Ufurahie Utumishi Unaomtolea Yehova
“Mtumikieni [Yehova] kwa furaha; njoni mbele zake kwa kuimba.”—Zab. 100:2.
1, 2. Mara nyingi watu wanatafuta furaha namna gani, naye Yesu alikuwa na maoni gani juu ya kinacholeta furaha?
WEWE unataka furaha? Huenda ukajibu, ‘Ndiyo, kwani kila mtu haitaki?’ Naam, watu wengi wanatafuta sana furaha maishani mwao, lakini wakaaji wengi wa dunia hawaipati amani hiyo nyingi ya ndani, hawapati uradhi unaoonyesha furaha ya kweli, yenye kudumu. Watu wengi wanaoamini kwamba mali zitawafurahisha wanatia bidii wapate mali zaidi. Lakini je! kutafuta mali ndiyo njia ya kupata furaha yenye kudumu? Ikiwa siyo, inaweza kupatikanaje?
2 Si vigumu kujibu maulizo hayo tujuapo kwamba furaha yenye kudumu haitegemei hali za kimwili hasa. Yesu alipotaja zile “heri” zake katika Mahubiri juu ya Mlima, hakutaja mali hata kidogo. Alisema: “Heri walio maskini wa roho . . . Heri wenye njaa na kiu ya haki . . . Heri wenye rehema . . . Heri wapatanishi.”—Mt. 5:3-9.
3. Je! ni vigumu kweli kuiona njia ya kupata uradhi na furaha ya kweli?
3 Ingawa watu wengine wanadhani furaha na uradhi wa kweli haiwezi kupatikana, si vigumu sana kuipata, kwa sababu inahusiana sana na ibada safi ya Muumba, Yehova Mungu. Anaitwa “Mungu mwenye furaha,” naye anatutaka sisi tuwe wenye furaha pia kwa sababu alimwumba mwanadamu kwa mfano wake. (1 Tim. 1:11, NW; Mwa. 1:27) Anafanya iwe vyepesi kwetu kujua analokusudia kutufanyia, na tunayopaswa kufanya. Mtume Paulo aliambia kikundi cha wanafilosofia Waathene kwamba Mungu ndiye aliyeumba wanadamu naye anawataka ‘wapapase-papase, wakamwone, ijapokuwa hawi mbali na kila mmoja wetu.’—Matendo 17:26, 27.
MAONI YA YESU JUU YA KINACHOLETA FURAHA
4. Kwa sababu gani tunaweza kulitegemea shauri la Yesu kwamba haimpasi mtu ajawe na wasiwasi wa kuhangaikia mali?
4 Katika ulimwengu huu watu wengi wanaona kwamba ni vigumu sana kujipatia riziki. Lakini ni vigumu kweli? Ni kweli kwamba jitihada inatakiwa ili kujipatia riziki. Lakini Yesu Kristo alionyesha kwamba si lazima kusumbukia mahitaji yetu. (Mt. 6:25) Yesu alijua alilokuwa akisema, kwa maana alikuwa amekuwa wakili wa Baba yake katika kuumba wanadamu hapo kwanza. (Kol. 1:15, 16) Alikuwa ameona uangalizi na mipango ambayo Mungu alifanyia wenye kumtumikia, kwa hiyo angeweza kukubaliana na maneno ya Daudi: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.”—Zab. 37:25.
5. Wakati wa huduma ya Yesu na baada ya hapo, je! hali za uchumi zilikuwa nzuri kuliko za wakati wetu, hivi kwamba maneno yake hayatuhusu sana leo?
5 Yesu alilijia taifa la Kiyahudi wakati wenye msukosuko. Alijua kwamba baada ya miaka michache msukosuko mwingi zaidi ungetokea. Tunaweza kuwa na hakika kwamba, kwa sababu alikuwa mjumbe wa Mungu aliye mkuu zaidi, alitoa shauri la kweli aliposema hivi: “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”—Mt. 6:31-33.
6. Je! mtu anayemtumaini Mungu anaweza kujikalia kitako tu akimngojea amtimizie mahitaji yake?
6 Yesu alijua kwamba Baba yake ndiye Mungu Aliye Hai, mwenye uwezo na nia ya kutumia nguvu zake nyingi ili kumruzuku mtumishi wake anayefuata Neno lake la kweli. Hiyo si kusema kwamba atalisha na kuvalisha mtumishi wake hata asipotia bidii. Lazima mtumishi wa Mungu awe na maoni ya kiasi, afanye kazi akitafuta mahitaji yake, lakini bila kushughulikia jambo hilo tu. Lazima ajaribu kufanya matakwa ya Mungu kwa kulichunguza Neno Lake. Lazima atangulize maisha yake ya kiroho. Ndipo Mungu atakapotimiza fungu lake, amwezeshe mtu huyo apate mahitaji yake.—Flp. 4:19.
