Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 2/1 kur. 62-66
  • “Uvumilivu na uwe na Kazi yake Kamilifu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Uvumilivu na uwe na Kazi yake Kamilifu”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UVUMILIVU UNA KUSUDI ZURI
  • LAZIMA ‘KUMJUA’ MUNGU
  • MFANO WA YESU
  • NAMNA YA ‘KUMJUA’ MUNGU
  • Shikamana na Tengenezo la Yehova
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • “Acheni Uvumilivu Ukamilishe Kazi Yake”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Uvumilivu—Muhimu kwa Wakristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • “Mfikirieni Sana Yeye Ambaye Amevumilia”
    ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 2/1 kur. 62-66

“Uvumilivu na uwe na Kazi yake Kamilifu”

“Uvumilivu na uwe na kazi yake kamilifu, ili mkamilike na kuwa timamu katika mambo yote, bila kukosa lo lote.”​—Yak. 1:4, NW.

1, 2. Ni kwa sababu gani inawapasa Wakristo wote wawe na uvumilivu? (Mt. 10:22, 36)

HAKUNA mtu anayemwamini Mungu awezaye kuepuka imani yake isijaribiwe. Hii ni kwa sababu roho ya ulimwengu inapinga kuwa na imani katika Mungu, na maelekeo yake ni kumkaza mtu aliye na imani, ili kuivunja. Kwa hiyo, yampasa Mkristo avumilie.

2 Jaribu la imani laweza kuja katika njia nyingi. Huenda likawa upinzani wa moja kwa moja kutoka kwa wengine, hata kutoka kwa jamaa na rafiki. Huenda likawa dhihaka, chuki, kutokufahamika vizuri, kushtakiwa uongo au kusingiziwa. Huenda yakawa mateso, hata yakaungana na ugonjwa.

3. Ni maulizo gani ambayo Mkristo anaweza kujiuliza mwenyewe anapopata majaribu?

3 Ulizo lililo mbele ya Mkristo ni, Nitavumilia mambo haya namna gani? Je! imani yangu itashinda majaribu hayo? Je! nitavumilia nikiwa na ufahamu, na kuona furaha ya kwamba imani yangu inafanyiza ubora wenye kudumu? Je! kusudi langu litakuwa kuvumilia kwa ajili ya haki, kumtukuza Mungu, si kujitukuza mwenyewe?​—Mt. 5:10.

UVUMILIVU UNA KUSUDI ZURI

4, 5. Kulingana na maoni ya Mungu, onyesha namna uvumilivu unavyotimiza kusudi, kwa kutumia maneno ya mtume Petro katika 2 Petro 1:5-7.

4 Mtume Petro anaonyesha namna uvumilivu unavyotenda kazi. Anasema hivi: “Tieni . . . kwa uvumilivu wenu kumwabudu Mungu, kwa kumwabudu kwenu Mungu shauku ya kidugu, kwa shauku yenu ya kidugu upendo.”​—2 Pet. 1:5-7, NW.

5 Basi, kwa maoni ya Mungu uvumilivu wako una kusudi​—kufanyiza watu wenye kumwabudu Mungu, watu wenye shauku ya kidugu. Kwa kuongeza, utasitawisha ndani yao upendo mkubwa zaidi na kuwaongoza wauonyeshe kwa wanadamu wenzao katika ulimwengu huu. Hawa ndio watu ambao Mungu anataka waishi katika taratibu yake mpya ya mambo. Bila shaka, Yehova Mungu hafurahii kuona watumishi wake duniani wakilazimishwa kuteswa na kuvumilia taabu, lakini yeye anataka kuwasafisha ili waweze kutimiza kabisa kwa moyo wote yale ambayo anataka kutoka kwa wanadamu, yaani, “kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu [wao]!” (Mik. 6:8) Mungu anafanya hivi kupitia kwa uvumilivu wetu. Kwa hiyo, uvumilivu ni wenye maana kubwa sana.

6, 7, Kulingana na maoni ya Mkristo, uvumilivu wamtendea mambo gani mema?

