Kutoa Utumishi Mtakatifu Kwa Nafsi Yote
”Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa Bwana, wala si kwa wanadamu, mkijua ya kuwa mtapokea kwa Bwana ujira wa urithi.”—Kol. 3:23, 24.
1, 2. (a) Kulingana na Kumbukumbu la Torati 30:20, kwa sababu gani ni jambo la maana sana kumtumikia Mungu? (b) Wengine watafurahia pendeleo gani la utumishi wa mbinguni?
PENDELEO kubwa zaidi ambalo mtu anaweza kuwa nalo ni kumtolea Muumba wa wanadamu wote utumishi mtakatifu. Kufanya hivyo kunaleta furaha sasa na vilevile mataraja mazuri sana kuhusu wakati ujao.
2 Biblia inataja tamasha fulani itakayotokea mbinguni wakati ujao, ambako “kiti cha enzi cha Mungu na cha Mwana-Kondoo” kinaweza kuonekana. Uko huko watu 144,000 waliotolewa kati ya wanadamu wanatoa utumishi mtakatifu wakati ule ule wanapotawala wakiwa wafalme mbinguni. Hao ndio watu ambao imesemwa hivi kuwahusu: “Watamwona uso wake, na jina lake litakuwa katika vipaji vya nyuso zao. . . . Nao watatawala hata milele na milele.”—Ufu. 14:1-4; 22:3-5.
3. Wengi wa watu waaminifu wana mataraja gani?
3 Lakini namna gani wanadamu wengine, wale wasioitwa kwenye “mwito wa mbinguni,” wanaomtolea Yehova Mungu utumishi mtakatifu pia? Je! wao pia wataonekana katika tamasha hiyo ya unabii? Naam, wataonekana, kwa maana malaika alimwonyesha Yohana “mto wa maji ya uzima . . . ukitoka katika kiti cha enzi cha Mungu, na cha Mwana-Kondoo, . . . Na upande huu na upande huu wa ule mto, ulikuwapo mti wa uzima, uzaao matunda, aina kumi na mbili, wenye kutoa matunda yake kila mwezi; na majani ya mti huo ni ya kuwaponya mataifa.” Kwa hiyo watu wanaoonyesha imani sasa, watu wa “mataifa” watakaoipita ‘dhiki kubwa,’ watakuwa na taraja hilo la kuzipata faida za mto huo wa maji ya uzima na matunda ya miti ya uzima yatakayowaponya na kuwaletea furaha ya milele.—Ufu. 22:1, 2.
4. Mtu anatakiwa na Mungu afanye nini ili kuokoka Har–Magedoni?
4 Je! wewe unataka kufahamu watu hao watakaoiokoka Har–Magedoni ni akina nani, na jinsi unavyoweza kuwa mmoja wao? Basi tunasoma hivi: “Akajibu mmoja wa wale wazee akiniambia, Je! watu hawa waliovikwa mavazi meupe ni akina nani? nao wametoka wapi? Nikamwambia, Bwana wangu, wajua wewe. Akaniambia, Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo. Kwa hiyo wako mbele ya kiti cha enzi cha Mungu, nao wanamtumikia mchana na usiku katika hekalu lake, na yeye aketiye katika kiti cha enzi atatanda hema yake juu yao. Huyo Mwana-Kondoo, aliye kati-kati ya kiti cha enzi, atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai.” (Ufu. 7:13-17) Je! wewe unajiona ukiwa kati yao? Unataka kuwa mmoja wa watu hao watakaoiokoka ‘dhiki kubwa’? Unaweza kuwa mmoja wao.
5. Yesu alikua na maana gani alipotaja habari ya kumpenda Yehova kwa “nafsi yote”?
5 Ikiwa unataka kuwa pamoja na “mkutano mkubwa” watakaokuwa wakisimama mbele za kiti cha enzi cha Mungu wakimtumikia usiku na mchana baada ya Har–Magedoni, huu ndio wakati wa kumhakikishia Yehova kwamba utaendelea kufanya utumishi wako usiku na mchana kama wasifaji hao Wake, bila moyo nusunusu, bila uvuguvugu, bila kuufanya-fanya safari hii na kuuacha safari ile nyingine. Ndiyo kusema inakupasa umtumikie Mungu kwa nafsi yote. Maneno yanayotaja “nafsi” katika Kiebrania na Kigiriki cha asili yana maana ya mtu mwenyewe—wewe nami. Kwa hiyo tunapotaja utumishi wa nafsi yote, maana yake ni kujitoa kabisa, katika kila njia inayowezekana. Yesu alipotaja habari ya kumpenda Yehova kwa ‘nafsi yetu yote,’ alikuwa na maana ya kumpenda kwa uhai wetu wote, kwa akili zetu zote, mioyo yetu yote na nguvu zetu zote. (Luka 10:27, NW) Inatupasa tutumie kila sehemu ya nafsi yetu (au, uhai tulio nao) tunapomtumikia Mungu. Maisha yetu yote yanapaswa yawe yamefungamana na utumishi wetu mtakatifu.