MAMBO MAKUBWA YANAYOLETA FURAHA HALISI
7. Ni furaha gani ambayo Labda ndiyo kubwa zaidi inayoweza kupatikana na mtu anayejifunza kweli?
7 Uhakikisho na ushuhuda huo ambao Mungu anatoa kuonyesha kwamba ahadi yake itatimia unaleta furaha. Furaha zilizo kuu ndizo hizi: Kwanza, kulifahamu kusudi la Mungu kwa dunia na wanadamu walio juu yake, na cheo ambacho mtu anacho katika kusudi hilo. Jambo hilo linampa mtu lengo au kusudi la kuishi, nalo kusudi hilo linaleta furaha kuliko mali.
8. Maneno ya mtume Paulo yaliyo katika 1 Timotheo 4:8 yanatuhusuje wakati huu?
8 Halafu, kuishi kulingana na matakwa ya Mungu kunaondolea mtu hofu na hatari nyingi. Kwa ujumla, wale wanaoangalia jamaa zao vizuri, kimwili na kiroho pia, wanakuwa na uhusiano wenye furaha zaidi katika jamaa. Watoto wao wanakua wakiwa na kusudi maishani. Inakuwa vyepesi zaidi kwa washiriki wa jamaa hiyo kuona ubatili wa kutafuta raha kwa kutumia dawa za kulevya, kufanya uasherati na kufuata miradi isiyoleta thawabu yenye kudumu. Kwa hiyo wanaepuka magonjwa mengi ya akili na mwili, yanayotokana na maisha mapotovu yanayofuatwa na watu wengi leo. Kuhusu jambo hilo, mtume Paulo alisema: “Utauwa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.”—1 Tim. 4:8.
9. Zaidi ya furaha zilizokwisha tajwa, mtu anapata furaha gani akiisha kuijua kweli na kuifuata?
9 Tena, kuna udugu wa kweli kati ya wale wanaomtumikia Mungu. Huenda wasipendelewe sikuzote na watu wa ukoo wao. Huenda wakaachwa na rafiki zao. Lakini, Yesu aliahidi hivi: “Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili na Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele.”—Marko 10:29, 30.
10. Ni furaha gani kuu inayoweza kupatikana na watangazaji habari njema peke yao?
10 Furaha kubwa sana inayopatikana kwa kuishi kulingana na Biblia ni furaha ya kusaidia wengine. Tofauti na lile wazo la kudhani kwamba furaha inatokana na kupata, Mwana wa Mungu alisema: “Ni heri kutoa kuliko kupokea.” (Matendo 20:35) Wale ambao wamejitoa maishani mwao wasaidie wanadamu wenzao kwa kuwa waganga, waalimu na wengineo, wamepata uradhi na furaha. Lakini furaha yao hailingani na ile inayotokana na kusaidia wanadamu wenzetu wamjue Mungu. Sababu ni kwamba, kujua njia na maagizo ya Mungu hakuleti manufaa ya muda tu, bali kunaleta manufaa katika maisha ya sasa pamoja na tumaini la kuishi wakati ujao. Watu wanapojifunza kweli, wanasaidiwa na Mungu wajue jinsi ya kuishi, kutatua matatizo yao au kuyavumilia. Nao pia wanaweza kusaidia wengine wajifunze maisha yanayoonyeshwa na Biblia. Yote hayo yanamwongezea furaha mwalimu wa habari njema, kwa maana anaona matunda ya kazi yake wakati habari njema zipanukapo na kufikia eneo kubwa ambalo yeye mwenyewe asingaliweza kufikia. Mfano wa jambo hilo ni kundi la kwanza la Thesalonike.—1 The. 1:8, 9.
11. Eleza furaha ambayo Paulo na Sila walikuwa nayo walipokuwa wakivumilia mateso Filipi.
11 Tukiweza kuwapa watu wengine furaha, sisi pia tunapata furaha. Bila shaka Sila na Paulo walistaajabu na kufurahi wakati Yehova alipofanya mwujiza akafungua milango ya gereza walimokuwa wamefungwa, katika Filipi mji wa Makedonia. Lakini lo! walipata furaha gani wakati mtunza gereza alipotambua kwamba walikuwa mawakili wa Mungu Aliye Juu Zaidi, kisha akawatoa nje na kuwauliza: “Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka?” Paulo na Sila walimweleza mambo ambayo Mungu anakusudia kutimiza kupitia kwa Kristo, halafu, “akabatizwa, yeye na watu wake wote wakati uo huo . . . akafurahi sana, yeye na nyumba yake yote, maana amekwisha kumwamini Mungu.”—Matendo 16:25-34.