6 Kwa maoni ya Mkristo mmoja mmoja, uvumilivu unafanyiza kibali ya Mungu. Mungu anapendezwa naye na anakaribia karibu zaidi naye. (Rum. 5:3-5; Yak. 4:8) Kwa kuvumilia kwake, Mkristo anajitoa zaidi kwa Mungu. Wakati wa majaribu makali, anajifunza kwamba inampasa amtegemee Yehova sana, kwa maana hakuna mtu mwingine anayeweza kumpa mahitaji yake na nguvu anazohitaji isipokuwa Yehova, kupitia kwa Yesu Kristo. (Flp. 4:13) Kwa sababu ya uvumilivu wake mwenyewe, anasitawisha shauku nyingi kwa ajili ya ndugu zake wanaojaribiwa​—majaribu yaliyo tofauti lakini yenye kuchunguza moyo. Unamsaidia aone huruma, si kulaumu, wakati matatizo yao na udhaifu wao unapowafanya wakose.​—1 Pet. 5:9.

7 Yote haya yanaongezea Mkristo kuthamini fadhili zisizostahilika za Mungu, zinazoonyeshwa katika njia nyingi. Kwa sababu hii anampenda Mungu. Tena, anasitawisha rehema zaidi katika moyo wake juu ya wale wasio katika kweli. Anaona shida zao zinazofanya waone taabu na kuugua. (Rum. 8:22) Na upendo wake unawafikia awasaidie katika uhitaji wao wa ujumbe wa kweli wenye kutoa uzima.​—Mt. 9:36.

LAZIMA ‘KUMJUA’ MUNGU

8. Maneno ya mtume Petro katika 2 Petro 1:8 yanaonyesha namna gani kwamba uvumilivu, pamoja na sifa ambazo unasitawisha ndani ya Mkristo, unamsaidia akamilike?

8 Lakini ‘uvumilivu una kazi yake kamilifu’ namna gani, na kwa njia hiyo Mkristo anafanywa ‘mkamilifu na kuwa timamu katika mambo yote’ namna gani? (Yak. 1:4, NW) Petro anaendelea kueleza: “Kwa maana mambo haya yakiwa ndani yenu na kujaa sana, yatawazuia msiwe ama wasiotenda ama wasiozaa matunda kwa habari za maarifa sahihi [“maarifa ya kipekee,” Rotherham] ya Bwana wetu Yesu Kristo.” (2 Pet. 1:8, NW) Hili ndilo jawabu​—⁠maarifa sahihi ya kipekee ya Bwana Yesu Kristo. Na hii ni kwa sababu kumjua Yesu Kristo ni kumjua Yehova Mungu, kwa maana Yesu alisema hivi: “Aliyeniona mimi amemwona Baba.”​—Yohana 14:9.

9, 10. Biblia inatumia namna gani neno hili ‘kujua’ katika maandiko kama Mathayo 11:27, Yohana 17:3 na 1 Yohana 4:8?

9 Yesu alieleza maana ya maneno hayo yaliyotangulia wakati aliposema hivi: “Nimepewa vitu vyote na Baba yangu, wala hakuna mutu anayejua Mwana, ila Baba; wala hakuna mutu anayejua Baba ila Mwana, naye Mwana anapendezwa kumufunulia kwake.” (Mt. 11:27, ZSB) Maana yenye kupita ya maarifa haya ilitiliwa mkazo zaidi na Yesu wakati alipotangaza hivi: “Uzima wa milele uko hivi, wapate kukujua wewe, Mungu yule wa kweli peke yako, na yule ambaye ulituma, Yesu Kristo.”​—Yohana 17:3, Byington.

10 ‘Kumjua’ Baba maana yake nini? Je! maana yake ni kujua kwamba Mungu yuko? au, zaidi, kumkubali Mungu kama Mwenye Enzi Kuu na kubatizwa kama mtumishi wake? Kujua mambo haya, ndiyo. Lakini mengi zaidi yanamaanishwa. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kujua’ lina maana kubwa zaidi kuliko ambavyo neno ‘kujua’ katika Kiswahili linavyomaanisha kwa kawaida, ijapokuwa mara nyingi tunaposema twamjua mtu tunamaanisha kwamba tunamfahamu na tunafahamu sifa zake. Katika vifungu hivi vya Biblia kile kiarifa (kitendo, yaani, verb) cha ‘kujua’ kina maana ya “kuwa na habari ya, kujuana na, kufahamu.” Katika Yohana 17:3 kunaonyesha uhusiano unaoendelea kati ya Mungu na mtu anayeongeza kumjua Mungu na Kristo; yanayojulikana juu ya Mungu si kupashwa habari kidogo tu bali ni bora au yenye maana kwa mtu anayeongeza maarifa. Kunaonyesha pia hali ya usiri. (Yohana 17:3, Kingdom Interlinear) Kwa kweli, mtume Yohana anasema hivi: “Yeye asiyependa, hakumjua Mungu.”​—1 Yohana 4:8.

