Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 9/1 kur. 10-16
  • Kuishi Kulingana na Uchaguzi Wetu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuishi Kulingana na Uchaguzi Wetu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • FUNZO LA BIBLIA NI LA MAANA SANA
  • ITUMIE ZAWADI YAKO SAWASAWA
  • NAMNA MATESO YANAVYOTUFAIDI
  • “Uvumilivu na uwe na Kazi yake Kamilifu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Je, Wewe Ni ‘Msimamizi-nyumba wa Fadhili Zisizostahiliwa za Mungu’?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Kusonga Mbele Baada ya Kupata “Imani”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Kitabu cha Biblia Namba 60—1 Petro
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 9/1 kur. 10-16

Kuishi Kulingana na Uchaguzi Wetu

1. Kila mmoja wetu anahitajiwa afanye nini ili aendelee kushikamana na uchaguzi wetu, kama vile inavyoonyeshwa katika Mithali 16:9 na 1 Petro 1:13?

KWA KUFANYA uchaguzi wa uzima ambao Mungu ametuwekea, vilevile tunachagua kutembea katika njia ya Mungu​—njia ya Kikristo iliyo kamili na ya haki. Ni lazima tushikamane na njia hiyo, nako kufanya hivyo kunahitaji imani katika ahadi za Mungu, pamoja na jitihada na uvumilivu. Walakini kwa Jitihada hiyo twamtegemea Mungu aongoze maamuzi yetu, huku tukishikilia wakati wote uchaguzi wetu wa kwanza ambao tulifanya baada ya kuufikiria sana. Maandiko yasema hivi: “Moyo wa mtu huifikiri njia yake; bali [Yehova] huziongoza hatua zake.” (Mit. 16:9) Petro asema hivi juu ya jambo hilo: “Hivyo kazeni akili zenu kwa ajili ya utendaji, tunzeni akili zenu kabisa; wekeni tumaini lenu juu ya fadhili zisizostahilika zitakazoletwa kwenu wakati wa kufunuliwa kwa Yesu Kristo.”​—I Pet. 1:13, NW.

2, 3. Ni nini kinachoweza kutusaidia sana ili ‘kukaza akili zetu’ kwa ajili ya tendo lenye kufaa?

2 Twaweza ‘kukaza akili zetu’ vizuri namna gani? Twaweza kuwa na hakika namna gani kwamba ‘tunatunza akili zetu’ na hatukosi usawa?

3 Kwanza, twaweza kuzitafakari baraka zisizo na kifani (zisizolinganika) tulizo nazo kwa kuwa wapokeaji wa kweli ya Mungu. Tuna maisha bora zaidi sasa, yenye uhuru mkubwa zaidi pasipo wasiwasi, majonzi na ole zinazopata ulimwengu. Tukiteseka, twajua kwa nini kuteseka kwatokea, na vilevile twatambua kwamba, tukivumilia kwa imani kamili na uhakika kamili, tutakuwa Wakristo bora zaidi na wenye kufaa zaidi. Nalo tumaini letu la ufufuo linaondoa woga mwingi wa kifo, na wa huzuni juu ya wapendwa wanaokufa. Hufanya mambo yote mabaya tunayopata kuwa si kitu kwa sababu ya uzima wa milele ulioko mbele. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Heri macho yaonayo mnayoyaona ninyi. Kwa kuwa nawaambia ya kwamba manabii wengi na wafalme walitamani kuyaona mnayoyaona ninyi wasiyaone; na kuyasikia mnayoyasikia ninyi wasiyasikie.”​—Luka 10:23, 24.

4, 5. (a) Ni jambo gani ambalo lingeweza kuwafanya malaika wapendezwe sana namna hiyo na mambo yanayohusu wokovu wa wanadamu, kama vile inavyooneshwa katika 1 Petro 1:12? (b) Kwa kujua maoni yao, inatupasa sisi nasi tuoneje?

