaonyesha kwamba jina la Yehova lilikuwa likitumiwa sana. Kwa mfano, hati (vitabu vya mafunjo vinavyoitwa Elephantine Papyri) za kuanzia karne ya tano K.W.K. kutoka makao ya Kiyahudi katika sehemu za juu za Misri zina jina hilo la kimungu. Hata hivyo, kuna ushuhuda fulani kwamba kabla ya kuharibiwa kwa Yerusalemu na Warumi, kulitokea maelekeo ya ushirikina ya kuepuka kutumia jina hilo la kimungu.a Huenda ikawa jambo hilo lilikuwa hivyo kwa sababu ya ufasiri usio na kiasi, wa kipumbavu wa amri ya tatu—kutotumia jina la Mungu katika njia isiyofaa. (Kut. 20:7) Lakini Mungu alipotoa amri hiyo, je! alimaanisha kwamba jina lake lisitumiwe hata kidogo wakati wo wote isipokuwa katika pindi chache, za pekee, pengine katika patakatifu pa hekalu? Haikuwa hivyo, kwa kuwa wakati jina la kimungu lilipokuwa likitumiwa sana (kama vile katika siku za Daudi), baraka ya Mungu ilikuwa inaonekana wazi katika Israeli. Walakini baraka ya kimungu ilikuwa imekosekana sana katika taifa hilo kwa ujumla wakati wa maisha na utumishi wa Yesu Kristo duniani wakati jina la Mungu lilipokuwa limeachwa kutumiwa kwa sababu ya mapokeo ya kidini ya Wayahudi. Viongozi wa kidini wa Kiyahudi wa siku hizo walikuwa wametenganishwa sana na Mungu na kanuni zake hata kwamba wakalificha jina lake na vilevile wakachukua daraka la kumwua Mwanawe mpendwa. Miaka michache baadaye, katika mwaka 70 W.K., Wayahudi walilipa bei kubwa sana kwa ajili ya hilo wakati majeshi ya Warumi yalipoharibu Yerusalemu mji wao mtakatifu pamoja na hekalu lake.
KRISTO NA WANAFUNZI WAKE WALIFANYA NINI?
Je! Yesu Kristo na wanafunzi wake walifuata mapokeo ya Kiyahudi kwa habari ya jina la Mungu? Bila woga, Yesu alilaani mapokeo ya Mafarisayo na waandishi, na kuweka wanafunzi wake huru kutokana na uongozi huo wenye kuua kiroho. Yeye aliwaambia hivi “wanafiki” hao: “Mbona ninyi nanyi huihalifu amri ya Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu? . . . Mkalitangua neno la Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu.”—Mt. 15:3-9.
Basi, je! Yesu na wanafunzi wake walilitumia jina la Mungu sana? Kwa hakika ndivyo, kwa kuwa wote walitaja mara nyingi Maandiko yaliyokuwa na jina la Yehova. Wakati mwingi walitumia tafsiri ya Septuagint Version, tafsiri ya Maandiko ya Kiebrania katika Kigiriki iliyoanza kutayarishwa katika Alexandria yapata karne ya tatu K.W.K., ambayo nakala zake bado zilikuwa na zile herufi nne. Ni kweli kwamba nakala za Septuagint Version zilizotengenezwa karne nyingi zilizofuata zilifuata mapokeo ya Kiyahudi ya kuondoa jina la Mungu. Walakini vitabu vya kukunja au visehemu vya Septuagint ya Kigiriki vya kuanzia wakati wa Yesu duniani vina zile herufi nne katika mwandiko wa Kiebrania.—Tazama Mnara wa Mlinzi wa Oktoba 1,1978 kur. 6-9.
Yesu mwenyewe alionyesha wazi kwamba alilitumia jina hilo la kimungu. Kwa mfano, alisema hivi katika kumwomba Babaye: “Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu . . . Nami naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo.” (Yohana 17:6, 26) Kuongezea hayo, Yesu aliwafunza wafuasi wake kuomba hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe.” (Mt. 6:9) Sababu gani Yesu atoe semi hizo isipokuwa awe alitumia jina la Mungu?
Kwa hiyo jina la Mungu lilitumiwa sana na watu wake wapya waliochaguliwa, Israeli wa kiroho, kundi la Kikristo. (Gal. 6:16) Hiyo ndiyo sababu tafsiri fulani za Maandiko ya Kigiriki (“Agano Jipya”) hutia ndani jina la Yehova. Kwa mfano, ndivyo ilivyo tafsiri ya Greek Scriptures katika Kiebrania, iliyoandikwa na Franz Delitzch (1877); The Emphatic Diagtott, iliyoandikwa na Benjamin Wilson (1864), na New World Translation of the Christian Greek Scriptures (1950), pamoja na tafsiri nyinginezo. Tofauti na hilo, tafsiri zilizo nyingi zimefuata mapokeo ya Wayahudi na kuliondoa jina la Mungu.
Muda mfupi baada ya siku za Yesu, uasi wa dini uliotabiriwa ulianza kuharibu fundisho na maana ya kweli ya Ukristo. (2 The. 2:3; 2 Pet. 2:1-3) Kipindi kirefu cha ukosefu wa maarifa kilipoingia matumizi ya jina la kimungu yalipotea.b Kwa muda wa karne nyingi, jina la Mungu lilijulikana tu katika makao ya watawa—likijulikana tu kwa wanachuo kama vile watawa.
Basi, je! jina la kimungu lilipataje kujulikana ulimwenguni pote, kama vile lijulikanavyo leo? Toleo la Mnara wa Mlinzi wa Agosti 1, 1980, litajibu ulizo hilo.
[Maelezo ya Chini]
a Viongozi wengi wa kidini Wayahudi wa karne ya kwanza W.K. waliongozwa sana na filosofia ya kipagani ya Kigiriki. Kwa mfano, Filo, mwana-filosofia Myahudi wa Alexandria, aliamini kwamba Plato, mwanafilosofia Mgiriki mwenye kujulikana sana, alikuwa ameongozwa na Mungu naye alifundisha kwamba Mungu haelezeki na, hivyo, hawezi kupewa jina.
b Kwa zaidi ya miaka 1,000 elimu ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo ilifuata mafundisho ya Plato. Tazama kitabu A History of Europe, cha H. A. L. Fisher uku. 52; kitabu The Encyclopædia Britannica, chapa ya 1964, Kit. 18, uku. 63.