Kusonga Mbele Baada ya Kupata “Imani”
“ Tieni uadilifu kwenye imani yenu, kwenye uadilifu wenu maarifa, kwenye maarifa yenu kujiweza, kwenye kujiweza kwenu uvumilivu, kwenye uvumilivu wenu utawa, kwenye utawa wenu shauku ya kidugu, kwenye shauku yenu ya kidugu upendo.”—2 Pet. 1:5-7, NW.
1. Kwa kweli ni jambo gani linalofanya hazina kuwa yenye thamani?
HAZINA yenye thamani inayoendelea kukaa ikiwa imezikwa katika ardhi haifai kusudi lo lote lenye faida. Inatofautiana kidogo na jiwe lililofichwa chini ya mchanga. Walakini hazina hiyo ina uwezo wa kufaidi mwenye kuwa nayo hata na wengine. Inaweza kutumiwa kusaidia walio wagonjwa na wenye uhitaji, au yaweza kutumiwa kama raslimali (kitu cha kuleta faida zaidi) kwa njia ya hekima. Zikiwa ni fedha nyingi sana, zinaweza kutokeza nafasi za kazi na hivyo kuwezesha watu wengi wapate riziki. Kweli kweli, wakati hazina inapotumiwa katika njia yenye kuzalisha, inakuwa yenye thamani zaidi.
2. Kwa kulingana na 2 Petro 1:1, Wakristo wamepata jambo gani lenye thamani?
2 Hazina ya kiroho waliyo nayo watumishi wa Mungu ina uwezo mwingi hata zaidi wa kutimiza mema. Katika barua yake ya pili aliyowaandikia Wakristo, mtume Petro anazungumza juu ya hazina hiyo yenye thamani, akianza na maneno yafuatayo: “Simoni Petro, mtumwa na mtume wa Yesu Kristo, kwa wote wale waliopata imani, yenye pendeleo lililo sawasawa na letu, kupitia kwa haki ya Mungu wetu na Mwokozi Yesu Kristo.” (2 Pet. 1:1, NW ) “Imani,” yaani, imani iliyo ya lazima ili kupata uzima wa milele, ilikuwa ndiyo hazina ambayo thamani yake ilizidi bei yo yote ile, imani ambayo ilikuwa imekuwa ya wale ambao mtume huyo alikuwa akizungumza nao.
Imani—Hazina
3. Sababu gani Petro angeweza kuisimulia imani ya wale aliowaandikia kuwa “yenye pendeleo lililo sawa-sawa na letu”?
3 Imani hiyo haikuwa ya Petro na mitume wengine peke yao au na wote wale, kama yeye, waliokuwa Wayahudi waliofanywa kuwa Wakristo. Waamini wote waliishiriki, Wayahudi na wasio Wayahudi. Mungu Aliye Juu Zaidi alikuwa amefanya iwezekane wapate imani hiyo. Kupitia kwa ujumbe wa “habari njema” zilizohubiriwa, aliwavuta watu kwake kupitia kwa Mwanawe. (Yohana 6:44) Yeye alifungua mioyo ya watu mmoja mmoja, kuwafanya waitikie “neno” au ujumbe wake.—Matendo 16:14; Rum. 10:8.
4. Imani inapatikanaje “kupitia kwa haki ya Mungu wetu na Mwokozi Yesu Kristo”?
4 Kama vile mtume Petro alivyoandika, imani hiyo ilipatikana “kupitia kwa haki ya Mungu wetu na Mwokozi Yesu Kristo.” Mwenye Nguvu Zote alifanya iwezekane kwa watu wa kabila, mbari, mataifa na rangi zote wapate hazina hiyo yenye thamani kubwa sana. Hivyo kwa kutokuonyesha kupendelea ko kote watu wo wote wakati wa kusamehe dhambi juu ya msingi wa dhabihu ya Mwanawe na kuwakubali wenye kutubu kuwa watu wake, Yehova Mungu alionyesha haki yake, wema, kutopendelea. Jambo hilo ndilo alilotaja Petro alipomletea akida Mwitalia Kornelio “habari njema” yeye pamoja na watu wa ukoo wake na rafiki za karibu. “Hakika,” mtume huyo akasema, “natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” (Matendo 10:34, 35) Mwokozi wetu Yesu Kristo anaoonyesha roho iyo hiyo ya kutopendelea. Yeye alitoa uhai wake kwa ajili ya watu kila mahali.—1 Tim. 2:5, 6.
Kufanya Maendeleo katika Maarifa ya Mungu na Kristo
5. Baada ya kupata Imani, tunakuwa na jukumu gani, na ni jambo gani la lazima ili kulitimiza?
5 Baada ya ‘kupata imani,’ wanafunzi wa Yesu Kristo wanakuwa na jukumu (daraka) la kibinafsi la kujipatanisha zaidi na zaidi wakati wote na yaliyo mapenzi ya Mungu kwao. Maarifa yaliyo sahihi yatatusaidia kufanya jambo hilo. Mtume Petro alikazia umuhimu wa maarifa sahihi na kamili, akasema: “Na mwongezewe fadhili zisizostahilika na amani kupitia kwa maarifa sahihi ya Mungu na ya Yesu Bwana yetu.”—2 Pet. 1:2, NW.
6. (a) Maana yake nini kuwa na “maarifa sahihi ya Mungu na ya Yesu”? (b) Twayapataje maarifa hayo?
6 Maana ya sisi kuwa na “maarifa sahihi ya Mungu na ya Yesu Bwana yetu” ni kuwajua kama watu—sifa zao, njia na matendo—na kuiga mfano wao usio na kosa. (Linganisha Yeremia 22:15, 16; Mathayo 7:21-23; 1 Yohana 2:3-6; 3:5, 6.) Kwa sisi kufanya maendeleo katika kujifunza na kuzitumia kanuni za Neno la Mungu, twapata kumjua Baba na Mwanawe kwa njia nzuri zaidi na zaidi. Jambo hilo linatokeza kufurahia kwetu fadhili zisizostahilika na amani kwa kadiri kubwa zaidi na zaidi.
7. “Fadhili zisizostahilika” zinaongezwaje “kupitia kwa maarifa sahihi ya Mungu na ya Yesu”?
7 Twaendelea kupata msaada na uongozi wa kimungu kwa kufanya yale tu yanayopendeza Yehova Mungu na Yesu Kristo. Kwa sababu tu wanadamu wenye dhambi, sisi wenyewe hatustahili. Kwa hiyo lo lote ambalo Muumba wetu anatufanyia ni wonyesho wa fadhili zake zisizostahilika. Walakini, ili tupokee fadhili zisizostahilika za kimungu inategemea kujitahidi kwetu kuwa kama Baba yetu wa kimbinguni na Mwanawe. Tunapofanya hivyo, twaweza kumkaribia Yehova Mungu tukiwa na uhakika kamili kwamba atajibu maombi yetu. Mtume Mkristo Yohana aliandika hivi:
“Lo lote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake. Na hii ndiyo amri yake, kwamba tuliamini jina la Mwana wake Yesu Kristo, na kupendana sisi kwa sisi, kama alivyotupa amri. Naye azishikaye amri zake hukaa ndani yake yeye, naye ndani yake. Na katika hili tunajua ya kuwa anakaa ndani yetu, kwa [hiyo roho aliyotupa].”—1 Yohana 3:22-24.
8. “Amani” inaongezewaje “kupitia kwa maarifa sahihi ya Mungu na ya Yesu”?
8 Tunapopata maarifa yaliyo kamili, si maarifa tu, juu ya Baba yetu wa kimbinguni na Mwanawe, twayaona waziwazi yanayompendeza. Twaendelea kuwa katika umoja na amani pamoja nao, tukifurahia urafiki wao wakiwa kama rafiki. Matokeo yake yanakuwa kwamba maendeleo yetu katika kumjua Yehova Mungu na Mwanawe kwa ukamili zaidi yanaleta kufurahia amani iliyoongezeka. jambo hilo linakuwa hivyo kwa sababu tunaepuka kwa njia kubwa zaidi maoni, usemi na matendo yanayotofautiana na mfano wa Mungu wetu na Bwana yetu Yesu Kristo.
9. Matokeo ya kutenda dhambi ni nini juu ya amani yetu na Mungu?
9 Kwa upande mwingine, kwa kufanya dhambi, tutakuwa tukiiharibu amani yetu na Aliye Juu Zaidi, kwa kuwa jambo hilo lingekuwa kutenda kinyume cha mapenzi yake. Ni msamaha wa Mungu peke yake, ukiwa juu ya msingi wa sisi kutubu kwa moyo mnyofu na imani katika faida zenye kufunika za dhabihu ya Kristo, ndio unaoweza kurudisha amani.—1 Yohana 2:1, 2.
Acheni ‘Nguvu ya Kimungu’ Iwachochee kwenye Utendaji
10. Ni nini linaloweza kutusaidia tufurahie fadhili zisizostahilika na amani kwa kadiri kubwa?
10 Bila shaka, Yehova Mungu na Yesu Kristo, wanataka tufurahie fadhili zisizostahilika na amani kwa kadiri kubwa. Kwa hiyo, twapaswa kushirikiana nao kwa kujitahidi sana kuwajua vizuri zaidi. Njia moja ambayo kwayo twaweza kufanya jambo hilo ni kwa kufikiri kwa njia ya kuthamini yale ambayo Yehova Mungu, kupitia kwa Mwanawe, amefanya kwa ajili yetu. Mtume Petro aliandika hivi: “Nguvu yake ya kimungu imetupa bure vitu vyote vinavyohusu maisha na utawa, kupitia kwa maarifa sahihi ya yeye aliyetuita kupitia kwa utukufu na uadilifu. Kupitia kwa vitu hivyo ametupa bure ahadi zenye thamani na zilizo bora sana, ili kupitia kwazo mpate kuwa washiriki katika asili ya kimungu, mkiwa mmekwisha kuachana na upotovu ulioko ulimwenguni kwa ajili ya pupa.”—2 Pet. 1:3, 4, NW.
11, 12. (a) Sababu gani ‘nguvu ya kimungu’ inashirikishwa na “maarifa sahihi”? (b) Jambo hilo linaonjeshwaje kwa habari ya Wakristo katika Thesalonike?
11 Angalia kwamba Petro alishirikisha ‘nguvu ya kimungu’ na “maarifa sahihi.” Jambo hilo linafaa sana, kwa kuwa neno la Mungu, au ujumbe, kuhusiana na Mwanawe, “habari njema,” zaweza kuwa na matokeo yenye nguvu juu ya maisha ya watu. Jambo hilo linaonyeshwa vizuri katika yale ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wathesalonike: “Habari njema tunazozihubiri hazikufika miongoni mwenu kwa maneno tu bali kwa nguvu pia.” (1 The. 1:5, NW ) Kuhubiriwa kwa “habari njema” Thesalonike kulikuwa na matokeo. Halikuwa jambo la watu kusikia maneno na kukosa kutenda kulingana nayo, yaani, halikuwa jambo la “maneno tu.” Wathesalonike waliochochewa wakaukubali Ukristo walichochewa watende, kuonyesha kwamba “habari njema” zilikuwa zimetoa nguvu. Wakristo hao wakawa mfano kwa waamini wengine katika kuvumilia mateso kwa uaminifu kwa ajili ya haki na katika kuendelea kutoa ushuhuda kwa kila mtu juu ya “habari njema.”
12 Kwa sababu Thesalonike ulikuwa mji wenye bandari, waamini huko walikutana na mabaharia, wafanya biashara na watu wengine kutoka sehemu za mbali. Wakristo wa Thesalonike walitumia vizuri nafasi zao ili kushiriki “habari njema” pamoja na wengine. Matokeo yake yakawa ni kuzungumzwa kwa imani yao katika sehemu za mbali na karibu. Wakati Paulo na wenzi wake walipotangaza na kufundisha kweli waziwazi katika miji mingine, waliambiwa juu ya Wakristo katika Thesalonike. Akizungumza juu ya jambo hilo, mtume huyo aliandika hivi:
“Maana kutoka kwenu neno la Mungu limevuma, si katika Makedonia na Akaya tu, ila na kila mahali imani yenu mliyo nayo kwa Mungu imeenea; hata hatuna haja sisi kunena lo lote. Kwa kuwa wao wenyewe wanatangaza habari zetu, jinsi kulivyokuwa kuingia kwetu kwenu; na jinsi mlivyomgeukia Mungu mkaziacha sanamu, ili kumtumikia Mungu aliye hai, wa kweli; na kumngojea Mwanawe kutoka mbinguni, ambaye alimfufua katika wafu, naye ni Yesu, mwenye kutuokoa na ghadhabu itakayokuja.”—1 The. 1:8:10.
13. Matokeo ya ‘nguvu ya kimungu’ tumeyapataje sisi binafsi, na kwa hiyo twapaswa kuendelea kufanya nini?
13 Vivyo hivyo, sisi waamini leo tumeiona ‘nguvu ya kimungu’ ikitenda ndani yetu kwa sababu ya sisi kuzikubali “habari njema,” neno la Mungu, au ujumbe. “Habari njema” hizo zimetufanya tufanye mabadiliko maishani mwetu, kujipatanisha wenyewe na mapenzi ya kimungu. Vilevile tumechochewa tutangazie wengine “habari njema.” Nguvu za kimungu zinazotolewa kupitia kwa “maarifa sahihi” yaliyomo katika “habari njema” zimetupa kila kitu tunachohitaji kwa ajili ya “maisha na utawa.” Hivyo, kwa sababu ya nguvu za kimungu, twaweza kuishi maisha ya unyofu, tukitazamia kuishi milele. Nasi twapaswa kuendelea kuziacha nguvu za kimungu zitusaidie tuwe kama Kristo zaidi na zaidi katika mwenendo na utendaji.
14. Yehova Mungu huitaje “kupitia kwa utukufu na uadilifu”?
14 Njia ile ambayo Yehova Mungu huita au kuvuta watu mmoja mmoja kwake yapaswa kuwa kitia moyo chenye nguvu cha kutufanya tuendelee katika Maisha ya Kikristo. Mtume Petro alitaja “maarifa sahihi ya yeye aliyetuita kupitia kwa utukufu na uadilifu.” Yehova Mungu ‘huita’ au ‘kuvuta’ kupitia kwa Mwanawe. Sana sana ni katika Yesu Kristo “utukufu na wema” unaonyeshwa kwa wanadamu. Mtume Mkristo Yohana aliandika hivi kumhusu Mwana huyo: “Neno akawa mwanadamu, akakaa kwetu. Nasi tumeuona utukufu wake, utukufu wake yeye aliye Mwana wa pekee wa Baba; amejaa [fadhili zisizostahilika na kweli].” (Yohane 1:14, HNWW) Yohana na mitume wale wengine, waliona katika maisha ya Bwana Yesu Kristo utukufu, fahari, adhama ambayo ingeweza kuonyeshwa na mtu ambaye alikuwa sura kamilifu ya Baba ya kimbinguni peke yake. Zaidi ya hayo, mtume Yohana, pamoja na Yakobo na Petro, walishuhudia kugeuka sura kwa Yesu Kristo. Katika pindi hiyo ‘uso wake uling’aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru.’ (Mt. 17:2) Kama vile tu utukufu unavyoshirikishwa na Mwana wa Mungu, ndivyo na uadilifu pia. Yesu Kristo alikuwa mwadilifu kwa njia ya pekee sana, mtu mwenye sifa ya adili. Hata msaliti Yuda Iskariote alikubali hivi: “Nalikosa niliposaliti damu isiyo na hatia.” (Mt. 27:3) Kwa hiyo Yehova ametoa wito huo kupitia kwa “utukufu na uadilifu” unaoonyeshwa katika Mwana huyo.
Ahadi za Mungu—Kichocheo cha Kufanya Maendeleo
15. Sababu gani ahadi zilizotolewa na Mungu ni “zenye thamani na zilizo bora sana”?
15 Mpango mzuri sana wa Mungu wa wokovu kama ulivyofunuliwa katika “habari njema” uliwapa Wakristo wa karne ya kwanza “ahadi zenye thamani na zilizo bora sana.” Ahadi hizo zilikuwa zenye thamani au bei katika kutoa faraja, kitia moyo na nguvu yenye kutegemeza katika kukabili chuki ya ulimwengu. Tunapofikiri kwamba waamini wale ambao Petro aliandikia walikuwa wakitazamia kushiriki katika ufalme wake, twalazimika kukubaliana na mtume huyo kwamba walikuwa wamepata ‘ahadi zilizo bora sana.’—2 Pet. 1:4a, NW.
16, 17. Ahadi hizo za kimungu zilikuwa na matokeo gani juu ya waamini?
16 Ahadi hizo ziliwafanyia nini waamini wa karne ya kwanza? Petro anajibu hivi: “Kupitia kwazo mpate kuwa washiriki katika asili ya kimungu, mkiwa mmekwisha kuachana na upotovu ulioko ulimwenguni kwa ajili ya pupa.” (2 Pet. 1:4b, NW ) Kwa maneno mengine, ahadi za Mungu zilitoa msingi kwao wawe “washiriki katika asili ya kimungu.” Tumaini la Wakristo wa karne ya kwanza lilikuwa kushirikishwa na Yesu Kristo katika ufalme wa kimbinguni na kuwa kama yeye. (Rum. 8:17) Kwa kuwa Mwana ni ‘wonyesho wa utukufu wa Mungu na mfano kabisa wa utu wake,’ wote wanaokuwa kama Yesu Kristo wanakuwa kama Baba huyo pia. (Ebr. 1:3, NW ) Mtume Yohana aliandika hivi: “Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo. Na kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu.”—1 Yohana 3:2, 3.
17 Hivyo, kwa kushiriki katika utukufu wa Mwana wa Mungu, Wakristo waliozaliwa kwa roho wanakuwa washiriki wa “asili ya kimungu.” Tumaini hilo zuri lenye msingi wake katika ahadi za Mungu hakika lilitoa kichocheo chenye nguvu kwao wafanye yote waliyoweza ili wajitakase na uchafu wote wa ulimwengu. Mtume Petro alitaja jambo ilo hilo la kuwa safi, kwa kuwa alionyesha kwamba “washiriki katika asili ya kimungu” walikuwa ‘wameachana na upotovu ulioko ulimwenguni kwa ajili ya pupa.’ “Pupa,” kutamani kitu kisicho haki ya mtu, ndicho chanzo cha upotovu na uchafu wa ulimwengu. Waamini walikuwa wameachana na uchafu huo walipotumia kwa faida yao njia ya Mungu ya wokovu na kisha wakajitahidi kujipatanisha na kanuni ya kimungu ya utakatifu, usafi au utakato. Kama ilivyokuwa kwa waamini wa karne ya kwanza, ahadi zilizoko katika Maandiko zaweza kutuchochea tuendelee kujitakasa wenyewe.
Mengi kuliko Imani Yanahitajiwa
18, 19. Baada ya kupata imani, twapaswa kuwa tukifanya nini kwa kupatana na 2 Petro 1:5-7, na sababu gani?
18 Leo watumishi wote wa kweli wa Mungu wamefaidika kutokana na nguvu za kimungu ambazo zimetolewa kupitia kwa “habari njema” na kutoka kwa ahadi bora sana zinazoshirikishwa nazo. Ndiyo maana tunayo sababu nzuri ya kujionyesha kuwa watu wanaoonyesha utu wa Kikristo na wenye kutenda katika kusaidia wengine, sana sana kiroho. Mtume Petro alisihi hivi: “Naam, kwa sababu ii hii, kwa kuitikia kwenu kutoa jitihada yenu yote ya moyo, tieni uadilifu kwenye imani yenu, kwenye uadilifu wenu maarifa, kwenye maarifa yenu kujiweza, kwenye kujiweza kwenu uvumilivu, kwenye uvumilivu wenu utawa, kwenye utawa wenu shauku ya kidugu, kwenye shauku yenu ya kidugu upendo.”—2 Pet. 1:5-7, NW.
19 Hatupaswi kutosheka kuwa na imani au sadikisho tu. Mahali pake, katika kuitikia au kama matokeo ya sisi kupata uwezo wa kuwa na imani kutoka kwa Baba yetu wa kimbinguni, twapaswa kutaka kusitawisha sifa nyinginezo zinazotoa ushuhuda kwamba tuna imani. Mtume Petro alisihi kwamba ‘tutoe jitihada yetu yote ya moyo,’ tujikaze kwa bidii kwa nguvu zote tulizo nazo, tuwe zaidi kama Mwana wa Mungu.
20. Maana yake nini kuongezea imani yetu uadilifu?
20 Kwa sisi kuongeza uadilifu kwa imani inamaanisha kwamba tutajitahidi kuwa watu wenye adili katika kumwiga Mfano, wetu, Kristo. Uadilifu huo, au adili, ni sifa inayofaa. Mwenye kuwa nayo si kwamba anaepuka kumdhuru mtu mwenzake tu, bali pia anatafuta kutenda mema, kuwapa wengine mahitaji yao ya kiroho, kimwili na ya moyoni. Hakika uadilifu ni wema unaotenda. Kwa njia hiyo maisha ya mtu mwadilifu hayatofautishwi tu na mambo yasiyofaa, kama vile yeye kuepuka uasherati, uchafu, udanganyifu na mazoea mengine yanayokataliwa na Mungu. Katika karne ya kwanza W.K., Mafarisayo walijiona kwa kiburi kutokuwa “kama watu wengine, wanyang’anyi, wadhalimu, wazinzi.” (Luka 18:11) Walakini hawakuwa waadilifu, kwa kuwa waliwadharau watu wa kawaida wala hawakuonyesha rehema na huruma.—Marko 3:1-6; Yohana 7:47-49.
21. Sababu gani ni jambo la muhimu kukua katika maarifa?
21 Pasipokuwa maarifa, uadilifu kama unavyoonyeshwa na Yesu Kristo hauwezi kuwapo. Maarifa yanahitajiwa ili kupambanua mema na mabaya. (Ebr. 5:14) Vilevile ni ya lazima ili kuamua namna wema unaotenda utakavyoonyeshwa katika hali fulani. (Flp. 1:9, 10) Tofauti na kuamini bila sababu, imani yenye msingi imara haitikiswi na maarifa. Kwa hiyo, kuwa wenye kutenda kulingana na Maandiko Matakatifu kutatia nguvu imani yetu tunapoendelea kukua katika maarifa ya Yehova Mungu na ya Mwanawe.
22. (a) Sababu gani maarifa ni ya lazima ili kusitawisha kujiweza? (b) Ni nini uhusiano kati ya kujiweza na uvumilivu?
22 Maarifa hayo hutuzuia tusishindwe na tamaa zenye dhambi, tusiwe wenye kukosa kiasi na wasiojiongoza katika mwenendo au katika njia nyinginezo kuwa wenye hatia ya kushindwa sana kuonyesha mfano wa kimungu katika maoni, maneno na matendo. Ndiyo, maarifa yanashiriki sehemu katika kutupa kujiweza, uwezo wa kuongoza utu wa mtu, matendo au usemi. Kwa kuendelea kuonyesha kujiweza, tutakuwa na sifa ya lazima ya uvumilivu. Tunapopatwa na mikazo inayotoka kwa ulimwengu kwa namna ya mahangaiko ya kila siku, watesi au tamaa ya anasa au mali, hatutatoa tamaa zetu kutoka kwa cheo chetu kama watumwa wa Mungu na Kristo bali tutaonyesha kujiweza.
23. (a) Uvumilivu unapatikanaje? (b) Utawa ni nini, nao unajionyeshaje?
23 Nguvu ya ndani ambayo uvumilivu hutokeza yaweza pia kutusaidia tusishindwe na tamaa zenye dhambi, kukana imani yetu tunapoteseka, au kuhangaikia sana mambo ya kila siku, anasa au mali. uvumilivu huo unatokana na kumtegemea Aliye Juu Zaidi atupe nguvu na uongozi. (Linganisha Wafilipi 4:12, 13; Yakobo 1:2-8.) Utawa, au kumwogopa Mungu, zote zapaswa kuongezewa uvumilivu. Woga huo wa kimungu hutofautisha mwendo wote wa maisha ya Mkristo wa kweli. Unajionyesha kwa kumheshimu Muumba ifaavyo na kuheshimu na kuhangaikia inavyotakiwa wanadamu walioumbwa katika mfano wa Mungu.—1 Tim. 5:4.
24. Sababu gani pasipo shauku ya kidugu hapawezi kuwa uchaji?
24 Pasipo shauku ya kidugu, hapawezi kuwapo utawa, au woga wa kimungu. Mtume Yohana alisema hivi: “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona.” (1 Yohana 4:20) Basi, twapaswa kujitahidi katika kusitawisha shauku nyingi kwa ajili ya waamini wenzetu, hivyo ‘kuipa shauku yetu ya kidugu utawa.’
25. Nani wanaopaswa kuonyeshwa upendo, na sababu gani?
25 Upendo ndiyo sifa kubwa zaidi tunayopaswa kuionyesha wazi maishani mwetu. Ndugu zetu Wakristo si ndio peke yao wa kuonyeshwa namna hiyo ya upendo. Ingawa tuna shauku kwa ajili ya ndugu zetu za kiroho, upendo unapaswa kuonyeshwa kwa wanadamu wote. Upendo huo hautegemei kama mtu ni mwenye adili au sivyo. Kama vile upendo wa Mungu kwa wanadamu, unavyoonyeshwa hata kwa adui. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu Kristo alisema hivi:
“Mmesikia kwamba ilisemwa: ‘Utampenda jirani yako, lakini utamchukia adui yako.’ Lakini mimi nawaambieni, wapendeni maadui wenu na kuwaombea wale wanaowadhulumu ninyi, ili mpate kuwa watoto wa Baba yenu aliye mbinguni. Kwa maana yeye huwaangazia watu wabaya na wema jua lake, na kuwanyeshea mvua watu wema na wabaya. Je, mtapata tuzo gani kwa kuwapenda tu wale wanaowapenda ninyi? Hakuna! Kwa maana, hata watoza ushuru hufanya hivyo! Na, mkiwasalimu ndugu zenu tu, je, mmefanya kitu kisicho cha kawaida? Hata watu wasiomjua Mungu nao hufanya vivyo hivyo. Basi, mwe wakamilifu kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.”—Mt. 5:43-48, HNWW.
26, 27. Ni jambo gani litakalotokea tuipapo imani mambo ya lazima yaliyotajwa na Petro?
26 Matokeo yanakuwa nini wakati sifa kama vile uadilifu, maarifa, kujiweza, uvumilivu, utawa shauku ya kidugu na upendo zinapoongezwa kwenye imani? Mtume Petro anajibu hivi: “Ikiwa mambo hayo yanakaa ndani yenu na kufurika, yatawazuieni msiwe ama wasiotenda ama wasiozaa matunda kwa habari ya maarifa sahihi ya Bwana yetu Yesu Kristo.”—2 Pet. 1:8, NW.
27 Ndiyo, matokeo ni utendaji na kuzaa matunda. Tunapoipa imani yetu mambo ya lazima ambayo mtume huyo alitaja na kuyafanya kuwa sehemu yetu na kufurika, hatutakuwa tumesimama, wasiotenda, waliokufa kiroho. Maendeleo yetu ya kiroho yataendelea. Tutakuwa tukionyesha tunda la utu ulio kama wa Kristo na kuzungumzia wengine juu ya “habari njema.” Tukiwa na sifa za kimungu mioyoni mwetu, zikiwa sehemu yetu kweli kweli, tutachochewa kufikiri, kusema na kutenda katika njia inayokubaliwa na Mungu.—Linganisha Luka 6:43-45.
Umuhimu wa Kufanya Maendeleo
28. Hali ya Mkristo wa kujidai anayeshindwa kufanya maendeleo ya kiroho ni nini?
28 Kama mtu angeshindwa kufanya maendeleo kama Mkristo, angeingia katika hali yenye hatari kubwa sana ya kiroho. Mtume Petro alisema hivi juu ya mtu huyo: “Iwapo mambo hayo [yaliyotangulia kutajwa] hayamo katika ye yote, yeye ni kipofu, anayefumba macho yake yasione nuru, naye amekuwa msahaulifu wa kusafishwa kwa dhambi zake za zamani sana.”—2 Pet. 1:9, NW.
29. Sababu gani mtu asiye na tunda la utu ulio kama wa Kristo ni kipofu kwa habari ya uchaguzi wake?
29 Mtu anayekosa kufanya maendeleo ya kiroho, ambaye dai lake la kuwa na imani linakosa tunda la utu kama wa Kristo, ni kipofu kiroho. Yeye haoni maana ya kuwa Mkristo. Upofu huo ni wa makusudi, kwa kuwa kukubali kwake “habari njema” kulimtaka aendelee kujitahidi awe zaidi kama Bwana yake, Kristo.
30. ‘Kusafishwa kwa dhambi” kwapaswa kumchochee Mkristo afanye nini?
30 Mtu wa namna hiyo angekuwa amekosa vilevile kuona uhakika wa kwamba alikuwa amesafishwa dhambi zake juu ya msingi wa damu iliyomwagwa ya Yesu. Kwa kupatana na kusafishwa alikopata wakati wa kuwa Mkristo aliyebatizwa, angepaswa kuendelea kujitahidi sana aendelee kuwa safi, kwa kweli, kujipatanisha kwa kadiri kubwa zaidi na kanuni ya kimungu ya utakatifu. Kwa yeye kushindwa kufanya hivyo, ingeweza kuongoza kwa urahisi kwenye uasi, akatae kabisa dhabihu ya Mwana wa Mungu.
31, 32. Kwa sababu ya hatari kubwa inayotokana na kushindwa kufanya maendeleo kama Wakristo, ni shauri gani la Petro linalopaswa kutiiwa?
31 Kwa sababu kuna hatari ya kiroho kwa kutofanya maendeleo kama Wakristo, twafanya vema kujitahidi katika kufanya maendeleo kuonyesha mfano wa kimungu. Akitoa maelezo juu ya jambo hilo, Petro alisema hivi: “Kwa sababu hiyo, ndugu, fanyeni zaidi na zaidi yote mwezayo ili mfanye kuitwa na kuchaguliwa kwenu kuwe hakika kwenu; kwa kuwa mkiendelea kufanya mambo hayo hamtashindwa kamwe. Kwa kweli, kwa njia hiyo mtapewa kwa wingi sana njia ya kuingia katika ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.”—2 Pet. 1:10, 11, NW.
32 Hakika, wote wale ‘walioitwa na kuchaguliwa’ na Mungu wawe watu wake wanapaswa kujitahidi sana waendelee hivyo. Maandishi ya Petro yaliyoongozwa na Mungu yalionyesha kwamba, kwa kuendelea kuongezea imani yao sifa kama za Kristo, hawatashindwa kufikia lengo la imani yao—wokovu. Hakuna cho chote kingewazuia wasiingie katika “ufalme wa milele” wa Yesu Kristo. Njia ya kuingia katika ufalme huo ‘wangepewa kwa wingi sana.’
33. Ni mambo gani yanayoweza kuhusika kwa Mkristo kupewa ‘kwa wingi sana’ njia ya kuingia katika ufalme?
33 Kutakuwa kuingia kwenye utukufu, sifa zao kama za Kristo zikionekana kwa uangavu sana. Hata hivyo, usemi ‘kupewa kwa wingi sana’ waweza pia kuonyesha kiwango cha juu zaidi cha kubarikiwa kitakachofurahiwa na wale ambao wamekazana kweli kweli katika mbio za uzima.—Flp. 3:14.
34. Kadiri kubwa sana ya kubarikiwa yaweza kuonyeshwaje?
34 Tofauti kati ya uzima peke yake na uzima unaoambatana pamoja na baraka za pekee yaweza kufananishwa na nahodha wawili wa merikebu. Mmoja anaweza kuongoza merikebu kwa ustadi ipite bahari iliyochafuka, kuleta merikebu hiyo salama salimini ufuoni. Lakini nahodha yule mwingine aweza kuvunjikiwa na merikebu wakati wa mchafuko uo huo wa bahari, aokoe maisha yake tu. Ingawa nahodha wote wawili waliokoka na maisha zao, yule ambaye merikebu yake ilisalimika ndiye angepata furaha na utukufu mwingi zaidi.—Linganisha 1 Wakorintho 3:12-15.
35. Hata ingawa uzima wa milele ni zawadi kutoka kwa Mungu, sababu gani jitihada ya mtu binafsi inahitajiwa ili kuupata?
35 Ingawa uzima ni zawadi ambayo imetolewa bure na Mungu, tunaombwa tuonyeshe tamaa yetu ya kutoka moyoni ya zawadi hiyo kwa kufanya yote tuwezayo ili tumpendeze Baba yetu wa kimbinguni. Uzima ni zawadi, kwa kuwa sisi wanadamu wenye dhambi tusingeweza kamwe kuupata kwa kujistahilisha. Walakini twaweza kukosa kuupata iwapo mwendo wetu wa maisha hauonyeshi tunathamini na kutaka zawadi hiyo kweli kweli. Kwa hiyo, ebu tuwe wenye kujitahidi katika kuwa kama Kristo kweli kweli katika maoni, usemi na kutenda. Kisha, kwa msaada wa kimungu, twaweza kuwa na hakika ya kufaulu, si kupoteza uzima wala baraka zo zote za ziada ambazo huenda Baba yetu wa kimbinguni akatupa kwa kuwa wenye kuzaa matunda.
36. Kama inavyoonyeshwa na Petro, ni mambo gani yanayofanya tuhitaji kukumbushwa?
36 Kwa hiyo, twafanya vema kujikumbusha umuhimu wa uaminifu. Hivyo ndivyo mtume Petro alivyotaka wasomaji wa barua yake ya pili wafanye. Yeye aliandika hivi:
“Kwa sababu hiyo sikuzote nitakuwa na maelekeo ya kuwakumbusha mambo hayo, ingawa mnayajua na mmeimarishwa katika kweli iliyomo ndani yenu. Walakini naliona kuwa jambo la haki, maadamu ningali katika hema hii, kuwaamsha ninyi kwa kuwakumbusha, kama nijuavyo kwamba kuvua hema yangu kutakuwa karibuni, kama ambavyo Bwana yetu Kristo alivyonionyesha pia. Kwa hiyo nitafanya yote niwezayo kila wakati pia ili kwamba, baada ya kuondoka kwangu, mweze kujitajia mambo hayo.” (2 Pet. 1:12-15, NW )
Kama vile wale ambao Petro alielekeza maneno yake kwao katika karne ya kwanza, twaweza kuujua umuhimu wa kuhubiri “habari njema” na kufanya maendeleo katika kuonyesha utu ulio kama wa Kristo. Twaweza kuwa tumeimarishwa katika kweli ya Kikristo kwa kadiri ile ambayo tumepata kuijua. Hata hivyo, sana sana tunapokabiliwa na majaribu au pengine mabishi ya ujanja ya waalimu wa uongo, twahitaji mambo ya kutukumbusha ambayo Petro aliandika.
37. Petro alikuwaje mfano mzuri katika kutoa mambo ya kukumbusha?
37 Ni vema kwetu kukumbuka sababu yake ya kuandika mambo hayo ya kutukumbusha. Mtume huyo alikuwa anajua kwamba atakufa karibuni, kwa kuwa Yesu Kristo mwenyewe alikuwa amemwambia kwamba angepatwa na kifo cha mfia imani. (Yohana 21:18, 19) Taraja hilo halikumhuzunisha Petro. Walakini aliazimia kutumia wakati uliokuwa umebaki akitia nguvu ndugu zake, akiwatia moyo wawe wenye kutenda na wenye kuzaa. Kwa hiyo, hata baada ya kuondoka kwake kwa kufa, wangeweza kupata vitia moyo kutokana na mambo aliyowakumbusha na kuyatumia katika kujengana.
38. Twapaswa kuwa tukifanya nini na mambo ya kukumbusha yaliyoandikwa katika barua za Petro?
38 Nasi vilevile na tupate kutiwa moyo na barua za Petro na kutia nguvu wengine kwa kuvuta fikira zao juu ya mambo aliyotukumbusha. Kisha, tunapotazamia kwa uhakika utimizo wa ahadi zilizo bora sana za Yehova, na tuendelee kutangaza “habari njema” na kufanya maendeleo katika kuwa zaidi na zaidi kama Baba yetu wa kimbinguni na Mwanawe.
—Kutoka The Watchtower May 1, 1980.
[Picha katika ukurasa wa 17]
“Tieni uadilifu kwenye imani yenu, kwenye uadilifu wenu maarifa”
[Picha katika ukurasa wa 19]
‘Tieni utawa kwenye uvumilivu wenu’
[Picha katika ukurasa wa 20]
‘Tieni shauku ya kidugu kwenye utawa wenu’
[Picha katika ukurasa wa 21]
‘Mambo yote hayo yakiwa kwenu, yatawazuia msiwe wasiotenda wala wasiozaa matunda’