4 Ndiyo, wokovu tunaofurahia ni tuzo lisilopimika, na kuhusu njia ya ajabu ambayo katika hiyo Mungu huuleta kwa wanadamu, Petro asema kwamba manabii walitamani kujua namna unavyotokea, na kwamba “mambo aya haya malaika wanatamani kuchungulia.” (1 Pet. 1:12, NW) Twajua kwamba malaika walikuwapo wakati dunia ilipoumbwa, na hata miaka isiyohesabika kabla ya hapo. (Ayubu 38:7) Walikuwa wameona utukufu wa Mungu, hekima na uweza na sehemu nyingine za utu wake katika mabilioni ya kazi zake za uumbaji. Walakini hapa duniani kulikuwako jambo jipya. Mungu angewezaje kuokoa wanadamu wenye dhambi? Malaika walikuwa wenye kupendezwa sana na jambo hili. Walikuwa wakitamani kujua namna dhambi ya wanadamu ingesamehewa juu ya dhabihu ya kibinadamu, kwa kuwa hawakuwa wameona jambo la namna hiyo likitukia. Sifa ya ajabu ya rehema, sehemu nzuri ya utu wa Mungu, yenye kuvutia hata zaidi na kuchangamsha moyo kuliko uwezo au hata hekima, ilionyeshwa kwa kumtuma Kristo akomboe wanadamu. Vilevile, upendo wake kwa watenda dhambi ulionyeshwa kwa kuwaongoza wale wenye imani katika Mwana wake.

5 Basi, ikiwa malaika wanahesabu rehema hiyo kuwa jambo kubwa kupita yote katika ulimwengu, sembuse sisi kwa nguvu zaidi, sisi ambao tumepata rehema hiyo na kuiona kila siku, twapaswa kuifurahia na kuithamini kuliko vitu vyote! Ni kichocheo gani kikubwa zaidi tungeweza kuwa nacho cha kufurahia na kushikamana na uchaguzi wetu?

FUNZO LA BIBLIA NI LA MAANA SANA

6. Kupatana na 1 Petro 2:2, 3, kusoma na kujifunza Biblia kwapaswa kuwe na sehemu gani katika maisha yetu?

6 Sisi leo twaweza kuazimia kufanya nini ili tulihakikishe tumaini letu? Petro anajibu hivi: “Kama vitoto vilivyozaliwa karibuni, kuzeni tamaa ya maziwa yasiyochanganywa kitu ya lile neno, ili kwamba kupitia kwayo mpate kukua kwenye wokovu, mradi mmeonja kwamba Bwana ni mfadhili.” (1 Pet. 2:2, 3, NW) Ni kwa kusoma na kujifunza Biblia kwa uangalifu na kwa unyofu tu, ndipo tuwezapo kupata nguvu za kiroho tunazopaswa kuwa nazo. Hakuna njia nyingine. Ni lazima sisi wenyewe tuisome Biblia, tufikirie yale inayosema, tuisome pamoja na jamaa zetu na kuzizungumza kweli zake. Tukifanya hivyo, tutasitawisha kulipenda zaidi neno hilo na kutamani mengi zaidi ya hilo. Ikiwa wafalme katika Israeli walitakiwa na sheria ya Mungu wajiandikie wenyewe nakala ya Sheria hiyo, ambayo walikuwa nayo katika siku zao, na kuisoma kwa sauti ndogo kila siku, itakuwaje sisi, tulio na Maandiko kamili, yanayoweza kutuhekimisha tupate wokovu, tusifanye zaidi?​—Kum. 17:19, 20; 2 Tim. 3:15.

7, 8. (a) Watu katika sinagogi la Beroya walifanya jambo gani lililowapatia sifa ya kimungu? (b) Ni kwa sababu gani kusoma kweli katika Biblia yenyewe ni jambo la maana sana?

7 Wakati mitume walipohubiri “habari njema,” Mungu alisifu nani kupitia kwa Neno lake? Ni wale watu katika sinagogi huko Beroya kwa kuwa, Biblia yasema, “walilipokea lile neno [la habari njema zilizonenwa na Paulo na Sila] kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko [kwa uangalifu] kila siku, waone kwamba mambo hayo [aliyosema mtume Paulo] ndivyo yalivyo.” (Matendo 17:10, 11) Waliyafanya mambo hayo kuwa yao wenyewe si kuyasikiliza kwa kukubali tu, walakini vilevile kuchunguza msingi imara wa Kimaandiko wa mambo waliyoyakubali katika akili na mioyo yao kwa hamu.

8 Yatupasa sisi tufanye hivyo. Kwa sababu gani? Kwa sababu twaweza kusikia kweli ikihubiriwa au ikifundishwa na waalimu wa kibinadamu, walakini tunapoisoma katika Biblia ndipo inapokuwa yenye kutegemeka kabisa, nguvu ya kudumu yenye kuchochea katika mioyo yetu, kwa kuwa “neno la Mungu li hai, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kutambua mawazo na makusudi ya moyo.” (Ebr. 4:12) Funzo la Biblia la wakati wote hutuzuia tusiendelee kuwa watoto wa kiroho. Neno la Mungu huingiza roho yake kwenye mioyo yetu,

9. Ni matokeo gani mabaya yanayoweza kutokezwa na magumu na mateso kwetu, nalo ni jambo gani linaloweza kutusaidia kuepuka kupatwa na matokeo hayo mabaya?

9 Katika kueleza yale ambayo sisi kama Wakristo tunapaswa kufanya ili tufanye wokovu wetu hatimaye uwe hakika, na ili tupate zawadi kutoka kwa Mungu, mtume Petro katika barua yake ya kwanza anatushauri tusivunjike moyo chini ya magumu, majaribu na mateso. Tusiache mambo hayo yatutie uchungu na kutufanya kuwa watu wasiotii, wasiozuilika. Kwa kuwa tumenunuliwa kwa kitu kilicho cha thamani zaidi, damu ya Yesu Kristo, ambaye alichukua dhambi zetu alipokufa kwa ajili yetu, twapaswa tuwe “wafu” kwa habari ya dhambi. Twatambua kwamba kwa kukubali dhabihu ya Yesu yenye kuondoa dhambi, tunakiri kwamba hatupaswi kuendelea kufanya dhambi. Kwa hiyo namna zote za ubaya, uongo, unafiki, wivu na kusengenya hazipaswi kuruhusiwa au kufanywa hata kidogo.​—1 Pet. 2:1.

10. Tunaweza kufuataje shauri la mtume kwamba mazoea machafu ya ulimwengu hata ‘yasitajwe kati yetu?

10 Mtume Paulo alilionyesha jambo hilo kwa nguvu sana, kwamba mambo ambayo ulimwengu hufanya na yale ambayo huenda Mkristo alifanya kabla ya kuijua kweli ni mabaya sana hata hayapaswi ‘kutajwa’ katikati ya Wakristo. (Efe. 5:3) Bila shaka, Paulo ‘alitaja’ mambo yasiyo ya kimaandiko lakini kwa sababu tu ya kuyaonyesha kuwa mabaya. Hata hivyo, alikuwa akiwashauri Wakristo wasidumu katika hayo, wakiyasimulia kwa undani wenye kutisha, kuzungumza juu ya namna ambavyo mambo hayo hufaanywa, au kuyatumia kama vichwa vya mazungumzo. Mtu ambaye katika wakati uliopita ametenda mambo hayo hapaswi kuyakumbuka kwa kusudi la kufurahisha mwili, walakini apaswa kuyaonea aibu.​—Rum. 6:21.

11. Katika 1 Petro 4:8, 9, Petro akazia mambo gani yenye kufaa yanayoonyesha imani yetu tunayopaswa kuhangaikia sana, nayo mambo hayo yataonyeshwaje?

11 Na kwa kuongezea, mwendo wa Mkristo kuelekea kwenye tumaini lililoko mbele una mengi zaidi ya kuepuka rnabaya, mambo maovu. Mtume Petro, katika 1 Petro 4:8, 9, aandika hivi: “Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi. Mkaribishane ninyi kwa ninyi, pasipo kunung’unika.” Tuna wajibu wa wakati wote kwa jirani zetu, sana sana wale walio na uhusiano nasi katika imani. Upendo wetu hautatazama makosa na dhambi nyingi katika ndugu zetu. Wakristo wa kweli hawazunguki-zunguki wakijaribu kupata makosa ya wengine au kuwa wenye kushuku (kutia shaka) au kuhukumu wengine kwa kuwa wanaona makosa yao. Je! tunatamani sana kuonyesha ukaribishaji-wageni? Je! tuko tayari kujitoa ili tuwe wafadhili na wenye kusaidiana? Au, je! tunaanza kunung’unika pindi kama hiyo itokeapo? Ikiwa twafanya hivyo, twajiondolea wenyewe furaha yote ambayo tusingepata kwa njia nyingine na vilevile twapoteza thawabu ambayo tungepata kwa kufanya mema. Mambo yasiyochochewa na moyo hayampendezi Mungu.

ITUMIE ZAWADI YAKO SAWASAWA

12. (a) Ni nani kundini wanaopokea “zawadi” zenye kusaidia, na je! Wote wanatazamiwa wawe na uwezo ule ule? (b) Ni katika njia gani hao wanapata kuwa “mawakili” wa Mungu, wakiwa na daraka gani?

12 Vilevile Petro anazungumza juu ya kutumia zawadi zetu. Kila mtu ana uwezo fulani au mwingi zaidi, walakini hakuna aliye na uwezo wote. Vilevile, wengine wana zawadi fulani kwa kadiri kubwa kuliko wengine. Hatuwezi kutazamia wengine wafanye kama tufanyavyo, au kuwa namna ile ile. Petro anasema hivi: “Kila mutu kwa kadiri alivyopokea zawadi aitumie katikati yenu, kama mawakili wema [wa] neema mbalimbali za Mungu.” (1 Pet. 4:10, ZSB) Ikiwa mtu ana uwezo unaosaidia kundi, apaswa kujiona kuwa wakili wa Mungu katika kuitumia zawadi hiyo. Yeye ajua kwamba zawadi hiyo yatoka kwa Mungu, Mtoaji wa kila zawadi njema na kamilifu. Mtu yule aliye na zawadi anakuwa wakili mwenye wajibu kwa mtoaji wayo na bwana wayo juu ya namna anavyoitumia. (1 Kor. 4:2; Yak. 1:17) Aliipokea kwa fadhili za Mungu zisizostahilika, na fadhili hizo zisizostahilika hulipa kundi la Kikristo vitu ambavyo linahitaji. Fadhili hizo zisizostahilika huonyeshwa kwa njia nyingi, mahitaji yakitolewa na watu mbalimbali kundini. Iwapo ye yote wetu ana uwezo na hautumii kulifaidi kundi, yeye anashindwa kuwa wakili.

13. Ni katika njia gani wale wanaosema kundini wanahitajiwa ‘waseme kwa maneno ya Mungu’?

13 Mtume huyo anaendelea kusimulia namna za zawadi na namna zipaswavyo kutumiwa. Yeye anasema hivi: “Mutu akisema, aseme kwa maneno ya Mungu.” (1 Pet. 4:11a, ZSB) Hii haimaanishi kwamba anaposema anaona kuwa wakati wote yeye hakosei, na kwamba watu wapaswa kufanya kama asemavyo. Walakini, asemapo hapaswi kusema maoni yake au kudokeza mambo bila uthibitisho. Yeye apaswa kuwa na uhakika kwamba anayosema ni kwel​i—yaani, msingi wake kabisa ni juu ya maneno ya Mungu na yanapatana na roho ya Biblia. Ni kwa njia hii tu aweza kuwa msaada kwa mtu.

14. (a) Kupatana na 1 Petro 4:11, mtu anawezaje ‘kutumikia’ wengine kundini? (b) Inampasa mtu kama huyo kukumbuka nini sikuzote anapotumikia hivyo, naye atathawabishwaje?

14 Kutoka kwa habari ya kunena, Petro sasa ageukia matendo, anaposema hivi: “Mutu akitumika, atumike kwa nguvu Mungu anazoleta.” (1 Pet. 4:11, ZSB) Mshiriki wa kundi mwenye uwezo wa mambo ya kimwili wa kumsaidia ndugu au jirani, au aliye na nafasi ya kutoa utumishi fulani wenye kutoa msaada, aweza kuendeleza sifa ya upendo kati ya ndugu. Ikiwa ana uwezo wa namna hiyo, anapaswa kutoa msaada huo akitambua kwamba nafasi na uwezo vilitolewa kwake na Mungu. Si kwamba hilo linampendeza Mungu tu, bali hufanya huduma ya Mkristo kuwa yenye matokeo vilevile, kwa kuwa Mungu atambariki yule anayetumikia kwa unyenyekevu. Mtu mwenyewe atathawabishwa kwa kadiri kubwa zaidi ya imani na nafasi ya kutimiza mambo, kama vile mithali ile isemavyo: “Nafsi ya mwenye ukarimu itanenepa, naye anayenywesha, atanyweshwa mwenyewe.”​—Mit. 11:25, ZSB.

15. Mungu aweza kutukuzwaje kupitia kwa Yesu Kristo kwa sababu ya sisi kutumia uwakili wetu kwa uaminifu?

15 Matokeo ya kwanza ya kutumia zawadi au uweza wetu katika njia hiyo ni nini? Je! inatuleta karibu zaidi na utimizo wa tumaini letu? Ndiyo, kwa kuwa inaleta kitu cha kwanza ambacho kwa ajili yacho tulifanya uchaguzi wetu wa kwanza wa kumtumikia Mungu. Yaani: “Ili katika maneno yote Mungu atukuzwe kwa Yesu Kristo.” (1 Pet. 4:11b, ZSB) Tunapofanya matendo mema yanayopatana na Biblia Kristo anatukuzwa, kwa sababu ni kupitia kwake tunapata hali inayokubalika mbele za Mungu, na mwishowe wokovu. Naye Mungu anatukuzwa, kwa kuwa yeye ndiye Mwanzishi wa tendo la kumtuma Mwanawe; kwa hiyo kwa kumtukuza Kristo vilevile tunamtukuza Mungu.

NAMNA MATESO YANAVYOTUFAIDI

16. Ni kwa nini Mkristo anaweza kuwa na sababu ya kufurahi hata anapokabiliwa na mikazo au mateso?

16 Njia hiyo ya maisha inamtukuza Mungu na Mwanawe Yesu Kristo, nayo inatokeza furaha sasa katika kuwatumikia. Twaweza kuwa na uradhi mwingi na moyo wenye furaha kwa kuwa na maarifa hayo. Huenda kukawa na mikazo mingi, hata magumu na mateso. Hata hivyo, twaweza kudumisha furaha katika njia yetu ya maisha. Mtume Petro anazungumza mengi katika barua zake mbili juu ya kuteseka​—sababu, kusudi na matokeo ya kuvumilia kwa uaminifu. Yeye aliwaandikia Wakristo wa siku zake juu ya tumaini lao na ulinzi ambao Mungu aliwapa, akisema hivi: “[Kwa uhakika huu mnafurahi sana], ijapokuwa sana, kwa kitambo kidogo, itawabidi kuhuzunika kwa sababu ya majaribio mbalimbali mnayoteseka. Shabaha yake ni kuthibitisha imani yenu. Hata dhahabu yenyewe, ambayo huharibika, hujaribiwa kwa moto; hali kadhalika na imani yenu, ambayo ni ya thamani zaidi kuliko dhahabu, ni lazima ijaribiwe ipate kuwa thabiti. Hapo mtapokea sifa na utukufu na heshima Siku ile Yesu Kristo atakapofunuliwa.”​—1 Pet. 1:6, 7, HNWW.

17, 18. (a) Ni kwa sababu gani mtume Petro anasema, “kama Mungu akipenda,” anaposema juu ya kuteswa kwa Wakristo? (b) Kama vile mtume Paulo, leo Mkristo anapaswa kuyaonaje mateso anayopata kwa sababu ya kushikamana na uchaguzi ambao amefanya?

17 Katika sura ya tatu ya barua yake Petro anavuta fikira kwenye kuteseka kwa Mkristo na kusema: “Maana ni afadhali kuteseka kwa sababu ya kutenda mema, kama Mungu akipenda, kuliko kuteseka kwa sababu ya kutenda uovu.” (Mst. 17, HNWW) Sababu gani asema juu ya kuteseka huko “kama Mungu akipenda”? Yeye anaeleza hivi: “Wapenzi, musishangae kwa majaribu ya moto yaliyo katikati yenu, yanayowapata ninyi kwa kuwapima ninyi, kama kwamba ni kitu kigeni kinachowapata ninyi. Lakini kama munavyoshiriki katika mateso ya Kristo, furahini ili kwa wakati wa ufunuo wa utukufu wake mufurahi kwa shangwe. Kama mukilaumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, muna heri; kwa kuwa roho ya utukufu na ya Mungu [inakaa] juu yenu.” —1 Pet. 4:12-14, ZSB; linganisha Matendo 5:41, 42.

18 Ingawa Mkristo hapendelei kuteseka, naye hatafuti kuwa mfia imani, yeye anafurahi akihitajiwa ateseke kwa ajili ya kumfuata Bwana wake, Kristo kwa uaminifu. Hakuna heshima kubwa zaidi inayoweza kumjia Mkristo kuliko kufia imani yake. Kabla ya kuchagua mwendo wa kumfuata Kristo, ambao ulitia ndani kuteseka kwingi, mtume Paulo alikuwa mtu mwenye mataraja makubwa ya kujulikana sana, heshima na cheo. Ebu angalia namna alivyoonyesha maoni yake juu ya jambo hilo: “Hayo yote ambayo ningeweza kuyafikiria kuwa ni faida, nimeyaona kuwa ni hasara kwa ajili ya Kristo. Naam, wala si hayo tu; ila naona kila kitu kuwa ni hasara tupu, kwa ajili ya jambo bora zaidi, yaani kumjua Yesu Kristo Bwana wangu. Kwa ajili yake nimekubali kutupilia mbali kila kitu; nimeyaona hayo kuwa ni takataka ili nimpate Kristo . . . na kuiona nguvu ya ufufuo wake, kushiriki mateso yake na kufanana naye katika kifo chake.” (Flp. 3:7-10, HNWW) Paulo alitamani kuwa kama Kristo katika kila njia, akihesabu kuwa utukufu mkubwa zaidi iwapo angetakiwa afe kama Kristo.

19, 20. (a) Mungu anaruhusu mateso ya namna hiyo yawapate watumishi wake kwa kadiri gani? (b) Hasira ya wapinzani na watesi yawezaje mwishowe kumtukuza Mungu? (c) Ni jambo gani jingine kuhusiana na kadiri ya mateso yanayoruhusiwa na Mungu linaloweza kututia moyo tuvumilie?

19 Na zaidi, Petro anataja, si kwamba tu kuna zawadi, bali vilevile kwamba wakati Mungu anaporuhusu mateso, anaruhusu kadiri ile tu itakayotoa mazoezi na adabu kwetu katika njia ambazo tunazihitaji sisi mmoja mmoja. Mtunga zaburi aliandika hivi: “Hasira ya mwanadamu itakusifu.” (Zab. 76:10) Iwapo Mungu anaruhusu wanadamu waelekeze hasira yao juu yetu, twaweza kuwa na uhakika kwamba kuteseka au kufa kwetu kutatokeza mema. Si kwamba tu itakuwa mazoezi kwetu, bali vilevile Mungu atazuia kusudi la watu waovu kwa kuwafanya wengine wamtukuze Mungu kupitia kwa kutazama kwao kuteseka kwetu kwa ajili ya jina lake. Na zaidi, kuteseka huko ni kwa muda mfupi tu, nako kutakoma.

20 Kwa hiyo Petro anawafariji Wakristo kwa kuwaambia hivi: “Baada ya ninyi kuteseka kwa muda mfupi, Mungu wa fadhili zote zisizostahilika, aliyewaita ninyi kwenye utukufu wa milele katika umoja na Kristo, mwenyewe atamaliza mazoezi yenu, atawaimarisha, atawatia nguvu.”​—1 Pet. 5:10, NW.

21. (a) Sasa ni maulizo gani tunayoweza kujiuliza sisi wenyewe kwa faida yetu? (b) Ni mambo gani yenye kutia nguvu anayosema mtume Petro anapomalizia barua yake ya pili?

21 Je! unaona moyoni mwako kwamba umefanya uchaguzi unaofaa? Je! unaona moyoni mwako kwamba unaweza kushikamana na uchaguzi huo, si kwa kuvumilia tu yanayokuja bila kutenda, bali pia kwa kutumikia kwa vitendo? Je! una nia ya kujitahidi sana kutumia zawadi zako ili usaidie ndugu zako? Je! una tamaa, ndiyo, juhudi ya kusaidia wengine wajifunze “habari njema” na kujifanyia uchaguzi ule ule, na, je! una nia ya kuwasaidia wasimame imara wanapofuata uchaguzi wanaofanya? Petro anatufariji na kututia nguvu kwa maneno ya kumalizia ya barua yake ya pili hivi: “Lakini ninyi, wapenzi wangu, mmekwisha jua jambo hili. Basi, muwe na tahadhari msije mkapotoshwa na makosa ya waasi, mkaanguka kutoka katika msimamo wenu imara. Lakini endeleeni kukua katika neema na katika kumjua Bwana wetu na Mkombozi Yesu Kristo. Utukufu uwe kwake, sasa na milele!”​—2 Pet. 3:17, 18, HNWW.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Ili kutoa msaada unaofaa, hakikisha kwamba shauri unalotoa lina msingi wa Biblia.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kutumia kwa unyenyekevu uwezo wetu katika kutoa utumishi wenye kusaidia kunazidisha sifa ya upendo nako kunapata kibali ya Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki