Kwa Nini Ufanye Yaliyo Haki?
‘NITAPATA kitu gani nikifanya hivyo?’ Wewe umesikia mara ngapi mtu akiuliza ulizo hilo kabla ya kuanza kufanya kazi fulani? Inaelekea umeona kwamba ni mara chache sana watu wanapotumia jitihada zao bila ya kuhakikishiwa watapewa thawabu fulani. Watoto huonyesha wazi nia hiyo mara nyingi na kwa kiasi kikubwa. Wao hukataa kutenda mambo kwa adabu njema ‘wasipohongwa’ (kupewa rushwa) kwa kuambiwa watapata kitu fulani wakitenda wanavyopaswa kutenda.
Biblia inaonyesha chanzo hasa cha tatizo hilo, ikisema: “Wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Rum. 3:23, NW) Wanadamu wanazaliwa wakiwa na maelekeo ya kufanya makosa kwa sababu walirithi dhambi. Jitihada nyingi zinahitajiwa ili mtu aweze kufanya yaliyo haki.
Je! nia hiyo inaweza kuhusu ibada ya Mungu? Ndivyo. Muumba anataka watumishi wake wafanye yaliyo haki. Kanuni yenye kuonyesha ni upi unaoweza kuitwa mwenendo unaofaa imewekwa katika Biblia Takatifu. Kutokana na chanzo hicho tunajifunza pia kwamba Mungu “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Ebr. 11:6, NW) Walakini, watu wasipojiangalia wanaweza kwa urahisi kuangukia kosa la kuona matendo ya ibada na ya kujitolea Mungu kama njia ya kujichumia (kujipatia kama mshahara) upendeleo wake.
Jambo hilo liliwapata hasa Wayahudi wa kale. Wao walikuja kuuona utii kwa sheria ya Musa kama njia ya kujipatia “ustahili” (sifa) mbele za Mungu, ustahili ambao ungewahakikishia kupata baraka nyingi wakati ujao. Mapokeo ya imani za marabi wa Kiyahudi yanataja kwamba rabi mmoja (mwalimu wa kidini) alisema: “Yule Mtakatifu, mbarikiwa ni yeye, alikusudia kuwapa Israeli ustahili; ndiyo sababu yeye amewazidishia ile Torati na sheria.” Kulingana na maoni hayo, ilifikiriwa kwamba kwa sababu amri za sheria ya Mungu zilikuwa nyingi sana ziliwapa Israeli nafasi nyingi sana za kujipatia ustahili kwa kuzitii. Jambo hilo linatusaidia tulifahamu vizuri zaidi ulizo ambalo Yesu aliulizwa na kijana mmoja aliyekuwa mwanamume tajiri: “Mwalimu mwema, nifanye nini ili nipate kuurithi uzima wa milele?” (Luka 18:18) Mwanamume huyo aliamini kwamba uzima wa milele ungeweza kuchumwa (kupatwa kama mshahara) kwa kutenda mema.
Wakristo hawako chini ya wajibu wa kufuata sheria ya Musa kama Wayahudi wa kale. Hata hivyo, Biblia inawatia moyo Wakristo wajishughulishe na “vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa.” (2 Pet. 3:11, NW) Matendo hayo yanatia ndani kutumia wakati ili mtu aeleze jirani kweli za Biblia, apatanishe njia yake ya maisha na maongozi ya Maandiko, na kukutana kwa ukawaida pamoja na Wakristo wenzake kwa ajili ya mazungumzo ya Biblia. —Mt. 24:14; 28:19, 20; Kol. 3:5-10; Ebr. 10:23-25.
Lakini ni nini kinachopasa kisukume mtu awe na mwenendo huo wa kimungu? Anapaswa asukumwe hasa na imani thabiti—imani inayomsukuma Mkristo ‘ajinyoshe akaufikilie mradi’ wa uzima wa milele. (Flp. 3:13, 14, NW; 2 Tim. 4:7, 8) Imani hiyo inaonyeshwa tunapomtolea Mungu wetu utumishi wa moyo wote, si katika utumishi mdogo tu unaofanywa mradi tu mtu awe na kitu cha kuonyesha amefanya utumishi fulani, wala si katika kushika sheria na kanuni fulani, kama walivyofanya Wayahudi. Paulo aliandika: “Hali tukijua ya kuwa mwanadamu hahesabiwi haki kwa matendo ya sheria, bali kwa imani ya Kristo Yesu; sisi tulimwamini Kristo Yesu ili tuhesabiwe haki kwa imani ya Kristo, wala si kwa matendo ya sheria; maana kwa matendo ya sheria hakuna mwenye mwili atakayehesabiwa haki.” (Gal. 2:16) Kwa hiyo, hakuna mtu anayeweza kujipatia kama mshahara upendeleo wa Mungu na baraka yake kwa kutenda matendo ya ibada ambayo ni desturi tu au kwa matendo ya kufadhili watu yanayofanywa kidesturi tu, hata yawe ni ya namna gani na yamefanywa kwa ukubwa gani. Msimamo wenye haki mbele za Mungu unapatikana tu ‘kwa kumwamini Kristo Yesu.’
Ifuatayo ni kati ya mistari ya Biblia inayojulikana, zaidi sana katika Biblia nzima: “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” “Amwaminiye Mwana yuna uzima wa milele; asiyemwamini Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu inamkalia.” (Yohana 3:16, 36) Mungu alimtuma Mwanawe, Yesu Kristo, akailipa bei kubwa sana ya kukomboa wanadamu katika dhambi na kifo. (Mt. 20:28) Yesu alitimiza jambo hilo kwa kufa akiwa dhabihu juu ya mti wa kuulia watu. Mtume Petro anaandika hivi: “Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti; ili, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki.” (1 Pet. 2:24) Kufanya hivyo kulifungulia watu nafasi za kupata “uzima wa milele”—lakini si kama thawabu wanayojipatia kama mshahara wa kuwa na mwenendo mwema. Biblia inaeleza uzima wa milele kuwa “kipawa atoacho Mungu.”—Rum. 6:23, NW.
Hata hivyo, mtu akiwa na imani halisi katika kipawa hicho kizuri ajabu, imani yake itajionyesha wazi katika kutangazia wengine waziwazi habari za tumaini lake na katika mwenendo wake mwema wa Kikristo. (Rum. 10:8-10) Imani hiyo haiwezi kuonyeshwa bila kufanya hivyo. Jambo hilo linafahamishwa wazi na Yakobo mwandikaji wa Biblia, anayesema hivi: “Ndugu zangu, yafaa nini, mtu akisema ya kwamba anayo imani, lakini hana matendo? . . . imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake. Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa.”—Yak. 2:14-17, 26.
Yakobo ana maana gani anaposema “matendo”? Hayo si matendo yanayofanywa kwa kusudi la kujipatia kitu fulani wakati ujao. Bali, ni matendo yanayotendwa kama ushuhuda wa imani ya mtu na kwa sababu ya kuthamini kitu alicho nacho tayari, yaani, msimamo mwema mbele za Mungu kama matokeo ya kumwamini Yesu Kristo.
Kulingana na hayo, kwa sababu gani watu wanaompenda Mungu humtumikia, wakifanya yaliyo haki? Kusudi la kufanya hivyo halipasi liwe la uchoyo, la kwamba ‘watajipatia kitu fulani wakimtumikia. Wakristo humtumikia Mungu kwa sababu wanajua jinsi Mungu ameonyesha anapendezwa na wanadamu na kwa sababu ya toleo lake la ukarimu la uzima wa milele ambao ni kipawa kisicho cha kulipia. Wonyesho huo wa upendo wa Mungu unaharakisha waabudu wake wamwige yeye. Ni kama vile alivyosema mtume Yohana: “Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu. Wapenzi, ikiwa Mungu alitupenda sisi hivi, imetupasa na sisi kupendana.”—1 Yohana 4:9-11.