Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Mkristo aliyebatizwa akikubali kutiwa kiungo cha kibinadamu mwilini, kama vile chamba cha jicho (cornea) au figo, je! kundi limchukulie hatua?
Kwa habari ya kutiwa nyama au mfupa wa kibinadamu kutoka kwa mwanadamu mwingine ni jambo linalohusu uamuzi wenye kuongozwa na dhamiri wa kila mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Huenda Wakristo wengine wakaona kwamba kukubali kutiwa nyama yo yote au kiungo cha mwili kutoka katika mwanadamu mwingine ni kula nyama ya wanadamu. Huenda wakashikilia kwamba nyama hiyo ambayo imetiwa mwilini imekusudiwa iwe sehemu ya mwili wa yule ambaye ameikubali ili iendeleze uhai wake na kumwezesha kutenda. Huenda wasione tofauti yo yote na kula nyama kupitia kwa mdomo. Maono ya namna hiyo huenda yakatokea kwa sababu ya kufikiria kwamba Mungu hakutoa ruhusa ya kula nyama ya mwanadamu wakati alipotoa ruhusa ya kula nyama ya wanyama iliyokuwisha kuondolewa damu yenye kuendeleza uhai. Huenda vilevile wakafikiria namna watu walioishi wakati Biblia ilipokuwa ikiandikwa walivyoona juu ya kuendeleza uhai wao kwa kula nyama ya mwanadamu. Kwa mfano, angalia habari katika 2 Wafalme 6:24-30; Kumbukumbu la Torati 28:53-57; Maombolezo 2:20 na 4:10. Katika Yohana 6:48-66, Yesu alisema kwa njia ya mfano juu ya kula nyama ya mwili wake na kunywa damu yake. Kwa kusikia mazungumzo hayo na kutofahamu maana ya kiroho ya maneno yake, wengine wa wanafunzi wake Wayahudi walichukizwa wakaacha kumfuata. Habari hizi huonyesha namna wanadamu wengine walivyoona juu ya kula nyama ya mwili wa kibinadamu.
Wakristo wengine leo wenye mioyo minyofu huenda wakaona kwamba Biblia haikatazi kabisa matibabu ya kutiwa viungo vya mwili wa kibinadamu. Huenda wakatoa sababu kwamba hiyo nyama ya mwili wa kibinadamu haikusudiwi iwe sehemu yenye kudumu ya mwili wa yule anayeipokea. Chembe za mwili wa kibinadamu zasemekana kwamba zinabadilishwa baada ya kila miaka saba, na ndivyo ingekuwa kwa habari ya sehemu yo yote ya mwili wa kibinadamu ambayo ingetiwa katika mwili wa mtu mwingine. Vilevile sababu yaweza kutolewa kwamba kutiwa kiungo cha mwili wa mtu mwingine ni tofauti na kula nyama ya mwili wa mtu kwa kuwa “mtoaji” hauawi ili nyama ya mwili wake itumiwe kama chakula. Katika visa fulani watu wanaokaribia sana kufa walikubali kwamba sehemu za mwili wake zitumiwe katika kutiwa katika miili ya wengine. Bila shaka, ikiwa kutiwa kiungo mwilini kulihitaji kutiwa damu ya mtu mwingine, kwa wazi hiyo ingekuwa kinyume cha sheria ya Mungu.—Matendo 15:19, 20.
Kwa wazi, maoni ya kibinafsi pamoja na maoni yenye kuongozwa na dhamiri juu ya ulizo hili la kutiwa viungo mwilini hutofautiana. Inajulikana kwamba matumizi ya sehemu za mwili wa kibinadamu katika miili ya kibinadamu hutofautiana sana kuanzia sehemu ndogo-ndogo kama vile vichocheo vya viungo (hormones) na chamba mpaka viungo vikubwa kama vile figo na moyo. Ijapokuwa Biblia inakataza waziwazi matumizi ya damu, hakuna amri ya Kibiblia inayokataza waziwazi matumizi ya sehemu nyingine za mwili wa kibinadamu. Kwa sababu hiyo, kila mtu mmoja mmoja anayeelekeana na ulizo la kuamua juu ya jambo hili apaswa kufikiria mambo kwa uangalifu na kwa sala kisha afanye uamuzi kwa kutumia dhamiri juu ya analopaswa kufanya asilopaswa kufanya mbele za Mungu. Ni Jambo linalohusu uamuzi wa mtu binafsi. (Gal. 6:5) Halmashauri ya hukumu ya kundi haiwezi chukua hatua ya kuadhibu mtu ikiwa amekubali kutiwa kiungo cha mwingine mwilini mwake.