“Matendo” ya Kikristo—Yanatia Nini Ndani?
“IMANI pasipo matendo imekufa.” (Yak. 2:26) Kwa maneno haya mwanafunzi Yakobo aliwatia moyo waamini wenzake waonyeshe imani yao kwa matendo kwa utendaji. Matendo ya Kikristo yanayofaa ni gani?
Haya si matendo ambayo kwayo Mkristo anaweza “kujipatia” thawabu (zawadi) ya uzima wa milele. Wengine wa waliotafuta uzima katika karne ya kwanza walifikiri kwamba hilo ni jambo linalowezekana, kwa kushika torati ya Musa. Walakini, Paulo, mtume Mkristo alisahihisha maoni yao. Chini ya uongozi wa Mungu aliandika hivi: “Mwanadamu hahesabiwi haki kwa matendo ya sheria, bali kwa imani ya Kristo Yesu.” (Gal. 2:16) Wanadamu wenye makosa hawawezi kushika sheria ya Mungu pasipo makosa, na kwa hiyo, inawaonyesha kuwa wenye dhambi wanaostahili kifo, si uzima. “Kwa matendo ya sheria,” yasema Biblia, ‘dhambi inatambulishwa kwa sheria.’ (Rum. 3:20) Kwa hiyo, haiwezekani mtu kuwa na msimamo unaokubaliwa na Mungu kwa matendo yake mema. Hilo linawezekana tu katika njia ile inayokusudiwa na Yehova Mungu, yaani, kupitia kwa imani katika Yesu Kristo yeye ambaye dhabihu yake inasafisha dhambi.
Kuwa na imani katika Yesu Kristo vilevile kunahitaji kuwa na imani katika Yehova Mungu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka.” (Rum. 10:9) Imani ya namna hii ni zaidi ya kuamini tu kwamba Mungu yuko. Inatia ndani kuamini ahadi zote za Mungu kama zilivyoandikwa katika Neno lake, Biblia. “Pasipo imani,” chasema Waebrania 11:6, “haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”
Angalia kwamba utendaji unakamatana na kuwa na imani hii. Mtu huyo inampasa awe mtu anayemtafuta Mungu kwa bidii, akitaka kujipatanisha na njia zake na mapenzi yake. Kujipatanisha huku kunahusu kila sehemu ya maisha. Biblia inashauri hivi: “Fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Kwa hiyo, ingawa mtu hawezi kujipatia uzima wa milele kwa jitihada zake mwenyewe, matendo mema ni sehemu ya lazima ya maisha ya Mkristo. Pasipo ushuhuda ulio wazi wa matendo ya Kikristo yanayofaa, imani ya mtu ingekuwa haina uhai, imekufa.
KAZINI
Kwa mfano, imani ya mtu katika Mungu, inapaswa ionekane kazini. Anapaswa kuwa akitenda kupatana na kanuni zilizoandikwa katika Biblia juu ya ushirikiano wa mtumwa na bwana wake. Tunasoma hivi: “Enyi watumwa, watiini wao walio bwana zenu kwa jinsi ya mwili, kwa hofu na kutetemeka, kwa unyofu wa moyo, kana kwamba ni kumtii Kristo; wala si kwa utumwa wa macho tu kama wajipendekezao kwa wanadamu; bali kama watumwa wa Kristo, mkitenda yampendezayo Mungu kwa moyo; kwa nia njema kama kumtumikia Bwana wala si mwanadamu.”—Efe. 6:5-7.
Kutii shauri hili kunahitaji nini? Mkristo anapaswa kumheshimu tajiri wake, akifanya yale anayohitajiwa kufanya kama kwamba anafanya utumishi wa Mungu na Kristo moja kwa moja. Hapaswi kupoteza wakati, akifanya kazi wakati tu anapotazamwa. Kwa kuwa na bidii, mwaminifu na kwa kuongozwa na dhamiri yake, Mkristo ataepuka kufanya Mungu na Kristo walaumiwe. Yeye atakuwa akionyesha kwamba imani yake katika Mungu imemfanya kuwa mfanya kazi bora, na kwa njia hiyo aufanye Ukristo wa kweli uwavutie wanaomtazama.
KAMA WAZAZI
Vilevile kutimiza daraka la kuwa mzazi kwa kufaa ni matendo yanayofaa ya Kikristo. Ni mapenzi ya Mungu kwa wanawake na akina mama “wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao; na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe.” Sababu ya hili ni kwamba “ili neno la Mungu lisitukanwe.” (Tito 2:4, 5) Waume na akina baba wanashauriwa na Maandiko: “Kila mtu ampende mke wake kama nafsi yake mwenyewe.” (Efe. 5:33) “Msiwe mkiwaudhi watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika adabu na rekebisho la moyoni la Yehova.” (Efe. 6:4, NW) Wanaume na wanawake wanaoishi kama linavyoshauri Neno la Mungu wanafanya matendo ya imani. Wanaonyesha kwamba wanaamini kwamba Mungu yuko na kwamba yale anayoshauri katika Neno lake ni yenye faida kweli kweli.
KUHANGAIKIA WANADAMU WENZAO
Zaidi ya hayo, mtu anapomwiga Mungu katika kufanya kazi pamoja na wanadamu wenzake kwa jumla, yeye anakuwa akifanya matendo yanayofaa ya Kikristo. Yehova Mungu ni mwenye fadhili na mkarimu hata kwa wanadamu wasioshukuru, akiwaruhusu wafaidike na jua na mvua. (Mt. 5:44, 45) Hata alichukua hatua ya kwanza kwa kuwawekea wanadamu wenye dhambi msingi ili wawe na uhusiano (ushirikiano) unaokubaliwa naye. Jambo hili lilimgharimu sana, akamtoa Mwanawe wa pekee kwa ajili ya wanadamu.—Yohana 3:16; Tito 3:4-7.
Kulingana na yale ambayo Yehova Mungu amefanya, Mkristo anapaswa kuwatendea wengine kwa fadhili, akihangaikia hali njema yao. Hiyo inamaanisha, kama Wagalatia 6:10 linavyotutia moyo, ‘kuwatendea wote mema.’ Kama iwezekanavyo, mtumishi wa Mungu aliyejitoa anapaswa kuwa na nia na shauku ya kuwasaidia wale walio na shida kweli kweli. Walakini, angetaka kuepuka kujionyesha, mahali pake, akifuata pendekezo la Yesu: “Wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; sadaka yako iwe kwa siri, na Baba yako aonaye sirini atakujazi.”—Mt. 6:3, 4.
KAZI YA MAANA SANA YA KUHUBIRI
Mojawapo wa njia bora sana za kuwasaidia wanadamu wenzetu ni kuwapa ufahamu juu ya yale yanayotakiwa na Mungu kwa wale ambao wangekuwa watumishi wake wanaokubaliwa. Kwa kweli, Wakristo wako chini ya amri wafanye hivyo. “Nendeni,” akasema Yesu, “mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—Mt. 28:19, 20, NW.
Wakristo wa karne ya kwanza walifanya nini ili watimize amri hii? Walitumia wakati washiriki “habari njema” na jamaa zao, wale waliojuana nao na wale wote waliokutana nao. Walakini hawakufanya utendaji wao wa kuhubiri kwa watu wale tu wangeweza kupashana habari nao kwa kawaida. Kama sivyo, wangewezaje kushtakiwa kwamba ‘wanaupindua ulimwengu’? (Matendo 17:6) Kwa wazi kulikuwako na juhudi na jitihada za ‘kujaza Yerusalemu’ pamoja na miji mingine mafundisho yao. (Matendo 5:21, 25, 28, 42; 8:4-6; 13:5, 14-16; 14:1; 16:13, 14; 17:17-21) Ndiyo, Wakristo wa kwanza walichukua hatua ya kwanza wawafikie watu wengi zaidi kama iwezekanavyo na ujumbe wao wenye kuokoa uhai.
Mara nyingi kuhubiri watu wote katika sinagogi au sokoni kulifanya wale wanaopendezwa wapatikane. Watu hawa walipoukubali Ukristo, walikuwa wakiwakaribisha nyumbani mwao watangazaji wa ujumbe wa Mungu. Kufanya hivyo kuliwafaidi sana kiroho waamini hawa wapya, kwa kuwa waliendelea kufundishwa nyumbani mwao.—Linganisha Matendo 16:15, 32-34; 18:6, 7.
Desturi iliyokuwako haikuruhusu wanawake wafundishe katika sinagogi na sokoni. Hata hivyo, kwa kuwa wanawake walioamini walikuwako wakati wanaume walipokuwa wakifundisha, wangeweza kuandika majina ya wale waliokuwa wakionyesha kupendezwa. Ndipo, wakisaidiana na waume zao, walishiriki kufundisha hata wanaume. Kwa mfano, wakati Akila na mkewe Prisila walipomsikia Apolo akinena katika sinagogi katika Efeso, “wakamchukua kwao, wakamweleza njia ya Bwana kwa usahihi zaidi.” (Matendo 18:26) Wanawake hawa mmoja mmoja walioamini bila shaka walichukua hatua wawafikie wanawake wengine vilevile, wakiwatolea habari zaidi juu ya yale yaliyokuwa yamezungumzwa hadharani na wanaume.
Maadamu Wayahudi Wakristo waliporuhusiwa kusema katika sinagogi, walienda huko kila siku ya Sabato. (Matendo 17:1-4) Hii iliwawezesha kuhubiri “habari njema” kwa jamii yote ya Kiyahudi katika kila kijiji au mji. Na kwa kutoa ushuhuda hadharani kwa ukawaida sokoni, watu wale wengine wote wangefikiwa na ujumbe wa Kikristo wenye maana sana. Kwa sababu ya utendaji kama huo wa hadharani, wanabiashara wasafirio pamoja na wageni vilevile wangejifunza juu ya “habari njema.” Vivyo hivyo, Wakristo waliposafiri kwenda sehemu nyingine, walishiriki na wengine imani yao. Na kama matokeo, kundi moja tu la waamini lingaliweza kufanya kweli isikiwe katika sehemu nyingi zilizo mbali sana katika nchi nzima.
Angalia alivyosema mtume Paulo juu ya hili kwa habari ya kundi lililokuwako Thesalonike. “Kutoka Thesalonike neno la Bwana limevuma; wala si katika Makedonia na Akaya peke yake, bali kila mahali imani yenu katika Mungu imeyafikia masikio ya watu. Hakuna maneno [yo yote] yetu yanayohitajiwa, kwa kuwa wao wenyewe wanaeneza habari za ziara yetu kwenu na matokeo yake: namna mlivyogeuka mkaziacha sanamu, mwe watumishi wa Mungu aliye hai na wa kweli, na kungojea kwa kutazamia kuonekana kwa Mwana wake Yesu kutoka mbinguni, aliyemfufua kutoka kwa wafu, Yesu mkombozi wetu kutokana na woga wa hukumu itakayokuja.”—1 The. 1:8-10, The New English Bible.
“MATENDO” YA HADHARANI LEO
Lakini kundi la Wakristo wa kweli leo linawezaje kujulikana sana kama lilivyojulikana kundi la Thesalonike? Kwa wazi, mengi yanahusika kuliko kuzungumza tu na watu wa jamaa, wale tunaojuana nao na wengine ambao huenda tukakutana nao. Bila shaka hili lapaswa kufanywa, nayo ni njia ya maana ya kueneza “habari njema.” Walakini, kuongezea hayo, kama alivyofanya Yesu Kristo pamoja na wafuasi wake wa karne ya kwanza, mashahidi Wakristo wa Yehova leo wanapaswa kuchukua hatua ya kwanza wawatangazie wengine ujumbe wa Mungu. Katika nchi nyingine, kuhubiri kwingi bado kunaweza kufanywa hadharani—viwanjani na sokoni. Hata hivyo, hata huko namna ya mazungumzo ya hadharani waliyotumia katika karne ya kwanza hayajulikani. Kuhubiri kwingi kwa namna hiyo leo katika sehemu zenye watu wengi kunafanywa kwa kuwatolea watu wanaopita magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, au kuzungumza na vikundi vidogo na watu mmoja mmoja. Kwa kawaida hiyo si njia ambayo wengi wa wakaaji wa kijiji au mji fulani wanayoweza kufikiwa nayo.
Hivyo basi, ushuhuda ulio mkamilifu zaidi unaweza kutolewaje? Yaliyoonwa na Mashahidi wa Yehova kwa muda wa zaidi ya miaka 50 yameonyesha vizuri sana kwamba jibu ni—KWENDA NYUMBA KWA NYUMBA KWA UKAWAIDA. Kwa hiyo, katika sehemu za dunia ambako kuhubiri nyumba kwa nyumba kunawezekana, wote ambao hali yao ya mwilini inawawezesha kushiriki kazi hiyo bila shaka wangetaka kuweka kando wakati wa kuishiriki kila mwezi. Kuhubiri nyumba kwa nyumba kunaendelea kuwa njia ambayo katika hiyo maelfu mengi ya watu yanaendelea kujulishwa ujumbe wa Biblia kila mwaka na kusaidiwa wawe wanafunzi wa Yesu Kristo. Zaidi ya hayo, inamsaidia Shahidi mwaminifu asitawishe na kuendeleza unyenyekevu kwa kumwiga Bwana.—Yohana 13:15, 16.
Matendo yale yote mengine yanayofaa ya Kikristo, kutia na mwenendo mzuri wa kibinafsi, yanaipa maana kazi yenye maana ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Yanaonyesha kwamba Ukristo wa kweli unaongoza kwenye maisha yenye uradhi, yenye maana na yenye furaha hata sasa. Zaidi ya hayo, kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi inawaonyesha wengine kwamba kuwa na imani katika Mungu ndiko kunakomwezesha mtu kuwa mfanya kazi mzuri, jirani mwenye kusaidia na mume na baba mwenye upendo, au mke na mama mwenye upendo.
Kwa kweli kuna matendo mengi yanayofaa ya Kikristo. Haya si matendo yanayofanywa ili mtu “ajipatie” thawabu ya uzima wa milele, kana kwamba kwa njia hiyo Mungu anakuwa na “deni” yetu. Mahali pake, hayo ni matendo ya imani, yanayoonyesha kwamba mtu anaamini kwamba Mungu yuko na kwamba anawapa thawabu watumishi wake. Ikiwa sisi tuna imani halisi kwamba Mungu ni mpaji wa thawabu, wengine wanapaswa kuona imani yetu ikitenda kazi katika kujipatanisha kwetu na njia zake na katika mwenendo wetu wote na katika bidii yetu katika kutangaza ujumbe wake kwa wanadamu wenzetu. Kunapokuwa na ushuhuda ulio wazi wa matendo kama hayo yanayofaa, imani ya Mkristo i hai, ina matendo.