WAKRISTO HAWAACHI UPINZANI UWAHARIBIE FURAHA YAO
12. Kwa sababu gani haitupasi kuogopa na kuvunjika moyo watu wengine wapingapo kweli na kutulaumu?
12 Lakini, watu fulani hawafurahii kuipata kweli, na huenda wakaelekea kuharibu furaha ya mtangaza habari njema. Huenda hata wakajitahidi kuzuia habari njema zisienezwe na kumtatiza mtangazaji kwa kumsingizia kwamba ana makusudi mabaya. Ndivyo mtume Paulo alivyotendwa. Hata hivyo, alipokuwa gerezani Rumi alijibu barua ya kundi la Filipi akawaambia: “Wengine wanahubiri habari za Kristo kwa sababu ya husuda na fitina; na wengine kwa nia njema. Hawa wanamhubiri kwa pendo, wakijua ya kuwa nimewekwa ili niitetee Injili; bali wengine wanamhubiri Kristo kwa fitina, wala si kwa moyo mweupe, wakidhani kuongeza dhiki za kufungwa kwangu. Yadhuru nini? lakini kwa njia zote, ikiwa ni kwa hila, au ikiwa ni kwa kweli, Kristo anahubiriwa; na kwa hiyo nafurahi, naam, nami nitafurahi.” Aliongeza, “wala [msiwaogope] adui zenu, katika neno lo lote; kwao hao ni ishara mathubuti ya kupotea, bali kwenu ninyi ni ishara ya wokovu, huo utokao kwa Mungu.”—Flp. 1:15-18, 28.
13. Mitume walionaje walipoteswa vikali Yerusalemu?
13 Wakati fulani kabla ya hapo, muda mfupi baada ya siku ya Pentekoste, mwaka 33 W.K., kuhani mkuu na Masadukayo walijawa na wivu kwa sababu mitume walikuwa wakiwapa watu ushuhuda hadharani, na hasa kwa sababu watu wengi walikuwa wakiwasikia na kuwa waamini. Waliagiza watiwe kizuizini. Walifunguliwa na malaika lakini baadaye wakakamatwa tena. Viongozi wa dini walipowasikia wakijitetea, ‘walichomwa mioyo yao; wakafanya shauri kuwaua.’ Lakini wakati Farisayo mwenye kuheshimiwa sana, aitwaye Gamalieli, alipowaonya kwa kuwaambia: “Waacheni . . . msije mkaonekana kuwa mnapigana na Mungu,” waliwapiga mitume mijeledi na kuwaamuru waache kutangaza habari zao. Je! walivunjika moyo kwa sababu ya kupona chupuchupu, wakaishiwa na furaha yao? Hapana, bali ‘walitoka wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo. Na kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.’—Matendo 5:12-42.
14. Je! tunaweza kutegemea tusaidiwe sana na Mungu kama kundi la Kikristo katika karne ya kwanza?
14 Wakati huo na nyakati nyingine, Mungu aliingilia mambo kwa kufanya miujiza ili kuonyesha kwamba alikuwa akiiunga mkono kazi ya kuzitangaza habari njema. (Matendo 12:1-11) Angali akiiunga mkono leo, maana Kristo na malaika zake wanaiangalia. Nyakati za kisasa watumishi wa Yehova wamekombolewa kiajabu mara nyingi. Wameona kazi ya kuzitangaza habari njema ikianzwa katika maeneo ambayo ilikuwa haiwezekani kuyafikia. Mungu ametumia roho yake akafanya watu waliokuwa wapinzani wakali wapendezwe na kweli, na hilo linatukumbusha jinsi Sauli alivyoongolewa, akawa mtume Paulo. (Matendo 9:1-16) Mifano ya kisasa haionekani waziwazi kuwa miujiza kama ile ya kundi la kwanza. Hata hivyo, watumishi wa Mungu wanaweza kuona uwezo wa Mwenye nguvu zote au “miujiza” ya Yehova ikisaidia katika visa hivyo.—Gal. 3:5.
15. Je! Wakristo wanajitafutia mateso, au yanawapata kwa sababu gani?
15 Watumishi wa Yehova hawafadhaiki kwa hofu, wala hawavunjiki moyo kiasi cha kuacha kazi yao kwa sababu ya kuonyeshwa ubaridi na watu wanaosema nao, maana wanasaidiwa na mkono huo hodari. Wanayakumbuka maneno ambayo Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu.” Vilevile, wanalikumbuka onyo la mtume Paulo kwamba “wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa.” (Mt. 10:22; 2 Tim. 3:12) Wakristo hawajitafutii mateso wala hawayatamani, wala hawayapendi, lakini wanapambana nayo yanapoletwa juu yao, wakijua kwamba kuvumilia majaribu kutawafaidi. Wanafuata maoni ya Wakristo wa kwanza: “Na tufurahi katika dhiki pia; tukijua ya kuwa dhiki, kazi yake ni kuleta saburi; na kazi ya saburi ni uthabiti wa moyo; na kazi ya uthabiti wa moyo ni tumaini [yaani, tumaini la kuipata thawabu]; na tumaini halitahayarishi.”—Rum. 5:3, 4.
16, 17. Askari za Israeli walitakiwa wafanye nini wakati wa kupigana na mataifa ya kipagani? (b) Je! sisi tunaweza kutazamia tusaidiwe ivyo hivyo tunapotolea watu ushuhuda?
16 Mtunga zaburi wa kale aliwatia moyo Waisraeli akawaambia: ‘Mtumikieni [Yehova] kwa furaha; njoni mbele zake kwa kuimba.” (Zab. 100:2) Aliwataka Waisraeli wote wakusanyike katika hekalu Yerusalemu ili kufanya ibada safi. Tunaweza kupata nguvu na moyo kwa kuiangalia hali na imani ya wale waliomtumikia Yehova huko nyuma. Iliwapasa waendelee kutii Torati, iliyokuwa na kanuni bora ya adili na kuelekea kuzuia Wayahudi waaminifu wasishirikiane na watu wasio waabudu wa Mungu wa kweli kwa kuwapa sheria za usafi na za ulaji. Walikuwa wamezungukwa na mataifa ya kipagani yenye kuzoea uasherati wa namna zote, ambao kwa kawaida ulihusiana na ibada chafu ya sanamu. Nyakati nyingine waliagizwa wapige watu hao ambao kwa ujumla walitaka kuwaangamiza Waisraeli na kuteka nchi yao.
17 Ebu wazia imani na ushujaa uliohitajiwa ili kwenda kupigana na mataifa hayo yenye askari waliozoea maisha ya vita, huku Waisraeli wakiwa wamezoea kufanya kazi za mashambani muda mwingi. Ebu jifikirie ukienda kushikana na maadui hao hodari. Waisraeli hawakushinda kwa nguvu zao wenyewe, maana walipoacha kumwamini Mungu mataifa hayo yaliwazidi nguvu. Tunatiwa sana moyo tusomapo masimulizi kama yale yaliyo katika 2 Samweli 23:8-22, kisha tunatambua kwamba, ingawa watu wanaotajwa walikuwa wenye nguvu na bidii, nguvu zao zisizomalizika zilitokana na kumwamini Mungu. Sisi pia tunasaidiwa hivyo leo. (Mt. 28:20; Ufu. 14:6) Kwa hiyo tusichoke kutenda mema wala tusirudi nyuma kwa hofu, maana Yehova “huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo. Haya vijana watazimia na kuchoka, na wanaume vijana wataanguka; bali wao wamngojeao [Yehova] watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.”—Isa. 40:29-31.
18. Furaha yetu inaweza kuongezekaje kwa sababu ya imani yetu, hata izidi ile ya waaminifu hao wa kale?
18 Si lazima tukabiliwe na kifo cha ghafula kila saa kama mashujaa hao, tunapozitangaza habari njema. Sisi tuna ujumbe wenye amani unaovuta mioyo ya wale wanaotaka kusikiliza kikweli. Kwa hiyo tunaweza kupata furaha nyingi zaidi. Badala ya kufanya vita kwa kutumia silaha za mwili zenye uharibifu, sisi tuna silaha za haki zisizo za kuulia watu, bali za kuondolea mafundisho na mawazo mabaya na kuponya watu. Furaha ambayo watu wanaosikia na kuamini wanapata mioyoni mwao inatuongezea furaha yetu wenyewe na kutia nguvu tumaini letu la kupata thawabu nzuri wakati ujao.—2 Kor. 6:4, 7; Kol. 3:23, 24.
—Kutoka The Watchtower, Aug. 1, 1977.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Tunaweza kupata furaha nyingi kwa kusaidia mfanya kazi mwenzetu ajifunze kweli ya Biblia