Msaada Hakika Kutoka Kwa Neno La Mungu
MTU huhijati sababu yenye nguvu imsaidie asishindwe na maono ya moyoni yenye kuharibu. Biblia hutoa sababu ya namna hiyo, na kumsaidia mtu ashindane kwa kufaulu na maono ya kuwa na hatia, wivu, wasiwasi juu ya kujipatia riziki pamoja na maono mengine ya moyoni yanayoweza kuharibu afya ya mtu.
KUSHINDANA NA MAONO YA KUWA NA HATIA
Mara nyingi, kujiona kuwa na hatia kunasababisha au kuzidisha magonjwa ya namna fulani. Huenda mtu akawa amejiingiza katika mwenendo unaosumbua dhamiri yake. Huenda akaona kama alivyoona Daudi, mfalme Mwisraeli aliyeishi yapata miaka 3,000 iliyopita. Akieleza matokeo ya maono yake ya kuwa na hatia, Daudi aliandika hivi: “Mifupa yangu ilichakaa kwa kuugua kwangu mchana kutwa. . . . Jasho langu likakauka hata nikawa kama nchi kavu wakati wa kaskazi.” (Zab. 32:3, 4) Maneno hayo yanadokeza kwamba jitihada za Daudi za kutuliza dhamiri yenye kusumbua zilimchosha. Kama vile mti ambao umenyimwa maji yanayohitajiwa wakati wa ukavu au kiangazi kikavu, chenye joto kali, ndivyo Daudi alivyoondolewa nguvu. Yeye alipataje faraja?
Yeye alimwungamia Mungu dhambi zake kabisa kabisa, na kwa imani, akakubali msamaha wa kimungu. Hiyo ndiyo sababu Daudi angeweza kuandika hivi: “Heri aliyesamehewa dhambi, na kusitiriwa makosa yake. Heri [Yehova] asiyemhesabia upotovu.”—Zab. 32:1, 2.
Biblia inafunua kwamba ye yote anayemgeukia Mungu na kutubu kwa unyofu, kwa msingi wa dhabihu ya Yesu yenye kufunika dhambi, anaweza kusamehewa dhambi zake. Mtume Mkristo Yohana aliandika hivi: “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, nakutusafisha na udhalimu wote. . . . [Yesu Kristo] ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.”—1 Yohana 1:9; 2:2.
Bila shaka ikiwa mtu haamini kwamba Mungu amemsamehe dhambi zake, ataendelea kupatwa na matokeo yenye kudhuru ya dhamiri yenye kusumbua. Hivyo, ni jambo la maana kwamba mtu atie nguvu imani yake juu ya nia ya Mungu ya kusamehe dhambi. Anaweza kufanya hivyo kwa kufikiria yale yanayosemwa na Biblia juu ya msamaha wa kimungu na juu ya watu waliosamehewa dhambi zao.
Kwa mfano, Waisraeli waliambiwa hivi: “Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu.” (Isa. 1:18) Kwa kuwa Aliye Juu Zaidi alikuwa na nia ya kusamehe matendo mabaya sana ya Waisraeli wasio na imani, twaweza kuwa na hakika kwamba atawasamehe vivyo hivyo leo watu wanyofu wanaotubu. Biblia inatuambia hivi: “Mimi ni Yehova; sijabadilika.”—Mal. 3:6, NW.
Ebu ufikirie mfano mwingine. Mfalme Manase; “akafanya mabaya mengi machoni pa [Yehova], hata kumkasirisha. Na Manase akazimwaga damu zisizo na hatia, nyingi sana, hata alipokuwa ameujaza Yerusalemu tangu upande huu hata upande huu.” (2 Fal. 21:6, 16) Baadaye alichukuliwa mateka mpaka Babeli. Jambo hilo lenye kuudhi sana lililompata Manase, likamfanya ajinyenyekeze mbele ya Mungu. Aliye Juu Zaidi akamsamehe mfalme huyo mwenye kutubu “akamrudisha tena Yerusalemu katika ufalme wake.” (2 Nya. 33:11-13) Ni watu wachache sana ambao wamejifanyia kumbukumbu baya la dhambi kama la Manase. Hata hivyo, kwa kuwa alitubu, alisamehewa. Jambo hilo laweza kuwa kitia-moyo kama nini kwa watu mmoja mmoja wanaosumbuliwa na kujiona kuwa na hatia!