11, 12. Basi, mtu anayemjua Mungu atakuwa namna gani?

11 Basi kumjua Yehova Mungu kungekuwa kupata urafiki wenye kufahamiana naye. Kwa kuwa yanayomaanishwa ni maarifa ya moyoni, si maarifa ya kichwani tu, kumjua Mungu Mkristo angepatana na Mungu na katika njia zake. Angeona kama Mungu anavyoona mambo. Angekuwa na maoni ya Mungu. Na anapokutana na mawazo ya uongo juu ya Mungu na njia Zake, angeona mara hiyo kosa. Hangemlaumu Mungu kwa majaribu na taabu zake.​—Yak. 1:13.

12 Mkristo anayemjua Mungu atakuwa mtu ambaye ‘amezoeza akili zake kwa kutumiwa, ili kupambanua mema na mabaya.’ (Ebr. 5:14) Kwa kawaida haitakuwa lazima aende kwenye kitabu kinachotoa maelezo juu ya Biblia wala kwa mtu mwingine ili ajue yaliyo mema au yaliyo mabaya juu ya kisa. Kwa sababu ya mazoezi ya Kikristo, itakuwa kawaida kwake kupenda yale ambayo Mungu anapenda na kuchukia yale ambayo Mungu anachukia.​—Rum. 12:9.

MFANO WA YESU

13. Matendo ya Yesu juu ya mabaya yanaonyesha namna gani kwamba kweli alimjua Mungu?

13 Yesu alikuwa mfano mzuri wa maendeleo haya makuu katika kumjua Mungu. Alisema hivi: “Baba mwenye haki, ulimwengu haukukujua; lakini mimi nalikujua.” (Yohana 17:25) Kwa vile alipatana sana na Baba yake, Yesu alikuwa na hali ya asili ya kupenda mema na kuchukia mabaya; alikuwa akitenda kwa moyo wake wote wakati alipokataa mara moja makusudi ya Shetani na shauri baya la Petro. (Luka 4:1-12; Mt. 16:21-23) Alikuwa amechukizwa sana na lawama lo lote lililotolewa juu ya jina la Mungu, au kukosa imani kwa wale waliojidai kuwa watu wa Mungu.​—Marko 3:5; 8:11,12; Rum. 15:3.

14. Matendo ya Yesu juu ya wanafunzi wake yalionyesha namna gani kwamba kweli alimjua Mungu?

14 Lakini Yesu alisema kwamba hakuna aliyekuwa mwema isipokuwa Mungu peke yake. (Marko 10:18) Kwa hiyo hakuwa “na haki kupita kiasi” hata akaona au akatafuta kuona makosa katika wanafunzi wake, kama ‘askari polisi wa kiroho.’ (Mhu. 7:16) Wala hakuwatwika mzigo wala kuwavunja moyo, kama Mafarisayo, akizifanya dhamiri zao zichukizwe kwa kuwadai ukamilifu. (Luka 6:1-4; 11:46) Aliwapenda na akasikitikia maono yao na hali yenye huzuni ambayo katika hiyo dhambi ilikuwa imepeleka jamii ya kibinadamu.​—Yohana 11:33-36.

15. Ile kanuni ya kwamba ‘uvumilivu wapaswa uwe na kazi yake kamilifu’ ilitumikaje katika habari ya Yesu?

15 Ile kanuni ya kwamba ‘ni lazima uvumilivu uwe na kazi yake kamilifu’ ilitumika hata katika habari ya Yesu, kwa maana imeandikwa hivi: “Ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata; naye alipokwisha kukamilishwa, akawa sababu ya wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii.” (Ebr. 5:8, 9) Kwa sababu ya uvumilivu bora wa Yesu wakati wa kuteswa “tunaye kuhani mkuu, si yule asiyeweza kusikitikia udhaifu wetu, bali yule ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila dhambi.”​—Ebr. 4:15, NW.

16. (a) Tunaonaje kwamba ili mtu ‘akamilike’ yampasa avumilie nyakati zote? (b) Mtume Paulo alikuwa na maana gani kwa maneno yake katika 1 Wakorintho 13:12?