6. Wakolosai 3:23, 24 inaonyeshaje kwamba kuhubiri habari njema silo jambo la pekee linalohusika katika utumishi mtakatifu?
6 Kueleza watu Neno la Mungu hakutoshi ili kufanya utumishi mtakatifu. Ni kweli kwamba hiyo ni sehemu ya mfano ambao Yesu aliwekea wafuasi wake, lakini utumishi mtakatifu unahusu kutendea watu mema pia, kuwagawia vitu—unahusu jinsi tunavyoishi kila siku. Kwa mfano, mwenendo wetu kazini unaletea ibada tunayomtolea Mungu sifa njema au mbaya. Ni kama Wakolosai 3:23, 24 isemavyo: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa Bwana, wala si kwa wanadamu, mkijua ya kuwa mtapokea kwa Bwana ujira wa urithi. Mnamtumikia Bwana Kristo.” Kila upande wa maisha yetu unaonyesha jinsi tunavyoitikia uongozi wa Yehova—tunapowapa watu ushuhuda, tunapokuwa nyumbani na kazini.
7, 8. Ni baadhi ya mambo gani tunayopaswa kufanya kwa nafsi yote, na kwa sababu gani?
7 Kwa mfano, wanaume na wanawake wana wajibu na migawo ya kutimiza katika jamaa. Wale wanaoheshimu uongozi wa Yehova katika maisha yao wanajua kwamba Mungu anaona kutimiza maagizo hayo yaliyotoka mbinguni kama sehemu ya utumishi wao mtakatifu. Ndiyo sababu Wakolosai 3:18-22 (katika tafsiri Good News for Modern Man) inatukumbusha hivi: “Wake, watiini waume wenu, maana hilo ndilo mnalopaswa kufanya kama Wakristo. Waume, wapendeni wake wenu, wala msiwawie wakali. Watoto, ni wajibu wenu wa Kikristo kuwatii wazazi wenu sikuzote, maana hilo ndilo linalompendeza Mungu. Wazazi, msiwachokoze watoto wenu, ama huenda wakavunjika moyo. Watumwa [ambao leo ni wafanya kazi], watiini mabwana wenu wa kibinadamu katika mambo yote, wala msifanye hivyo nyakati wanapowatazama tu, ili kukubaliwa nao tu, bali mfanye hivyo kwa moyo mnyofu, kwa sababu ya kumcha Bwana.”
8 Hivyo kuangalia jamaa kwa moyo ni sehemu ya utumishi mtakatifu wa mwanamke, kwa maana Yehova ndiye amempa mgawo huo. Inampasa autimize kwa nafsi yote kwa maana mgawo huo umetoka kwa Mungu. (Mit. 31:15, 27) Mume naye apaswa atimize mgawo wake wa kuipa jamaa mahitaji yao na kuiangalia kwa upendo. Kwa hiyo wake wanapotii waume wao, nao waume wanapopenda wake wao, na watoto wanapotii wazazi wao, inawapasa wafanye hivyo kwa nafsi yote ili kumpendeza Yehova. Inatupasa tujiulize hivi, Je! tunatumia vyeo hivyo tulivyo navyo katika mpango wa Yehova kwa njia takatifu, au tunavitumia kwa unajisi na kwa njia ya kilimwengu?
9. (a) Maandiko yanaonyeshaje utumishi mwingine ambamo Wakristo wa kweli wanashiriki? (b) Inatupasa tujiulize maulizo gani?
9 Zaidi ya madaraka hayo ya jamaa, sehemu nyingine ya maana ya utumishi wetu mtakatifu inahusu kuitolea kweli ushuhuda kupatana na mfano wa Yesu na mitume. (Mt. 24:14; Yohana 18:37; Ebr. 13:15; Ufu. 1:5; 12:17) Bila shaka, wakati ambao watu wanaweza kutumia katika utumishi wa hadharani utategemea umri wao, afya yao, madaraka ya jamaa, na mambo kama hayo. Lakini ulizo ni hili, Tunataka kufanya utumishi kiasi gani? Je! tunamwabudu Yehova kwa nafsi yote, hivi kwamba tunatumia vizuri nafasi na nguvu tulizo nazo ili kuitolea kweli ushuhuda?
10. Eleza maana ya Mathayo 13:23.
10 Katika Mathayo 13:23 Yesu alitoa mfano wa mbegu iliyopandwa juu ya udongo mzuri. Alikuwa akiwataja watu wanaolisikia neno na kulielewa kisha wanazaa matunda, huyu mia moja, yule mwingine 60, na yule mwingine 30. Tukifanya tuwezayo kwa nafsi yote, yawe ni machache au mengi, tutakuwa kati ya watu waliotajwa katika mfano wa Yesu, kwa maana namna zote tatu za watu waliotajwa walikuwa sehemu ya “udongo mzuri,” na kila mmoja alizaa kulingana na hali zake.
11. Paulo alikuwa na maoni gani juu ya kumtumikia Mungu, naye aliyaonyeshaje?
11 Watu fulani wana pendeleo la kumtumikia Yehova maisha yao yote, kama mtume Paulo. Si kwamba wanamtumikia kwa nafsi yote kuliko wengine, bali, zaidi ya kutaka kufanya utumishi wa Ufalme kadiri wawezavyo, wao wana nguvu za akili na mwili, tena wanaweza kurekebisha hali zao ili kutumikia wakati wote. Paulo aliiona nafasi yake ya kushiriki sana katika kazi ya kuutangaza Ufalme kama fadhili za Mungu asizostahili. Alisema: “Kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami . . . ndivyo tuhubirivyo, na ndivyo mlivyoamini.” (1 Kor. 15:10, 11) Hivyo ndivyo wewe unavyouona utumishi unaomtolea Mungu?
12. Ni faida gani zinazotokana na utawa?
12 Petro pia alitaja mawazo kama hayo. Alisema: “Uwezo wake wa kimungu umetupa sisi bure mambo yote yanayohusu uzima na utawa, kupitia maarifa sahihi juu ya yeye aliyetuita kwa utukufu na wema. Kwa mambo hayo ametupa sisi bure ahadi zenye thamani nyingi na ubora mwingi sana, ili kupitia kwazo mweze kuwa washirika katika uungu, mkiisha kuukimbia uchafu ulio katika ulimwengu kwa sababu ya tamaa.” (2 Pet. 1:3, 4, NW) Ingawa hapo Petro anasema na wale walio na matumaini ya kuishi mbinguni wakiwa “washirika katika uungu,” maneno yake yanahusu pia watu wote wenye utawa. Tukitumia maarifa sahihi ya Neno la Mungu kwa nafsi yote, tunaweza kuepuka uchafu na matata yanayowapata wenye tamaa mbaya. Tena tunayo ahadi nzuri sana ya kupata faida za milele kutokana na mto wa maji ya uzima na miti ya uzima.
UTUMISHI WENYE MAZAO
13. (a) Inampasa kila mtumishi wa Yehova apendezwe na nini? (b) Ni jambo gani litakalotusaidia tufaulu katika utumishi wetu?
13 Inawapasa wote wanaoonyesha utawa huo kwa kujitahidi kueleza watu kweli ya Neno la Mungu wahakikishe kwamba wana upendeleo wa Yehova na kwamba watafaulu katika mambo wanayofanya. Hilo ndilo jambo linalozungumzwa na Petro katika 2 Petro 1:5-8. Tena tunaona kwamba jitihada ya nafsi yote inahitajiwa. Ndipo Petro anapotaja sifa nyingine ambazo ni za lazima ili kutuzuia tusiwe “ama wasio na matendo ama wasio na mazao yanayohusu maarifa sahihi juu ya Bwana wetu Yesu Kristo.” Hasa, ikiwa mtu ana matatizo ya kiroho, anaweza kuitazama orodha ya sifa hizo aone jambo ambalo amekosa likamletea ugonjwa wa kiroho au hali ya kutotenda. Kwa upande mwingine, tukiyafuata mambo hayo, tutakuwa na matendo na mazao pia katika utumishi tunaomtolea Yehova.
14, 15. (a) Kwanza Petro alitaja sifa gani tatu, na kwa sababu gani ya kwanza ni yenye maana? (b) Kwa sababu gani tunahitaji imani?
14 Kati ya sifa hizo, Petro anataja jitihada nyingi, halafu wema. Ni wazi kwamba jitihada inatakiwa ili kutimiza jambo lo lote—ili kujifunza tupate ufahamu na kuimarisha imani yetu, kufuata mambo tunayojifunza au kueleza wengine mambo hayo. Lakini tunajua pia kwamba tunavuna tunachopanda, kwa hiyo tukitaka matokeo lazima tujitahidi kwanza.—Gal. 6:7.
15 Namna gani juu ya imani? Hatuwezi kuwapa watu imani ikiwa sisi wenyewe hatunayo. Tunaweza kufurahi kwa sababu imani ni mojawapo matunda ya roho, nayo inaongezeka inapositawishwa na kuangaliwa. (Rum. 10:17) Kwa sababu gani imani ni ya maana sana? Kwa sababu “pasipo imani haiwezekani kumpendeza” Mungu.—Ebr. 11:6.
16. (a) Wema ni nini? (b) Unahusuje utumishi wetu wa Kikristo?
16 Lakini, zaidi ya jitihada na imani, Petro anataja wema pia. Wema unahitajiwa sana kwa maana bila baraka za Yehova na bila ya yeye kuikuza mbegu ya kweli jitihada zetu zote za kuwapa watu ushuhuda zinakuwa za bure. Ni kazi bure kujaribu kutoa dhabihu ya sifa ikiwa hatuishi kulingana na kweli. Wema ni ubora wa tabia, nasi tunauhitaji ili kustahili kuwa kati ya wale waliovaa mavazi meupe. (Ufu. 7:9) Ni wazi kwamba mtu aliye macho kueleza watu habari za Biblia ingawa ana kazi nyingi, na anayeishi kupatana na mambo inayosema, anailetea kweli maendeleo kuliko yule anayeweza kutumia wakati mwingi akiwapa watu ushuhuda katika eneo fulani na kumbe haishi kupatana na Neno la Mungu. Wakati na jitihada zinazotumiwa kuwapa watu ushuhuda siyo mambo ya pekee yanayoleta mazao. Bali, Yehova ndiye anayeleta ongezeko, naye anatujua; anajua mambo tunayofanya na jinsi tulivyo.
17. Maarifa ya Biblia yanaweza kutusaidiaje?
17 Petro anaendelea kusema hivi: “Upeni wema wenu maarifa, nayo maarifa yenu myape kujiwesa, nako kujiweza kwenu mkupe uvumilivu.” Ni vyepesi kufahamu jinsi maarifa sahihi ya Biblia yatakavyotusaidia tuwe wenye mazao tunaposadikisha watu ubora wayo. Maarifa hayo yatatusaidia tuwe tayari sikuzote kuzitetea habari njema kwa matokeo mazuri, badala ya kuzitetea vivi hivi tu. Si hilo tu, bali pia yatatusaidia tujue mambo ambayo Yehova anataka tufanye ili kupata upendeleo wake. Tunapopata maarifa hayo tunaweza kuona wazi zaidi ubora wa kufanya mambo kupatana na njia yake, kwa moyo kamili na akili kamili.
18. (a) Ni baadhi ya njia gani za kujiweza? (b) Kulingana na mambo ambayo Paulo aliandikia Wagalatia, tunajuaje kwamba aliona ubora wa kujiweza?
18 Sasa tunaifikia sifa ya kujiweza. Tunawezaje kumtumikia Yehova kwa nafsi yote ikiwa hatufuati Neno Lake kwa kuuzuia mwili wetu na tamaa zake, au ikiwa hatuangalii mambo tunayofanya kwa mikono yetu, au mahali ambako nyayo zetu zinatupeleka, au mambo yanayosemwa na kinywa chetu? Tunawezaje kufanya maendeleo ya kiroho ikiwa hatujiwezi kiasi cha kuweza kufunga televisheni wakati wa kujifunza ufikapo? Tunatumia wakati mwingi tukifanya nini—tukitazama televisheni, tukiwa na tafrija ya namna nyingine, au tukiangalia mambo ya kiroho? Inatupasa tufikirie jambo hilo. Tunataka kutumiaje wakati wetu? Je! tunauthamini wakati tulio nao kama kitu tulichopewa na Yehova, tunachoweza kutumia “usiku na mchana,” si mara moja au mbili tu kwa juma, katika mambo yanayohusu ‘utumishi mtakatifu’? Tunatakiwa tujiweze ili kumtumikia Yehova kwa nafsi yote. Basi lazima tuelekeze nguvu na mawazo yetu juu ya Yehova, bila kujifikiria wenyewe au kufuata anasa tu.—Gal. 5:16, 17, 22-24.
19. Kwa sababu gani Wakristo wanahitaji uvumilivu na utawa?
19 Lakini hata maarifa na kujiweza ni kwa bure tu ikiwa hatuonyeshi uvumilivu na utawa, kushikamana na ile kweli tukiisha ipata. Ni kama alivyoandika Luka (21:19): “Kwa subira yenu mtaziponya nafsi zenu.” Naam, mataraja yetu ya kupata uzima yanategemea uvumilivu wetu. Wengine watalazimika kuvumilia wanapotendwa mabaya mwilini, kama Mashahidi wa Yehova katika Malawi. Huenda wengine wakafadhaika kwa sababu ya ubaridi wanaoonyeshwa na watu wanapojitahidi kuwaeleza habari njema, au kwa sababu ya mikazo na dhihaka za rafiki na jamaa zao, na wengine kwa sababu ya kupingwa vikali sana. Lakini kama vile Paulo alivyomwambia Timotheo: “Utauwa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.” (1 Tim. 4:8) Kwa hiyo tunahitaji uvumilivu na utawa pia ili tusonge mbele kwa uaminifu, tusiwe bila matendo au mazao katika utumishi mtakatifu tunaomtolea Mungu.
20. Shauku ya kidugu na upendo inatusaidiaje tuepuke kuwa bila mazao katika utumishi wetu?
20 Mwishowe, Petro anatuambia tuongezee utawa wetu shauku ya kidugu, kisha tuongezee shauku yetu ya kidugu upendo. (2 Pet. 1:7) Inatupasa tuonyeshe watu wote mambo hayo, si jamaa yetu ya kimwili tu. (Gal. 6:10) Kwa kawaida wale wanaopendezwa kikweli na watu, kuwaonyesha agape au upendo wenye kuongozwa na kanuni, wanawaona wakiwasikiliza wanapowaeleza habari zinazohusu kweli. Inatupasa tuonyeshe watu wote upendo na shauku ya kidugu kama vile Yehova anavyotuonyesha sisi upendo. Inatupasa tuwahangaikie mmoja mmoja, tuwe wanyofu tukitaka kuwasaidia kiroho. Tukifanya mambo yote hayo tutaepuka kuwa watu “wasio na matendo ama wasio na mazao yanayohusu maarifa sahihi juu ya Bwana wetu Yesu Kristo.”—2 Pet. 1:8, NW.
UTUMISHI UNAOLETA BARAKA
21, 22. (a) Ni shauri gani la Petro linalohusu kila mtu anayemtumikia Mungu kwa roho na kweli? (b) Tunaweza kuyatumiaje maneno ya Yesu yaliyo katika Luka 13:24, 25?
21 Petro anaendelea kusema maneno yake yenye kututia moyo: “Kwa hiyo ndugu, jitahidini zaidi kufanya imara kuitwa kwenu na uteule wenu; maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe. Maana hivi mtaruzukiwa kwa ukarimu kuingia katika ufalme wa milele wa Bwana wetu, Mwokozi wetu Yesu Kristo.” (2 Pet. 1:10,11) Tuwe kati ya mabaki waliotiwa mafuta walio warithi wa Kristo au kati ya “mkutano mkubwa,” kitia-moyo ambacho Petro anatoa kwa kusema “jitahidini zaidi” kinahusu kila mtu anayetaka kupata baraka za Ufalme.
22 Huu sio wakati wa kupunguza utumishi wetu mtakatifu. Bali, Petro anatusihi akisema: “Imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa, mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza.” (2 Pet. 3:11, 12) Yesu hakuwapa malaika mgawo wa kufanya wanafunzi, akiwatazamia wavae miili ya kibinadamu ili kutenganisha “kondoo” na “mbuzi.” Bali, aliwapa wale wanaoonyesha kwa utumishi wa nafsi yote kwamba wao ni wafuasi wake wa kweli. (Ufu. 12:17) Huu ndio wakati wa kumpendeza Mfalme wetu wa mbinguni kwa kufanya kazi ya Ufalme kwa ukawaida, si kwa kutoa dhabihu ya sifa yenye uwete wala iliyo nusu-nusu, ya mara kwa mara tu.—Mal. 1:6-8; Luka 13:24, 25.
23. Yako mataraja gani mbele ya wale wanaomtolea Mungu utumishi mtakatifu kwa nafsi yote?
23 Tunapojaza maisha yetu na utumishi mtakatifu wa nafsi yote, tunaweza kuwa na hakika ya kuwa kati ya mkutano wenye furaha utakaookoka Har–Magedoni ufurahie kuendeleza utumishi huo mchana na usiku mbele za kiti cha enzi cha Mungu, baada ya dhiki kubwa. Ndipo itakavyokuwa kama Ufunuo 7:17 unavyotuambia: “Huyo Mwana-Kondoo, aliye katikati ya kiti cha enzi, atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai.” Lo! tuna taraja zuri namna gani mbele yetu tukiendelea kumtolea Yehova utumishi mtakatifu kwa nafsi yote!