Kisa kingine kuhusiana na habari hii ni kile cha yule mwanamume aliyepata kuwa mtume Mkristo Paulo. Kabla ya kugeuka kwake, yeye alikuwa “mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri.” (1 Tim, 1:13) “Lakini,” akaandika Paulo, “kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele.” (1 Tim. 1:16) Ni jambo lenye kutia imani nguvu kama nini kufikiria yale ambayo Mungu, kupitia kwa Kristo, alifanya kuhusiana na Paulo! Ijapokuwa alikuwa amewatesa sana wafuasi wa Kristo, akawatendea jeuri na kumkufuru Mungu bila kujua, Paulo alisamehewa alipotubu. Baadaye alitumiwa sana awasaidie wengine wawe Wakristo na katika kuwatia nguvu waamini wenzake. Zaidi ya hayo, alipewa pendeleo kubwa sana la kuandika Maandiko mengi zaidi ya Kikristo yaliyoongozwa na Mungu kuliko mtu mwingine ye yote.
Nyakati nyingine huenda watu mmoja mmoja wakajiona kuhukumiwa moyoni, wakiogopa dhambi zao ni mbaya sana wasiweze kusamehewa. Hata hivyo, yale yanayosemwa na Biblia yanatoa msingi imara wa kumwamini Mungu kuwa Mwenye kusamehe dhambi. Jambo hilo laonyeshwa kwa nguvu sana na maneno yafuatayo ya mtume Yohana: “Tutaituliza mioyo yetu mbele zake, ikiwa mioyo yetu inatuhukumu; kwa maana Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua yote.” (1 Yohana 3:19, 20) Kuwa na uhakika katika maneno hayo yaliyoongozwa na Mungu kwaweza kuwa faraja kama nini kwetu na kutuondolea hali ya kujiona kuwa na hatia!
KUPINGA WIVU
Licha ya kujiona kuwa na hatia, kuwa na wivu wenye uchungu juu ya wengine huenda kukasababisha au kuzidisha ugonjwa mwilini. Wivu waweza kuzuia mtu asilale, waweza kufanya sehemu za mwili zikazane na kutokeza maumivu, waweza kutokeza tatizo la tumbo kushindwa kuyeyusha chakula au matatizo mengine ya afya. Kama vile Biblia inavyoweza kumsaidia mtu aondoe maono ya kuwa na hatia yenye kudhuru, inaweza vilevile kumsaidia ashinde wivu au chuki iliyoimarika sana. Walakini, kwanza, lazima mtu akubali kwamba ana tatizo la kuweka chuki moyoni.
Kulingana na Biblia sifa ya upendo inahitajiwa ili mtu aweze kushinda wivu. Maandiko yanatuambia kwamba “upendo hauna wivu.” (1 Kor. 13:4, HNWW) Ili tushinde chuki, tunahitaji kukubali na kutenda kulingana na kweli ya Biblia. Tutaliona kuwa jambo lenye kusaidia tukijitahidi kujuana vizuri zaidi na wale tunaochukia, tukijitahidi kuona sifa zao zilizo nzuri. Ni wazi kwamba, hakuna mtu awezaye kufanya kila kitu, na watu wote wanafanya makosa. Hivyo, kwa hekima, tutajiangalia tusikuze uwezo wetu wenyewe, tuthamini kwamba mambo mengi zaidi yanaweza kufanywa wakati, badala ya mtu mmoja tu, watu wengi wenye kustahili wanapoweza kutoa uwezo wao na ujuzi wao katika kufanya kazi inayofaa.
Biblia inaonyesha waziwazi kwamba tunawategemea wengine. Akitumia mfano wa mwili wa kibinadamu kuonyesha namna inavyopaswa kuwa katika kundi la Kikristo, mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa maana mwili si kiungo kimoja, bali ni vingi. Mguu ukisema, Kwa kuwa mimi si mkono, mimi si wa mwili; je! si wa mwili kwa sababu hiyo? Na sikio likisema, Kwa kuwa mimi si jicho, mimi si la mwili; je! si la mwili kwa sababu hiyo? Kama mwili wote ukiwa jicho, ku wapi kusikia? kama wote ni sikio ku wapi kunusa? Bali Mungu amevitia viungo kila kimoja katika mwili kama alivyotaka.” (1 Kor. 12:14-18) Kupatana na maneno hayo, tutafanya vizuri tukifikiria yale tunayoweza kufanya tuwajenge wengine badala ya kuonea wivu uwezo wao, cheo au yale wanayotimiza.
Sisi kama mtu mmoja mmoja, hatuna kitu cha kujivunia. Hatukujipa sisi wenyewe uwezo wa kusitawisha vipawa fulani au uwezo wa kutimiza mambo. Maandiko yanaweka mambo waziwazi kama ifaavyo, yakisema hivi: “Maana ni nani anayekupambanua na mwingine? nawe una nini usichokipokea? Lakini iwapo ulipokea, wajisifia nini kana kwamba hukupokea?” (1 Kor. 4:7) Zaidi ya hayo, jambo lililo la maana hasa si uwezo wetu wa kutimiza mambo lakini ni vile sisi tulivyo kama watu. Vipawa vya kipekee vina maana gani ikiwa aliye navyo ni mjeuri, mchoyo na mwenye chuki? Kwa hiyo, badala ya kuonea wengine wivu, tutafanya vizuri tukizingatia njia ya upendo, tukijionyesha wenyewe kuwa namna ya watu wanaokuwa na nia na tamaa ya kuwasaidia wanadamu wenzao wenye shida. (1 Kor. 14:1) Bila shaka ni jambo lisilo la hekima kuendeleza wivu, na kwa kufanya hivyo tuhatirishe hali njema ya mwili wetu na kushindwa kuwa namna ya watu ambao wangekuwa chanzo cha kuwajenga na kuwatia wengine moyo.
KUJIZUIA TUSIFADHAISHWE NA UDHALIMU
Si jambo rahisi kuvumilia tunapodhulumiwa au kutoweza kufanya kitu tunapoona wanadamu wenzetu wakionewa au kutumiwa vibaya na wanadamu waovu ili wajifaidi. Jambo hilo laweza kutufadhaisha moyoni na kutudhuru. Kuhusiana na jambo hilo, pia, yale yanayosemwa na Biblia yaweza kutusaidia tujizuie na maono ya moyoni yanayoweza kuharibu afya yetu.
Maandiko yanaonyesha waziwazi kwamba mara nyingi hakuna jambo tunaloweza kufanya. Mambo mengi sana yamepotoka ulimwenguni hivi kwamba mwanadamu hawezi kuyanyosha hata kidogo. Biblia inatuambia kweli inaposema hivi: “Yaliyopotoka hayawezi kunyoshwa, wala yasiyokuwapo hayahesabiki.” (Mhu. 1:15) Kufadhaikia udhalimu ambao huenda ukafanywa na wengine hakubadili hali wala hakumwondolei ye yote tatizo hilo. Bila shaka, ikiwa tunaweza kuendeleza haki ya hukumu katika njia yo yote yenye kufaa, hilo ni jambo lenye kufaa. Hatungetaka kufumba macho yetu kwa njia isiyo na huruma tusione kutaabika kwa kibinadamu ambako si kwa lazima.
Walakini, kwa habari ya hali ambazo lazima zikubaliwe na. kuvumiliwa, twaweza kupata faraja kutokana na ahadi ya Biblia ya kwamba Yehova Mungu atayanyosha mambo. Kwa habari ya siku ijayo ya kutoa hesabu, Maandiko yanatuambia kwamba ‘kupitia kwa Kristo, Mungu atayahukumu mambo ya siri ya wanadamu.’ (Rum. 2:16) Kwa kuwa itakuwako siku ya hukumu, hakuna udhalimu wo wote tunaoweza kupata katika ulimwengu huu uwezao kutokeza madhara yenye kudumu. Tunapokuwa na imani kwamba Muumba atayanyosha mambo, tunajiondolea maono mengi ya moyoni yenye kufadhaisha sana.
WASIWASI JUU YA KUJIRUZUKU
Kwa watu wengi, wasiwasi juu ya kujipatia riziki ndio mzigo mkubwa. Mzigo huo waweza kuwa mkubwa sana hivi kwamba unatokeza matatizo ya afya. Kuhusiana na jambo hilo, Biblia inatoa shauri gani lenye kusaidia? “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini?” akasema Yesu Kristo. “Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.”—Mt. 6:31-34.
Kwa hakika, hakuna kadiri yo yote ya kuona wasiwasi au ya kusumbuka itakayofanya kujitafutia riziki kuwe jambo rahisi zaidi. Kila siku, kama vile isemavyo Biblia, ina “maovu yake,” matatizo yake yenyewe. Kila siku ina matatizo yake yenyewe ya kutosha pasipo kusumbukia magumu ambayo huenda yakatokea katika siku ya kesho. Yehova Mungu hatawaacha wale wanaompenda wataabike isivyo lazima au pasipo kusudi, bali yeye ataitikia maombi yetu ya kutaka msaada. Tukiendelea kuamini kwamba Mungu ni Mtoaji wa riziki huku tukifanya sehemu yetu katika kujitafutia mambo ya lazima ya maisha kupitia kwa kazi inayofaa, tutapata tunayohitaji. Tutaona kama vile alivyoona Daudi, aliyeandika hivi: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.”—Zab. 37:25.
IGEUKIE BIBLIA
Hata mkazo unaoelekeana nao uwe wa namna gani, ndani ya Biblia mna habari inayoweza kukusaidia. Kwa hiyo, yachunguze Maandiko, na kufanya kanuni zake bora kuwa sehemu yenye kufanya kazi ya akiba ya maarifa yako. Ndipo, kwa kutumia kanuni za Biblia katika maisha yako ya kila siku, utaweza kuendelea kufurahia kuwa na dhamiri safi nawe waweza kujizuia usishindwe na maono ya moyoni yanayoweza kuharibu afya yako. Na lililo la maana zaidi, utakuwa ukitembea katika njia iongozayo kwenye uzima wa milele. “Afanyaye mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:17, NW.