16 Kutokana na mfano wa Yesu tunaweza kuona maana ya ‘kukamilika na kuwa timamu katika mambo yote.’ Twaweza kufahamu kwamba inampasa mtu awe Mkristo nyakati zote, akivumilia majaribu. Mitume walikubali hili. Paulo alisema: “Kwa ajili ya [Kristo Yesu] nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo; tena nionekane katika yeye . . . nimjue yeye, na uweza wa kufufuka kwake, na ushirika wa mateso yake.” (Flp. 3:8-10) Kama mtume Paulo alivyosema, mradi wake ulikuwa: “Wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana.” (1 Kor. 13:12) Ijapokuwa Paulo alimjua Mungu, alifahamu kwamba kumjua sana Mungu na uhusiano ulio wa karibu zaidi sana pamoja na Mungu Ungekuja wakati Paulo angepokea thawabu kamili ya mwendo wake wa Kikristo.

17. Je! mtu anaweza kumtumikia Mungu kwa muda mrefu bila ya kumjua? Onyesha mfano.

17 Kwa upande mwingine, huenda watu wengine wakawa wanatumikia katika kundi la Mungu kwa miaka mingi pasipo kumjua Mungu sana. Mfano wa hili walikuwa Waisraeli. Walikuwa na sheria ya Mungu. Waliyaona matendo yake na hata miujiza yake. Hata hivyo Mungu aliwaambia: “Baba zenu waliponijaribu, wakanipima, wakaona matendo yangu miaka arobaini. Kwa hiyo nalichukizwa na kizazi hiki, nikasema, Sikuzote ni watu waliopotoka mioyo hawa; hawakuzijua njia zangu.”​—Ebr. 3:9; Zab. 95:9-11.

NAMNA YA ‘KUMJUA’ MUNGU

18. Ni jambo gani moja kati ya mambo ya kwanza ambayo inampasa Mkristo afanye ili aweze kumjua Mungu?

18 Basi, Mkristo anaweza kuhakikisha namna gani kwamba atamjua Mungu? Kwanza, yampasa aendelee kuomba roho ya Mungu, kwa kuwa mtu anaweza kufahamu akili za Mungu na utu wake kupitia kwa roho takatifu peke yake. Sala ni mojawapo ya mapendeleo ya kipekee zaidi ambayo Yehova ametupa. Kwa kuumwaga moyo wake Mkristo anamfanya Mungu kuwa msiri wake. Nayo sala ina nguvu, kwa sababu Yehova anasikia na kujibu kweli sala katika njia inayowafaidi zaidi sana wale wanaomwomba.​—Zab. 65:2; Rum. 8:28

19. Inampasa mtu atumie Biblia namna gani ili amjue Mungu?

19 Imesemwa mara nyingi kwamba funzo na kutafakari juu ya Neno la Mungu ni ya lazima. Hii ni kweli. Lakini, zaidi ya hayo, yampasa Mkristo alitumie Neno hilo. Kwa mfano, wakati kunapotokea kisa au tatizo juu ya mwenendo katika maisha, je! Mkristo huyo anafuata wazo lake au anachunguza aone kama anapatana na njia za Mungu? Kama hana hakika sana, je! anahakikisha kabla ya kusema au kutenda kwamba yale anayosema au kutenda yanapatana na Biblia? Je! majibu anayowapa wengine ni maoni yake mwenyewe? au anaweza kuhakikisha anayosema na Biblia?

20. (a) Yesu alionyesha namna gani kwamba kweli alikuwa karibu sana na Mungu, akimjua na kutaka wengine wamjue? (b) Tumia maandiko fulani kati ya yale yaliyotajwa katika fungu uonyeshe namna Yesu alivyotumia Maandiko ya Kiebrania ili asadikishe wasikiaji wake.

20 Anayefanya hivi anafuata mfano wa Yesu mwenyewe, kwa maana alisema: “Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo; na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka.” (Yohana 5:30) Haikuwa sababu tu ya kwamba Yesu aliangalia andiko au hata akataja andiko moja kila wakati, bali, wakati wa kueleza au kukaripia, ama alitaja maneno ya Maandiko ya Kiebrania ama akaeleza kanuni iliyomo hata wasikiaji wake wakajua kwamba jibu lake lilitoka kwa Mungu. Katika kusoma maneno ya Yesu utaona ajabu ya uhakika wa kwamba sehemu kubwa ya yale aliyosema yalikuwa ama ni maneno yenyewe ama mtajo wa maneno ya Maandiko ya Kiebrania.​—⁠Linganisha Yohana 5:31, 32 na Kumbukumbu la Torati 19:15; Marko 10:27 na Mwanzo 18:14 na Ayubu 42:2; Mathayo 10:35 na Mika 7:6; Yohana 10:34 na Zaburi 82:6.

21. Maneno ya mtume katika Warumi 12:1, 2 yanaonyesha namna gani kwamba kujitahidi kunahitajiwa ili kumjua Mungu kweli kweli?

21 Kwa hiyo, inachukua wakati na kupauta ujuzi, pamoja na kujitahidi nyakati zote ili kufikia mradi huu Mkristo amjue Mungu. Mtume Paulo alishauri Wakristo hivi: “Ndugu, ninawasihi ninyi, kwa rehema za Mungu, mutoe miili yenu iwe zabihu iliyo hai, takatifu, ya kupendeza Mungu, ndio utumishi wenu ulio na maana. Na musifananishwe kwa namna ya dunia hii; lakini mugeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mupate kujua sana mapenzi ya Mungu, yaliyo mema, ya kumupendeza, na ukamilifu.” (Rum. 12:1, 2, ZSB) Ili utuhakikishe mapenzi ya Mungu yalivyo inatupasa tuone wema wake kwa kuyaacha yatende kazi katika maisha zetu, kwa kuyatumia. Kwa hili tunajua mapenzi hayo na ukamilifu wake​—njia ya Mungu ya kufikiri iliyo nzuri na kamilifu. Tunajua yanayokubalika kwake na katika njia hiyo tunapata kibali yake na uhusiano mzuri, wa karibu sana. Ndipo tunapoweza kuona kama vile mwana aliye na baba mwenye upendo sana anayemwangalia na kumsaidia kila wakati wa uhitaji.

22. Ni jambo gani kubwa ambalo inampasa Mkristo afanye ili ageuze fikira zake za ulimwengu, kama inavyoelezwa na Paulo katika Warumi 12:3?

22 Halafu akiisha kushauri Wakristo wajihakikishie yaliyo mapenzi ya Mungu, yaliyo merna, mtume anaendelea kuonyesha namna ya kuonyesha nia isiyofuata mtindo wa ulimwengu huu na fikira zake na mazoea yake. Anasema hivi: “Kwa sababu ya neema niliyopewa, ninamwambia kila mutu wa kwenu, asiwaze kujisifu kupita ilivyomupasa kuwaza, lakini awaze kwa akili, kama Mungu alivyogawia kila mutu kadiri ya imani.” (Rum. 12:3, ZSB) Katika njia hii Mkristo atajali sana ndugu zake, asijilinganishe na wengine au kwa sababu ana uwezo fulani, afikiri kwamba yeye ni bora au anastahili kunyenyekewa na kupewa mapendeleo makubwa zaidi. Mtume anaendelea kusema, akieleza sababu:

23. Uhusiano wetu unapaswa uwe wa namna gani pamoja na wengine katika kundi ili ‘tukamilike’ katika imani?

23 “Kwa maana kama vile katika mwili mumoja tuna viungo vingi, na viungo vyote havina kazi moja; vivyo sisi tulio wengi, ni mwili mumoja katika Kristo, na sisi sote ni viungo kila mumoja kwa mwenzake.” (Rum. 12:3, 4 ZSB) Ni kwa kusudi gani tumo katika kundi? Tusaidiane ili tuvumilie mpaka kutimiliza imani yetu kupitia kwa uvumilivu. Basi na tuone cheo chetu kilivyo katika kundi tufanye yote tuwezayo tutumikie humo. Mtume anamalizia hivi:

24. Ukitumia Warumi 12:6-8, eleza njia nyingi za utendaji ambazo Wakristo wanaweza kujitahidia, na roho ya kufanyia hivi.

24 “Lakini tukiwa na zawadi za namna mbalimbali, kwa kadiri ya neema tuliyopewa; kama unabii, tutabiri [kutia kusema na kuhubiri] kwa kadiri ya imani; ikiwa utumishi, tutumike katika utumishi wetu; ao mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kutoa zawadi, atoe kwa ukarimu; mwenye kusimamia, kwa bidii; mwenye kurehemu, kwa furaha.”​—Rum. 12:6-8, ZSB.

25. Mtume Petro anatutia moyo namna gani katika kujitahidi kwetu ‘tukamilike’ machoni pa Mungu?

25 Tukiyathamini maneno haya na kuyafuata sana, tutakuwa wakamilifu machoni pa Mungu, kama mtume Petro alivyoandika: “Baada ya kuteswa kwa muda, Mungu wa fadhili zote zisizostahilika, aliyewaitia utukufu wake wa milele katika umoja na Kristo, yeye mwenyewe atamaliza mazoezi yenu, atawafanya mwe imara, atawafanya mwe na nguvu.”​—1 Pet. 5:10, NW; Yak. 1:12.

​—Kutoka The Watchtower, Sept. 15, 1976.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki